The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Wednesday, 25 June 2025

Tunaongopa, tunaongopewa, na kuongopeana

Kuna mambo yanachusha, kukera, kutisha, kukatisha tamaa, na kusikitisha ingawa mafyatu hawatishiki japo watishwa. Tuweke sawa. Leo, nitafyatua baadhi ya mambo tufanyayo au kufanyiwa mafyatu. Mafyatu gani wasiofyatuka wakafyatua wanaowafyatua tena kirejareja kama ufjujaji na upigaje wa njuluku ndefu? Hatufyati tunapopaswa kufyatuka tukafyatua? Kuna mambo yanapaswa kudurusiwa kwa utuo ili yafanyiwe kazi lau mafyatu wanusurike na dhambi ya kujifyatua na kufyatuliwa. Je uliwahi kujiuliza kwanini tunacheka tupaswapo kununa? Je huku si kufurahia mauti yetu ya kujitakia? Je hayapo?
                 Je hatuongopi hata kuongopewa au kujiongopea tunapopaswa kusema na kuambwa ukweli? Wakweli wanachukiwa ilhali waongo wakipendwa. Wasafi wanachukiwa ilhali wachafu wakipendwa. Ni mapenzi gani haya ya hasara? Tunasifu tupaswapo kulaumu. Hatuishii hapo. Tunafurahi tunapopaswa kuchukia. Tunacheka, na kukenua, tupaswapo kununa na kulia. Tunakaa kimya tunapopaswa kupayuka. Kwanini tusifyatuliwe? Tunafyata badala ya kufyatuka! Halafu tukifyatuliwa, tunalalamika. Usipofyatuka ukafyatua, utafyatuliwa kuufyata kama si kufyata mkia. Kwa Kisambaa, huitwa the law of nature au kanuni asilia. Kazi mbi si mchezo mwema. Mjue.
                    Jiulize. Hatukubali tunapopaswa kutaa? Hatuungi mkono tupaswapo kupinga? Unapata unachotoa na kutoa unachopata. Ukipanda mbigiri, hutovuna mbirimbi. Hatupwakii tunapopaswa kususa na kutapika? Kwani, hayapo? Tunapopaswa kupoka haki, tunaiomba! Nani kakudanganya kuamini kuwa haki inaombwa na siyo kupokwa? Haki haiwezi kuwa hisani wala hisani kuwa haki. Uongo tumegeuza ukweli. Ujinga tumegeuza ujuzi. Tunaishi kwa fadhila badala ya haki. Tunaficha na kufichwa tunapopaswa kuweka wazi! Unafiki unatawala pahitajikapo kusema wazi.
Tunaogopa tunapopaswa kupambana. Tunakuwa wapole tupaswapo kuwa wakali. Tunadanganywa hadi tunajidanganya na kudanganyika mbali na kudanganyana! Je tunamdaganya nani wakati wahanga ni sisi na vizazi vyetu? Waweza kufua nguo au kuoga kwa maji machafu ukawa safi? Hamjaambwa kuwa ukiwachekea gendaeka, utavuna mabua?  Utamlaumu nani? Wangapi wanalala njaa lakini wanajiaminisha wameshiba? Wezi wanaitwa waheshimiwa ilhali watenda haki wakiitwa wanoko! Hamjayaona haya? 
            Dhuluma imegeuzwa haki. Nani hajui? Si wanasema ujanja kupata na siyo namna ulivyopata? Wangapi wanalala maskini na kuamka wakwasi huku tukiwashobokea tukiomba watuwezesha? Tuna tofauti gani na kuku hayawani aliwashaye mabaki ya mayai yake asihoji? Heri kuku ni hayawani kuliko mafyatu ambao ni waja. Kiza tunaita mwanga na mwanga kiza! Tunasema ni sawa wakati si sawa! Sawa vipi wakati mambo hayaendi sawa sawa? Penye usawa, tunabaguana. Je hatuibiani na hatubaguani kwa dini? Roho mtakatifu amekuwa roho mtakakitu na madhehebu yamegeuka maduka ya kuuza roho kwa uroho wa utajiri. 
        Ajabu, hatuwi wawazi, kusema, na kukemea! Mali ya umma inageuzwa ya wachache na wengi wanapigwa ganzi kuwa hii ni haki! Haki gani isiyo na usawa?
            Inatisha. Inaogopesha. Maskini anaitwa mwenye mali wakati yu hoi na hohehahe! Inawezekanaje fisi na mbwa wakalinda nyama au majambazi na wezi kulinda benki? Je hiki si chanzo cha ukapuku wetu? Wenye nguvu wanakula kwanza na kusaza ilhali wanyonge wakinyong’onyea hata kunyongwa na shida! Wapo wasemao eti ni haki na sawa! Kivipi? Haki vipi wakati ni dhuluma? Kwanini nisiogope na kusikitika? Je hili ni jibu au kufyatua? Heri nafyatua ili mfyatuke mfyatue, na ikibidi, tufyatuane kieleweke. Huwezi kuitwa mwenye mali wakati mali yenyewe huioni zaidi ya takwimu. Huwezi kuambwa kaya ni yako wakati ni yao. Kama ni yako, yao ni ipi, na kama ni yao, yako ni ipi? Haya ndiyo matokeo yangu kuwa fyatu mfyatuzi asiyeogopa kufyatua ili asifyatuliwe.
                Nani ataishi milele huyu mjanja tumuone? Je tumewaona wangapi wenye vifua kama ninga waliofyatuka wakaacha kila kitu wakatokomea kwenye kaburi la sahau? Mfalme aweza kuwa mfalme bila watawaliwa? Je wawili hawa nani anamhitaji au kumtegemea nani? Mbona faru na nyati huishi bila malkia wala mfalme? Nani mfalme wa ndege, viumbe huru waendao watakapo na kula watakacho japo hawazalishi? Farasi na ampandaye nani umhitaji na kumtegemea nani? Je farasi akibwaga mzigo ataumia au kupata nafuu? Mwoga na mpumbavu huogopa kifo na kuishia kufa. Si heri kupambana na adui ukafa kuliko kumuacha akudhalilishe? Heri kufa umesimama kuliko kuishi umepiga magoti. 
        Je kifo siyo faradhi? Fisi na simba hula wenzao. Je, hawauawi na kuliwa na wadudu wadogo? Tembo ana maguvu sana. Aweza kuangusha magogo kwa mamia. Je aweza kuwatisha nyuki? Pamoja na ukubwa wake, tembo huwaheshimu nyuki. Pamoja na udogo wao, koyokoyo humuua nyoka mwenye sumu kali. Je yupi bora kati ya nyoka na koyokoyo? Heri kibogoyo mwenye nyama kuliko mwenye meno asiye na nyama. Mwenye njaa asiye na chakula ni bora kuliko mgonjwa asiyeweza kula lakini akajaza chakula. Wangapi wana hamu ya kula na hawana chakula na wenye chakula hawana hamu ya kula?
            Leo, sifyatuki sana. Wala sifyati bali kuwaadhi. Hivi ni mchana au usiku?
Chanzo: Mwananchi leo.

Tuesday, 24 June 2025

Kama wakwezo wanga na wazazi wako ni wanga

Ni mara ngapi umesikia malalamiko na tuhuma za uchawi katika baadhi ya familia za wanandoa wawe wanaokuhusu au kutokuhusu? Je huwa unajisikiaje na kuelewaje? Si jambo jipya kusikia fulani akilalamika kuwa wakwe zake ni wanga. Mara nyingi, malalamiko haya hutolewa na wakamwana wanaposhindwa kuelewana na mama wakwe hata baba wake zao. Je malalamiko haya yana ukweli au ni ya kupuuza? Je ni ya kuchukulia kwa makini? Je huo wanga upo kweli au ni matokeo ya ukosefu wa sababu za msingi za kuelekea na kutatua tatizo? Je yakikuta wewe au ndugu hata rafiki, utachukua hatua gani mujarabu?

 Katika tuhuma za ‘wanga’, wengi wa watuhumiwa, au tuseme waathirika, ni mama wakwe. Baba wakwe, mara nyingi, huingizwa kwa kuunganishwa na wake zao ndipo wawe ‘wanga.’ Hata kwenye tuhuma za uchawi nje ya wanandoa, mara nyingi, wengi ni wanawake na si wanaume. Tunadhani hii ni tokana na ukaribu wa wakazamwana na mama wakwe zao. Pia, inaweza kutokana na ukweli kuwa, mara nyingi, watoto huwa karibu na mama zao kuliko baba zao japo si wote. Sababu nyingine inaweza kuwa mfumo dume unaowadhalilisha wanawake na kuwatwisha kila lawama na mizigo ya kijamii.

          Hata hivyo, wakati tukidurusu na kutafakari dhana nzima ya wanga, tujiulize maswali kadhaa:

          Je kweli wakwe wanaotuhumiwa ni wanga kweli au mwanga ni yule anayewatuhumu? Je wanga unaweza kuthibitishwa kisayansi? Kisheria, tunajua wazi, wanga hauwezi kuthibitishwa. Ni matokeo ya ujinga na imani za hovyo. Je ni kweli wanga upo na wahusika wanaufanya? Ili iweje?

Tukiangalia tuhuma za wanga dhidi ya wake, kuna baadhi ya maswali ya ziada ya kujiuliza. Je ilikuwaje, kama kweli ni wanga, waliweza kumlea huyo mumeo hadi akakua na kukuoa wasimuwangie hata kumua? Je angakuwa mama yako au wazazi wako wote ndiyo wanaotuhumiwa wanga na mwenzi wako ungefanya nini?

Katika kudurusu na kuchunguza dhana hizi za kijinga zitokanazo na chuki na ukosefu wa umakini katika kuendea matatizo, tunapendekeza hatua zifuatazo kuchukuliwa ili kuepusha kusambaratisha ndoa hata jamii.

Mosi, ni vizuri kwa wanandoa kujielimisha juu ya dhana nzima ya uwanga na sababu za kuwepo kwake ziwe za kweli, uongo, chuki, hata kisayansi. Hii ni kutokana na ukweli kuwa dhana hizi zipo. Hivyo, haziwezi kufumbiwa macho hasa ikizingatiwa kuwa madhara yake huwa mabaya na makubwa.

Pili, wanandoa waepuke chuki na dhana potofu ambazo nazo huchangia sana uwepo wa dhana hizi mbovu. Baya zaidi, wahusika wanaposhindwa kutumia akili kutatua tatizo ambalo laweza kwa chuki binafsi, uchoyo, hata umaskini, hupanua wigo wa tatizo kwa kuhusisha wapiga ramli, wachungaji, na hata mashoga ambao huongeza hatari kwa wanandoa na familia zao.  

        Mfano, muathirika anaweza kwenda kwa mganga wa kienyeji au mchungaji ili kuaguliwa, kuzindikwa, hata kuombewa bila kujua kuwa hao anaowapelekea matatizo yake, wakati mwingine, wanakuwa na matatizo makubwa kuliko yake.

Tatu, jamii inapaswa kuachana na unyanyasaji wa kijinsia ambapo waathirika wakubwa huwa ni wanawake zaidi ya wanaume. Katika utafiti aliofanya Daktari Philippa Carter, mwaka 2023, aligundua kuwa huko Marekani na Uingereza, kulikuwa na visa vya tuhuma za uchawi.                             Watuhumiwa wote walikuwa 802 kulingana na rekodi za mpiga ramli maarufu wa Uingereza Richard Nappier (1559-1 April 1634) na kugundua kuwa kati ya watuhumiwa hao, 500 walikuwa wanawake na wanaume 232 ambapo malalamiko 70 hayakuwa yameorodheshwa. Katika kitabu chake  Malleus Malleficarum (2023), mwandishi Heinrich Kramer alibaini kuwa, kutokana na kuwa hadhi ya chini ikilinganishwa na wanaume, ni chanzo kikubwa cha kutuhumiwa uchawi.

Nne, tunashauri kuwa kabla ya kuwashutumu wengine, jiweke kwenye viatu vyao na kufikiri nje ya boksi. Je utajisikiaje kama wifi yako atawatuhumu wazazi wako kuwa wanga wakati unajua si wanga bali chuki na hila tu? Je utakapozeeka, likikutokea hili, utajisikiaje? Japo hili hulioni, kwa namna ulivyo mnyama, Mungu lazima atakulipa. Kwani malipo ni hapa hapa. Usishangae yakakukuta haya unayowafanyia wenzako tena bila sababu yoyote bali ujinga, roho mbaya, uroho, na kushindwa kufikiri sawa sawa.


Wednesday, 18 June 2025

Mnaringia ‘kiinglish’ are you British or Brutish!!


 Juzi nilishuhudia vita ya kikumbaff na kizwazwa ya mafyatu, au niseme uchangudoa wa kimaadili, ushamba wa kiakili, na ulimbuekeni wa kitabia. Si baada ya mafyatu wa haki za mafyatu kutoka kaya jirani kwenda kusikiliza mtiti wa fyatu mwenzao aliyetaka kukinukisha ili wote wanuke. Walizuiliwa kizembe na kuregeshwa makwao wengine wakiwa hai japo hoi. Kwa sababu wanadai walifanyiwa kitu mbaya bila hata kutoa ushahidi. 

                Acha mafyatu wafyatuane na kuvuana nguo hadharani tena mchana kutwa wakati wenye ngoma yao ni wanene. Badala ya kuwafyatua wanene waliowafyatua wenzao, waliingia ntego na kuanza kufyatuana wenyewe kwa wenyewe. Kwanini mnacheza ngoma ya wengine mkidhani yenu nyambaff wakubwa? Mitusi mizito mizito ilianza kurushwa toka upande zote. Watukufu walitukanwa hadi kikanukishwa kifyatu.

            Nani angeamini kuwa na waishiwa toka pande zote wangetia timu kwenye huu ukumbaff? Walipoteza hata muda wa buge kwa ubugeubuge kama huu! Ukiachia mitusi husika kuhuzunisha na kushangaza, hakuna kilichonishangaza hadi nikaamua kufyatua hili onyo na suto tena kwa Kiswahili japo nshafyatua kwa kiinglish wiki mbili zilizopita. Katika kujitahidi kubagazana na kubaguana, mafyatu wa upande wa pili walishikilia uzwazwa mmoja. 

                Kila wakirusha mikombora ya mitusi, utasikia “nyinyi hamujui kiingeredha.” Kwanza, inshu ilikuwa ni nani anakimanya kibritish au kufyatuliwa haki za binadamu za mafyatu kama kuwekwa tunduni na kupiga persona non grata? Je hii ni nini? Rudi darasani ukasome. Kwa tuliowahi kuishi Kenya, wanaowatuhumu wenzao kutokijua kimombo aka kithungu au kithunguri, wao ndiyo usiseme. Hawakijui wala Kiswahili.

  Hapa naongea na akina Kariuki wa Muriuki au mfufuka aka Karish, Njoroge aka Njoro, Shiko, Waruguru, Khalwale, Awori, Sifuna, Wanyonyi, Ocholla, Omoro, Amoro, Maboi, na wengine wengi. Mwenzenu niliishi maeneo ya Valley Arcade kule Lavington kwa wanene. Hivyo, nawajua kuliko hata mnavyowajua wabongo wenzangu.

            Namaanisha akina Onyango Oburu wajiitao Mc Onyango. Hata mujiite Mac Donald bado ni manugu tu. Wengine wanajiita Doug badala ya Douglas. Si mujiite dog au mbwa ijulikane kama siyo ngui. Kwani nyinyi ni waingereza? Wathunguri au wadhungu wakiwadharau mnalaumu. Basi, badilisheni rangi muwe hao wathunguri. 

                Mbona kama ni kiingirish ni mali mbona mwapeleka vitegemezi vyenu kwa Bro M7 na kitegemezi chake the Avenger aka Muhoooooziiii kohooziiiii ziii? Sijui kama na waiingilish wanajivunia Kijaluo, Kikikuyu hata Kikamba ya kana ka mkamba wa Kaneza, Wamuseto na Wakaiti. Eti Wabongo hawajui Kiingereza. Kwani, nyinyi ni wabritish. Kama watawaona kama manyani, mtaanza kulalamika eti mnabaguliwa? Kumbe mfalme Charles ana koloni ambalo amelisahau la Black Brits. Great minds speak bout ideas, avarage minds discuss events, and small minds discuss people.

            Tokana na mitusi hiyo hapo juu, sijui uhuru wenu unamaanisha nini hadi mnajisifia kibritish wakati Wainglish wanawaona nyinyi ni brutish tuu tena weusi wanaobaguliwa na hao mabritish mnaowaramba makalio? Mbona hamli vyakula vya kibritish bali kathubu kanini, kamceri, makande, mutula, mukimo, madodo na kadhalika? Kabla ya kusema Wabongo hawajui kimombo, nenda kawasilikize akina Mvaithe. Utasikia fyatu akisema, nthis is nthe mbrother from my nconsitituency.  Ukija kwa akina Njoro, utasikia this is mokey business au idepedece yaani uhuru. Shame on you! It is time to stop self-dressing down now.

Acheni jamani. Wenye akili wanawacheka mnavyopwakia na kujivunia lugha za watu.

            Nilisikia wakidai kuwa Bongo bila Kenya haiwezi kuishi na pia ni maskini wakati ukweli ni tofauti. Mnamaanisha Kenya na Bongo ipi? Mnadhani hao waTZ hawawajui uzuri siyo? Mmenoeni tena sana. Wajua muishivyo kwa shida mazee. Nenda Kibera halafu urudi bongo ulinganishe na sehemu yoyote Uswekani. Wengi huwa tunasema eti Manzese ni uswekeni. Jamanini, nendeni Kawangware au ngwaro, Kibera aka kibra,  Mukuru kwa Njenga (wao husema Jenga), Kiandutu (cha funza), Korogocho, Muthurwa, nk. Msipigwe chenga la mato. Nendeni muone halafu mjue mnatukanwa na mafyatu gani.

                 Uliona wapi Bongo fyatu anapanga nyumba bila choo huku akiambiwa choo siyo sehemu ya nyumba? Je huwa wanafanyaje? Jikumbushe kipindi fulani pale jamaa zetu toka kule gabacho..rii walivyoanza kutumia kitu ambacho kwa wenzetu hujulikana kama flying toilets. Fyatu zima sijui na mke na watoi linajisikia kwenda kutua mzigo, linafungua mfuko wa plastiki na kumalizia mambo humo na kurusha mtaani. Hawa ndiyo wabrutish wetu wanaokimanya kibritish japo siyo wote.

            Sasa jiulize nani kapuku. Mwaka 2023, hao wajivuni walituuzia bidhaa zisozidi dolari milioni 14 wakati sisi tukiwauzia bidhaa zenye thamani ya dolari miloni 178 nyingi zikiwa vyakula wakati wao walituuzia bidhaa za viwandani. Ukienda mbele, wanachoringia kutuzidi GDP, utakuta mali nyingi inamilikiwa na watasha na magabacholi.

             Japo nasi tuna tatizo hilo, tunawazidi kitu kimoja. Hatuna wapangaji vijijini kama hawa jamaa ambao huishi kwenye reserves kama waanimo tena kwenye nyumba za mabati kama magari. Nyani angeona nonihino lake, bila shaka, asingewacheka wenzake. Ni ajabu nyani kumcheka mbuzi ambaye nonihino lake limefunikwa na mkia japo wote ni waanimo. Du! Hii mibangi!

Chanzo: Mwananchi leo.

Wednesday, 11 June 2025

Injili ya Fyatu kwa Mafyatu na maajabu ya Kaya

Katika kufanya utafiti wangu usio rasmi, nimegundua mambo ya ajabu. Naweza kujiita mgunduzi wa karne hii kwenye sayansi ya jamii. Nianze na niliyogundua. 
        Mosi, nimegundua kuwa fyatu anaweza kwenda shule asielimike. Kifyatu, hii inaitwa education for ignorance. Fyatu anaweza kuoga lakini akabaki mchafu achia mbali kutakata.
            Pili, Fyatu anaweza kula kwa miguu na mikono lakini akaishia kuwa na njaa asishibe. Kuna wagonjwa wanaoonekana wazima na wazima wanaoonekana wagonjwa. Kuna wajinga wanaoitwa wasomi na wasomi wanaoitwa wajinga. Usomi na ujinga vinapokosa tofauti, nini faida ya kusoma? Wapo walioelimika bila kusoma kama shehe Karume na waliosoma wasielimike kama maprofesa waliogeuka marais wakaangamiza kaya zao.  Kwani hawapo?
            Tatu, wajinga wanapogeuzwa wasomi na wasomi wajinga, kuna tatizo. Waadilifu wanapochukiwa wakapendwa wabadhilifu, uje kuna tatizo. Maadili yanapogeuzwa madili, jua kuna balaa. Haramu inapogeuzwa halali, unategemea nini? Dini zinapogeuzwa maduka na zana za kutajirika haraka, unategemea nini? Unategemea nini makaburi ya watakatifu yanapotunzwa na walevi na wazinzi?
             Nne, mafyatu wanapoacha kufikiri na kuchapa kazi wakashikilia kuomba na kungoja miujiza, ni nini kama si ajabu la maajabu? Kwani hayapo? Hakuna muujiza kama kuchuuzwa kwa neno la Mungu tena kufanywako na matapeli wa kawaida kwa kutumia ujinga na si weledi. Ni ujinga kiasi gani samaki kufa kwa kiu mtoni? Fyatu zwazwa anakwenda kwa mganga wa kienyeji maskini na mpumbavu kutafuta utajiri. 
        Lo! Kweli nguruwe anaweza kumfunza tausi usafi au mbwa kumfunza mbwa mwitu uhuru? Je nune anaweza kujua siri ya unene japo yu anenepa kwa kuishi kwenye kinyesi? Je kuku anaweza kumfunza uhuru kanga?
            Nyangumi, pamoja na ukubwa na umwamba wake huuawa na pomboo. Simba pamoja na ukali wake hawatishi nyuki. Ni heri kuwa nyuki mbele ya simba kuliko kuwa kondoo mbele ya mchinjaji. Nyoka, pamoja na sumu yake, huwagwaya vicheche. Nyuki, pamoja na ukali wao, hawafui dafu mbele ya nyegere. Je siri ya haya yote ni nini? Ni kujiamini, kujitambua, na umoja. Hii ndiyo injili yangu kwa mafyatu.
         Unaweza kutajirika lakini ukabaki maskini. Unashangaa! Jiulize. Kwanini wapigaji wengi wa mali za mafyatu ni matajiri lakini wasioacha kupiga? Kama siyo umaskini nini kuiba na kusababishia wengine mateso hata vifo kana kwamba hutokufa? Kama unashangaa bado, basi angalia bara la Afrika. Linasifika kwa kuwa na maliasili zenye thamani zinazohitajika na kutegemewa sana duniani. Ajabu, bado ni maskini wa kunuka! 
        Afrika inafyatuliwa ndani na nje huku mafyatu wakiendelea kufyatuliwa na kusota bila sababu yoyote ya msingi isipokuwa kukataa kufyatuka na kuufyata.
            Mafyatu wamegoma kufyatuka na kuuliza maswali ya kifyatu. Mfano, inakuwaje mkurugenzi anayesafiria ndinga la nusu bilioni, kila mwaka, anaripoti hasara? Je hapa mchawi ni biashara kugoma au israfu ya wakuu wa kampuni au shirika kama hili? Tumenunua mapipa, tena mapya, kutoka kila kona. 
        Ajabu ya maajabu, mafyatu wachache tuliowakabithi mashirika kama Eya Danganyika, Shirika la Relwe na mengine mengi yanayosifika kuingiza hasara si faida. Je njuluku inakwenda wapi? Je hii siyo biashara kichaa? Haiwezekani isiwe wakati ni kichaka cha upigaji. Ajabu, wakati haya yakiendelea, tunasifiana kudumisha amani! Amani gani ya imani? Kuna amani gani katikati ya dhuluma, jinai, wizi, uchawa, kujipendekeza, uzembe, ubabaishaji, na mazabe  mengine ya kizwazwa?  Hamjaambwa kuwa mjenga na mbomoa kaya ni mwanakaya mwenyewe?
        Wakati haya yakiendelea, utayasikia mabambataa mabingwa wa kwaya wakisifu hata uchafu. Mengine yamepiga book hadi uprofesa uliogeuka uprofedheha kama si fedheha. Kama kuku, tunazalisha tusichokula na kula tusichozalisha halafu tukiitwa kuku tunaamba twatukanwa! Ebo! Sasa mnataka muitwe nini wakati mfanyacho ni ukuku? 
        Juzi nilimsikia profedheha mmoja chawa na bingwa wa kujikomba akisema eti sisi tunaongoza kwa demokrasia duniani! Dunia gani au ile ya ndoto na mapambio? Tunaongoza vipi wakati fyatu mdogo aliyeteuliwa si kuchaguliwa anaweza kuzuia wapingaji kufanya mikutano yao ya kikatiba? Tunaongoza nini wakati wizi wa kura kwenye uchakachuaji ni sehemu ya maisha?                                 Tunaongoza vipi wakati bado tuna walaji wanaokula mafyatu kwa sababu ya surnames zao? Tunaongoza nini wakati tunajitahidi hata kufunga uhuru wa kufikiri mbali na kuhabarishana? Tuna sharia ngapi za hovyo za kukandamiza vyombo vya umbea? Je hii nayo ni demokrasia au kadhia? Demokrasia gani katika uchakachuaji na ukandamizaji?
            Mwisho, demokrasia ni pamoja na haki na uhuru vya mafyatu. Penye ubangaizaji, usanii, uzembe, upigaji, na ufujaji wa njuluku za mafyatu hapawezi kuwa na demokrasia wala haki. Demokrasia ni kula na kushiba na siyo kumeza mate wakati wachache wakifakamia na kupwakia kwa mikono na miguu. Hii ndiyo injili ya leo kama ilivyoandikwa na mwenye dhambi Daktari, Profesa, Muadhama, Shehe Fyatu Mfyatuzi. Hivi nitaruhusiwa lini toka hospitali ya vichaa?
Chanzo: Mwananchi leo.

Monday, 9 June 2025

Open letter to Kenya


May I, with sadness and shame, pen this letter to Kenya as I try to clear the air? I don’t intend to support or oppose, calm and engage but not to enrage. I seek to educate but not to abuse or debase. May I be the voice of reasoning as I pen this open letter. Contextually, we recently evidenced how blinkered, cantankerous, different, and duplicitous some of us can be as a people and countries. Again, those who forlornly involved themselves in this saga wrongly thought that they represented us. They’re ours and look like us whether we like it or not. Unfortunately, as it is, they’re our collective drawback. Thanks to them, we evidenced uncalled-for volley of abuses, accusations (false and farfetched of course), lies, condemnations, slanders, defamations, and all sorts of horrid and eldritch stuff sent from both sides of a subsequent redundant conflict, namely Kenya and Tanzania in the name of defending themselves. Essentially, after Tanzania expelled some Kenya Human Rights Activists including alas my elder brother and friend Willy Mutunga (PhD)–––who treated me cordially when I lived in Kenya–––many Kenyans, blindly, boorishly, and spitefully fabricated and fanned all sorts of abuses and barbs. 
However, one side, namely Kenya seemed to have won this game of psychotically, self-abuse. Concomitantly, a couple of things attracted my attention, pitched, and stirred me to pen this letter. First, the frivolity of the arguments. Secondly, nauseating systematic self-centeredness and stonewalling. Third, the rashness of the actors on both sides. Fourth, veiled hatred between the two people in question. Fifth, mind-boggling levels of witlessness and even foolhardiness about each other as well.
For example, Kenyans, though not all, accused (and others still do) Tanzanians of not ‘knowing’ or mastering English. Again, do we eat our English? Do Kenyans know English more than others? What should Uganda where many Kenyan pupils are exported to acquire apt education say? How do our ex-colonial masters view us for our craziness and obliviousness besides discriminating against ourselves, our cultures, and languages? Why are Kenyans jutting about English but not Kikuyu, Dholuo, Kamba, Luhya, Kiswahili, and others? What does this speak to? Ironically, generally, Kenyans do neither master English nor Swahili! Is language (colonial and far-off) something for which to waste our time or make us hollowly feel superior or inferior thereof? What does insanity mean if this isn’t? What are practical gains of such barefaced and pointlessly idolised, internalised, and normalised systemic coloniality and idiocy?
If Kenyans know English better and more than others, where do we put British in this psychosis? Ironically, those who fabricated and fanned such humbug don’t know English to well and such a discourse is academically unwholesome. Again, should we be bothered about the outlooks of such ignorant and foolish people who purportedly pretend to represent the two sides? I wouldn’t have wasted my ink and time to pen this letter had our Parliamentarians refrained from and negated to be part of this collective indignity. I heard one Tanzania MP saying that Kenyans have nothing to teach Tanzania. Equally, I heard a Kenyan senator brashly saying that Kenya should enact or put in place unspecified ‘radical’ measures against Tanzania. My doubts and jolt are why our leaders fell into this cheap ensnare? How and what’ll we benefit or gain from this untowardness? Are we such cavalier? 
Again, when I clinically, critically, and honestly look at and remember baffling and engrained snags the two nations face, I feel like puking. Perhaps, I’d honestly admit that I’m witnessing this goony tussle and duel of  the duet. Why Kenyans failed to address and tackle their Gen Z’s abductions about which I’ve already written a book to congratulate them, but still have the guts to holler for the ‘rights’ of Tanzanians? Charity begins at home though. The sage’s it that apes don’t see their nates except those of their colleagues, which are but typical replicas of theirs? Isn’t a sort of mental health challenge to demonise each other? I don’t know.
Thus, then, what should we do? Let us face I t and culpably and collectively say mea culpa, mea culpa, forgive each other, and move on. Let’s also be proud of our cultures and languages as we carefully spurn those of others even if we use them. More importantly, we’re blood kin whom our colonisers divvied and moulded for our perpetual degradation and exploitation. However, it becomes sacrilegious when we voluntarily snig ourselves and each other thinking we may languorously become better than others. Shame on us! Fool me once, shame on me. Fool me twice, shame on me.
Source: The Citizen today.

Thursday, 5 June 2025

Ni marufuku mafyatu kugwijimisha religion na politics


 Baada ya kushuhudia yaliyowakuta wenzetu kwenye kiama twawala, Fyatu Mfyatuzi nimestuka. Lazima nichukue hatua mujarabu bila huruma. Kabla ya zari la mtiti wa fyatu kidhabu kujifyatua na kujifanya akitaka kutumikia mabwana wawili na kujigeuza msemaji wa kiama akafyatua yasiyofyatuliwa, nimejifunza kitu japo mambo ya Ngoswe nawaachia akina Ngoswe. Niligundua kuwa ukiruhusu wachunaji, sorry wachungaji, mashehena, ashakum, mashehe kuwa wanasiasa, unachganya dini na politiki. Hapa, tatizo ni wawili kudhani wanatumiana wasijue watafyatuana tu katika utapeli wa kuuza dhahabu feki na kulipwa fedha feki. Huwezi kuwa popo ukakubaliwa na wanyama au ndege. Hatutaki wala hatutavumilia upopo. Lazima tuwapige kipopo.

        Nadhani wenzangu walifyatuliwa mkenge pale walipozidiwa kete na matapeli wakidhani wanafyatua kumbe wanafyatuliwa. Sasa kimeumana. Wanafyatuana. Yao nawaachia. Nirejee kwa mafyatu wangu. Nataka wasome na kuzingatia haya kwa makini. Wahakikishe wanayakariri kama sala ili wasijenigusa pabaya nikwagwijimi kinomi.

Mosi, kuanzia leo, mie ndiyo msemaji pekee wa Chama chetu cha Mafyatu (CccM). Haiwezekani kila fyatu aamke, tena kutoka usingizini au ulevini uwe wa kanywaji au maulaji, kuitisha press conferences na kunifyatua tena hadharani.

Pili, siyo kila jambo lazima liongelewe na yeyote atakaye na anavyotaka. Na si kila ukweli lazima usemwe. Mwingine unauma na kuudhi. Unaambwa mfalme au malkia kauramba halafu unasema eti yuko uchi. Hata kama yu uchi, inakuhusu nini? Mfano, sisi mafyatu tulishakubaliana na baadhi ya mambo kama vile utekanaji, upotezaji, na unyotoaji wa roho za wale wanaotishia ulaji wetu uanofanywa na wasiojulikana na kifo ni kifo ilmradi kisiniguse mimi na familia na marafiki zangu. Pamoja na kujuwa kuwa wasiojulikana wakajulikana ndiyo watekaji, mnaanza kulaumu laumu tu. Sasa tungekuwa tunawanawajua na wasiojulikana wakajulikana, si wangewakamata na kuwanyongelea mbali. Kuweni na subira. Mngoje wasiojulikana wajulikane, kama kweli hawajulikani na hawatajulikana, wakamatwe tukomeshe huu ukatili, unyama, na uzwazwa.

Tatu, hakuna fyatu anayepaswa kupingana na sera zetu. Wewe nani unayejitia kujuajua na kufyatukafyatuka hadi unapingana na sera yetu? Huwezi kuwa ndani na nje kwa wakati mmoja. Kama unataka kuwa nje, toka nje au nitakutoa nje. Pia, ieleweke, hakuna awazaye kuwa ndani akafyatuka kama wale waliioko nje akabaki ndani. Tutamtoa nje huko tulikomuokota kiwa na tongotongo aendelee kuchonga na kufyatua na kufyatuka atakavyo ilimradi achunge wasiojulikana wasimtembelee akaishia kutojulikana alipo kama Mdunde na wengine. Nkikumbushie kwa mara ya mwisho. Fyatu yeyote atakayetaka kukinukisha ili kutisha ulaji na maagizo yangu, atajilaumu mwenyewe pale wasiojulikana watakapomteka, kumpoteza, au kumnyotoa roho.

Nne, ni marufuku kuchanganya dini na politiki kuanzia sasa. Haiwezekani matapeli fulani wakala kuwili kama ndumilakuwili nasi tukawaacha. Sadaka wale wao na maulaji yetu ya kiunene nayo wafaidi. It can’t be. Kama kunisifusifu, kuniimbia mashairi na pambio ni dili, basi nitatumia umoja wa viyanki wetu kufanya kazi hiyo.

Tano, naonya. Yeyote atakayepimana nguvu nami, namfyatua. Ukiwachekea nyani, utakuvuna mabua. Hatuwezi kukupa ulaji wetu ukaugeuza wako na kula na kushiba, kujisahau na kuanza kututapikia na kufichua mambo yetu tusikufystue. Kuanzia sasa, nabatilisha na kupiga marufuku vyeo vya kujipachika. Kila atakayetaka kuhubiria dini mafyatu wangu, lazima awe na shahada ya dini isiyo ya heshima wala kughushi. Hivyo, vyeo vyote vya kujipachika vitachukuliwa kama jinai ya kawaida inayolenga kujitajirisha kwa kuwachuna mafyatu wetu wenye shida mbalimbali. Pia, nisisitize. Wahusika waabudu, kutumikia, na kutukuza miungu yao. Mie sihitaji hayo yote na wajue. Sina subira kama miungu yao. Ukinichengua, tunachenguana na nakufyatua bila kujali kama madai yako ni ya kweli au uongo. Chonde chonde, msiniguse wala kugusa ulaji wangu.

Sita, kuanzia leo, hakuna gea yoyote itakayokubalika kama vile kuniombea maisha marefu, ushindi kwenye uchakachuaji ujao, na mengine mengi kama kunilinganisha na manabii na mitume. It is too much. Mie si nabii wala mtume bali Daktari, Profesa, Jenero, Field Marshal, Papa, Mtakatifu, Mtukufu, Mwenye maono, Mponyaji, Muota ndoto, Mtabiri, Alhaji, Mhashamu, His Excellency, His Eminence, HH etc. Fyatu Mfyatuzi bin Mfyatuaji bin Mfyatukage wa Mfyatulizi mwana wa Mfyatukizi mjukuu wa Fyatuafyatua. Hata kwenye uapisho wangu sitataka kuwaona viumbe hawa wasio na shukrani. Sitaki tena unafiki wa kunipamba kumbe wananiponda.

Mwisho, nachukua fursa hii kuwaomba msamaha mafyatu wangu. Maana, wengi walinitahadharisha kuchanganya dini na politiki nikagoma nisijue ningejutia. Walinionya kuwa wengi walikuja na kunipamba kwa mapambio wakati, nyuma ya pazia, wananiponda na kujiona wajanja kwa kunitumia kupata maulaji yetu ya dezo. Sasa nimewastukia. Lazima niwafyatue kabla hawajanifyatua aka kunigwjiming. Nawahakikishia. Sitafyatuliwa kirahisi tena. Huwezi kunipaka mafuta kwa mgongo wa chupa nisikunyoe bila maji. Hivyo, tusilaumiane wala kuingiliana.
Chanzo: Mwananchi jana.

Tuweni makini na maduka ya roho yaitwayo makanisa

Kwa wanaofuatilia masuala ya dini, watakubaliana nasi kuwa imezuka biashara chafu ambayo ni karibu ya wizi na ujambazi japo tofauti ni kwamba imehalalishwa na serikali zetu. Hii si nyingine bali uanzishwaji wa madhehebu ya dini na makanisa yenye lengo la kutengeneza fedha na si vinginevyo. Siku hizi biashara ya dini inalipa karibu sawa na ya madawa ya kulevya. Anayeshuku hili aangalie utitiri wa madhehebu na makanisa na utajiri wa viongozi wake tena wa ghafla bin vu bila maelezo yanayoingia akilini.

Mwenyekiti Mao Zedong alilwahi kusema kuwa bila utafiti, hakuna haja ya kutoa madai. Pia, sheria inasema kuwa atoaye madai, atoe ushahidi.  Hivyo, katika makala ya leo, tutatoa ushahidi kama ifuatavyo.

Mosi, kama tulivyosema hapo juu, ukitaka kujua ukweli wa dhehebu la dini au kanisa, waangalia wale wanaojiita viongozi wake. Angalia aina ya maisha wanayoishi na mahubiri wanayohubiri. Wengi wa wahubiri na viogozi wa kujipachika vyeo kama vile mchungaji, askofu, mtume, nabii na vingine, hawafanyi kazi zozote za kuwapatia kipato. Ni matapeli wanaowaibia na kuwanyonya waumini wao wavivu wa kung’amua vitu rahisi ima tokana na ujinga au kukata tamaa. Je huu utajiri wanaupata wapi kama siyo kuwaibia wafuasi wao ima waliokata tamaa au wajinga tu? Wapo wanaojihusisha na biashara nyingine hata bila kulipia kodi na hivyo kuiibia serikali na kujiingizia fedha nyingi kinyume cha sheria. Kwanini mamlaka hazijiulizi swali hili rahisi ambapo kinachofanyika hakina tofauti na ujambazi wa kawaida ambapo jambazi hulala maskini na kuamka tajiri bila kutoa maelezo? Kwanini mamlaka hazitaki kuuliza au kuna namna?

Pili, kujua mbivu na mbichi, angalia mhusika amepata uongozi au ukuu wa dhehebu husika namna gani. kama amejipachika kama wengi tunaowaona hata wakijiingiza kwenye siasa, anachofanya mhusika ni biashara ya kusaka tonge na fedha kwa mgongo wa neno la Mungu ambalo siku hizi limegeuka biashara kubwa duniani ambapo matapeli na waroho wengi wa utajiri hujipatia utajiri na ujiko.

Tatu, angalia namna kanisa au dhehebu husika linavyopitisha madaraka inapotokea kiongozi akafa. Utaratibu tuliozea kwa dini za kweli ni kwamba akifa kiongozi wake, hufanyika uchaguzi na kumpata mtu anayefaa ambaye mara nyingi huwa ameandaliwa hata kabla ya kiongozi kufa japo si kwa din izote. Mfano, makanisa maarufu kama vile la Kiroma, Kianglikana, Kilutheri na mengine yanayoheshimika, huwa na utaratibu wa kuteua au kufanya uchaguzi wa mrithi wa kiongozi anapostaafu au kufariki. Hata uislam una utaratibu huu. Mfano, anapokuwa shehe mkuu, hufanyika uchaguzi wa shehe mkuu mwingine ambaye mara nyingi hana uhusiano wa damu na anayemrithi. Hata papa anapokufa au askofu mkuu wa baadhi ya madhehebu yanayoheshimika, hali ni hii. Hakuna kurithishana madaraka kama ambavyo hivi karibuni tulishuhudia hapa nchini ambapo alifariki mmojawapo wa waliojipachika madaraka ambaye kanisa lake––––kwa vile lilikuwa duka lake lililopachikwa jina la kanisa––––lilirithishwa binti yake. Je kweli kanisa la Mungu laweza kurithishwa au kutafutiwa mtumishi? Je makanisa haya yanayorithishwa kwa kufuata damu ni makanisa au maduka tu? Utarithije kanisa la au msikiti wa Mungu?

Mfano mwingine wa hivi karibuni ni pale alipokufa tapeli mwingine nchini Nigeria aitwaye Temitope Bolugun Joshua almaarufu TB Joshua. Baada ya kifo cha ghafla cha tapeli huyu, ulizuka mgogoro katika urithi wa kanisa ambapo mkewe Evelyn alirithi duka la mme wake. Wakati matapeli wenzake wakimpa urithi mke wa Joshua, walitoa sababu hafifu na mbovu kuwa Joshua alizaliwa mtume na mkewe aligeuka mtume kupitia ndoa hasa ikizingatiwa kuwa mume na mke ni mwili mmoja! Je kwa  huyu wa kwetu dhana hii chafu inasimama au tutaambiwa kuwa kwa vile binti yake ni damu ya mama basi nao ni kitu kimoja?

Nne, kujua kuwa dhehebu au kanisa husika ni duka la kuchuuza neno na roho, angalia namna wakubwa wake wanavyosaka umaarufu na matumizi makubwa ya vyombo vya habari au kujiingiza kwenye siasa. Nchini Uganda, Hayati Padre Simon Lokodo alifukuzwa upadre na Papa mstaafu Bendict XVI baada ya kujiunga kwenye mbio za kugombea jimbo la Dodoth ambalo alifanikiwa kushinda na kuliongoza hadi mauti yanamfika 29 Januari, 2022.

Tano, kujua kama dhehebu au kanisa husika ni la kitapeli au duka la kiroho ni kuangalia aina ya mahubiri ya viongozi au wenye duka husika wanayohubiri. Wengi wa matapeli hawa wakiroho uhubiri mambo makuu matatu, yaani utabiri, utajiri na kufanya miujiza ya urongo. Rejea mfano, yupo aliyeahidi kumfufua marehemu Amina Chifupa. Mbali na huyo, Joshua aliicha dunia hoi alipotabiri kuwa Hilary Clinton angeshinda urais wa Marekani akaishia kubwagwa na Donald Trump jambo ambalo lilifichua ujinga, utapeli na ubabaishaji wa tapeli huyu.

Leo sitaandika mengi zaidi ya kuwasihi wale wanaoibiwa kila uchao kutokana na imani zao, wawe makini. Wachunguze mambo matano tuliyodurusu hapo juu kujua kama wanachojiunga nacho ni duka la kiroho au dini. Wengi wanaibiwa na kuaminishwa kuwa kuna siku watabarikiwa na kuwa matajiri wakati hao wanaowaibia wanazidi kuwasikinisha, kuwadanganya, na kuwapotezea muda. Wakati wa serikali kuchunguza utajiri na taasisi za viongozi wa kujipachika madaraka umefika. Vinginevyo, serikali haiwasaidii wananchi wake. Pia, ifahamike. Imani katika miujiza ni chanzo cha uvivu na uuaji wa maarifa. Hivyo, licha ya kuathiri hali na uchumi wa wahanga, inaathiri uchumi wa taifa ukiachia mbali kuvunja sheria kwa kuhubiri uongo.

Chanzo: Mwananchi jana.