The Chant of Savant

Sunday 30 April 2017

Wanaolaumu Magufuli kuhusu Israeli wasome historia

  1. pi.JPG
    Rais John Magufuli akisalimiana na balozi wa Israel nchini Yahel Vilan ikulu jijini Dar Es Salaam
        Baada ya rais John Magufuli kuridhia kufunguliwa ubalozi wa tanzania nchini Israeli, wengi walishangaa hata wengine kumlaumu wakiona kama anakwenda tofauti na msimamo wa Tanzania bila kujua kuwa mambo yamebadilika tena sana. Kwani, alichofanya ni tofauti na msimamo wa Tanzania ulioasisiwa na baba wa taifa Mwl Julius Nyerere. Hivyo, wengi waliona kama anakiuka miiko ukiachia mbali kuonekana kama anaangalia ndani (inward looking) akipuuzia uhusiano wa kimataifa. Rais Magufuli alikaririwa hivi karibuni akisema “nimeamua kurudisha uhusiano na Israeli, kwa kumteua Balozi tu umekuja ujumbe wa watalii wapatao 600 kutoka nchi hiyo, fedha zimeingia.”
            Katika kudurusu hili, nitatoa sababu zifuatazo:
            Mosi, siasa za sasa na za wakati wa akina Mwl Nyerere ni tofauti sana. Wakati wa Mwalimu, dunia ilikuwa kwenye kile kinachoitwa vita baridi (Cold War) kati ya Marekani na Umoja wa Kisovieti wa Kirusi (USSR) kama mataifa mawili kandamizi na koloni bila kujali nani alikuwa upande gani. hata hivyo, baada ya kuanguka kwa ukuta wa Berlin hapo 9 Novemba,1989 dunia ilibadilika kwa kiwango kikubwa baada ya upande wa Magharibi ukiongozwa na Marekani kufanikiwa kuuangusha upande wa Mashariki  ukiongozwa na Urusi. Hivyo, siasa za wakati ule ni tofauti kabisa na za sasa. Wanaoona kama ni ajabu kuanzisha uhusiano na taifa la kizayuni lenye sifa ya kuwakandamiza Wapelestina, inabidi waelewe hili.
            Pili, tujiulize. Hivi kama Palestina ingekuwa huru na sisi tukiwa tunatawaliwa ingekuwa tayari kutoa sadaka ya uchumi wake eti kwa sababu ya taifa la Kiafrika kama Tanzania? Hili sitalijibu. Jibu lake unaweza kulipata mwenyewe kwa kuangalia ima uhusiano baina ya masalia ya waarabu yaliyoko Tanzania au tabia za nchi za kiarabu dhidi ya waswahili. Hivi karibuni kumekuwa na taarifa nyingi za vifo vya waswahili huko Mashariki ya kati vya wafanyakazi wa ndani wa kiswahili tokana na ubaguzi na ubaguzi, ujinga na unyanyasaji wa waajiri wao ambao bado huamini kuwa mtu mweusi ni mtumwa au abid.  Mbali na hilo, rejea namna hawa wapalestina tunaowakingia kifua walivyotuuzia ndege mbovu wakati wa utawala wa Mwalimu Nyerere pamoja na kuwaamini na kuwatetea.
            Tatu, ili kujua kuwa kwa sasa kila nchi inaangalia maslahi yake, rejea kitendo cha nchi ya kiarabu kama Misri kusaini mkataba na Israeli maarufu kama Mkataba wa Camp David uliofanyika huko Camp David mnamo tarehe 17 Septemba, 1978 baina ya rais wa zamani wa Misri Anwar El Sadat na waziri mkuu wa zamani wa Israeli, Menachem Begin. Kumbuka. Wakati Misri ikiingia mkataba na Israeli, mataifa yote ya kiarabu yalikuwa yameapa kutohusiana na Israeli. Lakini baada ya Misri kuona hatua hii inaathiri uchumi wake, iliamua kuingia mkataba wa makubaliano na ushirikiano na Israeli. Kama waarabu ambao ndiyo ndugu wa wenzao wa Palestina waliona madhara ya uhafidhina wao, sisi ni nani? nadhani tulichelewa.
            Nne, ukiachia mbali Misri, hebu angalia Palestina yenyewe inavyoshirikiana na Marekani ikitegemea itatue mgogoro taifa ambalo ndiyo mhimili mkuu wa uwepo na ustawi wa Israeli tokana na kuipa fedha nyingi za misaada kuliko nchi yoyote ulimwenguni. Hapa hujaongolea kuiwezesha Israeli kijeshi na kijamii. Tanzania ni nani kuendelea na misimamo ya kikale?  Ni vizuri kufahamu kuwa mahusiano ya kimataifa ya sasa yamejikita sana kwenye uchumi kuliko siasa na mambo mengine kama ilivyokuwa hapo zamani. Siasa za kisasa zinataka hivyo.
            Tano, kwa wanaokumbuka namna Tanzania na nchi nyingine zilizokuwa mstari wa mbele kupigania ukombozi wa Afrika Kusini zilivyoathiri uchumi na maisha ya watu wao kuhakikisha makaburu wanang’olewa, ni mashahidi kuwa namna ambavyo Afrika Kusini sasa inawatenza watu wao ni somo tosha juu ya kuhatarisha uchumi na maisha ya nchi kwa ajili ya siasa za nchi nyingine.  Hakuna anayeunga mkono ukaburu unaofanywa na Israeli dhidi ya Palestina. Hata hivyo, pia hakuna ambaye yuko tayari kuhatarisha uchumi wa taifa lake kwa ajili ya taifa jingine. Hii maana yake ni kwamba, badala ya nchi moja moja kujitoa mhanga kuhakikisha Palestina inapata uhuru wake, nchi zote zinapaswa kuungana pamoja na kukabili mataifa ya magharibi ambayo kimsingi ndiyo mihimili mikuu ya ukaburu unaoendelea nchini Palestina. Kwa nchi maskini kama Tanzania, kuendelea kuitenga Israeli na kupoteza fursa za kiuchumi, ni kujitia kitanzi kwa ajili ya jambo ambalo halitafanikiwa kutokana na hatua kama hiyo. Siasa za mapenzi ya mshumaa zimepitwa na wakati kama tulivyoeleza tokana na kuanguka kwa ukuta wa Berlin.
            Tumalizie kwa kumtaka rais Magufuli kuhakikisha anafanya biashara na Israeli lakini siyo kugeuzwa mmojawapo wa watu wa kutumika kuhalalisha ugaidi na unyama inaowafanyia wapalestina. Aeleze wazi wazi msimamo wake kuwa lengo lake ni mahusiano ya kibiashara lakini si kujiingiza kwenye siasa za ndani katika mgogoro huu.
Chanzo: Tanzania Daima Jumapili leo.

Saturday 29 April 2017

Kaya ya madaktari wengi na madudu kibao

          Karibu katika kila uteuzi hukosi kusikia dokta so and so ameteuliwa na dingi kuula somewhere. Hapa siongelei akina Bashiteshite wala Makorongo Muhanga. Naongelea wateule wanaoitwa madaktari wa kweli. Sijagusia maprofesa kibao waliojaa kwenye ofisi za umma wakitafuna kaya.  Tena hawa ni madaktari wa kweli na siyo kama wale aliowahi kuwashukia mwanaharakati Msemakweli Keinerugaba aliyefikia kuwatungia kitabu cha Mafisi na Mafwisadi wa Elimu Danganyika huku wengine wakifungua kesi na kubwagwa kiasi cha kushindwa kulipa hata gharama. Tukirejea kwa madaktari orijino, je huu ubobezi wao umeisaidiaje kaya hasa walevi kule madongo poromoka kama sisi tuishio kwa Mfuga Dog  na kumalizia maisha yetu kwenye kanywaji pale Uwanja wa Hyena?
            Kwanini nahoji usomi wa wateuzi na wateule wetu? Siachi kushangaa namna wanavyoshindwa kuutumia udaktari wao kujua kuwa matumizi yao ya hovyo yanafanya kaya yetu iwe kapuku na apechealolo. Kwani, bado wanatumia mashangingi ya bei mbaya wakati kaya yao ni ombaomba na kapuku wa kunuka. Je hili nalo linahitaji udaktari kulideku au ni ujinga tu wa kawaida utokanao na elimu? Leo nitauliza maswali bila kutoa majibu ili wao wanijibu kwa ufasaha kama wanaweza.
            Pili, kama haitoshi, bado  wanaolialia kuzuiwa kwenda kuzurura ughaibuni. Hamkuona wengi walivyonuna waliposikia kuwa Bashite na bi Nkubwa wake walikwenda kutanua majuu huku wao wakipigwa stop? Ajabu ya maajabu, tokana na sijui ujinga sijui uchizi juzi niliona wengi wakimshangilia Vasco da Gama kiasi cha wengine kusema bila aibu kuwa wanammiss! Si mlikuwa mkimalalamikia alipotumia ngwe yake yote akizurura. Leo kaja banabana mnakumbuka blanketi kumeishakucha. Ngoja nitakwenda kumpa orodha ya wote walioshangilia upuuzi ili awashughulikie kama alivyomfanyie Nipe Mapepe pale alipotaka kumgusa mwanae kipenzi aliyependezwanaye.
            Kaya inapojaa madaktari wengi wa politiki ni matatizo matupu. Juzi nilimsikia mduwanzi mmoja mpingaji akisema eti nabii Joshwa amemtabiria ushindi kwenye uchakachuaji ujao. Hivi kweli mlevi mwenye akili timamu anawaweza kumwamini tapeli huyu wa Kinigerieni kweli wakati alishawaliza wengi mmojawapo akiwamo dada yangu Joisi Banda? Ama kweli mtumu Paulo aliona mbali alipowauliza Wagalatia nani alikuwa amewaroga. Acha nami ntume Mlevi niwaulize wabongolalalanders, nani nyie aliyewaroga kiasi cha kuanza kuvamiwa na matapeli wanaokimbia njaa na kesi kwao eti kuja kuwalisha neno? Nani nyinyi aliyewaroga mnaoabudia kusaliwa kana kwamba mu maiti?
            Pamoja na kuwa na PhD kama kumi kubwa zikiwa za ulevi na uchomaji majani huwa siachi kushangaa mantwiki ya kuwa na wasomi karibu kila idara lakini bado kaya ikaishia kuombaomba tokana na kukosa vipaumbele. Hebu niulize tena kilevi. Ilikuwaje kaya nzima yenye wasomi kila ngeli kuruhusu mfano nchanga uliojaa madini kusafirishwa ughaibuni kwa miaka 20 bila kustuka? Ilikuwaje kaya yenye kujaa wasomi, kama ni wasomi kweli, iliingia mikataba ya kipumbavu kama Richmonduli aka Symbiosis ambayo hivi karibuni ilishinda kesi ya kufilisi kaya, IPtL, Kagoda, UDa na mingine mingi ambayo imegeuka kile watasha huita albatross around neck? Sitatafsiri ili wasomi ninaowalenga watafsiri.
            Ukiachia hayo niliyotongoa hapo juu, inakuwaje kaya yenye wingi wa wasomi inajaa woga kiasi cha watu wawili kuiteka huku wasomi wetu wakiendelea kuchelekea jinai hii kana kwamba hawakusoma vitabu vya magwiji kama Karl Marx, Nelson Mandela, Fredrick Engels, Socrates, Plato, Nkwazi Nkuzi Mhango Willa Ngwenyama aka Sibusiso Sibulele na wengine wengi? Naona yule anatikisa kichwa kana kwamba huyu mwanafalasa wa mwisho si gwiji. Nenda kasome tabu lake la Africa Reunite or Perish au lile la Africa’s Best and Worst Presidents; How Imperialism Maintained Venal Rules in Africa. Kama haitoshi kasome Born with Voice, Souls On Sale au Psalms of the Oppressed. Kama huupati umombo basi kasome Nyuma ya Pazia au Saa ya Ukombozi huku ukingojea Perpetual Search ambayo iko jikoni kabla ya Is it Global War on Terror or Global War over Terra Africana? How Global War is Used to Occupy Africa Militarily.  Pamoja na ulevi wangu, huwa naongea kwa ushahidi ili nisijeitwa au kudhaniwa kihiyo au msomi wa hovyo asiyezalisha chochote. Mimi sikwenda shule kujifunza woga na ujinga.
            Kwa vile nahisi kiu, ngoja nimalizie hapa kwa kuwaasa wasomi wa kweli waje tupige kanywaji pamoja niwatoe woga. Guys, Guess what. Fear nothing except fear itself. Tuonane wiki ijayo nikirejea toka Koromije kukoroma. Message sent and delivered.
Chanzo: Nipashe Jumamosi leo.

Wednesday 26 April 2017

Barua ya wazi kwa rais Magufuli


       Mhesimiwa rais John Pombe Joseph Magufuli,
            Naandika waraka huu wa wazi kwako kwa kusukumwa na uzalendo na usongo kwa nchi yangu. Hivyo, sitapindisha wala kuzua jambo zaidi ya kusema ukweli. Nimekusikia siku zote ukisema; Msemakweli ni mpenzi wa Mungu. Pia naandika kutokana na kujitenga na woga na unafiki wa kusema; kila kitu kiko sawa wakati si kweli. Hivyo, nitadurusu yafuatayo.
            Kwanza, nakupongeza; kumteua mpinzani japo mmoja kwenye serikali yako ingawa haitoshi.
            Pili, nakupongeza kwa dhati kwa kuwa na uthubutu wa kubadili mfumo mchafu na wa kijinai ingawa bado kuna mengi yanalalamikiwa kama vile kuchelea kufukua makaburi na kushindwa kuyafukia.
            Tatu, baada ya kukupongeza, nitoe machache yanayokufanya ulaumiwe kwa sababu za msingi kabisa.
            Mosi, ni ile hali ya kutoa amri kwa serikali kufanya biashara na vyombo vya habari vya serikali huku vya binafsi vikiachwa vife kifo cha taratibu. Hii si sawa.  Madhara yake ni kama ifuatavyo:
            a) kuvinyima vyombo vya habari binafsi matangazo ni kuviua hasa ikizingatiwa, vyombo vingi vya habari huendeshwa kwa fedha ya matangazo zaidi ya habari.
            b) ni kuwanyima riziki waandishi, wachangiaji na wafanyakazi wengine wa vyombo husika. Mfano, tangu utoe amri yako, vyombo vingi vya habari vinasuasua kiasi cha kuwakopa ima wafanyakazi wake ukiachia mbali wachangiaji. Je madhara ya hii ni nini? Licha ya kufanya wahusika waishi maisha magumu, itawashawishi kama si kuwalazimisha kuomba rushwa mbali na kuwa na chuki na utawala wako.
            c) huu ni ubaguzi. Sina namna ya kuueleza. Vyombo vya habari vipo kisheria na si matakwa ya mtu au taasisi yoyote zaidi ya dola; na pia ni mojawapo ya shuruti ya utawala bora na wa sheria.
            Tatu, nitagusia chanzo cha sintofahamu hii baina yako na vyombo binafsi vya habari. Japo zipo sababu nyingi, kubwa inaweza kuwa kuibua baadhi ya mambo ambayo hayakukufurahisha. Mfano mzuri, ni ile hali ya kuvamiwa kituo cha runinga cha Clouds kinachodaiwa kunakodaiwa kufanywa na mkuu wa mkoa wa Dar Es Salaam, Paul Makonda.  Sijui vyombo vya habari vinajisikiaje vinapoona mwenzao ametendewa jinai na mhusika kuendelea kukingiwa kifua?  Hapa hatujaongelea wabunge wanaotekwa na kufunguliwa kesi za kubambikwa. Rejea walivyoonyesha chuki kwa kumshangilia mtangulizi wako; haijawahi kutokea. Japo wasaidizi na washauri wako wanaoogopa kukupa ukweli, kimsingi, kashfa hii ni yako. Kwani anayeshutumiwa ni mteule na mwakilishi wako. Hivi huyu bwana ana nini kiasi cha kufanya hata waheshimiwa wabunge wahoji na kulalamika na wasisikilizwe? Je hii inajenga picha na uhusiano wa aina gani baina ya serikali yako na mhimili huu wa dola?
Kadhia hii imekuchafua kama rais. Kwani, vyombo vya habari viliamua kugomea kuandika habari za mteule wako huyu mwenye ushawishi mkubwa kwako. Nijuacho, mkuu wa mkoa ni mwakilishi wa rais. Anapogomewa, anagomewa rais. Je nini kifanyike? Ondoa katazo kwa taasisi za umma kutotoa matangazo kwa vyombo vinafsi. Kwani, malipo ya matangazo hayo hutokana na kodi za wananchi bila kujali itikadi.
            Kumbuka, Tanzania imejengwa kwenye misingi ya haki na usawa. Hivyo, anapobaguliwa mtu au taasisi kwa itikadi au mawazo yake ni uvunjaji mkubwa wa katiba. Nimekusikia mara nyingi ukisema; wewe si mnafiki na unachukia unafiki. Zaidi umekuwa ukisema wewe ni wa wote bila kujali dini, itikadi wala rangi. Sijui kama kubagua vyombo binafsi ndiyo huku kuwafanya na kuwaonyesha kuwa wote ni wako? Vipi?
            Wana tasnia ya habari wanaishi kwa mateso makubwa baada ya wewe kuondoa haki ya kupata matangazo toka kwenye asasi za umma. Ikumbukwe. Tanzania ni mali ya watanzania kwa sawa. Haiwezi kuendeshwa kwa matakwa ya mtu mmoja au kundi moja hata liwe na madaraka kiasi gani. Hivi ikitokea vyombo vya habari binafsi vikafunga shughuli zake hata kwa mwezi mmoja, serikali, licha ya kujenga picha mbaya, itawasiliana na watanzania vipi?
            Nimalizie kwa kugusia madhara yatokanayo na niliyosema hapo juu kama ifuatavyo:
            Mosi, inajengeka chuki dhidi yako na serikali bila sababu za msingi. Hili si jema. Si matarajio ya watanzania.
            Pili, ikishajengeka chuki, ushirikiano baina ya raia na serikali unatoweka kiasi cha kuweza kuhujumu juhudi zako mahsusi na adhimu.
            Tatu, hasira zitokanazo na chuki hii zinaweza kuipasua nchi na kuingia vurugu. Hata Rwanda ambako hupenda kutolea mfano, walianza hivi tokana na baadhi ya watu kuwa juu ya sheria kinyume cha sheria.
            Nne, inapotokea kutoaminiana au kuchukiana, uwezekano wa kulipiza visasi unakuwa mkubwa hasa kwa mipango na miradi ya umma. Sitaki hili litokee.
            Je nini kifanyike kuondokana na kadhia hii?
            Napendekeza kufuata katiba ya nchi na si ilani ya chama tawala tu. Hapa lazima tukubali kushindwa na kujadiliana. Mfano, watuhumiwa wa uchafu mbali mbali washughulikiwe bila kujali ukaribu wao kwako.
            Pili, dhana ya usawa itekelezwe kwa vitendo na si maneno. 
            Tatu, utende sawa na maneno yako. Mfano, dhana za usemakweli, kuchukia unafiki na kuwajali watanzania bila kujali dini, itikadi za kisiasa, rangi au watokako zitekelezwe kwa vitendo badala ya kuwa maneno matamu ya majukwaani.
            Japo yapo mengi, nakushauri  mheshimiwa rais upate nakala ya kitabu changu cha Africa’s Best and Worst Presidents: How Neocolonialism and Imperialism Maintained Venal Rules in Africa ambapo nimekuweka kwenye kundi la viongozi bora kama hutabadilika tokana na spidi na staili uliyoanza nayo kabla ya kujitokeza niliyosema hapo juu.
            Kwa heshima na taadhima, ndugu rais, acha niishie hapa.
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.

UDSM: Makufuli fungia makufuru ya kughushi kayani

        Juzi rahis Joni Kanywaji alisema kuwa yeye ni mgumu wa kushukuru. Aliyasema hayo wakati akifungua mabweni mapya ya chuo kikuu cha Manzese. Hata nami Mpayukaji ni jiwe inapokuja kushukuru. Tokana na mfano alioonyesha hivi karibuni wa kuamuru ujenzi wa mabweni ya chuo cha Manzese ufanywe na makandarasi wa ndani tena kwa njuluku kiduchu, amenikuna kwelikweli.
            Kama nilivyosema, mimi ni mwepesi wa kulaumu. Hamkuona nilivyokuwa nikimsakama kuhusiana na kashfa ya Bashit? Hamkuona nilivyokuwa nikimpa vipande pale alipotaka kuminya vyombo vya umbea na vyama vya upingaji? Uzuri naye ananifahamu. Huwa anapokea ushauri wangu na wa kijiwe kwa ujumla na kuufanyia kazi bila kusita kama ambavyo atapokea huu wa leo na kuufanzia kazi.
            Rasmi na toka moyoni, nampongeza mheshimiwa rahis kwa kuona mbali. Pamoja na kumshukuru na kumpongeza, namshauri awatumbue waliojenga mabweni ya Mabibo. Kwa maneno yake mwenyewe alisema kuwa yale mabweni yalijengwa kwenye miaka ya 2000 kwa gharama ya madafu bilioni 27. Sasa iweje miaka takriban 20 baadaye, mabweni kama hayo hayo yajengwe kwa moja ya tatu ya thamani ya miaka 20 iliyopita kama hakuna majipu ya kutumbua? Nashauri uchunguzi ufanywe na wote walioshiriki jinai hii nyingine watumbuliwe kwa kutaifishiwa mali walizopata tokana na jinai hii. Kama atashindwa aombe Kijiwe kimpe tafu kuwanasa na kuwafanyia kitu mbaya.
            Juzi baada ya rahis kusema hayo, wana Kijiwe walipigwa na butwaa kiasi cha kutamani waandamane kumtaka rahis aanzie pale pale chuo cha Manzese kutumbua angalau kwa kutaja majina ya waliotoa tenda na waliopewa tenda ili wachovu wawajue lau wawazomee. Nilimsikia mchovu mwingine akisema kuwa huenda hii Standard Gauge Railway ingejengwa zama za utawala wa kijambazi, huenda gharama zake zingekuwa mara kumi kuliko ilivyo sasa.
            Hebu tujiulize. Hivi tangu tunyake uhuru tushapoteza matrilioni mangapi ya madafu? Kama mabweni yalipaishwa bei hivyo, ilikuwaje kwenye ununuzi wa magari ya umma? Ajabu hawa hawa ndiyo walioruhusu wawekezaji ambao wamegeuka wachukuaji kuendelea kuiba madini yetu kwa miaka 20 bila kulipa hata ndururu! Kwanini wasikamatwe wakanyongwa ili uwe mfano na somo kwa wengine?  Kabla ya kusahau, nimuombe rahis ateue Makamu mkuu wa chuo mpya badala ya kurefushia mikataba waliostaafu muda wakati tunao vipanga wengi wanaoweza kuongoza chuo cha Manzese. Tokana na utamu wa maneno ya Dk Kanywaji, natamani kurejea chuo kikuu cha Manzese lau nisomee shahada yoyote hata kama ni ya kupiga ngoma au michezo.
            Tokana na gharama za kuishi kwenye mabweni ya Mabibo, kwanini yasiuzwe na kupanua ujenzi wa mabweni mengine karibu na chuo ili kuondoa usumbufu kwa wanachuo? Japo nakumbuka kichovu, wakati sisi tukipiga book zama zile, kila kitu kilikuwa swaafi kiasi cha kuotesha hata viriba tumbo. Wakati ule elimu ilikuwa mali siyo kama sasa inapoghushiwa ukiachia mbali wengi wachovu kupenda kuuza bwimbwi na kuukata haraka. Pia nichukue fursa hii kumpongeza rahis kwa ahadi aliyotoa wakati akifungua hayo mabweni ya kuwatumbua wenye vyeti feki bila kujali umbali wala ukaribu naye. Nadhani wengi tutapigwa na mshangao atakapoamua kufanya kweli na siku si nyingi.
            Kwa sasa miji yetu mingi ina ukosefu wa majumba ya wafanyakazi wa umma, je kama tutaamua kutumia Taifa Building Agency (TBA) badala ya mashirika kama National Social Insecurity Fund (NSIF) ambayo yameonyesha kufanya madudu kule Kigamboni, tungeweza kujenga majumba mangapi kwa ajili ya wafanyakazi wa lisirikali? Pia nimkumbushe Dk Kanywaji zile nyumba za wachovu zilizopunyuliwa na wanene zama za Ufichi na Uongo wa mzee Dugong. Je bado haoni kuwa hili nalo ni jibu au ni kaburi analoogopa kufukua asishindwe kulifukia? Kwanini hata ujenzi wa majumba ya kuuza ya umma yasifanywe na TBA hawa hawa ambao wameonyesha mfano wa kuigwa? Niwapongeze TBA kwa kuonyesha mfano kuwa hata makampuni yetu ya ndani yana uwezo na sifa za kufanya mambo tuliyozoea kuyapa makampuni ya kigeni baada ya kuahidi ten au twenty even thirty percent. Natamani hata siku moja Standard Gauge Railway nyingine ijengwe na makampuni ya nchini.
            Hakuna rahis Makufuli aliponiacha hoi kama aliposema ametia makufuli kwenye makufuru ya walaji wa kaya yetu. Nataka wote waliozoea kutuibia awatie makufuru kwa kuwatumbua na kuwataifishia mimali waliyojilimbikizia baada ya kutuibia. Kabla ya kusahau, akina Mgoshi Machungi, Kapende, Mipawa, Sofia Lion aka Kanungaembe, Mipawa, Mijinga, Mheshimiwa Bwege Mbwamwitu, Msomi Mkatatamaa na Kanji wamenituma kumpa kavukavu Dk Kaywaji kuwa utumbuaji hautakamilika wala kuleta maana bila kuwatumbua Bashit  na swahiba yake mchunaji Jose Gwajimmy vinginevyo awatangaze kuwa makaburi ambayo anaogopa kuyafukua kwa kuhofiak ushindwa kuyafukia. Hata hivyo, wana Kijiwe wako tayari kumpa tafu kwa kuyafukulia na kuyafukilia mbali makaburi yote kayani bila kujali ukubwa wala uozo wake. Otherwise, Congrats Dr Mugful.
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.

Sunday 23 April 2017

Barua kwa Ben Saanane

Image result for photos of ben saanane

Mpendwa Ben,
            Nakuandikia popote uliopo; uwe hai au marehemu, najua utasikia. Usiposikia wapendwa wako watasikia ukiachia mbali wanaochukia kile ulichofanyiwa. Sasa ni zaidi ya miezi mitatu tangu umepotea kimiujiza kwenye nchi yenye kila vyombo vya ulinzi vilivyoshindwa kukulinda wewe achia mbali kukutafuta kama siyo kukuhifadhi. Nikinukuu maneno ya Mbunge Zitto Kabwe kuwa ulitekwa na usalama wa taifa bila wao kukanusha, hali inatisha. Kwani tangu utekwe, wengine wametekwa. Hata hivyo, tofauti na wewe, wao walikuwa na bahati. Kwani waliteswa kidogo na kuachiwa. Kama huwajui, acha nikutajie. Waliotekwa ni Emanuel Elibariki aka Ney wa Mitego kwa kosa la kutunga wimbo wa "Wapo" ambao ulikuwa ukilaani jinai ya kughushi vyeti huku walioaminiwa na kutarajiwa kumtumbua wakimkingia kifua. Kama haitoshi, punde si punde mwingine aliyetekwa na utekaji huu kuendelea kuwa kizungumkuti ni Ibrahim Musa aka Roma Mkatoliki ambaye naye alitemwa na watekaji hawa baada ya umma kuja juu.
            Ukiachia watu waliotekwa, yametekwa hata maofisi. Kituo cha televisheni cha Clouds kilitekwa na mtu anayeitwa Bashite akiwa ameandamana na mapolisi. Ajabu ya maajabu, huyu mhuni na mhalifu aliyetenda jinai hii–huwezi kuamini–bado yuko kwenye ofisi ya umma akitanua tokana na kukingiwa kifua na mzito mmoja. Hii itakufanya uelewe ni kwanini suala lako halishughulikiwi. Ni kwa sababu sheria yetu siku hizi inafanya kazi kwa madaraja kulingana na nani yuko karibu au mbali na wakubwa. Kama alivyowahi kusema Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, ni kwamba wakati baba yako akisema Ben si mbuzi  wala ng'ombe wake bali mwanae aliyepotezwa, wenye madaraka hawakuangalii hivyo.
            Bwana mdogo Ben, hebu fikiria. Hivi kweli unaweza kutendewa haki wakati hata wakubwa waliojaribu kumchunguza, kwa mfano, mkubwa aliyetaka kufichua huu utekaji wa Clouds, aliishia kutimliwa ghafla bin vu kama mhalifu ili kumlinda mhalifu anayejulikana wazi wazi. Hata ndege wanamjua mhalifu huyu hata kama yuko juu.
            Bwana mdogo Ben, huko uliko, kama u mzima au mfu, nakuomba ujue kabisa kuwa kinachoendelea kuhusiana na utekaji nyara wa watu wasio na hatia unaanza kuzoeleka tokana na wanaopaswa kuushughulikia ima kuwa woga au kujidanganya kuwa hakuna mwisho wa uzandiki huu na unyama dhidi ya binadamu. Sijui kama Ben ungekuwa mtoto wa hao wanaowalinda wahalifu wanaoteka watu kutetea uchafu wao wangeweza kujiamini na kuendelea kutenda jinai na upuuzi kama huu. Sijui kama una uraia wa taifa lolote. Kama unajidanganya kuwa unao, jiulize. Kwanini nchi yako haikukutetea? Kwanini nchi yako imeshindwa kutoa maelezo. Kama hujui basi jua. Juzi aliuawa faru mmoja aitwaye John. Dogo, huwezi kuamini. Waziri wa wanyama na hata waziri mkuu hawakukaa ofisini. Ziliundwa kamati na mabilioni ya shilingi kutumika kujua nani au nini kilimuua hayawani huyu. Ajabu ya maajabu, hakuna anayetumia hata senti moja kutaka kujua nani walikuteka, kukuficha, kukuua na vyovyote ilivyo. Mpaka sasa, si wazazi wako, taifa wala yeyote anayejua hali yako zaidi ya waliokuteka na kukuonea tokana na itikadi na msimamo wako.
            Mpendwa Ben,
            Wazazi na wapenzi wako hawalali. Wana hasira na uchungu japo hawana namna tokana na kuogopa. Mimi ninayeandika siogopi kitu. Wapo wanaodhani naandika haya kutokana na kuishi mbali na watekaji. Wanakosea. Hata ningekuwa nchini ningeyaandika haya kutokana na imani yangu kuwa kufa si chaguo bali faradhi. Hivyo, ninapoandika haya, ujue fika ima ni mimi peke yangu niliyeona umuhimu wako au wachache. Najaribu kujiuliza. Ningekuwa wewe au baba na mama yako ningetaka nitendewe au utendewe vipi. Nimevumilia kuona maigizo na kujifanya hamnazo kuhusiana na kupotea kwako. Sasa nimefikia kikomo. Ndiyo maana nimeamua kukuandikia usome au usisome angalau moyo wangu utaridhika kuwa nimetenda haki ambayo nilipenda na nilipaswa kutendewa kama binadamu au kiumbe.
            Ben mpendwa,
            Ninapoandika, naamini haki itatendeka iwe kwa kutaka au kwa kulazimika, uwe hai au uwe marehemu, naamini kuwa ipo siku haki itatendeka. Kwani naamini hakuna lenye mwanzo lisilo na mwisho. Tuliwaona akina Idi Amin, Jean-Bedel Bokassa, Charles Taylor, Saddam Hussein na mahabithi wengine wengi. Je waliishia wapi? Binadamu ni nini hadi ajione wa maana wakati ni udongo tena wa daraja la chini? Binadamu ni nini zaidi ya mavumbi? Wako wapi watu watukufu kama akina Nelson Mandela, Julius Nyerere na wengine waliosifika kwa utauwa na usafi wao? Wamezikwa; na wameoza. Nani huyu atokaye kwenye tumbo na uchi wa mwanamke atakayeyashinda mauti? Nani mpumbavu huyu asiyepoteza muda kupinga na ukweli na kanuni za maumbile? Hata hayawani wasio na akili wanalijua na kulikubali hili.
            Ben Mpendwa,
            Hata kama binafsi sikujui, niruhusu nikuomboleze kwa kukuahidi kuwa haki kwa ajili yako itatendeka siku moja hata kama ni kwa kuchelewa. Damu ya binadamu si maji yamwagwe bila sababu. Uwe unanisikia au la, nasema iko siku milima na mabonde vitaongea kueleza nini kilikupata baada ya vyombo husika kushindwa kutupa jibu la nini kilikupata.
Chanzo: Tanzania Daima Jumapili leo.

Wednesday 19 April 2017

Punguezeni mikoa na wilaya vilivyoanzishwa kisiasa

       Image result for the map of tanzania
  Hivi karibuni Mbunge wa Nkasi Kaskazini Ally Kessy akichangia kwenye kikao cha bunge la 11 huko Dodoma alitaka rais John Magufuli aangalie uwezekano wa kupunguza utitiri wa wilaya ili kuleta mendeleo katika maeneo mengi ya taifa letu ambayo yako nyuma kimaendeleo. Pia kesi alikwenda mbali kudai kuwa kuna mikoa inayopendelewa kwa kupewa majimbo na fedha nyingine kulinganisha na mengine. Tokana na siasa za majitaka, tanzania kwa sasa inaweza kusemekana kuwa na mikoa na hata wilaya nyingi visivyolingana na uwezo wake kiuchumi. Yote hii ilitokana na baadhi ya viongozi waliopita kuangalia masuala ya kisiasa katika uanzishaji au upanuzi wa mikoa na wilaya. Mfano mdogo, Benjamin Mkapa alianzisha Mkoa mpya wa Manyara ambako anatoka waziri wake mkuu Fredrick Sumaye kwa tangazo la Serikali Na. 367 lililotolewa tarehe 27 Julai, 2002.
            Kikwete ndiye alivunja rekodi kwa kuunda mikoa mingi. Kwani hapo Machi 2, 2012, alianzisha mikoa ya Geita anakotoka rais Magufuli, Katavi anakotoka waziri mkuu mstaafu Mizengo Pinda, Njombe na Simiyu na wilaya Buhigwe, Busega,Butiama, Chemba, Gairo, Ikungi, Itilima, Kakonko, Kalambo na Kaliua. Nyingine ni Kyerwa, Mbogwe, Mkalama, Mlele, Momba, Nyang’hwale, Nyasa, Uvinza na Igwachanya.
            Kama alivyodai mbunge Kessy, ukiangalia ukubwa wa baadhi ya mikoa hata wilaya unashangaa ugawanywaji wake. Nini mantiki ya Mwanza na Shinyanga yenye jumla ya ukubwa wa kilometa za mraba70,876 kugawanywa kuunda mkoa wa tatu wa Geita wakati ukubwa wake ni chini ya ukubwa wa mkoa mfano, mkoa wa Tabora wenye ukubwa wa kilometa za mraba 76,15 au Rukwa wenye ukubwa wa kilometa za mraba75,240 kama si Morogoro wenye ukubwa wa kilometa za mraba72, 939? Kwanini Mkoa wa Geita wenye ukubwa wa kilometa za mraba 21,729 usiunganishwe na Kagera wenye ukubwa wa kilometa za mraba 40,838 Jiulize na kuunda mkoa mdogo kuliko Tabora?  Mkapa alifuata kigezo gani kama siyo kumzawadia rafiki yake na waziri mkuu wake mkoa iwapo mkoa wa kabla ya kugawanywa katika mikoa miwili ulikuwa na ukubwa wa kilometa za mraba
            Kwa mtu anayejua gharama za uendeshaji mkoa na wilaya, asingekubaliana na ushauri wowote wa kuanzisha mikoa minne ndani ya utawala mmoja ukiachia mbali wilaya nyingi. Hata hivyo, kwa wanaojua utawala wa Kikwete ulivyokuwa wa kisanii hawashangai hili kufanyika kiasi cha kuacha wenye kujua mambo wakishangaa.
            Kwa vile, tuna serikali inayotaka kubadili mambo, tungeshauri iangalie umuhimu au ulazima wa utitiri huu wa mikoa. Je wingi wa mikoa na wilaya hizi umeongeza ubora wa maisha ya wananchi au kuwaongezea mzigo wa kulisha wakubwa wachache wanaoteuliwa na rais kuwa wakuu wa mikoa na wilaya?
            Ni bahati mbaya kuwa wahusika walipoanzisha mikoa mipya, walifanya maamuzi ya kiuchumi bila kuzingatia uhalisia wa kiuchumi. Hata bila kuwa mchumi, akili ya kawaida haikubali kuanzishwa kwa mikoa minne kwa mpigo kwa nchi ambayo bado bajeti yake inategemea wafadhili ukiachia mbali kutotekelezwa hata kwa asilimia 50. Hadi sasa ni vigumu kujua mantiki, ujuzi, utaalamu, hata sababu vilivyotumika kuanzisha mikoa na wilaya hivi ndani ya utawala mmoja.
            Pesa zinazopoteza kuwalisha wateule hawa wachache zingeweza kuleta nafuu hata maendeleo kiasi gani kwa sehemu zilizomo hizi wilaya mpya kama zingetumia kwenye mambo ya msingi kama vile miundombinu, huduma za kijamii na maendeleo? Unashangaa utitiri wa wilaya ambazo tena ni majimbo ya uchaguzi. Kwanini zisibaki kuwa majimbo na wabunge wakazihudumia badala ya kujaza utitiri wa wakuu wa wilaya ambao umuhimu wao unazidi kupotea kadri miaka inavyopita?
            Kama tunataka kutenda haki basi mikoa inayopaswa kugawanywa tena si kwa kuungaunga ni kama vile Tabora, Rukwa, Morogoro na Lindi. Hakuna kinachokera kama kugundua kuwa mikoa hii mikubwa si kwa ardhi tu bali hata uzalishaji. Hebu fikiri mkoa kama Lindi na utajiri wake wa gesi asilia, korosho na mambo mengine unaachwa vinagawanywa vipande vya mikoa. Tunajenga picha gani hapa kisiasa? Je hili nalo linangoja upinzani uchukue dola ulirekebishe?
            Hata ukija kwenye ugawaji wa wilaya unashangaa kuona wilaya kama Siha kwenye mkoa ambao ni sawa na baadhi za wilaya za mikoa mikubwa tajwa. Kuna haja ya wabunge na wataalamu wanaotoka kwenye mikoa inayopunjwa kufanya upembuzi na kuja na mapendekezo kwa serikali ili kuhakikisha ima upanuaji wa wilaya na mikoa unafuata ukubwa wa eneo vinginevyo hii mikoa na wilaya vilivyoundwa kisiasa vibatilishwe na fedha ambazo zinapotea kule ziende kuwahudumia wananchi badala ya kikundi kidogo cha wamangi meza.
            Hata kama tutatumia kigezo cha idadi ya wakazi, bado  kuna ushahidi wa kisayansi kuwa mikoa mikubwa tajwa hapo juu ukiondoa mkoa wa Lindi ni miongoni na inayoongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wakazi.
            Tumalizie kwa kushauri serikali ya awamu ya tano iangalie mapungufu haya kwenye kuunda mikoa mipya. Pia iangalie namna ya kuivunja au kuipunguza mikoa mipya. Sipendekezi upanuaji mwingine. Vinginevyo tutaendelea kumtwisha mzigo mlipa kodi maskini ambaye mzigo alio nao unakaribia kumtoa roho.
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.

Kijiwe Chamtaka Makonda Aonyeshe Vyeti

Image result for katuni za bashite
       Baada ya kugundua kuwa kaya ina mkwamo utakanao na sekeseke la Daudi Bashite aka Makonda, kimeamua kuokoa jahazi kwa kuhakikisha kila mmoja anatendewa haki bila ubaguzi wala upendeleo. Hii inshu imeletwa na Msomi Mkatatamaa tokana na ubobezi wake kwenye mambo ya Utatuzi wa Migogoro kimataifa yaani International Conflict Resolution.
            Msomi akiwa leo amekula suti ya bei mbaya na tai nyekundu kama ya dokta Kanywaji anatia timu na kufunguka “wazee, nionavyo mimi ni kwamba kaya imekwama kama siyo kukwamishwa. Maana, nikiangalia kulia na kushoto naona mkwamo ukiachia mbali sanaa za akina Bashit kutaka wanusurike na kashfa zao lukuki wasijue hawa wanaowahadaa wataishiwa ganzi yao na kuwatumbua. Hamkumsikia dingi akisema anao vihiyo 9,000 sirikalini anaongoja kuwatumbua? Hakuna kilichonisikitisha kama vita dhidi ya mihadarati kuzikwa kwa haki huku uwajibikaji na usawa vikipaa bila kusahau vita dhidi ya miharati kugeuka kuwa adimu kama vyeti vya Bashite.”
            Kabla ya kuendelea Kanji anamchomekea “sasa kama veve naona kaya iko kwama sasa nini napendekeza vatu ifanye ondokana na kwamo hii au nataka ilielie kama Basite kwa kanisani? Mimi toa sauri moja kuba. Kama Konda iko na weti si itoe mambo yote nakwisha na nakata zizi ya fitna. Kama baba yake napenda kaya sauri yeye toa weti ili mambo ikiwise.”
            Msomi anajibu “kama usingedakia, ungejua ninachomaanisha. Nakuja huko Kanji wala huna haja ya kuhofia. Ninachomaanisha na kupanga ni kwamba sisi kama kijiwe chenye hekima kuliko wote duniani siyo kuishia kulalamika bali twende kwa Bashite na kumwomba jambo moja dogo tu, kuonyesha vyeti vyake ili mambo yaishe na maisha yaendelee au vipi? Akiendelea kuzungusha kama ambavyo amekuwa akifanya basi twende kwa baba yake tumpe ishu nzima lau ajue tunavyoichukulia bila kujali ukaribu wala sanaa za Konda. Tena tusishikwe na kigugumizi kama hawa wanaomkingia kifua wakati wakijua kuwa lisemwalo lipo; na kama halipo laja. Kwanini tugombanie kitu kidogo kama vyeti? Kama anavyo si atoe na kuonyesha; na kama hana si aseme tu; kwani yeye wa kwanza?”
            Mgoshi Machungi anakula mic “hapa Msomi umemigusa pabaya. Ukimwambia kitu kama hiki atakupiga mingumi kama siyo mingwaa. Jamaa hataki kusikia juu ya kutoa vyeti.  Amesindwa hata kutoa cheti cha kuzaiwa. Maana, wapo wanaosema kuwa huyu jamaa anaweza kuwa muundi. Vinginevyo isingekuwa noma waa soo kama angekubai kuonyesha vyeti ii mambo yawe shwai.”
            “Yakhe nkubaliana nawe. Kwanini kusimamisha maisha ya kaya kwa vitu vya kidohodoho kama vyeti? Kama anavyo au hana si aseme lau tujue ukweli ili tuzodolewe au tuwazodoe wale wanonkingia kifua?” anachomekea Mpemba.
            “Kwa ninavyomjua jamaa, kama angekuwa na vyeti jenuine angekuwa ameishamwaga. Hakuna kinachonishangaza kama daktari wa kutibu majipu naye kushikwa na kigugumizi utadhani lao moja. Kwa namna jamaa alivyokuwa na kasi na usongo wa kutumbua majipu, sikutegemea hili wallahi,” anachomekea Mijjinga huku akibwia kahawa yake.
            Sofia Lion aka Kanungaemba anakatua mic “hata mimi nashangaa. Nakumbuka hata baba yake kipenzi aliwahi kusema si lazima wachovu wasingizie wana masters au PhD. Alisema kama wana vyeti vya darasa la saba waseme tu kwa vile si lazima kila mchovu awe na shahada hizo kubwakubwa. Sijui  nini kimemkumba akajipiga mtama kwenye sakata hili au ni yale ya mwenye mapenzi  haoni?”
            Mheshimiwa Bwege anaamua kutia guu “jamani, tumelalamika sana. Sasa inatosha. Nadhani, kama warume, tunapaswa kuionyesha dunia hii kaya ni ya nani kati ya sisi na akina Bashite. Maana naona tunapoteza muda kwenye mambo ya hovyo huku mambo ya maana yakizidi kuharibika. Acheni ubwege pande zote. Hapa lazima, kama alivyosema rahis, lazima tuweke uzalendo mbele badala ya ubashite, ukondakonda na ugufuligufuli. Lazima kaya kwanza. Mengine baadaye. Hapa lazima tuepuka kuhubiri maji na kunywa mvinyo. Tuache unafiki na ubwege. Badala yake tuite koleo koleo bila kujali hadhi ya mchovu awe mzito au mwepesi. Enough is enough. Bashite must pack and hit the road vinginevyo tuchenchiane. Au vipi? Naungana na wale wanaotaka  twende kwa Bashite na kumtaka aondoke kwenye ofisi yetu. Akigoma twende kwa baba yake lau wajue kaya hii si mali binafsi bali mali ya wachovu au vipi?”
            Mipawa anakula mic “mheshimiwa Bwege nakuunga mkono  na mguu. Huu upuuzi na urushi vinavyoendelea ingekuwa majuu mambo kwisha zamani gani! Hapa ndipo tunapojivua nguo kama kaya. Inakuwa vigumu kushuhudia hata wale ambao hukuwatarajia wakijivua nguo kiasi cha kusaliti viapo vyao. Nadhani dingi aliapa peke yake na si pamoja na Bashite. Sijui kwanini anamg’ang’gania kiasi cha kutelekeza viapo vyake na kaya.”
            Wakati kijiwe kinaanza kunoga si likapita shumbwengu la Bashit. Wacha tulitoe mkuku kujua lau nani atatekwa usawa huu. Kama siyo ndata kutuzuia, huenda tungentumbua jamaa sisi wenyewe!
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.
Image result for katuni za bashite

Tuesday 18 April 2017

My New Book Is on Shelves Now!!!!!!!!!!

Perpetual Search
          Perpetual Search is a nerve-numbing piece of poetry that challenges all humans. The odes here want everybody to ask themselves who they think they are. So, too, it explores human nature based on both sides of the coin of the exemplification of human comportment. It is the pursuit aimed at interrogating some human behaviours and practices that are sometimes taken for granted despite having indelible impacts on people’s lives. It is about the quest for aptness, communitas, love, happiness, power, wealth, life without questioning how they are attained. It raises questions that seem to be simple but are in fact difficult. The quest for human desire based on the search for a better life and for perfection is at the heart of this collection.

Sunday 16 April 2017

Kushamiri utekaji: Barua kwa wahini na wahiniwa

Tanzania imekuwa na mambo ya maudhi hivi karibuni; si kwa watu binafsi bali kama jamii na taifa. Nimesikia wabunge wakiungana wa chama tawala upinzani kutaka kadhia ya utekaji ulioanza kuzoeleka kuchunguzwa. Hii ni baada ya kutekwa wanamuziki wawili na baadaye waheshimiwa wahiniwa watarajiwa wapatao 11 kutishiwa kutekwa. Wapo waliotaja waziwazi waliowatishia kuwateka kutokana na kutopendezwa na mambo au matendo yao. Mtajwa mkuu ni mkuu mmoja wa Mkoa ambaye anaonekana kuwa kipenzi cha mkubwa mmoja nchini kiasi cha kutoguswa; na kama akiguswa, anayefanya hivyo hata awe waziri atakiona cha mtema kuni. Hivyo, huyu ndiye mhini wetu na wote waliotishiwa au kuchukizwa na matendo yake ni wahiniwa. Nisema wazi, nami ni mhiniwa kama mwanajamii anayeshuhudia upendeleo wa wazi ukiachia mbali ulimbukeni na matumizi mabaya ya madaraka. Kinachogomba hapa ni mtu ambaye hakupigiwa kura hata moja kuwa na nguvu kuliko hata wahishimiwa waliotumwa na wananchi kuwawakilisha katika kuongoza taifa lao linalohinika kirahisirahisi kwa sasa.
            Historia ya utekaji hata hivyo, haikuanza jana. Wanaokumbuka namna Dokta Stephen Ulimboka aliyekuwa mwenyekiti wa chama cha madaktari na Absalom Kibanda aliyekuwa mwenyekiti wa jukwaa la wahariri, watakumbuka wawili hawa walivyotekwa tokana na msimamo wao dhidi ya utawala uliopita. Hata hivyo, tokana na tabia ya jamii ya wahiniwa yenye kufanya vitu vya hovyo kuwa vya maana na vya maana kuwa vya hovyo, wahanga hawa wa kwanza, hawakutangazwa wala kuzua gumzo na hofu kama ya hawa wahiniwa wa pili. Hawakuwa maarufu kama hawa wa pili ingawa kama tunatoa umaarufu tokana na mchango na stahiki ya mtu, wahiniwa wa kwanza walipaswa kuwa maarufu kuliko wahiniwa wa pili. Hilo tuliache. Unategemea nini kwenye jamii ambayo baa inaheshimika kuliko shule? Hii nayo, kwa wenye akili, inahini na kuchefua.
Je nini chanzo cha kadhia hii? Majibu ni mengi kuliko majibu; nami nitapapasa na kutongoa machache kati yake kama ifuatavyo:
            Mosi, ni kutokana na woga wa wale wanaowahini wenzao unaosababisha wawaone hawa wanaowadhania kuwa wabaya wao hadi wakawahini hata kuwateka kama tishio kwa madaraka yao.
            Pili, ni ukosefu wa utawala bora na wa sheria. Maana kama ungekuwapo, haiwezekani wahini wakaendelea kuwahini wahiniwa nao wasishughulikiwe lau kwa kuhiniwa kidogo. Japo baadhi yao walishahiniwa na maadui zao, wana rungu la kuwapondea.
            Tatu, ni ulimbukeni na ulevi wa madaraka. Kila palipo ombwe la utawala bora basi kuna ulimbukeni na ulevi wa madaraka. Heri ulevi wa pombe kuliko wa madaraka.
            Nne, mfumo mbovu wa utawala ambao kimsingi ni ule tuliorithi toka kwa wakoloni ambapo wakati mwingine unashindwa kubaini tofauti kati ya gavana generali wa kikoloni na maaskari wake na watawala waliochukua ofisi na mamlaka yake wakaendelea kutawala kutoka kwenye jumba lile lile kwa staili ile ile na falsafa na saikolojia ile ile.
            Tano, ni woga wa wahiniwa ambao hawataki kuungana na kuwakabili wahini lau kieleweke.  Na hii pia inatokana na kuendelea kujengeka hofu na woga kijamii bila msingi. Wakati mwingine unajiuliza: inakuwaje wahini wachache wawahini wahiniwa wengi kiasi hiki wasiwapatilize lau kuwafunza adabu?
            Sita, kusambazwa kwa hofu kwa kimombo fearmongering ambayo mara nyingi ni nyenzo kuu ya maimla wote duniani. Maimla wote licha ya kueneza hofu, nao wana hofu kadhalika. Wana hofu kiasi cha kuogopa hata vivuli vyao. Tuliona mifano kwenye nchi kama DRC wakati wa imla Joseph Mobutu mwizi mkubwa kuwahi kutokea barani. Tuliyaona Uganda chini ya mumiani na chinjachinja Idi Amin. Tuliyashuhudia Libya na Misri pale wahiniwa walipoamua kusema: “Sasa yatosha.” Tuombe Mungu na tuyasikie kwa  wenzetu. Tutolee mifano kwa wenzetu. Tusiombe wahiniwa wafikie kusema “inatosha.”  Siku zote punda anaonekana mnyama mpole na hodari wa kubeba mizigo. Ila anapofikia kusema “inatosha” huwa hapatoshi wala kukalika.
            Tumalizie kwa kuwaasa wahini na wahiniwa waangalie mienendo yao hasa wakijua kuwa binadamu ni viumbe ambao hawatabiriki na ni rahisi kubadilika. Japo wahini wetu wamekuwa wakitolea mifano ya Rwanda, husahau kitu kimoja; au tuseme huangalia upande mmoja, ya huko yalianza na viumbe kama Bashite. Yalianza na kutekwa kwa haki za kidemokrasia. Yalianza na kutekwa kwa wahiniwa. Yalianza na kutotenda haki. Yalianza na matumizi mabaya ya vyombo vya dola. Yalianza tokana na siasa za kujuana. Yalianza na siasa za kuburuzana, kujuajua ukiachia mbali kuangalia upande mmoja wa sarafu. Yote katika yote, hakuna  kitu kibaya kama wahini kuwateka wahiniwa wasijue wajibu wao ni kuwalinda na kuwahakikisha amani na usalama kwa njia zinazokubalika kisheria.
Chanzo: Tanzania Daima Jumapili leo.

Saturday 15 April 2017

A New Book on Terrorism Is Coming Soon!


The following is the letter I received recently informing me that my hereunder mentioned book has been accepted by Hamilton Publishers for publication. I am currently doing final touch to see to it that it comes out any soon from now. My readership must brace for a new baby this year. The following is the letter that Hamilton Books sent to me informing me of their readiness to publish my book. So, too, another book Perpetual Search will come out any time from now.


Dear Dr. Mhango,
I am pleased to inform you Hamilton Books has agreed to publish your book Global War on Terrorism. Attached to this message you will find a cover letter, our contract, and a W-9 form and W8 form (required for disbursing royalties).  Please read through these materials carefully and either email a copy or mail back two signed copies of the Agreement  to  me. Please sign and return the W9 form only if you are a US citizen. If you are not a US citizen, please sign and return the W8 form. I have also attached an Author Handbook and our Marketing Sheet for your review, but I suggest you look over the attached cover letter first. Please note that your initial print run will consist of hardbacks. I have copied Holly Buchanan on this email, and she will be your editor for this project.
Please let me know if you have any questions or concerns.
Best,
Emma
___________________________________________
Emma Richard
Assistant Editor to Holly Buchanan
Hamilton Books
An imprint of Rowman & Littlefield
4501 Forbes Blvd. Suite 200
Lanham, MD  20706
  

Hivi hawa wakioana watazaa nini yarabi?

Picha kwa hisani ya Maisha na Mafanikio Blog

Wapenzi wa miziki yetu furahini nami wiki hii


Tuesday 11 April 2017

Kashfa za Makonda zitalifikisha wapi taifa?

       Image may contain: 2 people     Japo mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam Paul Makonda anaweza kujiridhisha kuwa ndiye alianzisha vita dhidi ya biashara na utumiaji wa mihadarati, ukweli unabaki pale pale kuwa vita hii ilianza zamani. Hata hivyo, si vibaya kupongeza uthubutu wa Makonda kukumbushia vita hii japo kwa namna ya hovyo na yenye kuleta utata na kudhalilisha ukiachia mbali uvunjaji wa sheria, kuna kila sababu ya kupambana na balaa hili. Je, kama taifa, tunapambana na kadhia hii kisayansi na ilivyo?
            Tangu Makonda ataje majina ya vidagaa, hatuoni cha mno kinachotokea kama tulivyotegemea. Badala yake, tunaona juhudi kubwa zikielekezwa kwenye mambo ya hovyo kama kumtetea Makonda dhidi ya kashfa ya kughushi vyeti. Badala ya kuelekeza nguvu zetu zote kwenye janga la mihadarati, nguvu kubwa, kwa sasa, imeelekezwa kwenye kulindana, kulidhishana na kutafuta kila visingizio kwa mhusika kuendelea kuwa madarakani japo umma umeishaonyesha wazi kutomkubali mhusika tokana na uchafu wake binafsi.
            Hakuna kinachoshangaza kama ukimya wa serikali hasa rais John Magufuli katika kukabili kadhia hii ya jinai ya wazi. Tokana na mkwamo na kizungumkuti vilivyopo, inafikia mahali wengine wanakata tamaa kuwa kilichoibuliwa kama vita dhidi ya mihadarati ima ni nguvu ya soda au kutafuta umaarufu wa shilingi mbili. Tutatoa sababu kwanini hii dhana inaweza kuwa na mashiko.
            Mosi, jemadari wa vita dhidi ya mihadarati amekuwa akitangaza vita kila aina ilmradi kuiweka hadhira kwenye hali anayotaka yeye kwa ajili ya kuepusha janga kuu linalomkabili binafsi. Tunasema hivi kutokana na ukweli kuwa hata yale matamko, ukiachia mbali mikakati ya rais kupambana na kughushi kama njia ya kurejesha heshima ya elimu na uwajibikaji havisikiki tena. Tulizoea kusikia watu wakitumbuliwa tokana na kughushi vyeti vya kitaaluma. Lakini baada ya kashfa ya Makonda kufumka, juhudi zote dhidi ya kughushi zimeyeyuka. Huwa najiuliza hali ingekuwaje kama mtuhumiwa angekuwa mpinzani au yule asiyemfurahisha rais kama ilivyotokea kwa waziri mmoja aliyetimuliwa hivi karibuni. Je katiba yetu inatushauri tufanye  hivi kweli? Sijui kama wahusika  wanajua madhara wanayolisababishia taifa mbele ya mataifa mengine. Ukiachia hilo, sijui wanatoa mfano gani kwa jamii iliyowaamini madaraka ikitegemea watu wote watendewe kwa usawa.
            Kama haitoshi, rais Magufuli aliahidi kupambana na mafisadi na wote waliojilimibikizia utajiri wa kutia shaka. Makonda ametuhumiwa na baadhi ya wabunge kuwa ana mali nyingi kinyume na stahiki yake. Hakuna kinachosikika kumchunguza hata kutoa maelezo ya nini kinafanyika kuonyesha ukweli ni upi. Vyombo vyote husika vinaonekana wazi kumgwaya mteule huyu asiyeguswa tokana na ukaribu wake kwa rais. Je namna hii kweli tutashinda. Kwanini shughuli za umma zinafanywa kana kwamba ni suala la mtu binafsi?
            Kuna ushahidi tosha kuwa Makonda anaogopewa na vyombo husika. Rejea mfano wa hivi karibuni ambapo Spika wa Bunge la Muungano Mheshimiwa Job Ndugai alitoa amri ya kumkamata  mbunge wa Kawe Halima Mdee kwa kumtukana spika. Unashangaa inakuwaje nguvu kubwa kama hii kutumika wakati  Makonda alipowatukana wabunge wote kwa ujumla wao kutotumika nguvu kama iliyoamrishwa itumike kumsaka Mdee. Je ni kwa sababu Mdee ni mbunge wa upinzani au ni kwa vile Makonda ni mkuu wa mkoa na mtu wa karibu na rais? Nani mara hii aliyesahau mbunge wa CCM, Peter Serukamba aliyewahi kutukana wazi wazi tusi zito kama eff you  h akutumiwa polisi wala hakuchuliwa hatua? Hii inatia doa na kujenga shaka kwa utawala wa Magufuli. Sijui kama yeye na washauri wake wanaliona hili kama lilivyo.
            Ukiachia mbali hili la kutukana wabunge, Makonda anatuhumiwa kuvamia kituo cha Clouds na kusababisha mtafaruko kwa maslahi binafsi. Tokana na kuogopewa na vyombo husika, hata Waziri mwenye dhamana alipounda tume ya kuchunguza tuhuma dhidi ya Makonda ili atumbuliwe, aliishia kutumbuliwa kama onyo kwa wengine wanaotaka kushughulikia kashfa zinazomkabili Makonda. Hivyo basi, tunaweza kusema; vyombo kama Baraza la Mitihani la Taifa, Tume ya Maadili ya Viongozi, Tume ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) , Jeshi la Polisi na Idara ya Usalama vyote vimeonyesha wazi kumgwaya mhusika kiasi cha kuanza kujengeka chuki dhidi ya serikali tokana na ulegelege wake na upendeleo wa wazi kwa Makonda.
            Tumalizie hapa kwa kuwataka wahusika wafanye kile kiitwacho soul searching kwa kiingereza yaani kujisuta na kuchukua uamuzi ugumu kwa pamoja au kila mmoja kivyake wakijua fika kuwa kuna kesho. Haiwezekani mambo mengine yakakwama tokana na matatizo ya mtu mmoja au watu wawili. Ofisi za umma si sehemu ya kuimarishia urafiki,ukaribu au jambo lolote zaidi ya shughuli za umma. Kwa taasisi zinazohusika na jinai husika, zinapaswa kuondoka kwenye woga zikizingatia kuwa hakuna mwenye kuweza kuzidi taifa hata awe anapendwa au ana mamlaka kiasi gani.
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano kesho.