The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Thursday, 17 April 2025

Napanga kuuza au kubinafsisha ubongo wangu


 

Sihitaji ubongo tena. Kwanza, umenifyatua nikafyatua wengine hadi wanatishia kunifyatua kwa kuninyotoa roho. Ubongo umesababishe kero na hatari hadi nikageuka machukizo ukiachia kujiudhi mwenyewe. Ubongo umenibomoa badala ya kujijenga. Nilifyatua wengine ili wafyatuke na kuwafyatua wanaowafyatua nikaishia kujibomoa. Mbali na ubongo kuniletea madhara kwa vile unachemka, zipo sababu zilizoko nje ya uwezo wangu zinazoniaminisha kuwa lazima niuuze lau nipate njuluku ya kupatia kanywaji. Zifuatazo ndizo sababu zilizonisukuma kuuza hata kuubinafsisha ubongo wangu ili niwe huru:
Mosi, siku hizi sihitaji ubongo. Wa nini wakati nina simu janja, kompyuta na gadgets nyingine ambavyo hufikiria kwa niaba yangu? Hapa sijaongeza akili mnemba (AI).
        Pili, nina wanasiasa wanaoniwakilisha kwenye vyombo vya kufikiri kama vile kunitungia sheria hata kama zinanikandamiza au hazinifai? Hawa waungwana, kwa kutumia bongo zao, wanafanya ubongo wangu uende likizo. Hebu fikiria. Kila ufikapo msimu wa kutengeneza kura za kula, wajanja hawa huja na kunihonga udohoudoho na udonodo mwingine tena kwa siku moja. Mie, huwapa kura ya kula kwa miaka mitano. Kwa ambao hawajajiandaa, msimu huu wa kulishwa ili kuliwa soon utaanza. Mafyatu kaeni chonjo saa mbaya.
        Tatu, nina viongozi wanaotenda miujiza kiasi cha kufanya maisha yangu yawe poa. Juzi nilimsikia mmoja akisema kuwa ukiona wanakopa na kuomba, jua ni wakwasi. Kwani, makapuku huwa hawakopi kwa vile hawaaminiki. Hakuna kilichonitisha kama upupu huu. Kama ni kweli kuwa kubomu na kukopakopa ni sifa ya utajiri na siyo sifa ya kipuuzi, inakuwaje kaya zinazokopa na kufadhiliwa zinaitwa kapuku? Kama fyatu kama huyu anapewa uongo, sorry uongozi, nini haja ya kuwa na ubongo unaoudhi kama wangu wa kifyatu? Lazima niupige seli kulalike.
        Kwa vile ninao viongozi tena wenye bongo zinazochemka, shahada za juu na maono, kazi yangu ni kutafuna na kusifia miujiza hii badala ya kupoteza muda kufikiri kiasi cha kutaka zaidi ya kile nilichopewa. Hivi kuku akianza kufikiri na kutamani kulala kitandani, amfugaye atamfanya nini? Je kuku akiwa na ubongo kama wangu akaanza kuhoji ni kwanini analishwa nafaka kavu na amlishaye anakura mayai yake yenye protein, ataishia wapi? Mnajua mfugaji tamfanya nini? Na akimfanya nini, atamlaumu aliyemfanya nini au ubongo wake?
        Nne, sihitaji ubongo kwa sababu baada ya viongozi wangu kutenda miujiza na kufanya maisha yangu kuwa swaaafi katika imani, siuhitaji. Kazi yagu ni kuimba mapambio na kusifia na hii ahihitaji ubongo bali utumbo. Kusifia hakuhitaji ubongo vinginevyo chawa wasingepata umaarufu kwa kufanya kazi hii isiyohitaji ubongo.
        Tano, sihitaji ubongo kwa sababu wengine niliowahusudu kama maprofesa walionifundisha wameonyesha wazi kuwa dunia ya sasa inahitaji usiwe na ubongo bali meno, maneno matamu na utumbo ndipo uuufyatue kabla haujakufyatua. Watoto wa kihuni huita kuukata. Ukiwa na ubongo, unakukata badala ya kuukata.
        Sita, kama ni masuala ya imani, ninao viongozi wa kiroho hata wenye uroho na roho mtakakitu hata kama nyingine ni za ajabu wanaoniombea kiasi cha kutohitaji ubongo kwa kazi yoyote ya Mungu hata shetani. Kwa vile dini yangu hainigeuzi kondoo ili wachunaji wanichune, sihitaji ubongo. Ubongo wa nini iwapo naweza kula na kunywa kwa miujiza na sara? Anayebishia ili, ajiulize ni kwanini watu wanapanda neno badala ya mbegu na kuvuna utajiri tena chapchap na hakuna mwenye ubongo anayehoji. Je hii siyo miujiza? Palipo na miujiza hapahitaji kuwa na ubongo bali imani. Na imani haitaki ubongo bali kukubali kila jambo hata kubadilishiwa jina na ubinadamu.
        Saba, lijapo suala la kupata njuluku, sihitaji ubongo ndiyo nizipate. Wa nini wakati, siku hizi, hata chawa anapata njuluku nyingi kuliko mchumi. Katika usawa huu ambapo wachumi wamegeuka wachumia tumbo, na utumbo unauzidi ubongo, ubongo wa nini wakati ukifikiri kwa tumbo unapata njuluku?
        Nane, nina uzoefu mkubwa wa kutumia ubongo kufikiri. Kwanza, kufikiri kunaumiza kichwa na hata kuuchosha mwili. Pili, kufikiri kunaamsha na kujenga tabia ya kuhoji na kupinga kiasi cha mwenye kuwa nao kuonekana mchokozi na mpingaji. Nani anataka ubongo ili autumie kujiumiza kwa kuhoji na kushuku hata kupinga wateule tena wa Sir God?
        Tisa, sihitaji ubongo kwa sababu kuwa na ubongo ni dhambi kuu katika mazingira ya jinai. Ubongo ni kiungo kidogo, kama mdomo, madhara yake makubwa. Unadhani bila ubongo, waandishi wa umbea wangebanwa kama wanavyobanwa na wenye mamlaka?
        Kumi, ukiwa na ubongo, unadai kila kitu na kukigeuza haki wakati wewe si mwenye haki. Kwa kutumia ubongo wangu, kuna kipindi nilijidanganya kuwa mimi ni mwenye kaya wakati wenyewe wapo. Baada ya kugundua walivyoniangalia na kutaka kunifyatua, niligundua kuwa dawa ni kuuza au kubinafsisha ubongo. Hivyo, usinishangae na kudhani nimefyatuliwa na mibangi hadi napanga kuuza ubongo. Je wewe unao? Du! Kumbe naota!
Chanzo: Mwananchi Jana.

Thursday, 10 April 2025

‘Niite’ Fyatu Mfyatuzi Nchonga Kambarange Nyerere

 


Juzi nilimsikia tapeli na zwazwa mmoja akijita kitegemezi cha mzee Nchonga (RIP). Ajabu, nasi mafyatu wake tuliufyata tukafyatuliwa utadhani huu si utapeli. Haraka haraka, niliwasiliana na Madaraka mwana mwenyewe wa Nchonga aliyewahi kunikaribisha Mwisenge nikahiji kwenye kaburi la baba wa kaya na kuniahidi kirungu. Ilikuwa ni baada ya kung’aka baada ya tapeli mmoja wa kisiasa aitwaye Washiti kupewa. Kwa busara na unyenyekevu, alinijibu “mwalimu alikuwa baba wa wote.” Kiakili, kifyatu, na kibusara, alinikata kilimilimi nikakubali yaishe. Pamoja na kuwa kitegemezi original wa baba wa taifa, Madaraka, huwa hapendi kujiita au kuitwa Nyerere zaidi ya Madaraka.
            Kwa kuangalia uhalisia na busara za Madaraka, inakuwaje matapeli wa kawaida tena wachovu na wachafu kujivisha ubini wa Nyerere nasi tunaangalia kana kwamba ni jambo dogo na la kawaida. Japo Nchonga ni dingi wa wote, hakuwa muasharati wa kuzaa nje ya ndoa yake. Hivyo, hata kama unampenda na kumheshimu kiasi gani, hupaswi wala huna haki ya kubeba ubini wake. Isipokuwa uwe fyatu kama mimi.
        Kwanza, kama wote tutabeba ubini wake, wabaya wake watasema tunamwabudia kutokana na kutupumbaza kiakili.
        Pili, tutakuwa tunawanyang’anya au kuwanyima vitegemezi vyake wa damu utambuliko na haki zao vya msingi.
        Tatu, watatokea matapeli hata maadui kutaka kumtumia ili wafanya upumbavu wao.
        Nne, tujikumbushe. Dingi wa kaya hakupenda kusifiwa wala kuabudiwa. Kwa wanaokumbuka, alivyowahi kusema kuwa, kidini, yeye aliuwa mwanaharamu kwa vile alikuwa mtoto wa mke wa tano.
 Hata huu utakatifu anaokaribia kupewa, kama angekuwa hai, ima angehoji hata kuukataa kwa heshima kuonyesha ubinadamu na unyenyekevu wake.
 Hivyo, badala ya kubariki iwe kwa kutojua au bahati mbaya utapeli na dharau kwa dingi wa kaya, tusimame imara si kukemea, bali hata kukomesha mara moja. Tusikubali kutumiwa kwa kuwaita matapeli waliojipachika ubini wa Nyerere kwa kuwaita hivyo. Bila kujua, tutakuwa tunaingizwa mkenge na katika kumtukana na kumdhalilisha dingi wa kaya. Vitegemezi vya dingi wa taifa vinajulikana viwe hai au kutangulia mbele ya haki.
            Tano, hakuna mfano wowote wa mafyatu wa kuvaa ubini wa kiongozi wao. Hata wakristo, walipewa ukristo na siyo ubini wa Yesu kwa vile hakuwa na watoto. Walivaa ukristo kama upakwa mafuta. Kuna kipindi maadui wa uislam toka ulaya walianza kuwaita waislam Mohammedans. Waislamu walichachamaa kwa sababu, a) huwa hawamwabudii Mtume Muhammad bali kumheshimu. Pili, wao si watoto wa Muhammad kwa vile Muhammad mwenyewe, kabla ya kufariki, aliwahi kuwaambia wazi kuwa yeye si baba wa yeyote bali baba wa watoto wake.
            Mbali na kuwa uzwazwa na utapeli, kujipachia ubini wa dingi wa kaya, ni ushahidi kuwa wanaofanya hivyo wameishiwa ubunifu. Wanaonyesha, kukopa maneno ya mwanafunzi wa Mwalimu, Benjamin Mkapa, kuwa ni wavivu wa kufikiri. Wanaonyesha wanavyotumia utumbo kufikiri badala ya ubongo. Niliwahi kuandika makala kuwakata watanzania kumuita rais Samia Suluhu Hassan hasa wale ambao wamemzidi umri waliomwitua maza. Hii ni kutokana na ukweli kuwa wanafanya hivyo kumdanganya, kumtukuza, na kutaka kumtumia mbali na kumzeesha. Kila mtu ana dingi na maza yake. Samia ana watoto wake na––––kama ilivyo kwa dingi wa kaya–––hana historia ya kuzaa kabla ya kuolewa au nje ya ndoa.
            Ukiachiwa kuishiwa na kukosa ubunifu mbali na utapeli, wengi wanaojifanya kubeba ubini wa dingi wa kaya, kwanza, hawana hata dalili moja ya kufanana nae mbali na kuigiza sauti yake au kujichora kama yeye. Kiusanii, tunawaruhusu wafanye hivyo. Kiuhalisia, hapana. Haiwezekani, ukamnasifibisha simba na panya. Pia, si vizuri walevi na vichaa kufagilia makaburi ya watakatifu. Ni ujinga wa pamoja, kuwaruhusu wazinzi kufanyia uchafu wao juu ya makaburi au majina ya mafyatu wetu maarufu waliopigania uhuru wetu.
        Juzi, niliona klipu ya mmoja anayejifanya kitegemezi cha dingi wa kaya akishindwa kusoma hata hotuba ya kimombo aliyoandikiwa. Nyerere alikimanya kimombo. Sasa inakuwaje anayemuingiza ni mbumbumbu na kihiyo? Ukimuigiza mtu, lazima ujitahidi ufanane naye ili kuleta maana na kuwasilisha ujumbe juu yake mbali na kuamsha kumbukumbu juu yake. Haiwezekani nune akamuigiza simba. Nune ni mdudu na simba ni mfalme na malkia wa pori. Kupe hata kwa usanii na utani, hawezi kubeba ubini wa tembo wala ng’ombe. Wawili hawa ni tofauti kabisa.
            Nimalizie kwa kuwaasa mafyatu tusikubali uchokozi wa matapeli, vilaza, na vihiyo wanatafuta riziki hata kwa njia chafu kuwachafua mashujaa wetu walioleta uhuru huu tunaofaidi na kuringia. Wote wanaojiita watoto wa Mwalimu Julius Nyerere wakome na kuacha ili kuwaachia watoto na família yao wafaidi haki na utambuliko wao. Japo hili linaweza kuonekana ni jambo dogo, madhara yake ni makubwa. Hivi nimesema naitwa Fyatu Kambaage au Nyerere?
Chanzo: Mwananchi Jana.

Monday, 7 April 2025

Umuhimi wa Wanandoa Kutunza Siri

Kuna busara wakati wa kuwafunda wanawali katika jamii moja nchini Uganda isemayo kuwa wanapoolewa lazima wajifunze kufunga miguu na kufungua macho badala ya kufungua miguu na kufunga macho. Hii hufanyika wakati mwali akijiandaa kwenda kwa mumewe. Wazazi hufanya hivyo kwa kujua kuwa nyumbani kwa mwali huacha kuwa kwao na huko aendako ndiko hugeuka kwake. Hamjasikia kwa Waswahili wakimwimbia bi harusi kuwa ‘sasa wenda kwako, utarudi huku kutembea?’

 Busara hii, licha ya kuzuia vishawishi vya  uasherati, inalenga kuwaambia wanandoa kuwa makini na waliowazunguka kuhusiana na maisha na ndoa zao. Inawahimiza kuchambua mambo na kujua ya kusema na ya kutosema. Siyo kila jambo lazima lisemwe au kuwekwa wazi kwa wasiohusika. Tumeshagusia kwenye kitabu cha kwanza namna mashoga wanavyoweza kuvunja ndoa. Pia, tuligusia juu ya imani au ushauri visivyofanyiwa utafiti vinaweza kuvunja ndoa. Ndoa nyingi zimevunjika na nyingine zitavunjika kwa sababu hizo. Hivyo, kama njia ya kuwafunda vijana, tumeamua kuchagua kisa hiki kufikisha ujumbe na ujuzi kadhalika.

            Kuna kisa cha mama tulichosoma kwenye gazeti moja la nchini Zimbabwe. Kisa hiki ni juu ya mwanandoa mwenye majivuno na asiyetunza siri za ndoa yake. Akiwa amekwenda kusuka nywele kwenye saluni, alizoea kumlaumu mumewe kwa wenzake kuwa alikuwa akimwachia pesa kidogo. Maskini, kayaya huyu hakujua kuwa alichoona kidogo, kilikuwa kikubwa kwa wenzake. Hivyo, baada ya kuwa akijisifu kwa kumsimanga mumewe kwa ‘kutomwachia’ pesa nyingi, walitokea waliotamani wangeolewa naye wakaanza kumuandama hadi ndoa ikavunjika na  mhusika akashangaa kujikuta aliyechukua nafasi yake alikuwa ni  mmojawapo wa mashoga yake aliyezoea kumlalamikia juu ya tabia za mumewe. Kimsingi, huyu mama hakufunga miguu na kufungua macho. Alipaswa afunge mdomo na kufungua masikio. Je ni wangapi wameishashuhudia au kukutwa na haya? Je hapa utamlaumu nani kama siyo wewe mwenyewe? Huwa tunawashauri na kuwahimiza wanandoa kutofanya maisha yao au ndoa zao magazeti au matangazo.

            Je ni wangapi hufunga miguu na kufungua macho au kufanya kinyume? Je hili halina faida kubwa kwao kama watalishika, kulikumbuka na kulitekeleza?   Unaweza kujisikia raha kuwasimulia wenzako juu ya maisha yako bila kujua madhara yake. Hata hivyom si wasikilizaji wako wote hujisikia kama unavyojisikia. Hivyo, si vibaya kushauri na kusisitiza kwa wanandoa kuchambua na kujua ya kusema na kutosema. Tunajua kuwa si wote wanapata bahati au kuwa na desturi, mila, na tamaduni za kufanya hivi hasa wakati huu wa utandawazi ambapo vijana wanaweza kukulia mbali na jamii zao hadi kuoa au kuolewa. Hivyo, kwa kuliibua na kulikumbushia hili, tunalenga kuwasaidia wasio na fursa au walio nayo lakini wasizingatie.    

            Wewe na mwenzi wako ni sawa na kata na mtungi. Siri ya mtungi apaswaye kuijua ni kata tu. Hivyo, unapofungua mdomo ukaziba masikio, utaumia tu taka usitake. Kama hujaumia, ni suala la muda na si kama bali lini utaumia. Pia, ni vizuri kubainisha kuwa unapaswa kujua mambo ambayo ni siri na siyo siri. Kama hujui, acha kuongea kabisa ili usijikute ukivujisha siri ukidhani siyo siri wakati ni siri. Kwani usiposimulia juu ya maisha yako utakosa nini ikilinganishwa na kuyasimulia ukaishia kujuta? Hata habari huwa hatuzipati bure. Ima utanunua chombo cha habari kama gazeti, runinga, au redio ndio uzipate au ulipie kwa wanaozitoa. Mbali na majanga na misiba, hakuna habari za bure duniani hasa wakati huu ambapo kila kitu ni bidhaa inayoweza kutumiwa na baadhi ya watu kutengeneza faida hata kama ni kwa hasara ya au kuwaumiza wengine.

            Turejee tulikoanzia. Mbali na kushauriwa ufunge miguu na kufungua masikio, tuseme wazi. Je unakosa nini usipofichua siri zako? Je unapata nini unapozisambaza? Kwani, lazima kila unachofanya wakijue watu wakati hujui wafanyayo? Hata ukiyajua wafanyayo, kwani lazima uyafahamu kwa kuhatarisha maisha, ndoa, na siri zako? Hivyo, usikubali kuwa habari kwani si kila habari ni nzuri. Waandishi wa habari husema heri upate habari kuliko wewe kugeuka habari.

Chanzo: Mwananchi J'pili.


Saturday, 5 April 2025

Wamefyatuka wanafyatuana mbele ya mafyatu!


Juzi tilishangaa sana. Mwe! Nani angeamini kuwa mafyatu wanene na wanono wangefyatukiana na kufyatuana hadharani? Unene kweli taabu japo una raha ya kula bila kutoa jasho! Si fyatu mmoja aliyekaribu na mwenyewe kapwakia ulaji kiasi cha kuanza kuwapayukia walaji wa chini yake wasio na nasaba na mwenyewe! Fyatu huyu mwenye kutia shaka, inaonekana, hagusiki. Nani anaweza kumgusa Keinerugaby Mwana wa Mu7 pale jirani? Nasikia shemela zake nao wanafyatua ulaji simply because wanashea bedrooms na vitegemezi vya Mu7. Haka kaugonjwa kanaanza kuenea. Ukiachia mbali Mu7, Jake Zoomer wa Bondeni aliwahi kuruhusu kitegemezi chake kiitwacho Insectzane kutumia maulaji yake utadhani ufalme. Pale kwa Nyayo ya zamani, Billy Rootor na vitegemezi vyake ndo usiseme. Vinafyatua kama havina akili nzuri. Hali ilikuwa chafu hadi ikawapo ofisi ya first daughter. Mafyatu wa k ule walishupaa ikafyatuliwa mbali.
                Nchini Equatorial Guinea, kitegemezi cha mdingi ndiye makamu wa dingi yake. Wakati kaya ya jirani karibu na Diarasee, kitegemezi cha mdingi kinafyatua njuluku kama za dingi wake. Kule Gabon, kitegemezi cha king’ang’anizi aliyefyatua na kuibia kaya ile kwa zaidi ya miaka 40 kilifyatua maulaji baada ya dingi kufyatuliwa na Sir God mwenyewe. Hata hivyo, nacho kilifyatuliwa na geshi kikaishia kuuona unene runingani. Kule Tchad na Togo, bado vitegemezi vinatesa baada ya midingi yao kufyatuka na kurejesha namba.

Nirejee kayani. Japo si kwa sana ikizingatiwa kuwa Stone hakuendekeza ujinga huu sawa na Nchonga na Brother Ben Nkapa. Kamchezo ka kupeana ulaji kiukoo kanaanza kugeuka donda ndugu. Ajabu, mafyatu wanachekelea badala ya kufyatuka wakafyatyua hawa wanaowafyatua! Leo sifyatui majina ya mafyatu fyatuzi wanaofyatuana baada ya kuwafyatua mafyatu nikaishia kuchengetwa kama siyo kufyatuliwa au kuzuiwa ili nifyate. Natamani niorodheshe vitegemezi vya wanene vinavyofyatua mafyatu just because of their surnames. Wengine hata hawana surnames nene bali za madingi wa washirika wao wa bedroom kama aliyefyatuka juzi akamfyatukia fyatu mwenzake mbele ya mafyatu jamaa anayesifika kwa kufyatuka na kupayuka bila kichwa kuwasiliana na midomo.

Brother Al Chakumila upo hapo? Nilijisikia vibaya dogo fyatu wa mwenyewe alivyokufyatua mbele ya mafyatu asijue anaweza kuwafyatua wakafyatuka na kufyatua. Je kipindi hiki utapona kweli? Ilikuwajekuwaje ukamgusa pabaya fyatu wa mwenyewe? Umesahau ulivyopayuka ukafyatuliwa na kukaa pembeni hadi mwenye alipokuhurumia akakurejeshea ulaji unaoanza kudodesha? Inaonekana ufyatu umeanza kukuzidi hadi unajifyatua na kuishia kufyatuliwa. Kwanini hujifunzi au huna kumbukumbu? Ungejua namba unazocheza nazo, wala usingejifyatua ukaishia kufyatuliwa ukafyata. Umewapayukia wengine usijue duniani malipo ni hapa hapa. Sasa ona umefyatuliwa tena hadharani na unafyata. Ingekuwa mie, kwa ufyatu na ufyatuzi wangu, mbona nshajifyatua na kuachia ngazi zamani gani.

Kuna kamsemo kuwa madaraka hulevya chakari. Yakishakulevya, unapoteza uwezo wa kufikiri, kujifunza, kukumbuka, hata kuona na kukubali ukweli. Sijui kwanini mafyatu hawataki kujifunza toka kwa mafyatu waliotesa kama akina Nebukanezza, Mchonga, Jiwe, na wengine! Kufyatukiana na kufyatuana hadharani si uongozi bora bali bora uongo na uongozi. Inaboa na kukera my friends. Japo mafyatu waligoma kufyatua, angalieni msifyatuane mkaishia kuwafyatua wakawafyatua bila kutarajia.

Japo brother Moody alipomfyatua na kumfyatukia brother Al, alikuwa na pwenti, kwanini wasikutane faragha wakayamaliza au ni yale ya kutafuta ujiko wasijue wanavifua na kufuana nguo hadharani bila sababu za msingi. Huwezi kuruhusu ndinga zipitie kwenye uwanja wa mapipa hata kama una power. Huu siyo uzembe bali ni hatarishi kwa madebe na ndinga mbali na abiria. Inakuwaje kayani kila fyatu anajifanyia atakavyo kana kwamba hakuna sharia na miongozo? Huwa nashangaa kusikia eti mkuru wa uilaya anazuia say mikutano ya hadhara kwa vile wanaoiitisha ni wapingaji. Kwani wapingaji si wanakaya na wapo kinyume cha katiba? Mnamfyatua nani kwa kujifyatulisha? Mkifyatuliwa, mnaanza kulalama kama vichanga wanapofyatuliwa kutokana na ufyatu wao uchwara.

Sasa ufanye nini? Nakupa ushauri wa dezo. Achana na kufyatukafyatuka na kupayukapayuka hovyo. Utafyatuliwa. Shauri yako. Usijesema sikukuonya. Unene wa kupewa si unene kitu. Wapo wanaoulinda wakilala na kuamka wakiota ni jinsi gani waanzishe kwaya za sifa ili ulaji usiwatoke. Wapo ambao wako hata tayari kukufuru ilmradi waendelee na ulaji.

Hakuna fyatu anayenifurahisha hata kama sifurahi kama yule aliyefulia. Jamaa likifungua domo kufyatuka ni makufuru na sifa. Mara mwenyewe katenda miujiza, mara kavunja rekodi, mara hivi, mara vile ilmradi siku ziende na ulaji na ukamuaji viendelee. Kwa tunaojua haya mambo na dynamics zake usawa huu, unatumia busara ya Kijamaika isemayo play fool to catch wise. Ukijitia kujuajua na kufyatukafyatuka ukapayukapayuka, unafyatuliwa na wengine wanatesa. Nakushauri utafute the 48 laws of power upone. Hivi nshaamka usingizini?

Chanzo: Mwananchi J'tano iliyopita.