The Chant of Savant

Wednesday 5 April 2017

Kijiwe chanasa kwenye mitego ya Nay wa Kutega

Huwa wanakijiwe hawapendi mipasho wala muziki wa rapurapu uliojaa marapurapu kimawazo na kifalsafa. Mara hii, Nay wa Kutega katutega hadi tunajikuta tukiizunguka radio tukirudi ngoma ya Wapo akina Bashite kiasi cha kutegwa kama wale waliotegwa wakapiga marufuku mkuu akategua baada ya kunaswa. Unacheza na ngoma iliyowachengua na kuwachanganya wenyewe. Hakuna aliyechenguliwa  kama Kijiwe na dokta Mwakiwembe na Kanywaji hadi wakachangia mistari. Unafanya nchezo nini?
            Mbwamwitu kajilawa leo. Ajabu ameingia na radio. Kabla ya kuamkua, Mkurupukaji anamkurupusha “mzee vipi mbona umekuja na radio utadhani Mipawa kijijini kwao Kolomije Usukumani au una cha mno cha kutujuza. Mwaga pweti basi?”
            Mbwamwitu anajibu “wewe unaishi dunia gani usiyejua kinachoendelea Danganyika bin Bongolalaland usawa! Ama! Hujui kuwa ninatesa na mitego ya Nay wa Kutega aliyowatega wasiotegwa wakategeka na kunasa kiaibuaibu hadi wakamkubali? Hebu kula ngoma hii.” Anafungulia radio na muziki wa Wapo unahanikiza. Wapo wanaoburuzana, wapo, wapo wanaosagana, wapo , wapo wanaolindana, wapo, wapo wanaodanganyana kwa kulindana , wapo, wapo wanaodai wanajiamini wakati ni woga, wapo, wapo, wapo akina Bashit, wapo, wapo akina Bashite, wapo…. Wapo wapo wapo wapo tu.”
            Baada ya kutengua kitendawili kwa kusikiliza muziki wa Bashite Wapo, Kapende ananena “alaa! Unaongelea hili zali lililowaacha watukufu uchi huku wakijifanya kukubali na kusifia kilichowatia ukakasi wasijue tunajua mchezo mzima? Ama kweli, ukisikia sanaa ndiyo hizi. Yako wapi; walituzodoa kuwa tunapenda udaku wakaishia kuupwakia tokana na kujifanya hawashauriki?”
            “Mwenzenu niiposikia nikajua mtego umenasa tena kirahisi. Kwanini  hawakutaka kujua kuwa huwezi kujua yote na azima Basheti atumbuiwe tu? Why didn’t they undershtands a simple thing aik this?” Mgoshi Machungi anaamua kujikumbusha darasa lake la nane na nkoloni.
            Mijjinga anakula mic “sasa kama kujichanganya nakunasa kwenye mitego huku, Nipe Mapepe wamefukuza wanini wakati jipu lenyewe linazidi kuiva kiasi cha kuanza kujitumbua lenyewe ukiachia mbali uoza wake kuzidi kumchefua hata daktari mwenyewe? Au anataka mtumbuaji atoke Koromije au hadi akina Ney wakorome na kukoromija zaidi kuwaamsha wachovu? Je wengine waliofungiwa miziki yao watafunguliwa lini au hadi wawaguse wanene na kuwaaibisha baada ya kuwashika na umma kuwaijia juu? Beng’we ni makoye gambiti lulu.” Kabla ya kuendelea Mzee Maneno anachomekea “hiyo lugha gani ndugu yangu au unaongea kwa lugha kama matapeli wa neno? Si utafsiri lau kiduchu lau tuelewe na kuhoji mantwiki ya kunachotaka kueleza au vipi?”
            “Hiyo ni lugha ya kiKolomije ambayo maana yake ni  jamani haya matatizo kweli kweli sasa hasa usawa huu ambapo mtoto wa Kolomije anakoromewa na kuromijiwa hadi munene anaanza kujipiga mtama kwa kuruhusi vigongo vinavyomnanga au ndiyo mwanzo wa kuvunja ndoa yao ya mashaka? Who knows  what doctor Booze is contemplating ?” anajibu Mijjinga.
            “Wapo wapo wanene waliofoji vyeti; wapo waniolindana; wapo wakoromije:.” Radio ilihanikiza baada ya Mbwamwitu kuifungulia ghalfa. Acha nasi tuanze kuitikia “wapo tena wapo wapo wapo wakingoja kutumbuliwa hata kama ni wa Koromije.”
            “Yakhe sasa hii nvurugu. Sie tusojue rapu mwatuweka wapi au nami nirapu kipemba?” Mpemba analalamika.
            Msomi Mkatatamaa ankula mic “Hapa lazima tuseme ukweli. Hakuna cha kupenda wimbo wa Nay wa Kutega bali kuficha uso ili kuepuka aibu. Amewachonganisha na umma kiasi cha kusoma alama za nyakati na kuramba matapishi yao. Kama waliupenda wimbo huu, kwanini waliupiga marufuku na kumkamata wa Kutega? Wameumbuka; hata wafanye vipi kutuweka sawa, tunajua wameumbuka kweli kweli tokana na ubangaizaji na ukandamizaji wao. Eti wasivyo na aibu wanasema nasi tukaao vijiweni tuingizwe kwenye wimbo."
            Kabla ya kuendelea Kanji anakula mic “hii Kokomije naleta tabu sana kwa kaya. Sasa kama vote nasema toka nangoja nini? Mimi iko kwenda Koromije kukoromije yeye na ile nalinda yeye.”
            Sofia Lion aka Kanungaembe anamchomekea Kanji “thubutu yako urejeshwe Bombei bila nguo. Huyu haguswi. Ni kipenzi cha mwenyewe kwa sababu wajuazo. Ama kweli walisema wahenga. Ukishangaa ya Kanywaji utaona ya Koromije! Hivi kunani katika kulindana huku na kwanini? Inaonekana dokta kazimia kwa mgonjwa halo halo!”
            Mheshimiwa Bwege anakula mic “Mie muziki huu umenikuna. Sijawahi kuona wanene wakipashwa na kupashika hadi wananasa kwenye mitego kama ilivyotokea. Tokana na kujikomba, kila kigogo sasa anataka apige picha na Ney wa Mitego wakati ni unafiki mtupu. Kama muziki huu unawakuna, kwanini waliupiga marufuku? Sijui hapa wanamdanganya nani kushindwa kukiri kuwa wameurejeshwa kwa kuogopa hasira za umma? Mie nashauri waliupiga marufuku muziki huu na kumweka lupango wa Mitego washughulikiwe lau tujue walifanya makosa badala ya kutufunga kamba kuwa wanauzimia huu muziki wakati rohoni wanaugulia wakitafuta namna ya kumkomesha aliyewatega. Asipochunga ataishia kutegwa badala ya kuwatega wao.”
Kijiwe kikiwa kinanoga si akapita dokta Mwakiwembe na Nay wa Kutega! Acha tumpe kampani wa Kutega huku tukimzomea doc kwa kuramba matapishi yake. Kufumba na kufumbua si yakapita mashankupe ya ndata na BASUTA? Acha tuwasute na kuwazomea kwa kujikomba!
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.
           
           
          

No comments: