The Chant of Savant

Monday 31 January 2011

Jeshi lamtosa Mubarak



Mkuu wa majeshi ya Misri Lt Gen Sami Hafis Anan

Rais wa Misri Hosni Mubarak amepata pigo jingine baada ya jeshi kukataa kuwashambulia na kuwatawanya waandamanaji. Kama Mubarak atanusurika basi utakuwa muujiza wa karne hii.Waandamanaji wanasema kuwa hawatatoka mitaani wala hawako tayari kujadilina na yeyote bali kumuona Mubarak akiachia ngazi. Wamemchoka na hawamtaki. Marekani nayo imesema wazi kuwa inangojea serikali ya mpangilio ya mpito.

Baada ya polisi kujikomba na kuua watu, kwa kuogopa kile wachambuzi wanachosema Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC), Mubarak alilazimika kuwaondoa polisi mitaani.
Mkuu wa majeshi ya Misri Luteni Jenerali Sami Hafis Anan alilazimika kukatisha ziara yake ya kikazi nchini Marekani.

Jeshi limesema wazi kuwa madai ya waandamanaji ni ya halali na ya haki. Hivyo, halioni haja ya kuwashambulia wala kuwatisha. Hakika hili ndilo jeshi la wananchi kwa maana halisi siyo haya mashimboshimbo yetu yanayotumiwa na mafisadi kututisha. Ni jeshi linalotumia akili na si kutii amri hata kama ni za kipuuzi na kiuaji kama polisi wetu na majeshi mengine zandiki ya kiafrika.

Akina Shimbo wanapaswa kusoma hili kwa makini na kuacha kujikomba kwa watawala majambazi. Siku ikifika hata ulete vifaru mizinga na madege yanayokunya moto huwezi kushinda NGUVU YA UMMA. Je yanayoendelea huko Misri yanatoa somo gani kwetu ambao tuko kwenye hali mbaya kuliko hata hao wamisri?
Pamoja na juhudi za waandamaji kuungwa mkono na dunia nzima, kuna swali moja kuu. Je baada ya kumdondosha Mubarak, nani atachukua hatamu? Wachambuzi wengi wanahofia Misri kuwa kama Iran ambapo wahafidhina wa kiislamu (Muslim Brotherhood) wanaweza kujipenyeza na kutengeneza himaya nyingine ya kihafidhina kama ya Mahayatollah wa Iran. Hili likitokea litakuwa pigo kwa Marekani na Israel na ulimwengu wa magharibi.

Sunday 30 January 2011

Kwanini Kikwete hataki kujifunza toka kwa Mkapa?






Kabla ya rais mstaafu Benjamin Mkapa kuachia ngazi, hakuna aliyejua siri zake kuhusiana na kujitwalia mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira. Hata kama alikuwepo, aliogopa kupatilizwa. Hakuna aliyejua kuwa mgodi wenye thamani ya shs. 4, 000,000,000 ungeuzwa kwa bei mchekea ya shs milioni 70. Pia, kabla ya Mkapa kuachia urais, hakuna aliyekuwa na ubavu wa kusema ukweli kuwa alijitwali Kiwira yeye marafiki zake, watoto zake hadi wakwe zake wala kukemea biashara haramu za mkewe na mashoga na kaka zake.

Vyombo vya habari vilipojaribu kumkosoa tu kwa ujumla,baadhi ya wakubwa wake walitangazwa kutokuwa raia wa Tanzania huku wakiulizwa walipopata mtaji wa kuvianzisha bila kuwa fisadi.

Hakuna ubishi, licha ya kuyatumia vibaya madaraka, Mkapa alijua jinsi ya kuyamilki akifanya alivyotaka kama mfalme. Ilifikia mahali Chama Cha Mapinduzi na serikali yake wakaanza kumuabudia bila kujua. Walianza kuandaa maandamano ya kumpongeza kwa kila alilofanya au kusema hata kama ilikuwa ni wajibu wake au lenye walakini. Gonjwa hili limeendelea hadi kwenye utawala wa sasa ambapo rais Jakaya Kikwete anaabudiwa. Sijui kama yeye anajua hili. Ila kimsingi, kuanzia Mkapa hadi Kikwete hawakuabudiwa kwa sababu walipaswa au walikuwa miungu zaidi ya wahusika kuwatumia kupata kula yao.

Anayebishia hili arejee tukio la kutia aibu na simanzi lililofanywa na wanaojiita wazee wa Dar es salaam kuitisha mkutano kulaani madai ya katiba mpya wasijue watawageukwa waaibike kiasi cha kuonekana ‘mtu mzima hovyo’. Maskini eti walimpongeza rais kwa kukubali kuandikwa katiba mpya utadhani kufanya hivyo ni hisani na si haki ya watanzania!

Je wazee wa namna hii hata wasiotaka kufikiri na badala yake wakajirahisi kutumiwa na wababaishaji, wezi na mafisadi wanaweza kuheshimika katika jamii? Je hawa wana Mungu kweli zaidi ya njaa zao?

Turejee kwenye mada ya leo. Kwanini Kikwete ni mugumu wa kujifunza na hataki kujifunza kwa Mkapa? Leo watanzania wana uchu wa kujua nani mmilki wa Dowans ingawa anajulikana kuwa ni Rostam Aziz mshirika mkuu wa Kikwete. Wanataka kumjua Kagoda ambaye ni yule yule. Je huyu yuko pekee?

Ukiangalia Daniel Yona alivyokuwa na Mkapa huwezi kuhoji Rostam ni nani na Kikwete ni nani katika hili. Nani amesahau tambo zake kuwa mwenye ubavu aende mahakamani? Ziliishia wapi kama siyo kutokea mbele ya mahakama akiwa amelowa kama jogoo aliyenyeshewa mvua? Hata jogoo ana nafuu maana anaponyeshewa huwa hainamishi kichwa kwa aibu na butwaa kama ilivyotokea kwa mlevi huyu wa madaraka.

Nani aliamini mtu mbishi na mjivuni kama Mkapa kukaa kimya huku akitegemea ulinzi wa aliyewahi kuwa mtumishi wake yaani Kikwete?

Leo tunaongelea ya Mkapa. Kesho tutasimulia ya Kikwete baada ya madaraka kumponyoka. Na hakika haya ni majaliwa ya kila mtu. Muhimu si kulewa na kupuuzia bali kujifunza. Asiyejifunza huzidiwa hata na hayawani ambao yajapo majira ya baridi huandaa makazi yao.

Nani alijiona na kujigamba kama Saddam Hussein au Mobutu Seseseko? Wako wapi zaidi ya kufa vifo vya aibu. Je yote haya si madarasa tosha kwa wenye akili?

Mkapa alishutumiwa kwa kuendekeza ziara za ughaibuni na kulifilisi taifa. Ajabu Kikwete anafanya yale yale tena akizidisha hadi kufikia kubembezwa kama kichanga alipokuwa Jamaica akitoa mapendekezo ya ajabu kuhusiana na mambo ambayo si muhimu kwetu kama vile kuwekeza kwenye mbio na miziki ya reggae.

Mkapa alisifika kwa kuendeshwa na matakwa ya mkewe na mashemeji zake. Alifikia kuamuru polisi wawapige wafanyakazi wa TANESCO pale walipokataa menejimenti ya ulaji iliyokuwa ikipigiwa debe na shemeji zake.

Alisifika kwa kunyamazia biashara ya NGO ya mkewe. Ajabu ya maajabu Kikwete amerudia kosa lile lile hadi kwenda mbele na kuwafanya wanafamilia wake wabia katika serikali yake.

Mkapa alisifika kwa matumizi mabaya ingawa kwa kiasi fulani alifanikiwa kuficha hili kwa kubana mzunguko wa pesa. Kikwete amekwenda mbele hatua mia. Hasikii wala haambiwi. Amepanua baraza la mawaziri na kuongeza wilaya na mikoa bila kujua athari zake. Mkapa aliongeza mkoa mmoja. Kikwete ameongeza mitatu.

Mkapa aliwakumbatia akina Suleish Vithlani na Jeetu Patel ambao Kikwete amewarithi akiwapa hata nafasi ya kuingiza ikulu magari yao ya fahari kuonyesha walivyo nazo. Hata hivyo nafasi ya kufanya dili kali na kubwa hawana tena zaidi ya Rostam Aziz. Kama Mkapa angekuwa madarakani bado, Rostam angejulikana wapi wakati hakuwa karibu naye?

Kikwete amemkumbatia Rostam Aziz kiasi cha kuwa hata tayari kuhatarisha madaraka yake. Laity angejifunza kwa yaliyotokea hivi karibuni kule Tunisia, huenda angenusurika aibu hii ya uzeeni na kwenye ustaafu.

Siku zote la kufa halisikii dawa. Leo Kikwete ana chiriku wa uharibifu kama vile Yusuf Makamba na Salva Rweyemamu wakimburudisha kwa pambio za sifa kwa kila afanyalo liwe halali au haramu, bora au dhaifu. Ila anasahau kitu kimoja. Ulaji ukimponyoka ni wale wale watakaokuwa wa kwanza kumuumbua. Wasipomuumbua wataendelea kumshika mateka ili wasitoboe siri zake.

Je ni kwanini Kikwete hataki kujifunza toka kwa Mkapa?

Chanzo: Makala hii ilipaswa itoke kwenye Mwanahalisi lakini hatujui sababu za kutotoka.

Friday 28 January 2011

Je huu ni mwanzo wa mwisho wa Mubarak na wenzake Afrika?









Je hawa jamaa unawafananishaje?


Kwangu wote wana majina yanayoanza na herufi J. Pia hakuna mtaji uliowaingiza madarakani zaidi ya umaarufu na kuwavurugia wenzao. Jakaya Kikwete aliwatumia waandishi wa habari nyemelezi wakiongozwa na Salva Rweyemamu kuwachafua akina Fredrick Sumaye Salim Ahmed Salim na wengine waliokuwa tishio.

Jacob Zuma alimsukia zengwe rais wa zamani wa Afrika Kusini Thabo Mbeki na kuchukua nafasi yake.

Wanapenda matanuzi na kuruka ruka nje ya mchi. Wanapenda kuvalia suti za bei mbaya.
Wana watoto wengi hata wengine hudiriki kusema nyumba ndogo.Pia wana kasheshe za mambo ya down. Rejea kufungwa kwa mwanamuziki mmoja wa DRC aliyekuwa akifanya shughuli zake za muziki Bongo.Zuma anasifika kwa kubaka sawa na Kikwete ambaye amebaka demokrasia nchini Tanzania kwa uchakachuaji.

Kiakili wote wako sawa ingawa mmoja ana shahada na mwingine hana hata darasa moja.

Wote wanaongoza nchi zenye raslimali nyingi. Tofauti na Kikwete, angalau kwa Zuma raslimali zile zinalinufaisha taifa hasa wazungu.

Wote wameruhusu watoto wao kuwa rais wadogo. Hapa tunaongelea Ridhiwani na Duduzane almaarufu Dudu ambao wanatumiwa na wafanyabiashara na wasaka ngawira kuyaibia mataifa yao.

Hawa jamaa wanawaweza kuwa mapacha. Kazi kwako kuongeza sifa nyingine zinazofanana walizo nazo.

Wednesday 26 January 2011

UVCCM mmejikanyaga na kujichanganya, wanafiki tu




Tamko la hivi karibuni la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) limefichua uoza na migongano ya ndani ya chama.

Kwanza halieleweki vizuri ukiachia mbali kujichanganya na kuparaganya mambo kiasi cha kuharibu dhima nzima ya maana na lengo walivyotaka kuwasilisha. Kwanini hawakuwatafuta wataalamu wa uandishi angalau wakawashauri kama siyo kuwaandikia rasimu nzima ya walichotaka kuwasilisha?

Hebu tuangalie matini mazima ya taarifa ya vijana kwa umma kupitia vyombo vya habari. Kwanza, wao wanaongea kama nani iwapo walishakasimisha mamlaka yao hata ya kufikiria kwa chama chao? Je vijana wameamua kuasi ingawa ni kwa njia ya kichovu?

Suala la kwanza waliloongelea na kusisitiza ni kupendana baina ya mawaziri. Kupenda au kuchukia ni suala la mtu binafsi siyo kufundishwa wala kushinikizwa. Huwezi kumfundisha mke au mme kumpenda mwenzake. Hapa wamenoa sana tu.

Huwezi kumpenda adui yako. Ni mtu gani anayechukia ufisadi anaweza kuwapenda mafisadi au maajenti wao waliojazana CCM na serikalini? Walichoonyesha kuhusiana na mawaziri kupingana, ni wao kutokuelewa demokrasia na mkinzano wa mawazo. Kwa mfano wamewashutumu mawaziri wawili Samuel Sitta na Dk Harrison Mwakyembe hadi kuwaamuru hata waachie ngazi utadhani waliwateua wao.

Sababu ya kufanya hivyo? Kwanini walipingana na waziri wa nishati na madini William Ngeleja alipotetea ufisadi na uoza wa Dowans?

Vijana hawa wanaotia kila aina ya shaka kuhusiana na usomi na welewa wao, walishindwa kujiuliza swali moja muhimu na rahisi. Kama wanachofanya hakifai kwanini aliyewateua hawatimui?Mbona sera ya CCM inajulikana-Kulindana na wao wameikiuka!

Kama wao wanasema mawaziri wanaopingana wakitoe kwa vile wanahujumu mshikamano na uwajibikaji wa pamoja, wao mbona wanapingana na chama chao na hawakitoi? Ama kweli nyani haoni kundule.

Ingawa UVCCM wamejitahidi kuficha walivyo nyuma ya upuuzi wote tunaoshuhudia kwa kujifanya wanapinga kulipwa kwa Dowans, tumewastukia kutokana na kuwashambuliwa mawaziri wale wale wanaopinga hili kufanyika. Hii maana yake ni kwamba wamechomeka hoja yao ya Dowans kufanya kile wazungu huita to get away with it. Kimsingi hawa ni watoto wa Dowans na wanufaika wakubwa wa mradi huu wa majambazi wakubwa.

Imenishangaza na kunihuzunisha sana niliposoma nukuu kuwa mpuuzi mmoja aitwaye Martin Shigela akikopi maneno ya kasuku wengine kama Tambwe Hiza na Salva Rweyemamu kusema eti katibu mkuu wa CHADEMA na mgombea aliyekuwa tishio wa urais Dk Wilbrod Slaa ni kichaa. Nilishangaa haya yanatoka wapi? Nilihuzunika kuona kijana mdogo saizi ya kumwita Slaa baba yake kujiamini na kuitisha mkutano wa waandishi wa habari kujivua nguo. Ukimtukana mwanaume anayelingana na baba yako umemtukana baba yako mwenyewe. Kama Slaa ni kichaa basi watanzania wote ni vichaa wakiwamo baba zao na mama zao.

Tatizo ni nini? Hawa vijana wamelelewa na kulewa pesa za kifisadi kiasi cha kukosa hata uwezo wa kutumia akili ya kawaida (common sense!

Hawa vijana ni wa ajabu kidogo. Hivi hawajui kuwa kulipa Dowans siyo suala la kisheria tu bali la kichama na kiserikali kutokana na maslahi ya nyuma ya pazia? Hivi hawajui kuwa Dowans wana Baraka za baba zao? Kimsingi ni kwamba wanajua ukweli wote. Ila kutokana na unafiki na kujifanya wajanja ili kuwahadaa watanzania wanajifanya hawajui na wako against the whole deal that feeds them. Shame on them.

Sasa wametoa “tishio na msimamo” wao. Kwanini hawakueleza nini kifanyike kama serikali haitaheshimu ushauri wao? Je pesa ya umma ikilipwa kwa Dowans watafanya nini zaidi ya kuzodolewa na wazazi wao wakanywea? Je kwanini umoja wa vijana umeamua kuvunja mwiko hata kwa kujichanganya? Je ni ile mitandao ya kumrithi Jakaya Kikwete imeanza kazi?

Je umoja wa vijana unadhibitiwa na nani kati ya yule fisadi rafiki wa Kikwete anayetaka asafishwe agombee mwaka 1015 na yule mwenye ushawishi kwenye UVCCM mwenye kashfa ya kughushi vyeti? Je wote wamejipima hata wakigeuziana silaha? Je umoja wa vijana hautumiwi jambo ambalo ni aibu?

Kwanini waliokuwa meza ya mbele kwenye mkutano na waandishi wa habari waliongea isipokuwa Ridhiwan Kikwete? Je amemgeuka baba yake au anatafuta ushirika mpya wa kumwezesha na kumlinda baada ya baba yake kuachia ngazi?

Nani amewatuma hawa vijana kupayuka waliyopayuka ingawa hawatafanikiwa kumhadaa mtu. je ni yule jamaa mwenye ushawishi UVCCM ambaya anajulikana alivyoghusi vyeti na kujipachika udaktari sambamba na yule aliyeua mradi wa mabasi ya wanafunzi wa Dar es salaam.

UVCCM waliongelea suala la kuchelewesha mikopo ya elimu ya juu na walihoji ni kwanini wanafunzi wanapogoma leo kesho yake matatizo yao yanatatuliwa?

Kama hawajui jibu, wakamuulize mwenyekiti wao ambaye ameunda serikali isiyowajibika kwa umma isipokuwa mafisadi. Pia huu ni unafiki baada ya kuona joto lilivyouwakia utawala zandiki wa zamani wa Tunisia. Wao wanaathirika nini iwapo wana nafasi za umma kusoma nje hata kughushi vyeti?

Kwanini kutambua tatizo hili baada ya wanafunzi kulitatua kwa njia ya migomo? Vijana waathirika wasiingie mkenge na kuhisi UVCCM inawajali. Hakuna cha kuwajali wala nini bali kutaka kuwatumia kuficha uoza wao. CCM imegeuka kila adui wa mtanzania. Mwenye mapenzi mema na watanzania na Tanzania hawezi kuendelea kuwa CCM hata alalamike na kupinga vipi.

Upuuzi na udhaifu ulioonyeshwa na UVCCM unaweza kuandikiwa hata msahafu.

Chanzo:Tanzania Daima Januari 26, 2011.

Dowanis ikilipwa najichoma moto


Baada ya kumaliza mazishi na maombolezo ya mashujaa wa Arusha, nilivuka mpaka na kuingia Kenya tayari kupanda ndege kuelekea Tunis kuhudhuria mazishi ya shujaa mwingine na wengine waliouawa na vibaka wenye sare baadaye.

Msiba huu ulikuwa ni wa rafiki yangu mwanafunzi wangu na mwanamapinduzi Mohammed Bouazizi ambaye baada ya kumaliza chuo kikuu na kukosa kazi aliamua kubangaiza kwa kuuza matunda na kahawa kijiweni kwake.

Serikali ilipoingilia biashara yake, Bouazizi aliamua kujichoma moto na kufariki baadaye huku akiacha ameuchoma mshale utawala wa dikteta Zine al-Abidine Ben Ali. Jamaa huyu ambaye tulikutana alipokuwa mlinzi wa hayati Habib Bourguiba alijigeuza Mungu akitawala kwa kutumia familia yake na walamba viatu.

Alijisahau. Aliiba pesa ya umma kama hana akili mbaya. Aliamuru kuuawa kwa waandamanaji walioandamana kuomboleza kifo cha Bouazizi huku wakipinga hali mbaya ya maisha. Walipinga ufisadi, matumizi mabaya ya vyombo vya dola, matumizi mabaya ya njuluku za umma, uwekezaji mbovu, kujuana, usanii na upuuzi mwingine uliofanya maisha yao yakose maana.

Hakuna mtu aliyekuwa mwizi na kuchukiwa kuliko hata Ben Ali kama mkewe kikwapuzi Leila Ben Ali (binti Trabelsi) ambaye watunisia walizoea kumwita Imelda Marcos wa ulimwengu wa kiarabu. Mama huyu habithi, kwa habari nilizopata mitaani Tunis ni kwamba ametoroka na vito vyenye thamani ya dola za kimarekani 35,000,000.

Alipataje ukwasi huu? Aliupata baada ya kumlisha limbwata rais na kumtawala yeye na ukoo wake. Kwa ufupi ni kwamba alimgeuza rais bwege na kifaa cha kujitajirisha yeye na ukoo wake bila kusahau mashoga zake.

Hasira za watunisia kwa mama huyu ungeziona kwa jinsi walivyochoma mahekalu yake na kaka yake bila kusahau kukojolea picha zao wakiapiza siku wakiwapata kuwavua nguo na kuwaamuru wanajisiane. Haya si maneno yangu. Ni maneno ya waarabu hawa wenye miili midogo lakini yenye mioyo mikubwa.

Mama alikuwa mshenzi sina hamu. Unajua kuwa baada ya kuwa mhudumu wa saluni halafu akaolewa na Ben Ali alihakikisha ndugu zake wote 10 wanatajirika kupitia mgongoni mwa shemeji yao bwege kama ilivyokuwa kwa Anna Tamaa Tunituni na sasa Shari si Salama Njaa Kaya na genge lake la majambawazi watumiao ushemeji na udugu wa jamaa kutumalizia kaya?

Ukoo huu wa mapanya watu walao kwa miguu na mikono tena bila kunawa na wakinya kama mainzi, ulikuwa ukimilki karibu kila kitu kuanzia internet café, uuzaji wa magari, hisa kwenye mabenki, shirika la ndege la taifa la biashara ya mihadarati? Je Leila habithi huyu unakupa picha gani kuhusiana na kaya yako?

Pamoja na ukuu wangu wa kijiwe msijemuingiza hani wangu mshirika wa bedroom nikanyotoa mtu roho kabla ya kujimwagia petroli na kuiaga dunia kama Dowanis watalipwa njuluku za walevi kutokana na kusababisha kiza na kupanda kwa gharama za mameme.

Nilijifunza kitu kimoja kikuu. Yale yaliyofanyika AR yangefanyika Tunisia mbona jamaa na Imelda wake na Riz-one wangekuwa historia? Mbona Kagoda Rostitamu na washenzi wenzake wangeishanyotolewa roho kama siyo kutoroka?

Siku hizi tumegundua njia nyingine ya kujikomboa na kuondoa uonevu na ufisadi.

Mbinu hii mpya ya ukombozi inalenga kutoa ujumbe kuwa hawa wanaotunyanyasa wajiulize. Kama twaweza kujichoma wenyewe, tukiwapata wao tutawafanya nini?

Turejee Tunisia. Siku benki ya Zeituona iliyokuwa ikimilkiwa na mmoja wa kaka zake Leila ilipochomwa na waandamanaji si nikaenda lau niondoke na madolari. We acha tu. Ufahari na kiburi chote cha familia hii habithi kilitoweka ndani ya dakika chake baada ya kijana asiye na kazi kuwasha moto ulioangusha vigogo. Nani alijua kuwa muuza nyanya, kahawa na mboga mboga angeweza kumuangusha rais tena aliyejiona mungu mtu? Sasa imetokea wenye akili na mikakati tieni akili. Hata wale gendaeka wanaojiona miungu watu kwa sababu ya madaraka waliyopewa na umma wakae mkao wa kuliwa.

Nani angeamini kuwa ofisi za chama tawala cha Rassemblement Constitutionel Démocratique (RCD) au Kusanyiko la Kikatiba na Demokrasia kwa kimakonde zingevamiwa na kubomolewa huku alama zake zote zikiangusha mchana kutwa? Wenye tabia ya kujiona kuwa watatawala milele nao wakae mkao wa kuliwa.

Kwangu RCD ni Ruling Corrupt Devils. Genge hili la mibaka halikuwa na demokrasia ya maana zaidi ya demokrasia ya kifisadi ambapo fisadi mkubwa huwaruhusu mafisadi wenzake, wake zake, watoto zao hata mbwa wake kuibia taifa bila kushughulikiwa. Na huwezi kuamini. RCD ilikuwa ikihubiri amani na mshikamano na kutishia watu walipoanza kuhoji ugumu wa maisha ilhali genge la majambazi na mibaka yenye madaraka na hata mbwa wao walikuwa wakineemeka tena bila kufanya kazi.

Nakumbuka mpumbavu mmoja changudoa msemaji wa rais aliyefurushwa aliwakejeli wananchi kwa lugha za mitaani kama shangingi wa kihaya afanyavyo kayani. Yuko wapi? Ameikimbia Tunisia kwa mtumbwi baada kibanda chake kupiga nari.

Huu ni ufunuo kwa wadanganyika na wadhulumiwa wote barani kuwa siku moja kama mtaamua kuacha ukondoo mtajikomboa na kuwa huru kabisa kama watunisia waliomtunishia misuli mwizi mkuu aitwaye rahisi wa ufisadi akatimka na mbweha wenzake.

Nilipokuwa nikishangaa wenzetu wanavyojijua baada ya kufanya mapinduzi ya kifikra na kimkakati, nchi nyingine zililipuka. Kule Misri jamaa mmoja ambaye tuliwahi kuwasiliana kwa mtandao aitwaye Mohcin Bouterfif alijitia nari akitaka wamisri waamke na kumkabili farao wao Hosn Mohamed Mubarak. Nchini Mauritania mke wa shujaa Yacoub Ould Dahoud alinitumia email kuwa mumewe alikuwa naye kajitia nari. Baada ya kuona wanakijiwe wenzangu wa nchi zilizoachana na ukondoo wanajitia nari, name napanga kujitia nari kama Dowanis italipwa njuluku za walevi wachovu. Nitakwenda mbele ya jumba jeupe lililojaa uoza na kujitia nari. Naona na UVsisiemu nao wameanza kushtukia dili za madingi wao!

Wache niende kununua kibiriti niwachome kabla ya kujichoma. Ngoja nijiimbie wimbo wa Sipho Makhabane aliowaimbia makaburu.

Zawelale indonga. Indonga zawelale. Ngome zimeanguka na ngome zitaangushwa. Tuimbe sote. Ngome zitaangushwa na walioko nyuma yake wataanguka na kuaibika. Indoga zawelale indonga zawelalelale.

Ziangushwe ngome ngome za ufisadi ngome za Dowanis ngome za Kagoda ngome za Njaa Kaya ngome za Ewassa ngome za za za. Nasikia harufu ya EPA harufu ya Dowanis na Njaaa Kaa na Kiama cha Mafisadi.


Chanzo: Tanzania Daima Januari 26, 2011.

Monday 24 January 2011

Ni Tambwe Hiza huyu anayewaita wenzie vichaa?

Tazama picha hizi uone ni nani au wapi wanaelekea kuokota makopo.





Tambwe Hiza mganga njaa na nyemelezi anayeweza kurukia chama chochote ili mkono uende kinywani ni mugumu wa kujifunza. Sijui ni kutokana uelewa na elimu ndogo au kuzidi kujipendekeza ili aongezewe malipo yatokanayo na mabaki ya ufisadi?

Hivi karibuni alikaririwa akimshambulia katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Dk Wilibrod Slaa. Akisema: “Ninachoweza kusema kwa sasa ni kwamba kiongozi huyo amepandwa na wazimu, alichobakiza ni kuvua nguo tu…amechanganyikiwa na ndiyo maana anatapatapa kutafuta lolote la kusema.”

Tuwe wakweli jamani. Hivi kati ya Dk Slaa aliyemtingisha hata bosi wa bosi wake Jakaya Kikwete na kidampa kama Hiza nani anakaribia kuvua nguo? Nani hajui kuwa Hiza aliljivua nguo alipojiunga na CUF na kutimua baada ya kushindwa ubunge?

Kwanza, sijui kama haya maneno ni ya Hiza au ni Martin Shigela au Salva Rweyemamu mkuu wa Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu ambao, sawa na Hiza, wameonyesha kuwa uhuni haumtoki mtu ukiishamuingia. Tuachane na aliyemkopesha nani uchafu huu. Maana uhuni ni uhuni hata kama anayeufanya anatetea ikulu au chama tawala.

Kuna haja ya kujiuliza ni kwanini Hiza ameteka madaraka chamani. Nadhani, ingawa CCM imekuwa ikishutumu vyama vingine kwa ukabila, Hiza anafanya hivi kutokana na kuwekwa alipo na mtu wa kabila lake Yusuf Makamba (katibu mkuu wa CCM) ambaye baada ya kumpachika mwanae serikalini na chamani ameonyesha wazi anavyotumia madaraka yake kwa ajili ya familia na hata kabila lake.

Niliwahi kumtaka Hiza hata mjomba wake Makamba wanipe vigezo vitatu tu vya kufungua ofisi ambayo hata kwenye katiba ya CCM haimo ya Propaganda. Bahati mbaya kutokana na ukweli na uzito wa hoja yenyewe waliingia mitini na kunywea.

Kwa anayejua uchu na udhalili wa Hiza, hashangai kuona akimvamia Dk Slaa. Huenda ana hasira baada ya kushindwa kusimama ubunge ukiachia mbali kuanza kustuka kuwa kadri anavyokaa kimya bosi wake anapunguza mlo. Ndiyo, mbwa ili alipwe lazima awinde au hata kubweka kama afanyavyo Hiza. Ila kwa umri wake, huku ni kuchelewa kukomaa kiakili na kisifa kama mwanaume.

Hiza na Makamba wamegeuka midomo ya mafisadi. Wanatumiwa kirahisi kutokana na uwezo wao mdogo wa kufikiri na ile hali ya kuendeshwa na tamaa.

Ningemshauri Dk Slaa na CHADEMA wasimjibu. Maana wakifanya hivyo licha ya kupata umaarufu, wanamtengenezea kitumbua kwa bosi wake. Hiza kweli ameishiwa. Anatoa tamko la kipumbavu leo, kesho yake umoja wa vijana wa CCM unakuja na kile kile. Hii maana yake ni kwamba zee hili ambalo linajiona ni kijana limewafundisha uhuni vijana.

Kwanini Hiza haoni ukichaa wa mjomba wake aliyechekelea mauaji ya Arusha asijue kila mtu atakufa? Mbona CHADEMA hawakuchekelea kuanguka anguka hovyo kwa mwenyekiti wake?

Hiza anasema CCM ina mpango wa kumfunga na kummaliza Dk Slaa. Huu ni uzushi na vitisho vya kipumbavu. Tangu lini CCM ikawa mahakama? Na kwa kusema hivi amemsaidia Dk Slaa bila kujua. Maana akifungwa tutasema ni shinikizo la CCM. Laiti angekuwa na elimu lau akatumia busara kujua hata mambo madogo ya kisheria. Lakini hakuna haja ya kumshagaa au kumuonea Hiza kutokana na shule kumpiga chenga. Na hii ndiyo maana hata hiyo ofisi ya propaganda na zile za wilaya zimejaa vihiyo wasio na usomi wala busara.

Hivi kati ya bosi wake Hiza na Slaa nani anakaribia kuokota makopo? Arejee anavyosakamwa kukisambaratisha chama kutokana kupayuka hovyo huku akiwatumia wahuni na vihiyo kama Hiza kuchafua hewa chamani.

Hiza amesahau kuwa kampeni za uchaguzi zimekwisha. Hata waganga njaa wenzake kama vile yule mtabiri muongo na mashehe wengine njaa bila kusahau hata maaskofu njaa wamejua kuwa wakati wa kugeuzana miradi umepita na anachoongea kinafuatiliwa kwa makini!

Je kwanini CCM wanapenda kumtumia Hiza na si watu wenye akili angalau na mashiko hata kama ni mafisadi? Je wanajua anavyodharauliwa, hivyo kutoweza kushitakiwa? Maana wangewatumia watu wenye mashiko nadhani kesi ingefunguliwa haraka. Lakini nani yuko tayari kumpeleka mahakamani mtu ambaye ni karibu na hayawani?

Hata kama Hiza anasumbuliwa na njaa na hawezi kula bila mafisadi kumtumia makombo baada ya kujikomba, inabidi aanze kukomaa na kujifunza. Asisahau kuwa alipokuwa CUF alikuwa akitamka mambo ambayo kwa sasa anayaramba kuonyesha alivyoharibikiwa kiakikili. Je mtu wa namna hii si kichaa? Je tabia hii ya mbwa ya kuramba matapishi yake inamfaa mwanadamu?

Wengi wanajua. Hiza baada ya kuukosa ubunge na kuwa na kisomo kidogo kiasi cha kutoweza kufaa kuajiriwa, alijirejesha CCM kama mbwa koko afanyavyo baada ya kudokoa kwa aliyemfuga. Siku zote nimekuwa nikitahadharisha kuhusiana na siasa za ukuku, ufisi na umbwa. Kuku hula asichozalisha na kuzalisha asichokula. Hiza anazalisha migongano na kula pesa ya walipa kodi.

Kwa vile Hiza ameridhia kufugwa kama kuku, basi aachane na kanga wanaojitafutia kwa heshima hata kama wamekondeana. Asiwacheke wakati wao ndiyo wapaswao kumcheka ingawa hawafanyi hivyo.

Wengi wanaomjua Hiza wanamjua kama mtu wa kuhurumiwa ambaye hali hadi achochee wenzake. Wanamjua alivyo na uchu wa fisi jambo ambalo linamfanya ashindwe kujitofautisha na changudoa awezaye kulala na yeyote ilmradi ale. Hii siyo sifa inayomfaa mwanadamu tena mwanaume.

Kama tungekuwa hatuna adabu kama Hiza basi tungemshambulia mwenyekiti wake kutokana na sasa kuishiwa hadi hata umoja wa watoto wa chama chake kuanza kutoa matamko makali baada ya kumuona kimya na hafai hata kidogo. Lakini bado tunamstahi ingawa ni wa hovyo kiasi cha kutumia watu wa hovyo kama Hiza hata yule msemaji wake ambaye naye alimshambulia Slaa kwa staili hii hii. Hata hivyo hatuwashangai hawa kutokana na kujulikana wanavyoishi kwa kujikomba hata kwa kukiuka kanuni taratibu na maadili. Huko leo si mada.

Kwanini Hiza asimwambie mwenyekiti wake aache kuwaangusha na kuwadhulumu watanzania? Ametimiza ahadi gani na ngapi tangu aingie madarakani zaidi ya kutumia muda mwingi kufikiri jinsi ya kuua kashfa zinazomkabili, watu wake, chama na serikali yake?

Kwanini Hiza hashupalii Dowans? Hawezi kukata mkono unaomlisha yeye na bosi wake na yule mhuni mwenzie wa ikulu.

Sijui kama Hiza hununua magazeti. Maana watoto wake au mkewe wakisoma, watavunjika moyo na kujilaumu kwa kuwa na mume au mzazi kama yule hata kama aibu yake inawalisha.

Bwana Hiza kama propaganda zimeisha si uende Lushoto ujifunze lau uganga kuliko huo uganga njaa? Hivi mjomba wako siku akitimuliwa utaondoka naye kama mwana wa kufikia au utadandia chama gani?

Watanzania mdharau na kumpuuzia Hiza kwani mnajua njaa ikipanda kichwani matokeo yake ni kuwa tayari kutumiwa na kila atakaye wa kutumia kama mtumwa Hiza anavyofugwa na CCM. Isitoshe angekuwa amekwenda jando kichwani na si kukeketwa basi tungemchukulia kwa uzito wa ziada. Je wanaomtumia nao hawajaishiwa kama yeye? Je huyu ni Tambwe Hiza yule nyemelezi nimjuaye? Simba na mbwa aina ya chiwawa wapi na wapi?

Chanzo: Dira ya Mtanzania Januari 24, 2011.

Sunday 23 January 2011

Je watawala wezi na mafisadi wa Kiafrika husoma haya?


Hekalu la fashisti Mobutu Seseseko wa DRC iliyoko Monaco

Hekalu la dikteta Theodor Obiang Nguema wa Equatorial Guinea liliko Malibu


Hekalu la Omar Bongo mwizi wa zamani wa Gabon lililoko Paris na ni moja kati ya 33 aliyokuwa akimilki.








Hivi karibuni shirika la habari la Uingereza (BBC) liliripoti kisa hiki hapa chini kama kilivyo bila kuongezewa wala kupunguzwa.

Hii ni siku chache baada ya mabenki nchi Switzerland kutangaza kuzuia akaunti za dikteta wa zamani wa Tunisia Zine al-Abidine Ben Ali.

Kasri hili la bei mbaya (chateau) ni mali ya dikteta wa zamani wa nchi maskini kabisa ya Afrika ya Kati, Jean-Bedel Bokassa ambaye naye alikufa maskini baada ya kufuja chumo la wizi. Alifia gerezani akiwa kapuku hakuna mfano. Umaskini ulimchoma hadi akajirejesha mwenyewe kama alivyofanya dikteta wa zamana wa Haita Jean Claude Duvallier maarufu kama Baby Doc.

Je ni wezi wangapi walioko madarakani wana mali kama hizi huko Ulaya zikingoja kufichuliwa na kutaifishwa baada ya kupigwa teke na wimbi la mapinduzi ya nguvu ya umma linalozidi kupata kasi barani Afrika?

Kwa habari zaidi soma habari hii hapa chini.



African dictator Bokassa's chateau sold at auction




A French chateau that once belonged to African dictator Jean-Bedel Bokassa has sold for 915,000 euros (£760,000).

The dilapidated 'Chateau d'Hardricourt' was bought by an anonymous bidder at an auction in Versailles.

Bokassa spent several years living in the mansion in the western Paris suburb of Hardricourt after he was overthrown as leader of the Central African Republic (CAR) in 1979.

It has since fallen into disrepair and needs major refurbishment.

"Electricity, water, heating - all need to be overhauled," Pascal Koerfer, lawyer for the administrator of the Bokassa estate, told Associated Press.

The property overlooking the Seine comes with 10,000 square metres (108,000 sq ft) of surrounding parkland, a house for a caretaker and a double garage.

But Mr Koerfer estimated it would take up to 3m euros (£2.5m) to restore it to a "liveable" condition.

More than 80 potential buyers are reported to have viewed the property before the sale.
'Lamentable' state

One curious visitor, described only as Marcel, told Europe 1 radio network that the chateau was in a "lamentable" state: "The manor is not heated, there are broken windows and ceilings falling in."

The chateau was occupied by one of Bokassa's wives and two of his children up until a few years ago. One of the daughters, Marie-France, is quoted as saying they did not have the money to maintain the property.

One of Bokassa's sons, Georges, who was at the auction, had urged French President Nicolas Sarkozy to intervene to prevent what he called the plundering of his family's heritage.
Former Central African Republic ruler Jean-Bedel Bokassa poses with seven of his children at 'Chateau d'Hardricourt' in a suburb of Paris, 6 December 1984 Bokassa with some of his children at the chateau in 1984

The self-proclaimed Emperor of Central Africa had an estimated 50 children.
Source: BBC

Saturday 22 January 2011

Nawalilia mashujaa wetu Arusha




MWENZENU juzi nililia kama kichanga kutokana na uchungu na nyomi ya watu iliyoujaza mji wa AR. Nilikuwa kule kuwaaga mashujaa waliouawa wakipingana na kupigana na ufisadi.

Hawa ni mashujaa wa kweli dhidi ya ufisadi. Siyo sawa na wale mashujaa njaa waliopewa vipande vya vyeo wakasaliti mapambano na kuwa sehemu ya maadui. Sam Six na Mwakiwembe mnanipata?

Nasikia mkipiga kelele na kuangusha machozi ya mamba eti Dowanis isilipwe. Kama kweli mnamaanisha kufanya kweli, jitoeni huko mje huku na kujiunga na makamanda na mashujaa wa kweli wakiongozwa na Daktari Slaa.

Kwa ufupi, ni kwamba tuliwaaga kwa heshima zote mashujaa waliouawa na majambawazi wenye sare. Niliona wale majambawazi wa sare wakitumbuatumbua mimacho kwa aibu kama panya aliyenaswa kwenye mtego.

Tuliwazomea na kuwasomea ili wajue jinsi wanavyotumika kama nepi kuzoa uchafu wa wakubwa fisidi waliowaamuru kuua mashujaa wetu.

Juzi nilifurahi niliposikia lisirikali likiwakana hawa jamaa zangu kusema eti walikurupuka. Kwa wenye akili, hili zaidi ya kuwa suto, ni somo kuwa waache kujirahisi na kutumiwa kama mbwa au vifaa vya mafisadi hawa.

Huwa najiuliza kama hawa jamaa wana ubongo na kama wanao kama una akili au matope. Maana yenyewe yakiamriwa, hata bila kutumia busara yanaangamiza yasijue waathirika ni ndugu, mama zao, dada zao hata wenzao!

Hivi haya yakistaafu yatakuwa nani kama si raia wa kawaida? Kuna haja ya kuyafundisha haya majamaa kutumia akili badala ya matumbo.

Najua Njagu mkuu Saidia Wema anapresha kwa sasa kutokana na kutakiwa aachie ngazi yeye na bosi wake Chemsha Vurumai Nahodhi. Mie nshawasiliana na madevu Mureno Ocampoe kuja kufanya vitu vyake dhidi ya kikundi hiki cha magaidi kayani.

Hata leo nasema tena bila kufumba. Kitoeni wahalifu nyie hata kama mna vyeo vikubwa.

Sasa nasema tena kwa kinywa kipana na herufi kubwa Njaa Kaya na wauaji wenzako kaa mkao wa kula. Tutaandamana hadi kieleweke. Tumechoka na usanii, ufisadi, uchakachuaji wa kila kitu na upuuzi mwingine.

Hatutishwi na tutaandamana hadi kuku, kenge, fisi, mijusi na wanyama wengine watuunge mkono kama hawa wanaopaswa kutusikia wamejigeuza hayawani.

Tutapinga ufisadi kuanzia Dowanis hadi HEPA. Tutaliandama liserikali na mafisadi wake hadi kieleweke.

Kaya nzima lazima iamshwe kabla hawa majambawazi hawajatuuza na roho zetu.

Wameuza madini, mashamba, ardhi, mbuga za wanyama. Hawajatosheka wanatuuzia hata giza na ukame! Wanatuuzia matusi kiasi cha kutuua tunapowapa ukweli.

Wanatumia kodi ya walevi kuwaua na kuwadhalilisha! Hivi hawa wana roho kweli? Wana akili kweli hawa? Hivi hawajui kuwa maulaji yana mwisho na mwisho wake huwa mbaya hasa kwa wale waliokula bila kunawa tena kwa miguu na mikono kama wanavyofanya sasa?

Hapa najua wataajiri machangudoa wa kimaadili kama yule shangingi wa kihaya kutukana watu ili kutetea mabwana zao.

Juzi nilimpaka hadi akalalamika. Alijua mie gari kubwa. Angejitia kujibu ningemuumbua kuanzia afya yake hadi nyumbani kwake. Hayo tuyaache yana siku na mahali pake.

Sasa natangaza mafisadi na mbwa wao wanaotumika kuua na kuonea walevi wajue na kujiandaa. Wamelikoroga. Tutaandamana hadi kwa jamaa wa nyayo ambao nao walipoteza ndugu yao aliyekuwa amebatizwa na majambazi kuwa Mkurya wakati ni Mgikuyu wasikie.

Si mlizoea kuwaita manyang’au wakati manyang’au ni nyinyi wenyewe. Tutawaandama mafisadi hadi wajue hii kaya ni yetu si yao.

Jamaa hawa waajabu kweli. Wanaomba msamaha mabalozi badala ya sisi utadhani waliouawa ni mabalozi na si wadanganyika! Baada ya kushtuka kuwa wamefanya makosa mengine, eti wanakanusha kwa kutishia kufunga magazeti ya umbea.

Sumu ishasambaa kuwa mlikurupuka kama mbwa wenu na kuomba msamaha mabalozi badala ya walevi. Huu nao ni ulevi wa madaraka na matumizi mabaya yake.

Mtashitaki wangapi? Bwana Ben Mende nadhani ananipata. Utashitaki wangapi ndugu yangu? Thubutu.

Umma wa walevi lazima uelimishwe kuhusiana na hawa magaidi wa kayani. Hata wakiomba misamaha mia tena uchi bado ni mafisadi na wauaji wanaopaswa kuteketezwa kabla hawajaiteketeza kaya.

Wasivyo na bongo eti wanaamua kuua kwa vile waliambiwa ukweli. Kama wasingekuwa mafisadi si wangekanusha badala ya kunyotoa roho za wachovu wasio na hatia?

Hivi waliouawa wangekuwa watoto au jamaa zao wangefanyaje? Wakijibu swali hili watapata jibu la wanachopaswa kufanya kuhusiana na familia za marehemu mashujaa wetu.

Kwanza, wangewalipa fidia wathirika wote. Pili, wangehakikisha ujambazi huu haufanyiki tena. Tatu, wangeanza kuwaandama hata kuwaua mafisadi badala ya wanaowaambia ukweli. Nne, waliotoa amri waachie ngazi na kupelekwa Segerea au wapigwe mawe kama vibaka. Tano, walaaniwe. Sita, walipaswa kutubu na kuomba msamaha walevi.

Saba, walipaswa kuachana na malipo kwa Dowanis. Nane, wawataje wamilki halisi wa Dowanis hata kama wakubwa wenyewe. Yote tisa lamia waache mgao wa kiza tena wa kulangua.

Kwa vile walevi wangi wanataka kujua Dowanis ni nani na mali ya nani, na wenzao hawataki kujitaja, mie nitawataja.

Nina sababu nzuri tu ya kuwataja. Kama wahusika wasingekuwa wadowans wenyewe si wangetaja majina ya wamilki wa Dowanis badala ya kuja na majina ya wamachinga wa Kizungu kama walivyofanya.

Wanadhani hatujui kuwa hawa wanaowataja ni vidampa wao wa kawaida hata kama ni Wazungu?

Sasa natoboa. Dowans ni Rostitamu, Ewassa, Endelea Chenga na Ziro Kadamage na wengine ambao wasomaji nanyi malizieni kutaja.

Kijiwe cha leo ni kwa heshima na kumbukumbu ya mashujaa waliouawa wakipambana na ufisadi. Walaaniwe mafisadi wote. Walaaniwe wauaji wote. Wote washindwe na walegee. Aaaamina.

Naona Andengenyeke anakuja na vibaka wenzake wacha nikitoe nisije nkauawa bure. Ngoja niwafundishe kukimbia!

Chanzo: Tanzania Daima Januari 19, 2011.

Friday 21 January 2011

Kizazi kipya cha ndege chatangazwa


Lockheed imekuja na hii

Northrop Grumman imetoka na kitu hiki

Nao Boeing hiki ndicho kifaa chao



Shirika la Mambo ya Anga la Marekani (NASA) limetoa mifano ya ndege zitakazotumika kufikia mwaka 2025.

Shirika hili lilitoa tena kwa makampuni ya Lockheed Martin, Northrop Grumman na Boeing mwishoni mwa 2010 kutengeneza ndege yenye kwenda kwa angalau 85% ya mwendo wa sauti. Pia ndege hii ilipaswa kutochafua mazingira, yenye kutumia mafuta kidogo na isiyopiga kelele na iwe tayari mwaka 2025.

Kadhalika, ndege hukika ilipaswa kuwa na uwezo wa kubeba mzigo kuanzia kilo 22,680 hadi 45,360.

Aina tatu za disaini ya ndege hii ya kimapinduzi imewasilishwa na makampuni husika kama unavyoona kwenye picha. kwa wale mashabiki wa ndege kama mimi hii ni habari kubwa tu.The three designs submitted by the companies are radically different.

Disaini inayoonyesha kuvutia ni ile ya Martin Lockheed yenye injini ya ndege iliyoningèinizwa mkiani mwa ndege.
Wengi wanahofia kama ndege hii itaanza kutumika kama ilivyolengwa kutokana na Boeing Dreamliner 787 iliyoanza kutengenezwa mwanzoni mwa 1990. Hata hivyo imekumbwa na mikwamo kibao kiasi cha hata sasa miaka kumi baadaye kuwa bado haijazoeleka ikilinganishwa hata na Airbus 380 dege lenye uwezo wa kubeba watu kibao kuliko nyingine duniani.

Kutokana na tatizo hili la Dreamliner ndiyo maana NASA ikaanza kufikiria ndege ya 2025 mwaka 2011.
Mambo ya teknolojia hayo.
Chanzo: Internet.

Barack Obama anapogeuka jambazi!

Je ni ushabiki,ujambazi, chuki au ubaguzi?





A man who robs banks wearing a rubber mask of US President Barack Obama has struck again, Austrian police said Friday.

The disguised thief robbed a bank in the town of Handenberg in Upper Austria just before the bank closed at 6:00 pm (1700 GMT), police said in statement.

Police believe the same man, disguised by his Obama mask, has been carrying out such bank raids for the past two years.

He threatened the bank's employee with a gun, shouting: "This is a hold-up. Give me the money."

The robber -- who apparently spoke with a local dialect -- initially fled by foot with the money in a black shoulder bag.

Witnesses said they then sped off in a dark car with a Salzburg region number plate.

No one was hurt during the hold-up, police said.

The statement did not say how much money the robber made off with, but the daily Kronenzeitung, in its online edition, put the amount at 10,000 euros (13,500 dollars).

Wednesday 19 January 2011

Wafahamu wana wake waliowateka na kutawala marais

Ben Ali na Leila

Kikwete na Salma

Museveni na Janet
Kibaki na Lucy

Mugabe na Grace
Zenawi na Azeb
Mkapa na Anna

Ingawa wengi wanaangalia kwa juu kutimuliwa madarakani kwa rais mwizi wa zamani wa Tunisia Zine al-Abidine Ben Ali, ukweli ni kwamba mkewe Leila Trebelsi na ndugu zake 10 ndiyo walimwingiza matatani kutokana na uroho na ujinga wao.

Mama huyu aliyejulikana kama Imelda Marcos wan chi za kiarabu anaamika kutorokana na vito vyenye thamani ya dola za kimarekani 35,000,000.

Msusi huyu wa zamani ndiye analaumiwa kumwingiza majaribuni mumewe kiasi cha kufilisi nchi kutokana himaya ya ukoo wake wa ndugu 10. Ukoo huu ulijiingiza kwenye kila aina ya biashara kuanzia mihadarati, uuzaji magari, internet café, hisa katika mabenki na shirika la ndege la Tunia na mwisho wa yote kama mmoja wa Leila kumilki benki ya Zeitouna ambayo ilichomwa moto sambamba na mahekalu ya ukoo huu fisadi hivi karibuni sambamba na mahekalu ya ukoo huu.

Mwingine katika mchezo huu mchafu ni Grace Marufu Gucchi Mugabe ambaye amepewa jina la Gucchi kutokana na kupenda nguo za fasheni. Ni mama huyu aliyewahi kwenda benki mwaka juzi na kuchukua dola 10,000,000 cash wakati wazimbabwe wakihaha kwa njaa.
Ni mama huyu aliyewahi kumwambia mke mpya wa rais wa Malawi Calista Chapola-Chimbombo kuwa kama mke wa rais atumie na kufanya atakacho bila kusikia wambea (wananchi) wanasema nini. Ni mama huyu huyu ambaye amemnunulia bintie Bona Mugabe hekalu huko Hong Kong anakosoma. Binti hiyi mchanga ana watumishi huko Hong Kong karibu idadi sawa na wafanyakazi wa ubalozi wa Zimbabwe kule.

Watu wengi hawamjui mke wa waziri mkuu wa Ethiopia Meles Zenawi aitwaye Azeb Mesfin au Queen of Mega (Corruption) kutokana na kujihusisha na ufisadi wa kiasi cha kuu au mega corruption kwa kimombo. Huyu kama Leila ana himaya ya biashara nchini Ethiopia na nje si kawaida.

Bila shaka wote mnamjua Janet Keinembabazi Kataha Museveni mke wa dikteta wa pili wa Uganda Yoweri Museveni. Huyu amehakikisha ukoo wake, wakwe zake, wajomba zake, dada zake na kila anayemhusu kuwa marais wadogo nchini Uganda. Kimsingi, ndiye mshauri mkuu wa Museveni ambaye kwa pamoja licha ya kuunda utawala wa kabila lao la wanyankole, wameunda urais wa familia. Nani alitegemea angeteuliwa na mumewe kuwa waziri baada ya kuonyesha tamaa ya siasa? Wapo wanaodhani anaotea kumrithi mumewa kama alivyofanya rais wa sasa wa Argentina Cristina Fernandez Kirchner.

Naye Salma Kikwete na Rahma al-Kharoos bi. mdogo wa Kikwete nao hawajaachwa nyuma tokana na kuwa na mashirika na biashara zao zilizotundikwa nyuma ya mgongo wa ikulu. Salma ni rais wa WAMA. Na Rahma ni rais wa kampuni ya mafuta ya RBP OIL & INDUSTRIAL TECHNOLOGY (T) LIMITED.

Salma alirithi uroho na upogo huu toka kwa Anna Mkapa ambaye aliutumia utawala wa mumewe kufanya kama Leila yaani kuneemesha ndugu na marafiki zake. Rejea kashfa ya Net Group ambapo mmojawapo wa wakurugenzi wa kampuni iliyoleta kampuni hii toka Afrika kusini kuwa mtoto wa darasa la tano wa kaka yake Anna.
Lucy Kibaki naye si haba. Kufumka kwa kashfa ya mahindi nchini Kenya kulimuacha uchi baada ya kugundua kuwa kumbe ilikuwa biashara zake.
Je wananchi wanapanga kuwafanya nini watawala wanaotawaliwa na wake na vimada wao?

Sunday 16 January 2011

Kombani, Mwema, Nahodha na Werema wanangoja nini?






Katika kile kinachoonekana kuwa mpito wa kupata katiba mpya ya Tanzania, mambo mengi yalitokea.

Baada ya upinzani, asasi zisizo za kiserikali, vyombo vya habari, wanataaluma na watu mashuhuri kuja juu kuwa lazima Tanzania iwe na katiba mpya inayokwenda na wakati, kulitokea mambo na kauli ambavyo usingetegemea.

Aliyefungua pazia la kufanya visivyofanywa wala kupaswa kufanywa naye ni waziri wa sheria na katiba, Celina Kombani. Bila aibu wala kuchelea jinsi mawazo yake yangepokelewa hasa kama mtendaji mkuu anayemwakilisha rais kwenye masuala ya katiba na sheria, Kombani aliamua kujiongelea kizembe kiasi cha kuamsha moto mkali.

Alipoulizwa kuhusu uwezekano wa kuandikwa katiba mpya alisema kuwa haoni sababu jambo ambalo lilichukuliwa kama kutokujua mipaka ya mamlaka yake. Wengi walimshutumu na kumkosoa vya kutosha. Ajabu hakuondoa kauli yake ambaye kimsingi ilipingana na nafasi yake. Wengi walijiuliza mantiki ya kuteuliwa kwake ilhali akionyesha kupwaya kwenye nafasi husika. Wengine walikwenda mbali na kumueleza kama waziri asiye na ujuzi wowote wala kufaa kushika nafasi hii nyeti.

Wa pili kuwasha moto si mwingine bali mwanasheria mkuu wa serikali jaji Fredrick Werema ambaye alitamka kizembe, kama Kombani, alisema kuandikwa katiba mpya mwiko na ruksa kuweka viraka.

Wengi walishangaa sana kuona mtu mwenye taaluma ya sheria na wadhifa wa jaji ukiachia mbali uanasheria mkuu wa serikali kujisemea kama mtu wa mtaani. Hata alipotakiwa kujiuzulu au kuondoa kauli yake, aliporomosha matusi mengine akidai kuwa wanaomtaka ajiuzulu wana mawazo ya kitoto!

Wengi walishindwa kutofautisha utoto wa wanaomtaka atende haki na wake.

Kwa watu wenye nafsi zinazowasuta, Kombani na Werema walipaswa kuwa wamejiuzulu. Kama hili limewashinda kutokana na kutokuwa na moyo huo, inashangaza ni kwanini mamlaka zilizowateua zinaendelea kuwavumilia ilhali umma hauwataki wala kuwaamini tena!

Walioptakiwa wajiuzulu, hawakutoa uzito kwa madai haya kutokana na kujiona kama hawana kosa. Kisheria wana makosa makubwa tu. Kosa lao kubwa ukiachia mbali kuwadharau wananchi, si jingine bali kupingana na rais ambaye ni bosi wao.

Kwani wakati wakisema hakuna haja ya kuwa na katiba mpya, rais Jakaya Kikwete, kwenye hotuba yake ya kuukaribisha mwaka mpya, aliwazodoa kwa kutangaza kuwa lazima kuwepo katiba mpya.

Licha ya kupingana na rais jambo ambalo ni hatari hata kwa serikali, walikiuka kanuni muhimu ya uwajibikaji wa pamoja, yaani collective responsibility. Hali ya kuwa na misimamo tofauti baina yao na bosi wao, inawaondoa kwenye serikali yake waliyoapa kuitii na kuitumikia.

Kama Tanzania ingekuwa na utamaduni wa kuwajibika au kuwajibishana, mwaka huu ungeweka historia katika hili kutokana na watendaji wengi kujiingiza kwenye mvutano na aibu bila msingi wowote.

Mwingine aliyetia fora anayepaswa kuwajibika tena haraka si mwingine bali waziri wa mambo ya ndani Shamsi Vuai Nahodha. Hii ni kutokana na kuruhusu jeshi la polisi kujiingiza kwenye mauaji ya raia waliokuwa wakitimiza haki yao ya kidemokrasia-kuandamana. Rejea mauaji ya hivi karibuni yaliyofanywa na polisi kule Arusha ambapo watu watu walipoteza maisha na wengine wengi kujeruhiwa pia mali nyingi kuharibiwa.

Huyu sambamba na mkuu wa jeshi la polisi Said Mwema, walipaswa kuachia ngazi usiku wa tukio. Bahati mbaya wanatafuta wa kutwisha mzigo mojawapo wakiwa eti ni askari walioua. Je waliua kwa amri ya nani kama siyo hawa wakubwa wawili? Pia ukiangalia hata jinsi wanavyoshughulikia kadhia hii kwa kutaka mkutano na viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) utaona jinsi wanavyojifunga moja kwa moja.

Hawa walijiruhusu kufanya maamuzi bila kufikiri na kufikiri baada ya kutokea maafa. Wengi wanajiuliza mantiki ya kuwa na mkutano na CHADEMA baada, na si kabla, ya mauaji haya ya kinyama.

Kinachosikitisha na kukera zaidi ni ile hali ya kupendekeza mkutano wa 'kuweka mambo sawa' ilhali walishindwa hata kuyalaani mauaji yenyewe. Hapa, kimsingi, kinachotakiwa si kukaa pamoja bali kuwajibika kwa kuachia ngazi ili watu wengine wenye uwezo na ustaarabu wachukue nafasi na kufanya kazi vilivyo.

Kutokana na uchafu, usugu, upofu, uroho, ubabe na kutojisuta kwa watawala wetu, wahusika wanaweza kuendelea kukaa kwenye ofisi za umma hata kama wameishapoteza udhu, kimsingi wanazidi kujidhalilisha na kumdhalilisha na kumdhalilisha rais kwa kushindwa kutumia madaraka yao vizuri.

Chadema wamefanya jambo la maana kukataa kukaa meza moja na watu waliowanyanyasa kuwaua na kuwadhulumu. Laiti hata wangelaani mauaji ndipo wakafikiria kufanya huo mkutano ambao nao si muhimu zaidi ya kuwajibika.

Hawa wanapaswa kujiuzulu ingawa walikuwa wanatimiza amri ya bosi wao rais Jakaya Kikwete aliyetamka wakati wa mvutano na wafanyakazi na baada ya kudaiwa kuchakachua kura kuwa atalazimika kutumia nguvu ya ziada na watakaoumizwa na polisi wasilaumu. Sasa yake yametimia. Hawa wanaotaka mazungumzo nao si wanapingana na nia na tamko lake?

Wengi wanaendelea kushangaa ujasiri wa wahusika tajwa na bosi wao kushindwa kujiwajibisha au kuwawajibisha wateule wake! Je namna hii tunaweza kusonga mbele kidemokrasia? Je zile tambo za amani na utulivu bado zinaleta maana au uhuni mtupu?

Kwa vile wahusika wamesiliba pamba masikioni, kuna haja ya umma wa watanzania kushinikiza watu wasiofaa kuachia ngazi. Kwani ofisi wanazotukana si mali yao wala baba zao bali watanzania.
Chanzo: Dira ya Mtanzania Januari 17, 2011.

Friday 14 January 2011

Tunisia wamtimua rais fisadi na imla

Ben Ali pichani






Kwa wapenda mageuzi na demokrasia barani Afrika na Dunia kwa ujumla, kilichotokea Tunisia usiku wa kuamkia leo ni ushindi na zawadi ya mwaka mpya. Imla wa nchi ile aliyeitawala kwa zaidi ya miaka 20, Zine al-Abidine Ben Ali alilazimika kuyatema madaraka baada ya waandamanaji kudhoofisha utawala wake nchi nzima.

Baada ya kugundua kuwa maji yamezidi unga na hawezi kushindana na nguvu ya umma, Ben Ali aliamua kutimua mbio akikasimu madaraka ya rais kwa waziri wake mkuu Mohamed Ghanouchi ambaye amejitangaza kuwa rais wa mpito.
Ghanouchi ametangaza kuwa atakaa madarakani kwa muda huku akishauriana na wadau wote nchini juu ya mpito mzima.

Kosa kubwa alilofanya licha ya ufisadi ni kuamuru polisi kuua waandamanaji waliokuwa wakipinga ufisadi wake. Watu wapatao 23 wanasadikiwa kuuawa na polisi hadi imla huyu akikimbia kuelekea ima Ufaransa ambapo inasemekana amekatazwa kutua au Montreal ambako mkwe wake ana nyumba.

Ukiangalia kilichotokea Tunisia hakina tofauti na kilichopaswa kutokea Tanzania baada ya mauaji ya waandamanaji waliokuwa wakipinga ufisadi. Hili ni somo muhimu kwa watanzania kuwa umma ukishikilia madai yake wezi wanaweza kutimka na familia zao kwenda kuishi ukimbizini bila manjonjo na makandokando ya madaraka.

Rais Barack Obama wa Marekani amewapongeza waandamanaji kwa kuwa na mioyo mikubwa hadi kumtimua huyu mwizi mkubwa. Kwanini watanzania wasiingie tena mitaani kuhakikisha Bwana Dowans son of Kagoda the grandson of EPA anatimka na wezi wenzake?

Maswali muhimu ni je kwanini Tunisia waweze Ivory Coast washindwe? Je wezi na maimla wa kiafrika wamejifunza nini? Je huu ni mwanzo wa mapinduzi matakatifu ya kuondoa watawala wezi, wababaishaji na mafisadi?

Laiti Uganda, Rwanda, Sudan, Tanzania, Zimbabwe, Congo-Brazzaville, DRC, Equatorial Guinea,Ethiopia na kwingineko kwenye watawala madikteta na wezi wangelishika somo hili.

Thursday 13 January 2011

Kikwete kweli msanii na hovyo


Kama kuna watu wanamuuza na kummaliza rais Jakaya Kikwete, licha ya kukosa busara si wengine bali washauri wake. Hivi, kwa mfano, kwenye picha hiyo hapo juu, alishindwa kutumia common sense kujua kuchagua hata aina ya mavazi? Suti na upandaji miti wapi na wapi? Suti na mbolea wapi na wapi? Kwanini anashindwa kutumia common sense jamani?
Hakika waliosema kuwa Kikwete ni msanii hawajakosea kama mambo ndiyo haya.

Leo utamuona akizindua mradi wa mbolea. Baada ya mwezi kila kitu kimeyeyuka kama tofali la barafu. Je mnakumbuka ilivyovumishwa kwa mbwembwe na hoi hoi kuwa Dar itakuwa na usafiri wa uhakika kwa kuzindua mabasi yaendayo kasi?

Hata huyu upuuzi wa Dowans unaolisumbua taifa, nakumbuka. Rais baada ya kutoka Marekani kuitafuta Richmond, bila kufikiri, alilitangazia taifa kuwa mgao wa umeme utakuwa historia asijue utaweka historia ya kumuumbua.


Baada ya kusoma habari hii na kuangalia picha hiyo hapo juu, hebu soma habari hii hapa chini ulinganishe kazi aliyofanya waziri mkuu wa zamani wa Australia ambaye ni waziri wa mambo ya nchi za nje kwa sasa.

Tanzania: Peace and Tranquillity Elusive



What transpired in Tanzania on 5th January tells it all. The ‘Peace-and-tranquillity’ mantra that rulers have always sold is no more. It was reported that three people were killed by police when they were quashing a peaceful demonstration orchestrated by Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) in the northern city of Arusha. Many other people were injured and some property set ablaze in this chaos. Unconfirmed reports have it that one policeman was killed and other three seriously injured.

CHADEMA wanted to demonstrate to force the government of Tanzania to stop paying Tshs 185,000,000,000 to an all-dubious company known as Dowans that is linked to the bigwigs in the regime. Apart from pressurizing the government it sees as nasty and corrupt, CHADEMA too wanted the authorities to divulge the owners of the said company.

The government in Dar es Salaam was not happy with this. Things took a deep plunge into anarchy after CHADEMA secretary General who, too, was a presidential candidate openly alleged that president Jakaya Kikwete and his cabal were behind this scam. This peppered the situation. Prior to staging peaceful demonstration, authorities had given green light to it. But after this formal statement implicating the head of state was out, abruptly, the IGP cancelled the demonstration citing that it would breach peace.

The bone of all these killings and subjugation is stinking corruption sorrounding Dowans –the company that sued the Tanzania National Electrical Supply Company (TANESCO) to the International arbitration court that ordered the government to pay this huge amount thanks to breaching the contract. This company is said to have been formed by influential politicians to act as the conduit by which to siphon money from the public coffers. And mind you, this is not the first mega scandal in the country.

In 2005 shortly before the elections, over Tsh 155,000,000,000 was stolen from the Central Bank under the External Payment Arrears (EPA) account. Thanks to the opposition's eagle eye, it unearthed the scandal and came out with findings that stunned the nation. The opposition still maintain that the loot was used to finance Kikwete's campaigns. Neither Kikwete, his government nor his party has ever gainsaid these damning allegations. This for general public was taken as sign of admission of the alleged crime.

Going back to Dowans, this company landed a deal of providing emergency power after another bogus company known as Richmond was booted out. This company brought a lot of problems to the government. For it was unveiled that it was bogus and on top of this, it was favoured by top officials including Kikwete. When CHADEMA brought this scandal to light, the parliament formed a select committee that vindicated the opposition. In its findings, the select committee, thanks to be formed by the parliament controlled by ruling Chama Cha Mapinduzi, came out with its verdict. If it were not for technical know who and other manipulation, its was to show the whole government the door. To avoid this, former Prime Minister Edward Lowassa who also is an ally to Kikwete was sacrificed to save the government of his friend.

Many Tanzanians goofed. They wrongly thought that this would be a lesson to Kikwete and his consgliore. But nay. He needed more money. This, they say, forced him to bring Dowans to take over from such proved-to-be-an-illegal-and-bogus company. Thus, Dowans is Richmond if not a prolongation of this conspiracy.

The rumour mill in Dar has it that the said amount that the government easily agreed to pay to Dowans goes to top government officials or reimburses those that rendered financial supports to Kikwete during his comeback heated campaigns. Among much trumpeted to be behind all this apart from Kikwete are Rostam Aziz, Edward Lowassa, Peter Noni and Andrew Chenge (former AG). This is the same gang of politicos that is alleged to be behind all mega billions scandal in the country.

Tanzanians used to be cowered whenever they raised their tails. Peace and tranquillity were two wands CCM has always used to fool them. Now that they recently took to the street so as to send the message, what will rulers do?

To add salt to injuries, the same CHADEMA is agitating for the 'true new constitution' even after Kikwete promised the same. They are saying clearly that they don't want a president or hoity toity made constitution but hoi polloi made one. This is the crossroad Tanzania is currently at as it hangs off the cliff. Will it triumph or go down just like others who tries corruption as means of ruling? Time will tell.

Source: The AFrican Executive Magazine Jan. 12, 2011.

Wamiliki wa Dowans wanafahamika

KWA MUDA mrefu sasa, jamii na vyombo vya habari vimekuwa vinashinikiza serikali imtaje mmiliki au wamilki wa kampuni ya Dowans ambayo ilishinda kesi hivi karibuni dhidi ya serikali na kuamriwa ilipwe Sh. Bilioni 185.

Kwanza, hiki ni kiwango kikubwa cha pesa hasa kwa nchi maskini, ombaomba na tegemezi kama yetu. Pia ni kwa ukubwa wake, kiwango hiki, kwa akili za kawaida, hakipaswi kulipwa bila maelezo.

Tunataka tujue tunamlipa nani. Nitashangaa kama wafadhili hawatapiga kelele au hata kusitisha misaada na michango yao kwa serikali isiyojali pesa ya umma. Vinginevyo nao wawe na faida na chumo hili la wizi.

Pili, kwa namna serikali ilivyojiandaa kulipa pesa hii, si bure. Kuna dalili zote kwamba kuna mkono mtu au watu, tena wakubwa.

Je, hii iliandaliwa wakati wa kufunga mkataba, huku wahusika wakijua mwisho wa siku watashinda kiulaini kutokana na kufanya makosa ya kisheria kwa makusudi?

Nitoe mfano. Kama wewe ni hakimu ama uliyekula rushwa au kuwa na maslahi na kesi iliyo mbele yako na unataka kumsaidia mshitakiwa, unaweza kufanya makosa ya kisheria ili akikata rufaa ashinde kesi.

Unaweza kumfunga kifungo kikubwa kuliko kinachotamkwa na sheria au kupuuzia baadhi ya masuala muhimu katika kufikia hukumu.

Hivyo basi, ieleweke kuwa walioingia mkataba na Dowans walijenga mazingira ya kuweza kushinda kesi kupitia kuvunjwa mkataba. Na hii yaweza kuwa mojawapo ya sababu zilizopelekea mkataba husika kukatizwa siku 90 kabla ya mwisho wake.

Hii haihitaji kujua sheria. Kwanini wavumilie muda wote walipotekeleza mkataba, halafu wauvunje siku chache kabla ya kufikia mwisho wake?

Je, kwanini mkataba wa Dowans ulikatishwa kabla ya siku 90? Na aliyefanya uzembe huu atachukuliwa hatua gani? Je, Dowans ni nani na mali ya nani?

Je, ilikuwaje Dowans kupata uhalali wa haraka kuchukua kazi ya kampuni ambayo ilitimuliwa kutokana na kuwa ya kitapeli?

Haya ni baadhi ya maswali ambayo umma unajiuliza, ingawa serikali haitaki kuyatolea majibu zaidi ya kuwashawishi wakubali kuingizwa mkenge; kuibiwa mabilioni ya shilingi kulipa kampuni yenye kila alama ya utata ukiachia mbali mtangulizi wake.

Je, Dowans si Richmond? Kwanini serikali haitaki kushughulikia maswali rahisi lakini muhimu kama haya na badala yake inakurupukia kulipa pesa ya umma kwenye dili zenye kila aina ya dalili za ufisadi na ujambazi?

Je, serikali ya namna hii itatuvusha kweli? Richmond walikuja wakachota. RITES nao walikuja wakachota. Na sasa Dowans ikiwakilisha mama yake Richmond inachota kwa mara nyingine. Hii imekuwa nchi ya matapeli na mafisadi kujichotea ilhali umaskini unazidi kuongeza makali yake?

Je, ni kweli kuwa wamilki wa Dowans, kama Kagoda, hawajulikani? Tutawapa mbinu rahisi ya kuwajua.

Ili kuwajua, waweza kuwauliza waliowaingiza hadi kuwawajibikia. Mmojawapo wa watu wanaoweza kutusaidia ni Edward Lowassa.

Kwa mujibu wa ripoti ya Kamati Teule ya Bunge iliyoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe, Lowassa aliibeba saba Richmond (akiwa waziri mkuu), na taarifa zinasema alipofika mahali akaona mambo yangekuwa mabaya kwa serikali na wahusika wengine, akaamuru ifukuzwe; akakataliwa.

Na kwa kuwa tunajua kuwa Richmond ilijivua mzigo na kuuvalisha kwa Dowans, serikali itakuwa inalinda siri za Dowans kama itasema kwamba haijui Dowans ni nani.

Ajabu ni kwamba serikali hii hii inayoficha kuwataja wamilki wa Dowans, bila aibu, inataka kuwalipa Dowans hao hao fedha ya umma!

Kama Lowassa atasema hajui kitu kuhusu Dowans, kitu ambacho hawezi kufanya, basi waulizwe waliosaini mikataba ya Dowans. Katika hili, ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali haina ujanja.

Kama na hawa nao watasema hawajui kitu, basi benki zilizowadhamini ziulizwe, ingawa zitasema hili si jukumu lake. Kama benki zitakataa, basi rais aulizwe kwani serikali yake ndiyo ilisaini mkataba na Dowans.

Ikishindikana, basi umma uamue kuiwajibisha serikali; maana pesa inayolengwa kulipwa si ya wamangimeza hawa wanaokataa kuwataja watu wao.

Haiingii akilini. Iwe serikali au mtu binafsi, huwezi kuingia mkataba na mtu usiyemjua au asiyejulikana. Kwenye sheria za mikataba hili ni jambo la lazima, na lisipotimizwa mkataba huwa batili.

Wanaogopa nini na kwanini? Kimsingi, serikali inajua wamiliki wa Dowans, bali inaogopa ucahfu wa kile ilichokifanya na Dowans.

Kama Dowans ni “mtoto” wa Richmond tunayoijua, maana yake ni kwamba serikali yetu si makini au ina ushirika na mafisadi.

Je, haya yanathibitisha madai ya muda mrefu kuwa serikali ya awamu ya nne iliingia madarakani kwa mtaji wa fedha za ufisadi wa EPA, madai ambayo hayajawahi kukanushwa kikamilifu?

Nani yuko tayari, kwa mfano, kutoa maelezo ya CCM ilikopata mabilioni yaliyoingizwa kwenye uchaguzi uliopita? Jikumbushe fulana, mabango, khanga, kapero na upuuzi mwingine uliosambazwa nchi nzima, bila kusahau msururu wa helikopta za mgombea urais, ndege za serikali na za kukodisha.

Je, upenyo huu unaweza kutuelekeza na kutafsiri maana ya serikali kutaka kuilipa Dowans kirahisi?


Tuhitimishe kwa kusisitiza kuwa wamilki wa Dowans wanajulikana ila kinachogomba ni washirika wao waliomo serikalini kuogopa sura zao halisi katika ufisadi kujulikana.

Mficha maradhi kilio humfichua. Kuna siku watajulikana na kuaibika, ukiachia mbali kuadhibiwa hasa ikizingatiwa kuwa mamlaka yana mwisho.

Tuwakumbushe. Rais mstaafu Benjamin Mkapa alifanikiwa kuficha kashfa yake ya Kiwira. Alipoondoka madarakani ilifichuka na akaaibika. Analindwa tu na rais aliye madarakani.

Je, serikali inayojidai ni ya wananchi inawaficha wananchi shughuli zake ili iweje? Je, na wananchi wataendelea kugeuzwa majuha na kuibiwa kila uchao wasichukue hatua?

Tufanye kila liwezekanalo, serikali iwataje wamiliki wa Dowans na isipofanya hivyo tugomee pesa yetu kuibwa mchana kweupe.

Chanzo: MWANAhalisi Januari 12, 2011.

Kijiwe chatoa medali za mwaka 2010

KWA heshima na taadhima, nichukue fursa hii kuwafahamisha wasomaji wa safu hii ya muda mrefu kuwa, kwa niaba ya Kijiwe, tunatoa medali kwa watendaji wa serikali, watu binafsi na mashirika walioonyesha utendaji uliotukuka mwaka uliopita na kabla ya hapo.

Tulitaka kutoa medali hizi mwaka 2008 wakati shujaa Eddy Ewassa, waziri mkubwa aliyetimuliwa... sorry... aliyejitoa mhanga kwa ajili ya kuokoa siri-kali lakini hatukuwa na uwezo.

Tulitambua mchango wake katika kuleta mvua na umeme nchini. Tulitambua juhudi zake za kukuza uchumi kupitia uwekezaji ambao wengi hawakuuelewa hadi Dowans ilipojishindia kesi ya kitita cha shilingi 185,000,000,000 bila jasho. Hii ni sayansi ya hali ya juu inayopaswa kufundishwa mashuleni.

Pia Ewassa alililetea heshima taifa letu kwa kuliondolea aibu ambayo ingelikumba kama sirikali nzima ingetimuliwa na kufumka.

Tulijiwekea mikakati na maazimio kuwa miaka miwili baadaye tufanye hivyo. Sasa kwa heshima na utii wa hali ya juu, ninayo furaha, kama mwenyekiti wa Kijiwe, kuwataarifuni wapenzi wote kuwa mwaka huu tumetimiza ahadi yetu.

Sisi si wasanii wala wabangaizaji. Tukisema humaanisha tunachosema kama ambavyo tumekuwa tukifanya kile tusemacho.

Bila kupoteza muda, kwa niaba ya Kijiwe kitukufu ambacho kimsingi ni serikali na nchi mbadala napenda niwaleteeni washindi wa tuzo ya juu sana ya Kijiwe iitwayo The Buring Spirit of the Nation au BSN.

Hii ni tuzo ya kijiwe daraja la kwanza ambayo haijawahi kutolewa kwa yoyote na kama ingetolewa basi ingekwenda kwa mashujaa wa bara hili ambao hawakutambulika kama vile Mfalme wa Jean-Bedel Bokassa, Idd Amin, Sani Abacha na Mobutu Sese Seko kutokana na uzalendo wao kwa bara letu. Kwa vile waliishakufa, hatutawapa. The dead tell no tales.

Waliofuzu kupewa tuzo hii ya juu sana ya heshima ya BSN mbali na Ewassa ni mkuu Njaa Kaya ambaye ametimiza ahadi zake zote na kuwapeleka walevi Kanani tena kwa muda mfupi.

Ameahidi katiba mpya na kufanya walevi wafurahi. Hata isipopatikana. Maana kwao ahadi inatosha kutokana na ulevi wao wa milele.

Najua wapuuzi watabisha. Hivi kama hakukuza uchumi, jiulize. Hii pesa yote iliyotumika kwenye kampeni hadi kukodi madege na mahelikopta tena kusafirisha wana ukoo na familia kwenda kwenye kampeni wangeipata wapi?

Pia rejea serikali kuwa na pesa nyingi hadi kuweza kutoa shilingi 185,000,000,000 tena bila kujihangaisha na kukata rufaa. Kuna neema zaidi ya hii jamani?

Hapa lazima nisisitize. Sisi siyo kama wale matapeli wanaotoa shahada za udaktari ili wawatumie wahusika kufanikisha ulaji wao.

Sisi si kama wale watabiri, wachungaji, mashehe na manyang'au uchwara na wezi wanaoabudia cheo, ukuu, utukufu, kufu na mambo ya kipuuzi. Sisi hatujipendekezi zaidi ya kuwa wazalendo wa kweli.

Mwingine aliyepitishwa kupata tuzo hii ni Benny Makapu Tunituni kutokana mchango wake katika kuelimisha umma juu ya ujasiriamali. Rejea kujitwalia na kuendeleza mgodi wa Kiwira.

Anayefuatia ni Mgosi Joseph Makambale ambaye aliweka rekodi ya kuwapayukia wapingaji hasa wale wanaodai tuandike katiba mpya wakati hii iliyopo inalinda ulaji wetu.

Pia Riz Kitweke ametunukiwa tuzo hili kutokana na mchango wake wa kumsaidia mzazi wake kiasi cha kuonyesha ukomavu wa kuweza hata kumrithi.

Sambamba naye ni Roasttamu Laziz ambaye alisimamia makampuni mengi ya uwekezaji yaliyoliingizia taifa faida kubwa hasa kuwezesha kiama kushinda kwa kishindo.

Petero No-nii hakusahaulika hasa mchango wake wa kubuni mpango endelevu maarufu kama EPA au Empowering the Party on Agenda (hidden one).

Salima na Rahama Njaa nao walionyesha ukomavu katika matumizi ya majukwaa wakati wa kampeni. Nao wametunikiwa tuzo hii ya juu sana.

Bila Ninrod M-hand kupewa tuzo hii ingekosa maana. Mchango wake katika EPA hauna kifani. Did-us Masamburiri, Makorongo Muhanga, Emmy Nchimvi na Samuel Chitaahira hawakusahaulika kutokana na ubunifu wao katika kukuza taaluma na kudhibiti uhalali wa vyeti vya kitaaluma.

Annae Makidamakida anapewa tuzo hii kutokana na kutumiwa vizuri kuwakomesha wakorofi waliotaka kuingilia ulaji wetu kwa kimbelembele walichokiita viwango.

Genero Hamnaamani Shimbombo anapewa tuzo kutokana na kuwatisha wakorofi waliotaka kutuzuia kuula.

Orodha haiwezi kukamilika bila kumtaja Shehena Ubwabwa Njaa Yahya Hossein kwa kuwatisha pia wakorofi akiwafunga kamba na kuwatabiria maafa na maanguko kabla ya kuchakachuka.

Lewisi Ukame na Rajab-abu Kiravuitu wanatunukiwa tuzo hii kutokana na kuwezesha uchakachuaji ambao ulizalisha kura nyingi kiasi cha kutokuwa na mambo ya mseto ambao mara nyingi ni uchuro.

Wa mwisho katika category ya watu binafsi ni Nshomile Rweye-pendekeza-'mu ambaye amefanikiwa kutumia taaluma ya uandishi wa habari kuwa uhandisi wa habari hata kama wengi wanasema ni za uongo na kujipendekeza kama jina lake.

Kwa upande wa makampuni na mashirika, tuzo hii haiwezi kukamilika bila kampuni ya Richmonduli kupata. Hawa walikuja na ubunifu wa hali ya juu. Waliweza kujipenyeza na kuzoa tenda kiasi cha watu wenye roho mbaya kuwazushia kuwa walikuwa feki. Kama walikuwa feki waliingiaje? Je, hapa feki ni Richmonduli au walioiingiza?

Kampuni nyingine ni binti Dowans bin Richmonduli. Hii imechaguliwa kutokana uwezo wake mkubwa wa kutunza siri. Kushindwa kujulikana wamilki wake kumekiacha kijiwe hoi kiasi cha kuamua kuwapa tuzo hii.

Kampuni nyingine zilizotunikuwa tuzo hii ni Kagodoka, ambayo sawa na Dowans, imefanikiwa kutunza siri ya wamilki wake. Pia kampuni ya Mageresi Chembazi imepata tuzo kutokana na kusimamia vizuri mradi wa EPA.

Makofi milioni moja toka kwa walevi kwenda kwa washindi.

Kwa vile sasa katiba mpya imegeuka gea ya kuwaliza tena walevi, acha niishie haraka kwenda kuandika katiba mpya ya familia yangu ili kuhalalisha ubaradhuli wangu. Mke na watoto wangu wakae mkao wa kuliwa. Hakuna cha katiba mpya bali sanaa. Naona minjago inakuja wasije wakani Arusha.

Chanzo: Tanzania Daima Januari 12, 2011.

Saturday 8 January 2011

Welcome South Sudan, then Darfur




South Sudan's seceding is more a fact that a thought. It is unstoppable. Come January 9th, southerners, as they've already indicated, will vote for freedom. Yeah. Freedom. Everybody wants to be free and, of course, everybody deserves to be free. Freedom means, among other things, honour, sense of belonging and deciding one's destiny.

This being the truth, what will north do? It must be noted. Northern Africans calling themselves Arabs or Jallaba , for long, have enslaved, killed, robbed, raped and subjugated southerners. In doing this, they forgot one cardinal thing: all goodies they thought are God given come from south. Look at oil, farm produce, water, pastures for their animals and what not.

Though in the beginning northerners rebuffed the idea of independence of southern Sudan, now that it is the fact, it is time for them to lick their wounds.

Notorious and obnoxious north has always been, it is time for it to behave well. For even Arabs who used to brainwash and use them will go where yum yum is- south.

We're encouraged by the stance taken by Sudanese dictator Omar Bashir shall he live up to his promise of honouring the verdict of the people in the coming referendum.

To us, freedom of South Sudan is the stepping stone for the freedom of Abyei, Nuba Mountains and Darfur. What agonize to the bone is what BBC recently reported, if it is true, that Southern Sudanese new regime promised Bashir not to support Darfur rebels. This is tarnishing the good name and promise this 54the new nation has. If other countries supported and helped SPLA what is wrong with helping Dafuris? Is this better than thou or reporting out of context?

Obviously, some can assert that when SPLA was fighting Khartoum, Darfur was in bed with Bashir thanks to his propagation of Islam. They, so too, goofed. They need to be forgiven.

I vividly remember the words of the late John Garang de Mabior as if he said them just yesterday . He was addressing the war prisoners from north and some government soldiers from Darfur.

He told them that what they are fighting for was not Islam but criminality dressed in the good suit of Islam. He went further as saying that once north is done with SPLA would turn to Darfur thanks to being regarded as slave simply because they don't identify themselves with Arab.

And indeed, this messianic prophecy was fully fulfilled even before his demise. For after signing the CPA, Khartoum turned to Darfur with new vim and zeal. To cut a long story short,what followed is history.

After all, Khartoum has always supported anti-SPLA elements to see to it that south does nary go solo. What's wrong with supporting Darfur?

We understand. Salva Kiir Mayardit and south Sudanese are mature and brave people. Being that is not the end in itself. They need others especially east Africa and other Sudanese states under siege.

So too, they need to abide by the law of reciprocity whereas they are duty bound to help their brethren in Darfur. Their enemy is one and the same. They all suffer the same anathema thanks to being black not a bit lighter like those Arab-duped northerners.

If, indeed, it is true that GOSS intends to expel Darfur fighters, this will indeed defeat its zeal of being an ideal new nation.

We urge south Sudanese not to tarnish their good image. In Africa we have a great saying that when you come across the stick that was used to whack your colleague you burn it. In this case the adage tells it all. Don't entertain or spare the stick that whacked your friend or neighbour as it has been the case in Sudan.

Look at the accompanying map and decide where real life lies. North needs south more than south needs north. So whatever north is promising not just because it is willingly. It is just because it has no way.

Source: Afro Spear Think Tank Jan. 8, 2011.