The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Saturday, 31 May 2025

WaKÄ©-Nyaa mkome kutaka ‘kutovuka na kutuvurugia’


Kwanza nikiri. Ukitaka kufyatuka na kufyatua wanaokufyatua, hakikisha hukosi kutumia zana za kileo hasa mtandao. Hivyo, Fyatu Mfyatuzi nami ni geek au gwiji wa mtandao. Juzi, katika kupitia mitandao baada ya bi mkubwa kuchefukwa na kukinukisha, nilikuta matusi ya nguoni toka kwa mafyatu wa kaya jirani wakimtukana yeye na mafyatu wote. Nilishangaa, kuchukia, na kusikitika kiasi cha kuamua kufyatua hiki kitu ili wahusika wakome na kukomaa. Naonya. Asitokee yeyote akaniita chawa awe wa baba au mama. Mie siyo wala sijawahi kuwa chawa. Mie ni Fyatu. Period. Bi nkubwa ambaye kitaaluma ni doktari wa karibu kila kitu na mafyatu wote wananijua uzuri kuwa huwa siiti koleo kijiko kikubwa bali koleo. Huwa sitetei ujinga na uzwazwa. Nachukia jinai, ubabaishaji, ukandamizaji, hata usanii vifanywe kwa kisingizio chochote iwe amani, imani, siasa, au visasi.
    Cha mno, baada ya bi nkubwa kumfyatua mtundu Tunda ambaye, kwa ‘utundu’ wake, anataka kutishia ulaji wake, kaya nzima ililipuka, kufyatuka, na kugawanyika pande mbili. Wanaounga ‘uzalendo’ na wanaoipinga. Kwani, hawajui kuwa Mtundu anasulumbiliwa na utundu tu na uharibifu? Maji yalizidi unga hadi kuvutia mafyatu jirani. 
            Kwanza, nafyatua hii kitu kuwaonya mafyatu wangu na bi nkubwa hawahitaji msaada wao kwa wanachodai ni haki za binadamu. Mafyatu ni mafyatu. Hawahitaji haki za binadamu bali kufyatuka ili wazisake wenyewe wajuavyo. 
            Pili, naonya dhahiri mambo ya Ngoswe aachiwe Ngoswe. Maza anashangaa. Lini walituona kwao tukienda kuwatetea kana kwamba hawana uwezo wa kujitetea kama sisi, sorry, kama wao? Unakwendaje kumsaidia fyatu ambaye hajakuomba msaada? Wapo wanaodai eti wanataka kutumia fursa hii kutanua ughaibuni wakisingizia kutetea mafyatu wa kaya yetu. Natoa angalizo na onyo. Hakuna haja kuchukiana au kudepotiana. Tuamke. Tuache kutumiwa kama kichwa cha mwendawazimu walevi kujifunzia kunyoa. Tufyatuke na kujitetea. Tusingoje kutetewa au kufyatuliwa ndiyo tufyatuke.  
    Tatu, wafurukutwa wanahoji, kama tutakuwa wakweli, kuna lisirkal habithi kama la kwao? Fyatu mmoja aliuliza “je mbona hawajamaliza mtiti wa mauaji, utekaji, na upoteaji wa Gen Z? Au wanataka kuwafyatua Gen Ziro na mafyatu wetu wafyatuke na kuwafyatua watukufu walioletwa na Sir God mwenyewe? Mshindwe na kulegea hadi mlegelege. 
        Hapa, naona ufyatu. Kama ni utekaji, upotezaji, na unyotoaji roho, upo kaya zote aliwahi kusema maza au hamkumuelewa? Mbona juzi alinyotolewa roho mwishiwa tena katikati ya jiji la Nairoberry mbali na kasisi aliyejenga usuhuba na mpingaji maarufu wa kwao aliyefyatuliwa. Nani kashikwa? Kwanini? Hawa ‘viherehere’ wamefanya nini? Lazima waeleweshwe na waelewe. Kwetu ni amani tupu hata kama ni ya imani. Hatujanyotoa roho ya mwishiwa yeyote. Kama ni kasisi, wetu alifanyiwa massage bila kunyotolewa roho sawa na kwao. Isitoshe, ‘tumeishawashika’ watuhumiwa. Pia, wajue. Ndata wetu hawajadata kama wao. Hamkuona juzi, pale kwa pilato, walivyoonyesha amani na imani kiasi cha mafyatu kwenda kuchonga na Mtundu bila kupigwa, kutishwa, wala kuingizwa tunduni?
    Nne, sikupenda walivyomuudhi bi nkubwa wetu kiasi cha kumlazimisha azoze. Sasa nasema. Mkome na kama mbaya mbaya msije kutovuka na kutuvurugia ulaji wetu. Yenu yawashinda. Yetu yawahusuni? Leo, mwaja na gea ya kutetea wapingaji ambao ‘hawapendwi’ hata na chawa achilia mbali mafyatu. Kesho, kwa vile huu ni mwaka wa uchakachuaji ambapo nimeishajihakikishia ushindi wa kishindo na miujiza, mtakuja kuhoji uchakachuaji wetu kana kwamba kwenyu hawachakachui na kuchakachuana kama ambavyo nasi tunafanya na ngoma inakuwa droo. 
    Tano, nimekasirika sana kwa watundu kumkasirisha bi nkubwa wetu mpendwa, mbeba maono, aliyefungua kaya na kutenda miujiza kiuchumi. Nadhani wanatuonea wivu. Haiwezekani waje kutufundisha namna ya kufyatuana hata kama tumegoma kufyatuka na kufyatua hao wanaotaka tuwafyatue. Haraka ya nini? Msituvurugie. Wakati wa kufyatuka na kufyatua ukifika, wala hatutahitaji msaada wenyu wala tuisheni juu ya namna ya kufyatuka na kufyatua. Hata hivyom, wana bahati. Ningekuwa mimi, ningewaweka tunduni kama yule Mtundu wakaishi naye kama wanampenda sana. Ebo! Tuheshimiane. Iweje fyatu atake kukinukisha nao wamuunge mkono? Kikinuka kikanukishwa, si tutanuka wote? Hata kama tunanuka tayari, nani anataka kuongezewa harufu mbaya baada ya kukinukisha? Isitoshe, tukinukishe au kutokinukisha, wao yawahusuni? Pilipili usizokula zakuwashani? Wasitake kujua kunguni wa kitanda wasicholalia. 
    Mwisho, nawajuza hawa ‘viherehere’ kuacha ‘kiherehere.’ Sisi, japo mafyatu, tumegoma kufyatuka hadi Mwana wa Maria arejee ndiyo tufyatuke na kwenda kutesa mbinguni. Kama wanaona wivu namna bi nkubwa anavyoupiga mwingi, si waende awamegee maono nao watende miujiza ya kuzuia mafyatu wao kufyatuka na kukinukisha? Wanacheza na kukinukisha! Wanajua maana na madhara ya kukikunikisha? Kikinukishwa, mafyatu wanene watakosa raha na usingizi wakati kugoma kufyatuka ndiyo sera mbadala tuliyochagua wenyewe kwa sababu ni mafyatu wa amani katika kisiwa cha imani ya amani. Msituvurugie amani. Tutailinda amani hata kama ni kwa shari mradi iwepo hata kama ya imani.
Chanzo: Mwananchi J'tano iiyopita.

Sunday, 18 May 2025

nani kasema kitanda kinazaa haramu?


Kuna imani kuwa kitanda hakizai haramu. Uzoefu wetu unaonyesha kuwa kitanda kinazaa haramu japo uhalalishwa kwa visingizio mbali mbali kama mila, ujinga, na ubutu wa teknolojia. Ujio wa kipimo cha DNA unaonyesha kuwa kitanda kinazaa haramu tu.  Kusema kitanda hakizai haramu ni uchafu kimila. Ni hatari, majuto, na makosa makubwa kwa wasioamini wala kukubali uchafu huu kuoa au kuolewa kwenye makabila haya. Kwani, hawana uwezo wa kudumisha mila.

Tuanze na mfano wa Jerome (si jina lake) ambaye anathibitisha kuwa kitanda kinazaa haramu. Jerome ana siri iliyojificha kwenye mila chafu za kujamiana ndugu kwani, anafanana na babu yake kuliko baba yake. Pia, kuna minong’ono kuwa mama yake alipewa mimba na baba mkwe. Siyo siri tena kwa wanaomjua. 
        Kisa kingine ni cha Giloli (si jina lake) binti anayetoka kabila moja na Jerome. Tofauti, yeye ni mtoto wa kaka wa baba yake aliyezaliwa kwenye ndoa. Siri ya Giloli ilifichuka alipopata mchumba. Naye, hafanani na baba yake bali baba mkubwa. Alipochumbiwa, mchumba aliambiwa apelekwe kutambulishwa kwa baba mkubwa. ‘Baba’ yake aliishi mbali. Wanaojua, waling’amua na kufumbua fumbo lilojificha miaka mingi. 
        Jerome na Giloli wanatoka kwenye kabila lenye utamaduni wa kuchukuana ndugu kwa ndugu. Je katika jamii zetu wapo wangapi? Tafakari. Wakati ukitafakari, ujiulize. Ni watoto wangapi hufanana na baba zao wakubwa, wadogo hata wajomba hata majirani uliowahi kusikia habari zao?
Akiwa bungeni, Profesa Paramagamba Kabudi aliwahi kuwasihi Watanzania wasipime DNA za watoto wao. Fufuatilia clip hii. https://www.youtube.com/watch?v=sr3MZn9SMcE. Huu ni ushahidi wa kwanza kuwa kuna Jerome wengi kuliko unavyoweza kufikiria.
Kuna makabila na watu wenye tabia ya kuzaa watoto nje ya ndoa wakiwa katika ndoa au nadhiri hasa makasisi. Pia, zipo jamii zilizokubali na kuhalalisha jinai hii ambayo ni hatari kwa watoto na waliobambikiziwa. Katika makabila haya, watu hawa wako wengi, wanajulikana, na wengine wanakubalika chini ya dhana chafu ya kitanda hakizai haramu.
Je jinai hii husababishwa na nini? Kimsingi, zipo sababu nyingi kama vile ukosefu wa uaminifu katika ndoa, mila mbovu, tamaa, kutoweza kupata watoto wa jinsia fulani kwa baadhi ya wanandoa, kubakwa, uzinzi, na mengine mengi. Mila mbovu za ndugu kuchukuana ni chanzo kikubwa. Mfano, kuna makabila ambapo ndugu huchukuana kama mbuzi au panya bila kujali au kujua madhara ya kufanya hivyo. 
            Je utawajuaje? Utasikia kila baba anayekuja nyumbani ni ‘anko.’ Huu ‘uanko’ unaficha mengi.  Kuna makasisi wana watoto waliozaa na mahawara wao ambao huitwa anko na watoto wao wenyewe wa kuzaa. Watu na makabila haya yapo na yanakubali mila na tabia hizi chafu kama vile watoto wa babu na bibi mmoja huchukuana na hata wengine kuoana. 
        Huyu anamchukua mtoto wa baba mdogo, mjomba, shangazi, na wengine hata kuchukua wapwa zao ilimradi ‘wadumishe mila.’ Pia, kuna makabila yanayogeuza ndoa mali ya ushirika kwa kuruhusu baba mkwe au shemeji kumrithi mjane. Kama kurithi wajane ni jambo la kawaida, inashindikanaje wahusika kuchukuana hata kupeana mimba hata kabla ya kufiwa?
        Ikitokea mtu atokaye kwenye jamii isiyokubaliana na mila hizi chafu kuoa au kuolewa katika jamii hizi, lazima ataumizwa. Pia, watoto watokanao na dhambi hii huathirika kisaikolojia hata kiuchumi. Mfano mtoto ambaye baba yake halisi siyo mume wa mama yake, hawezi kumjua au kumfaidi mzazi wake. Hivyo, kijamii, anakuwa ametenganishwa na mzazi wake halisi na kuunganishwa na mzazi bandia. 
                Pia, inapotokea mzazi wake ana mali, hana uwezo wa kumrithi ukiachia kutowajua au kukua na ndugu zake. Pia, inapobainika, uwezekano wa kuvunja ndoa ni mkubwa. Hamjasikia visa vya baadhi ya wanaume kuua watoto wanasio wao au wanandoa wanaoua wenzao wagunduapo wamebambikiwa watoto? Je hapa kitanda hakijazaa haramu na jinai?
            Je nini kifanyike kuepuka unyama na utapeli huu? Tunashauri jamii zisifumbie macho jinai hii. Badala yake, tuelimishane madhara ya jinai hii kuepusha mateso kwa watoto, talaka, na vifo vyao hata wazazi wao. Hakika, kitanda kinazaa haramu. Kuweni macho.
Chanzo: Mwananchi leo.

Friday, 16 May 2025

Nitashinda urahis wa mafyatu kimiujiza na vishindo


Najua. Kaya yetu inafanya uchakachuaji, sorry, uchaguzi mwaka huu. Sambamba, nasi mafyatu tutafanya uchaguzi si uchakachuaji wa rahis wa mafyatu Mheshimiwa, Daktari, Profesa, ustaadh, Al haj, Muadhamu, Mtakatifu, Muona Mbali Fyatu Mfyatuzi. Hivyo, ili kujihakikishia ushindi wa kishindo na wa miujiza, nimeweka mikakati ifuatayo:
            Mosi, nitahakikisha nashinda hata kwa bao la kisigino watake wasitake. Mwenye wivu si ajinyongelee mbali.
             Pili, nitatoa ahadi kama sina akili nzuri. Lazima niwaaminishe mafyatu kuwa mimi ndiye ninafaa hata kama sifai. Lazima wajue kuwa bila mimi, watayumba na kuteseka sana.
Tatu, nitahakikisha wapingaji wenye kuonyesha ushawishi wanafunguliwa kesi za wizi wa kuku au za kubambikizwa. Pia, nitawaambia na kuwaaminisha mafyatu kuwa wanapaswa kuwaogopa wapingaji kama ukoma. Hii ni kutokana na ukweli kuwa wanatumiwa na ‘maadui’ wa mafyatu toka ughaibuni wanaotaka kuharibu amani, ulaji, na utulivu vyetu.
             Nne, nitaamuru migambo yetu kuwasweka ndani wote wanaoonyesha kutishia ushindi wangu. Hapa, lazima kusiwe na huruma, haki za mafyatu wala nini bali kufanya kweli kwa kuteka, kutembeza kipigo, na ikibidi kuweka ndani bila kutoa maelezo wala kufuata sheria za mafyatu.
             Tano, nimehakikisha mafyatu wananipitisha siyo kunichagua kama kanuni za katiba ya mafyatu inavyotaka kwenye kura za mchujo na uchaguzi wa ndani ya chata letu tukufu. Mafyatu wasenzi kweli. Si wapo waliotaka eti nipambanishwe na wanachama wengine wa Chama Cha Mafyatu (CcM) ili kupata mgombea anayekulika. Niliwazuia kutenda dhambi hii ya kunipambanisha mie mtukufu na watukutu katika chama chetu. Nani hajui kuwa mie napendwa na kukubalika? Anayebisha aulize miti, wadudu, hata wanyama. Mie nakubalika bwana. Anayeendelea kushuku hili, ajiulize ni kwanini nasifiwa kwa kila jambo hata lisilopaswa.
            Sita, nitahakikisha wakati wa kampeni hakuna kuwapa nafasi wapingaji wangu kufanya kampeni. Tena nitumie fursa hii kutoa angalizo na onyo. Yeyote atakayeshirikiana na wapingaji wangu ajue. Atakipata cha moto. Wao kama nani wafanye kampeni sawa nami wakati wanajua wazi mshindi ni mimi? Nani aruhusu wapingaji wavuruge amani na utulivu wa mafyatu? Mafyatu hawajui kuwa niliapishwa kulinda ulaji na si wao? Je huu siyo muujiza unaolenga kuleta amani na mshikamano chamani?
           Saba, kwa mjibu wa katiba ya CcM, mwenyekiti ana turufu ya kuteua wasimamizi wa wilaya na mikoa kama ilivyo kwa lisiri kali. Hivyo, nimewaamuru watendaji wangu wote kuhakikisha wanatumia mamlaka niliyowapa kuzuia upuuzi unaoitwa mikutano ya hadhara. Hii si mikutano ya hadhara bali ya madhara. Nani anapenda madhara wakati huu wa kusaka ulaji wa dezo tena mnene? Atayekaidi agizo hili ambalo, kifyatu, ni sheria, natengulia mbali uteuzi wake tuone kama atakula mafi yake nyambaff.
              Nane, nitaamuru vyombo vya umbea vyote vya kifyatu kutangaza sera zangu pekee huku vikihakikisha vinawabana na kuwakadia kwa kuwanyima fursa ya kutangaza utopolo wao wapingaji. Atakayekaidi na kutangaza ujinga wa wapingaji, ima nitamfungia au kumnyima matangazo ya biashara, au kufutulia mbali chombo chake nione kama atakula jeuri yake.
             Tisa, nitanunua na kupandikiza vyama pandikizi ili ‘vishindane’ nami ili kuhalalisha miujiza yangu katika kushinda uchakachuaji, sorry, uchaguzi kwa kishindo na miujiza vinafanikiwa. Viongozi wa vyama hivi lazima niwapige njuluku walainike na kujifanya wananipinga wakati game letu ni moja au siyo? Kwa usawa huu, bila kuja na mikakati kama hii, unaweza kuadhirika bure mzee mzima ukatupwa nje ya ulaji na kuchekwa hata kufunguliwa mashtaka kwa makosa ambayo nimeshafyatua. Nawajua mafyatu. Hawana akili nzuri wala dogo.
            Kumi, napanga uchakachuaji, sorry, uchaguzi uwe wa amani na utulivu. Hivyo, ili kuhakikisha hivi vinafanyika, migambo watatembeza kipigo kwa yeyote anayetaka kutishia amani na utulivu wa ulaji wangu na wapambe wangu.
             Kumi na moja, ili kuwaweka sawa mafyatu, nitaanza kuhubiri amani kwa kuwatishia na migogoro na vita vinavyoendelea kwenye kaya za mafyatu jirani. Lazima wajue kuwa bila mimi kuukwaa urahis, mafyatu wote watakabiliwa vita na matatizo makubwa. Kufanikisha hili, nitaamuru runinga zote za mafyatu kuonyesha madhara ya migogoro na vita husika. Kwa niwajuavyo mafyatu, bila kuwatisha, wanaweza kunitisha hata kutishia ulaji wangu mtukufu.
          Kumi na mbili, kuanzia sasa hadi uchakachuaji, sorry, uchaguzi, nitaanza kumwaga misaada kila mahali ili mafyatu wanichague. Najua. Walivyopigika, hawatatoboa. Pia, kwa walivyochelea kufyatuka wakafyata, hawatauliza hisani hii ni ya nini wala njuluku nitakazomwaga zimepatikanaje au nitazirejesha vipi. 
         Kumi na tatu, nitahakikisha mwanangu mwenyewe ndiye atakayesimamia wizara ya mafyatu inayosimamia mambo ya uchakachuaji ili tusije kupigwa bao la kisigino na wabaya wangu waliojazana kwenye chama chetu.
            Kumi na nne, nitaanza vita na mataifa yanayojifanya vijogoo na kutaka kutufundisha demokrasia na haki za mafyatu kana kwamba mafyatu wangu ni wao.
Du! Ndoto nyingine zikichanganyika na bangi ni balaa! Kumbe naota urahis siyo urais!
Chanzo: Mwananchi Jtano iliyopita.

Sunday, 4 May 2025

Fyatu afyatua figa na fwakit kuhusu Kanada

Tangu nifyatukie Kanada, nimekuwa nashuhudia mambo ya ajabu toka kwa mafyatu. Wapo wanaoomba mialiko ili waje huku wagome kurejea kwao na kufanya niwatunze hadi nifyatuke. Wapo wanaonipiga mizinga tena mingine ya kijinga siyo kifyatu. Hivi, unajisikiaje fyatu ambaye ameishastaafu kukubomu dolari 500 kwa ajili ya harusi ya kitegemezi chake na si kwa ajili ya matibabu yake? Akili au matope? Kwanini kuoa, kuoza, na kuozwa kwa mifuko ya mafyatu? Je wao walipooa au kuolewa uliwachangia lau moja ya kumi ya hizo unazoiitisha?
        Ajabu ya maajabu, siku hizi, mafyatu wanaweka hata kiwango cha chini cha nchango wa harusi kana kwamba wanajua una kiasi gani benki au uchagoni! Hakuna mafyatu waliokosa ubunifu kama wangu. Hata mamlaka zinahangaika na njuluku za madiaspora wakati haziwatendei yoyote zaida ya ntima nyongo. Ukitaka kujua huu ni ukumbaff, sorry, unyonyaji na uzwazwa, itisha nchango wa kupeleka kitegemezi shule au mgonjwa hospitalini, hawajachangii. You know what? Loo! Nimesahau naongea na mafyatu wa kibongo na si wa kitasha siyo!
        Hayo ya kimombo na watasha tuyaache. Ukichunguza nchango, wengi hawachangii harusi wala nini bali kupata fursa ya kula, kunywa, na kufanya mambo yao. Kwa mafyatu wanaopenda kudumisha mila, wanajua ninachomaanisha hapa au siyo? Wanajificha migombani na kumaliza mambo yao. Kwa ufupi, ni kwamba hawakuchangii harusi wala wewe bali wanajichangia kwa kisingizio cha kukuchangia. Ni ajabu. Wavyele wengi hawaipati hii. Chao ni kujisifu kuwa harusi ilinoga wakati yote ni malengo na mifuko ya mafyatu wasioona mbali. Kwanini hiyo njuluku mnayounguza kwenye utopolo kama harusi msiichangie kwenye kununua hisa hata kwenye masoko ya njuluku?
        Turejee kwa Kanada au Kanuki kama waiitavyo wenye kaya yao hasa wale originali siyo sisi wa nkorogo tuishio kwa vibali vya ukazi hata watasha walioivamia na kuitwaa na kuigeuza yao kiasi cha kutuuliza sisi nyie mwatokea wapi kana kwamba wao si wakuja kama sisi. Kanada ina ukubwa wa kilometa za mraba 9,093, 507 ikilinganishwa na Bongo yenye 947, 303. Hii maana yake ni nini? 
    Ni kwamba Kanada inaimeza mara tisa na nusu na ushei. Mkoa (Himaya) mkubwa kuliko yote Kanada wa Nunavut unaweza kuimeza Bongo mara mbili na ushei kwa ukubwa wa kilometa za mraba 2,093,190. Jiulize. Pamoja na ukubwa wote huu, ina mafyatu wangapi? Cheka taratibu. Ina jumla ya mafyatu 41, 414. Kama mafyatu wa Nanavut wakiamua kugawana himaya wao, kila mmoja atapata si chini ya kilometa 30 za mraba kama shamba lake ikilinganishwa na Bongo ambapo kila mbongo atapata kilometa za mraba 14. Kwa Visiwani, kila mmoja atapata 000.13!
            Shangaa sasa. Hata mkoa mdogo kuliko yote wa Kanada wa Prince Edward Island (PEI) yenye ukubwa wa kilometa za mraba 5,660 ni mkubwa kuliko Visiwani yenye ukubwa wa kilometa za mraba 2, 462 ambayo ni mara mbili na ushei? Je wajua kuwa Visiwani ni 1 ya 383 na ushei ya Bara? Ajabu, zote mbili zina haki sawa katika muunganiko! Ukiuliza mantiki, sijui kama utapata jibu lifyatualo akili zaidi ya siasa na sanaa. Katika siasa, moja na 400 ni sawa! Japo sina takwimu, ukweli ni kwamba wazenj wengi, kupitia mgongo wa muungano wa mnyonyano, sorry mpendano, wapo wengi bara kuliko visiwani. Ni udugu na upendo kiasi gani kiasi cha 1/383 kutoa hata mnene wa kaya? Du! Ningekuwa braza Mtikisa wa Tikisa gabacholi, ningeuliza. Je nani iko roga nyinyi ambaye nanyonwa lakini haipo fanya hesabu na hoji dugu yangu?
            Ukija kwenye pato la jumla la Kanada, ni Dola 37, 317 ikilinganishwa na Bongo yenye dolari 2,500. Hii maana yake ni nini kifyatu? Ina maana Mkanada mmoja ana uwezo wa kiuchumi mara 15 ya fyatu wa Kibongo. Ajabu, mafyatu wa Kikanada hawachangishani kwa ajili ya harusi. Je wajua Kanada ina idadi ya mafyatu wangapi? Jibu ni rahisi. Ina 41,528,680. Siombi msamaha kwa wale wanaochukia namba. Wapo waliodhani kuwa Fyatu Mfyatuzi hajui kuzifyatua namba kwa vile ni mwanasharia na mwandishi wa umbea. Kwenye namba, nilikuwa nampa taabu ticha wangu zama zile za ujima. 
        Wengi hawajui kuwa nina tuzo ya Nobo ya namba! Pia, nina tuzo ya juu ya takwimu. Nina uwezo wa kufanya mahesabu hata ya maji na uji na namna unavyoingia tumboni mwa mafyatu. Nina uwezo wa kuhesabu matone ya mvua na michanga ya bahari. Unadhani natania? Niulize michanga ya bahari au matone ya mvua ni kiasi gani. Hata usipouliza, acha nikupe jibu la kimahesabu kuwa ni mengi na mingi. Kkkk. Umenipata siyo?
            Una habari kuwa mimi ndiye niligundua formula ya mahesabu kuhusiana na idadi ya vitu. Mimi ni mgunduzi na mvumbuzi wa fomula ya ingi. Hivi, nimesemaje?
Chanzo: Mwananchi, Aprili 30, 2025.

Talaka na Madhara Yake


Tunajua fika kwa uzoefu wetu hata utafiti. Hakuna binadamu wala mwanandoa anayependa wala kushabikia talaka hata kama baadhi ya dini na sheria vimeiridhia kutokea ikilazimu. Hivyo, katika kipengee hiki tutajadili talaka na madhara yake hasa kwa wanandoa, familia, na jamii hata nchi kwa ujumla. Kwa vile siyo kila kitu kinaweza kutafsiriwa au kueleweka kwa mujibu wa kamusi, tutaepuka kuwachosha na maana au tafsiri za talaka kwa mujibu wa mamlaka mbali mbali kama vitabu vya kidini na vya kisheria. Tunaamini kuwa talaka, kwa lugha, nyepesi ni kinyume cha ndoa.
         Kwa ufupi, talaka ni kifo cha ndoa. Palipo na ndoa hakuna talaka na palipo na talaka hakuna ndoa na viwili hivi haviwezi kuishi kwa pamoja katika sehemu moja yaani ndoa kwa wakati mmoja.
Pia, ifahamike. Talaka, tofauti na ndoa, ina madhara makubwa kwa wanandoa binafsi, watoto, jamii na nchi. Mfano, chukulia mfano wanandoa wanaomilki mali kwa pamoja kama vile gari, nyumba, hata shamba. Wanapotalikiana, huwa maskini. Kwani, wakigawana mali zao, wanabakia watu wasio na vile walivyokuwa navyo kabla ya kuachana. Pia, ieleweke.
         Kuna vitu visivyogawanyika kama watoto ambao wazazi wakitalikiana, huwachanganyikiwa kwa vile ni vigumu kuwagawana wazazi au kugawana mapenzi yao kwao kwa usawa. Hapa, ndipo ilipo kadhia ya watalaka kuuana hata kuhujumiana kiasi cha kudhoofishana wao na watoto wao hata jamii. Zaidi, kesi za talaka hutumia muda na fedha nyingi kiasi cha kuathiri utendaji na uzalishaji wa wahusika. Hivyo, ndoa ni sehemu ya kutunza mafanikio ya wawili na hata jamii kwa ujumla mbali na kuwapa watoto kinga na utulivuv na mafanikio katika maandalizi ya maisha yao. Athari na hasara za talaka ni nyingi mno kiasi kwamba hatuwezi kuzielezea zote kwa ukamilifu katika kipengee kimoja. Cha msingi, ni kuiogopa, kuitahadhari, na kuiepuka kadiri iwezekanavyo. Kwani, haijengi zaidi ya kubomoa.
        Hata hivyo, upendo ukiwa wa kweli na kufanikisha lengo la ndoa, ni kinyume. Wahusika wataridhika, watafurahi, watafanikiwa, wataongeza upendo, na kuishi maisha marefu ikilinganishwa na walioharibikiwa au kutalikiana. Tunapoongelea madhara ya talaka kuhusiana na uchumi na mahusiano ya wahusika, hatugusii vifo vitokanavyo na kuachana. Kwa mfano, kwa mujibu wa National Library of Medicine (2022), takwimu za mauaji ya watalaka katika nchi ya Ufini, zinaonyesha kuwa kati ya 2003 na 2013, yapata 65% ya wanawake waliouawa nchini humo waliuawa na ima wenzi wao wa sasa au wa zamani iwe ni katika ndoa au mke na mume waishio kinyumba.
           Mwaka 2007 pekee, chini Marekani, wanawake wapatao 45% waliuawa na wenzi wao wa sasa au wa zamani. Hapa inaonyesha kuwa mauaji ya wanandoa yanayofanywa na wenzao ni janga la dunia na wahanga wengi ni wanawake. Hii haina maana kuwa hakuna wake wanaoua waume zao iwe ni wa sasa au wa zamani. Kwa mujibu wa jarida la Forbes (2024), idadi ya wanandoa waliouwa na wenzao ilikuwa 1,363 katika kila 100,000 kwa watalaka ikilinganishwa na 779 katika kila 100,000 kwa walio katika ndoa. Kwa mujibu wa Forbes (2024), talaka huathiri wanawake kwa viwango tofauti na wanaume. Mfano, wanaume huathiriwa na janga la ndoa kwa uwiano wa 1,772 kwa kila wanandoa 100,000 ikilinganishwa na wanawake 1,095 kwa kila wanandoa 100,000 Hapa somo ni kwamba kuna wanandoa wanaaendelea kuishi kwenye ndoa hatarishi hadi kuua au kuuliwa.
            Hali hii hatarishi inajenga maswali mengi juu ya ni kwanini watu waliokutana wakaamua kupendana na kuoana huuana. Japo hatuja jibu na sababu zote, tunaamini kuwa mauaji ya namna hii, ima yanatokanana kulipizana visasi, kuchanganyikiwa, hata kukata tamaa ya kuishi. Hivyo, namna ya kujiepusha na balaa hili ambalo linaweza kumkumba yoyote ni kujielimisha juu ya ndoa ili kulizuia hata kuliepuka. Kila gonjwa lina dawa. Na dawa ya kuimarisha na kufaidi ndoa ni kuielewa sawa na ambavyo tunapoumwa, huenda hospitali na kupata dawa na kupona ingawa si kwa magonjwa yote. Wahenga wanaasa kuwa ni heri kuzuia kuliko kutibu japo kutibu si vibaya ila kuzuia bado ni bora kwani humwezesha mhusika kuepuka baadhi ya magonjwa hata kifo.
Chanzo: Mwananchi J'pili jana.