How the Berlin Conference Clung on Africa: What Africa Must Do

How the Berlin Conference Clung on Africa: What Africa Must Do

Sunday 13 October 2024

Wanandoa Si Njiwa wala Chui

Kuna imani kuwa njiwa ni viumbe wenye mapenzi ya kweli. Ni wapole na wapenda amani. Mara zote, utawaona wawili wawili, akiongezeka basi jua ni makinda yao mawili ambayo nayo yakishapevuka, huondoka wawili wawili kwenda kuanza maisha yao ya wawili katika uwili huu wa kuvutia. Kutokana na maisha na tabia za njiwa, viumbe hawa wanahusishwa na sifa zote nzuri kubwa zikiwa ni amani, upendo, na usafi. Wanazo nyingine nyingi tu.
            Kwa upande mwingine, kuna ndoa ya hovyo ambayo hakuna yeyote angepeda kuwa nayo. Hii ni ndoa ya chui. Kawaida, chui wanakutana wakati wa kujamiiana. Mama akishatunga na baba kutungisha mimba, wawili hawa wanamalizana kila mmoja kivyake.  Hawa wanyama ni wanyama wapenda milki au territorial. Wanaishi kwenye maeneo yao kila mmoja na lake. Inapotokea mwingine akaingia kwenye eneo lisilo lake, atafukuzwa hata kuumizwa na mwenye eneo. Hivyo, chui, kimsingi, hawana ndoa zaidi ya kujamiiana na kila mmoja anachukua hamsini zake. Hata hivyo, hawa ni hayawani walionyimwa utashi ingawa hata njiwa ni wanyama ambao huenda upendo na ustawi wao si chaguo bali matokeo ya majaliwa yao.
            Sasa tuje kwa binadamu. Kwanza, kiakili, binadamu si wanyama ingawa kibaolojia ni wanyama. Hivyo, wana vitu viwili vya ziada yaani akili kubwa na utashi ambavyo wanyama hawana ingawa bado vitu hivi vinaweza kutumika vizuri au vibaya kulingana na mazingira, malengo, na sababu za wahusika kufanya hivyo. Kwa binadamu, japo siku hizi ni chaguo, ndoa ni lazima. Maana, bila ndoa, idadi ya watu katika eneo au nchi fulani hata duniani itapungua. Hivyo, pamoja na mambo mengine, ndoa ni kiwanda cha kutengeneza watu kwa ajili ya kesho japo siku hizi mambo yamebadilika kiasi cha watu kuoana kwa ajili ya kuishi pamoja bila kuzaa. Huu nao unaitwa uhuru hata haki ya binadamu ambayo haiulizi kama wazazi wa hawa wanaoamua hivi nao wangekuwa kama wao, wao wangekuwa wapi. Leo, hili halitushughulishi. Kwa wale waliokwisha kuoa na kuolewa, hakuna jambo lenye furaha kama kuingia kwenye taasisi hii. Jambo hili, mara nyingi, huwahushisha watu zaidi ya wawili ingawa wawili ndiyo wenye shughuli. Hii ni kutokana na ndoa kuwa kiungo baina ya familia hata jamii. Kadhalika, hakuna jambo linatia karaha na kusikitisha kama kuvunjika kwa ndoa. Hii ni kutokana ukweli kuwa wawili walioingia kwenye mahusiano ya maisha kwa malengo ya kuishi pamoja hadi mauti, wanapofikia kugeuza kibao kiasi cha upendo kuwa chuki, madhara yake si madogo wala ya muda mfupi.
        Siku zote, ndoa huanza na mapenzi na chaguo lililo bora japo laweza lisiwe. Katika macho ya wahusika, anayechaguliwa ndiye anayeonekana bora na wa kufaa katika wengi. Hivyo, tunaweza kusema kuwa ndoa nyingi huanza baina ya njiwa na kuvunjika baina ya chui. Hivyo, basi, ieleweke, wanandoa ni wanandoa na si njiwa wala chui. Yawapasa kulijua hili na kuwa tayari kukubaliana na madhaifu na ubora vyao ili kuweza kuishi na kutumiza ahadi na nadhiri walizojiwekea.
Jambo la kujiuliza ni kwanini ndoa huanza kwenye unjiwa na kuishia kwenye uchui? Hakuna jibu moja wala rahisi hasa ikizingatiwa kuwa maisha binadamu ni mchanganyiko na mkusanyiko wa mambo mengi yawe ndani au nje ya wahusika. Kama wataweza, japo hili wamefanikisha wachache kulinganisha na walioshindwa, wanandoa wajenge ndoa yao kama njiwa ili kuepuka kujenga ndoa ya chui. Hapa zinahitajika juhudi za makusudi kulifikia lengo hili pia, ni kazi ngumu inayochukua muda mrefu.
        Mwisho, lazima kuzingatia kuwa, licha ya kuwa taasisi, ndoa ni mchakato wa maisha wenye kila aina ya changamoto na vikwazo ambavyo wanandoa wanapaswa kuvijua na kutafuta namna ya kuvigeuza kuwa fursa wakijua kuwa wenzi wao siyo njiwa wala chui bali binadamu na wanandoa wenye kila aina ya mapungufu na ubora kadhalika. Shikilieni yaliyo bora na kuachana na yasiyo bora. Angalieni na kushikilia mambo yanayowaunganisha kuliko yanayowatenganisha mkijitahidi sana kuwa njiwa na kuepuka kuwa chui.
Chanzo: Mwananchi leo.

Garagaring Mbinu Rahisi ya Kuula Kirahisi

Juzi nilikumbuka msemo kuwa wajumbe si mafyatu. Nikiwa najivinjari na kutafuta namna ya kufyatua njuluku au unene bila kuhangaishwa kuandika application au kutaja sifa za kufanya hivyo, niliwakumbuka wanafalsafa watatu. Hawa jamaa, kwa wakati tofauti, waligundua kuwa wanene wanapenda sifa na kuabudiwa. Hivyo, kama unatafuta cheo au njuluku toka kwao, wewe jishushe, garagara chini na kuwaramba miguu, watakupa utakacho bila kutoa jasho zaidi ya sanaa. Kifyatu, hii inaitwa garagaring au sanaa ya kuula kirahisi bila kujihangaisha au kuhagaishwa.
Katika kusoma saikolojia, nimegundua kuwa wenye power wanapenda sana kuliwazwa, kuduwazwa, hata kufyatuliwa kisanii. Unawapa wanachotaka, unapata unachotaka. Unakumbuka kisa cha mfalme zwazwa aliyehadaiwa na mganga wake kuwa akitoka uchi, atangudua namna wajoli wake wanavyomgwaya. Bila hata chembe ya aibu, mfalme aliwaita wajoli wake hekaluni akavua nguo zote na kuamuru atembezwe macherani ili aone wajoli wake watafanya nini.  Na kweli, amri ya mfalme ilitimizwa. Alibebwa uchi wa mnyama na kuzungushwa mbele ya kadamnasi akiwa mwenye furaha na mashawasha kujua nini kitatokea.
Kwa vile tabia ya wajoli ni ndiyo mzee au ndiyo mama, walianza kumshangilia kwa nguvu. Mfalme, bila kujua sanaa na unafiki wa wajoli alifurahi na kuamini alikuwa amevalia vazi la kupendeza asijue walikuwa wanamchora na kumuingiza kichaka ili wajaze matumbo yao. Ukiondoa Fyatu Mfyatuzi na watoto wachanga, nani angemwambia ukweli mfalme kuwa alikuwa uchi? Nani angemwambia wakati wengi waliomzunguka na kumsifia walikuwa ni wachumia tumbo waliokataa kutumia vichwa na ubongo wakaamua kutumia matumbo na utumbo? Nani angemwambia ukweli mchungu wakati alikuwa amezungukwa na wanafiki, wasanii, na wasasi wa ngawira wanaoweza kuuza utu wao ilimradi tonge liingie kinywani? Angeabiwa na nani wakati alikuwa amezungukwa na wanyonya damu kama chawa?
Ukiachia kisa cha mfalme juha, kuna kisa kingine. Baada ya watu wa kaya ya kombaland kujikuta hawana hakaki na majaliwa yao hasa wale waliokuwa wamepewa ulaji tokana na usanii wa kugaragara chini, waligundua kuwa bila kumsoma dingi na kujua apendacho, unaula wa chuya. Hivyo, walikuja na usanii mmoja. Kila walipomuona dingi, walianguka chini wengine kupiga magoti, wengine kusujudu, wengine kuita ‘baba baba’ kila fyatu lake ilmradi apate mradi wake. Kwa wanafalsafa kama mimi, kilichokuwa kikitokea ni utapeli ambapo mmoja hununua dhahabu feki kwa fedha feki wote wawili wakiamini wamempata mwenzao. Sasa nini faida za mchezo huu? Faida ya kwanza, ni kupata usichostahiki kwa kutumia mbinu zisizostahili. Faida ya pili, ni kupata dezo bila kuhenyeka japo kujigaragaza si kuhenyeka tu bali kujidhalilisha na yule unayemgaragaria.
Je nini hasara za usanii huu unaonuka? Kwanza, ni kupata stahiki bila ya stahiki. Pili, ni kwa mtoaji kuamini wasioaminika, kuwadhalilisha na hata kujidhalilisha bila kujua. Tatu, ni kujenga tabaka la wababaishaji, waganganjaa, na wasanii ambao ukwasi ukikutoka wanakutosa kimasomaso bila aibu kwa vile hawana aibu. Nne, ni kutopea katika udhalilishaji wa mafyatu japo nao wanajidhalilisha kwa kutumikia matumbo badala ya jamii.
Japo mbinu hii inaweza kuonekana rahisi, si rahisi. Maana, wahusika, kwanza lazima wajidanganye na kudanganyana. Pili, lazima wadhalilishane na kuhadaana. Waswahili husema kuwa hii ni sanaa ya kupakana mafuta kwa mgongo wa chupa au kukumbatiana wakati mmeshika visu au mikuki. Tatu, ni kuibuka tabaka la kupe hata chawa wasiojiamini au kuaminika. Ukizungukwa na mafyatu, wasaidizi, au watumishi wa namna hii, licha ya wao kutojiamini, nawe huwezi kujiamini au kuwaamini. Maana, kila aliye na tonge yeye ni wao na asiye nalo si wao hata kama alikuwa wao jana. Viumbe wa namna hii ni kama chawa. Hawana kumbukumbu wala hisia zaidi ya hamu na nia ya kufyonza damu. Bila kunyonya, hawaishi. Na bila kunyonywa huwapati. Unaweza kuwapata, mwishowe watakupata udhani umewapata. Bwana Mkubwa Mwana wa Maria alipoingia Jerusalemu, alitandikiwa mitandio, vikoi, vitenge na matawi akiimbiwa kila nyimbo za sifa. Siku ya kusululubiwa ilipofika, hao hao waliomkweza, kumsifu na kumshangilia walikuwa wa kwanza kusema ‘asulubiwe asulubiwe.’ Na kweli alisulubiwa wakamuona mshamba!
Je inakuwaje fyatu mwenye akili na madaraka akaangukia mtego huu? Kwanza, lazima akubali kujirahisisha au kurahisishwa ili apatikane kirahisi. Pili, lazima apende au kuwa mlevi wa sifa hata zipatikane kwa njia haramu na zisizo na sifa kitu zaidi ya rongorongo. Pili, lazima ujidanganye ili wakudanganye. Tatu, lazima upende vitu vya rahisi rahisi ambavyo mwisho wake ni kukurahisishia maanguko yako. Tano, lazima ushindwe kujua kuwa unaodhani wanakupenda na kukuogopa hawakupendi bali kukuponda na kukudharau. Kuna mfalme mmoja alikuwa na wajoli aliowateua kuwa wasaidizi wake na kufanya kosa kuwaamini. Siku moja, shushu wake akipita kwenye kigwena chao, aliwasikia wakimnanga mfalme. Aliamua kuwarekodi na kumpeleke mfalme mpenda kuabudiwa. Mfalme hakuamini hadi anakufa kuwa kumbe rahisi inaweza kuwa aghali.
Tumalizie. Rahisi rahisi yaweza kuwa aghali na hatari. Hilo ndilo somo la leo. Hivi, ninaongelea nini?
Chanzo: Mimi.

Wednesday 9 October 2024

Nikiwa Rahis Nitanunua Matrekta na Nyavu si Mashangingi

 


Mwaka huu, inshallah, nitagombea urahis. Kwa vile kaya yetu ni ya vyama vingi, natimiza wajibu wangu. Kwanza, nataka nilete siasa mbadala ambapo kipaumbele change kitakuwa ni kuwakomboa mafyatu kiuchumi na kijamii kwa kuwawezesha kula na kushiba na kujidai kama fyatu yeyote aliye huru kwelikweli. Pili, mimi ni mpenzi wa maendeleo shirikishi ambapo kila fyatu lazima aonje keki ya kaya yake na kuifaidi. Pia, naamini kuwa uhuru halisi na wa kweli maana yake ni kwa mafyatu wote kufurahia maisha yatokanayo na uhuru walioupata baada ya kuupigania hadi wengine kumwaga damu. Huwa naamini pia, katika usawa wa mafyatu wote iwe katika kufanya kazi au kula. Hatuwezi kufanya kazi pamoja halafu kwenye kula, wale wachache na wengi waendelee kufa au kulala njaa. Hivyo, mikakati yangu ya kutaka mnichague niwafyatue, sorry, niwatumikie na si kuwatumikisha ndiyo hii hapa. Hivyo, jueni. Sasa mie ni rahis mtarajiwa. Aaamina. Nionye. Sera zangu nimezisajili na nina hati milki yake. Hivyo, atakayedukua sera zangu, nitamfanyia kitu mbaya kuliko anavyoweza kudhania.

Nikichaguliwa kuwa rahisi wa kaya, sirkal yagu haitapoteza mabiioni kununua mashangingi na mashankupe kwa ajili ya wanene kujienjoy na kufaidi wakati mafyatu tukifyatuliwa na shida. Ninunue mashangingi na mashankupe ya nini wakati tunayo ardhi lakini hatuitumii vilivyo zaidi ya kuikalia? Sambamba, tuna walaji lakini hakuna la maana wanalofikiria wala kupanga zaidi ya kula, kula, na kula zaidi. Mataifa mengi kama yale ya Mashariki ya kati hawana ardhi japo wanakula tena sana tu. Hivyo, nitanunua matrekta na kuwakopesha wakulima ili walime tuwalishe walaji hawa wenye ukwasi wa kutisha utokanao na wese.

Nitanunua mitambo ya kuchimba madini yetu ili yaweze kunufaisha mafyatu wote na vizazi vyao badala ya kunufaisha wachukuaji. Cha mno, nitasomesha vitegemezi vyetu hasa elimu ya uchimbaji gasi na madini ili faida ibaki kwetu badala ya kwenda nje kuwanufaisha wengine tena wasioyatolea jasho zaidi ya kusaini mikataba uchwara.

Juzi, nilipiga mahesabu na kugundua kuwa trekta moja ni bei chee na kidogo kuliko shangingi na shumbwengu. Je njuluku inayofujwa kwenye mashangingi ingeweza kununua matrekta, vitabu au kulipa madaktari na maticha wangapi? Hiyo njuluku ingetengeza ajira ngapi? Ingeondoa au kupunguza ukapuku kiasi gani? Ingeleta usalama kiasi gani? Zingeondoa au kupunguza ujinga kiasi gani? Zingeokoa maisha ya mafyatu wangapi? Je mnapoifuja zaidi ya kuongeza magonjwa ya moyo, ulahibu, unene, dhambi, na woga wa wale mnaowafyatua, mnapata nini? Don’t buy land cruisers. Instead, invest on landLet tractors till the land instead of cruisers to cruise the land.

Msipoteze njuluku kununua takataka kama midude ya bei mbaya aka magari ya starehe inayowafilisi kwa kunywa mafuta mengi na kuzidi kufilisi mafyatu wenu, vidani na upuuzi mwingine kwa ajili ya wake na washikaji zenu. Hiyo midude inachafua mazingira hata mifuko mbali na jamii ya mafyatu wachovu wanaoona kama wanaenjoiwa na wachache waliofanya kosa kuwaamini maulaji yao yaliyobinafsishwa na genge dogo. Kwani, mkistaafu au kupoteza ulaji wala hawawezi kuvivaa na kujidai na kujienjoy bila vibaka kuwang’oa masikio kwa upande wa vidani. Kwa mashangingi, mtayasikia bombani.

Angalia mnavyoishi kwenye magereza yaliyozungushiwa mikuta kwa kuwaogopa mnaowafyatua kwa mauti yenu. Mimi sitaigiza ufujaji kama ule unaofanywa na matajiri wa Du Buy wanaoendesha vijikaya vile kama maduka yao binafsi tokana na kuendeshwa kifalme. Wao wanatanua na wako salama tokana na mifumo yao. Wana uhaba wa mvua lakini si akili kama sisi wenye uhaba wa ubunifu, ukweli, upendo, na uoni wa kesho. Siku mkifyatuliwa na kuzama kaburini hamtachukua hata picha zake. Umekuja bure, utarudi bure. Hata ukijenga uwanja wa njiwa kijijini kwako, ukifa, unageuka jiwe wazi la kuanikia mazao ya wale uliowafilisi. Badala ya kujiangalia, nitawaangalia waliniamini na kunipa ulaji wao. Sitaufanya ulaji wa mafyatu kuwa wangu, marafiki au familia yangu. Mie nitanunua vitabu ya kiada tena vinavyofaa badala ya vile vinavyotungwa na mafyatu wezi wanaojuana na wenye kuvipitisha ili watoto wa mafyatu wapate elimu safi. Nitanunua madawa ili kupambana na magonjwa. Zaidi ya hapo, nitawalipa matabibu na maticha vilivyo ili kuwaelimisha na kuwatibu mafyatu watakaoniamini na kunipa ulaji wao.

            Kabla sijasahau, nitahakikisha nanunua magari ya wagonjwa. Je nitafanyaje hivi? Kama ninavyopanga kuyapiga kalamu mashangingi na mashumbwengu, nitapiga kalamu ndinga za ndata. Kwanini, kununua zana za maangamizi badala ya zana za kunusuru maisha?

Namalizia. Naombeni mafyatu mnipe kura ya kula ili nile. Sorry, nimesemaje? Natania. Sitakula bali kulisha wale wenye njaa walionipa ulaji wao. Tumeelewana? Basi, fanyeni kweli tulete mapinduzi ya kweli kwetu na mafyatu wooooote. Hizo ndizo sera zangu. Kumbe naota! Hii mibangi na mipombe, we acha tu.

Chanzo: Mwananchi leo.

Monday 7 October 2024

Ndoa, Tendo, na Faida Zake

Leo tutadurusu ndoa na mambo mengine yanayohusiana nayo. Moja ya mambo yanayohusishwa na ndoa nit endo la ndoa. Sisi tutaiita ibada. Wengine wana majina yao. Wapo waiitayo ibada, dawa, chakula cha usiku nakadhalika. Ukilidurusu neno ndoa, inakuwa rahisi kuliunganisha na kitendo, yaani tendo la ndoa. Hapa, hatuhitaji kuelezea nini tunamaanisha.         Ndoa ni mambo mengi ingawa kubwa na la kwanza nit endo, tendo la ndoa. Ni tendo la ndoa linalozalisha watoto. Ni tendo hili huongeza upendo, amani, na furaha katika ndoa. Hivyo, bila tendo lake, ndoa siyo ndoa na bila ndoa hakuna tendo la ndoa ingawa wapo wanaolishiriki katika kile kiitwacho uzinzi ila si tendo la ndoa. Ni zinaa. Tendo la ndoa huwa tendo la ndoa pasipo ndoa, ni uzinzi wa kawaida tu. Badala ya kuwa ibada, tendo la ndoa huwa machukizo na hufichwa kwa vile ni aibu na dhambi. Linapotendwa na wanandoa, tendo huwa baraka, ibada, na kitu cha kuonea fahari mbali na kuridhika nalo.
            Bila tendo, hakuna ndoa. Zifuatazo ni faida na sababu za Mungu kuumba tendo la ndoa ili kudumisha na kuendesha ndoa.
Mosi, bila tendo la ndoa kwa wanandoa, hakuna ndoa bali msiba, lawama, majuto, hata kifo. Kama mwanandoa au wamanandoa hawawezi tendo la ndoa, hakuna ndoa, na kama ipo, ni kwa muda tu.
            Faipili, tendo la ndoa ni dawa ya usingizi. Kwa walioko kwenye ndoa, jiulize au jikumbushe. Nini hutokea baada ya tendo la ndoa?
            Tatu, dawa ya msongo wa mawazo (stress) na upweke ukiachia mbali kuupa mwili mazoezi ya kiakili na kibailojia. Tendo hili, hasa kwa wanaume, huunguza karoli nyingi kiasi cha kuwapunguzia siyo stress to bali mafuta mwilini. Kwa mujibu wa jarida la Women’s Health (2018), wanasayansi waligundua kuwa wanaume huunguza karoli nyingi kuliko wanawake kwa uwiano wa 101  kwa 69 mtawalia ndani ya dakika 25.  Hata hivyo, kwa wanaolifanya tendo hili bila kuoa au kuolewa, laweza kuongeza msongo wa mawazo hasa hofu ya kubeba au kubebesha mimba. Ndiyo maana tunasisitiza kuwa tendo la ndoa linawafaa wanandoa kuliko wasio wanandoa.
            Nne, licha ya kupunguza msongo wa mawazo, tendo la ndoa linaweza kuondoa mawazo na kuleta ridhiko na liwazo. Kwa upande wa pili, hali siyo hivyo kwa wale wasio wanandoa.
            Tano, ni daraja na kiunganishi baina ya wawili. Kwa wanandoa, kadri muda unavyokwenda na kupata uzoefu, kuna aina fulani ya mazoea na utegemezi hujengeka baina ya wawili hawa. Wanandoa wanapofikia kiwango hiki, huwa na ridhiko kiasi cha kuona kama kuchepuka ni ujinga, ugonjwa au kujitengenezea balaa hasa ikizingatiwa kuwa kufanya hivyo kunaweza kusababisha kumpoteza mwenzako.
            Sita, ni hakikisho na ushahidi kuwa wawili wanapendana na kuhitajiana. Wengi wa wanandoa wenye ugomvi au kutokuelewana, huchokana kiasi cha ima kusalitiana hata kuuana ili wapata fursa ya kupata wale wanaodhani wanaweza kuwapenda au kuelewana nao.
            Saba,  chachu na kichocheo cha ushirikiano, upendo, na uhakika wa utegemezi baina yao. Wanandoa wenye ushirikiano na upendo wa kweli, hutegemeana karibu kwa kila kitu. Kwa wale ambao wazazi au mababu na mabibi zao wameishi kwenye ndoa hadi uzee, anapokufa mmoja, mara nyingi, wanaume hufuata tokana na kukosa ule ushirikiano, mazoea, upendo, na hakikisho katika maisha. 
       Jarida la PLOS (Machi, 2023) lilifanya utatifi juu ya matokeo ya ujane katika nchi za Singapore, Uingereza, na Denmark na kugundua kuwa wanandoa wenye kuanzia miaka 65 kwenda juu wanaweza kufariki ndani ya mwaka mmoja wa kufariki kwa mwenzi wao ambapo wanaume walikuwa 70% ikilinganishwa na 28% kwa wanawake. Hivyo, msishangae kuona wanaume wanakufa wanapofiwa na wake zao. Ni kutokana na mazoea na utegemezi na ukosefu wa hakikisho kimaisha.
            Nane, ni kitu cha lazima na muhimu katika maisha. Ni sawa na chakula au mahitaji mengine muhimu kwao. Ndiyo maana wapo wanaoliita chakula cha usiku.
    Mwisho, ni chanzo cha furaha hata huzuni. Ni mara ngapi umesikia kuwa mwanandoa fulani kaua mwenzake kwa kunyima tendo la ndoa (ibada)? Ni kipimo cha afya ya mwili, roho, na mapenzi.
Chanzo: Mwananchi Jana.

Friday 4 October 2024

Barua ya Wazi kwa Waziri, IGP, na Bosi wa TISS


Wapendwa,
Kwanza, nimshukuru mhe. Rahis kwa kuwapa muda mjitafakari na kufanya maamuzi kabla hajawawajibisha kuliko tumuwajibishe tokana na ushauri wangu. Sijawahi kuwasiliana nanyi. Hii ni mwanzo hadi kieleweke. Kwa uchungu, japo kichizani, nina hisia, mapenzi, maoni, mawazo, na haki kama nyinyi. Naomba niwaulize maswali yafuatayo nikiwakilisha mafyatu kama kiongozi wao:
            Kwanza, mna hisia kama machizi mnaowaangusha? Je mnaonaje hii jinai, kadhia, na kashfa isiyoisha ya utekaji, upotezaji, ufungaji, na uuaji wa mara kwa mara­­­–––kama wahusika, mnaionaje? Kama mnaifahamu na kuelewa, mmefanya nini kutatua na kukabiliana na janga hili? Mwajua wajibu wa nyadhifa zenu? Kama wazito, nini kazi yenu? Mmechukua hatua gani? Je nafsi zenu huwa zinawasuta? Wanaotekwa kupotezwa wangekuwa watoto, wake, ndugu, hata wakubwa zenu mgefanya nini? Mmewahi kuvaa viatu vya wahanga na wapendwa wao lau kihisia? Je, mmeshindwa tatizo hili, kwanini? Nini kifanyike kwa nafasi na nafsi zenu? Mnajua maana ya neno kuwajibika au mnangoja kuwajishwa? Kama hamjui, makelele na mashinikizo na ushauri vya bure kufanya maamuzi magumu mnavisikia na kuvielewa au la? Kama hamvielewi, kwanini? Kama mnavielewa, mmefanya nini au kwanini? Msaada gani mngetaka wahanga na umma wa machizi wahanga wawape kuepusha aibu kwenu, taifa, na bosi wenu na umma walioaamini dhamana hii? Mnataka wangapi wafe, kutekwa, kupotezwa, kuuawa, kuteswa, kudhalilishwa, kudhulumiwa, na kuhujumiwa iwaingie akilini? Je, mnapokea mishahara na marupurupu kwa nini? Mmewahi kujitathmini lau kiduchu? Kama mngeambiwa mjitathmini, mngejipa maksi kiasi gani, na kwanini na nini mungeamua? Kuna ugumu katika hili au mngependa/kutaka muwajibishwe?
            Mkitafakari maswali, mengine kapuni, ngoja nizamie historia iliyotukuka yenye mafunzo mengi ya mzee Ali Hassan Mwinyi (RIP Sana bro) walipouawa watu kule Kanda ya Ziwa––––mmojawapo akiwa [N]zegenuka kama sikosei––––hakungoja kuwajibishwa.  Roho ilimuuma. Nafsi ilimsuta. Imani yake ya kidini ilimkaripia. Nadhani hata washirika zake wa bedroom walimuonya. Kwanza, hakuhusika. Pili, hakuweza kuvumilia uoza. Tatu, alifanya maamuzi magumu. Nne alijiuzulu Januari 22, 1977. Tano, tokana na uadilifu, usafi, na weledi, baadaye kitendo hiki kilimwezesha kuwa dingi wetu kwa miaka kumi akiacha urathi uliotukuka. Sita, aliepuka kumfedhehesha bosi wake na kumtishwa mzigo wake japo haukuwa wake peke yake. Saba, alikubali yaishe kumondolea bosi wake taabu ya ima kuwajibishwa au kujieleza kama siyo kuonekana wa hovyo, asiyefuata sheria na viapo, au asiyewajali waliomwamini na kumpa maulaji aliyompa katika vicarious liability (kwa kisambachikwa wasomi wenzangu. Kama si wanasharia, niulize au waulize wenzangu walioko karibu yenu.
Tuache usomi kisheria, tuongee na kuulizana kichizani. Je mnajua kadhia hii? Kama hamjui, kwanini? Kama mnajua, inawafundisha nini? Je mnaielewaje na mantiki yake? Je mnaweza kuidurusu lau mpate somo na uamuzi mujarabu wenye faida kwenu, wahanga, na taifa? Mnaelewa madhara na uzito wake? Mmetafuta ushauri kisheria?
            Nataja majina. Bw. Hamad Yusuf Masauni, Camillus Mongoso Wambura, na Suleiman Abubakar Mombo mpo? Mwangojani?  Kwanza, mnaichukuliaje kashfa hii inayoishia milangoni mwa ofisi zenu? Inawahusu au la? Kama ndiyo, mwangoja nini? Kama haiwahusu, inamhusu nani zaidi ya bosi wenu? Mngependa au kupanga mujiwajibishe, kuwajibishwa, au kutaka hata bosi wenu awajibike wakati hahusiki moja kwa moja ingawa anahusika hasa ikizingatiwa kuwa ndiye aliwapa nyinyi maulaji? Kwa kashfa hizi za kinyama zilizogeuka donda ndugu, huwa mnalala usingizi kama mimi na wengine? Kama mnalala, kwanini? Kama hamlali, mpaka lini? Majina yenu ni ya dini hata kama ni za kigeni. Mnaamini kweli? Kama kweli, mmezitumiaje kuona mwanga? Je mmepuuzia imani zenu au ni waumini jina? Mlipoapishwa na mkaapa, mlibeba vitabu tulivyoaminishwa ni vitakatifu hata kama ni suala kujadilika? Kama mlivishika na kuviinua juu, mnavitenda haki au kuvihujumu mbali ya kujihujumu binafsi, taifa, bosi wenu, hata familia zenu mbali ya ufyatu na uumini wetu?
            Mkitafakari/kupanga kujibu maswali yangu­­­––––hata kama msiponijibu bali kujijibu––––tafakarini sana. Mngekuwa familia, jamaa, na ndugu za wahanga, mngetaka mfanyiwe nini au nini kifanyike? Je mmewahi kuwashirikisha washirika zenu wa bedroom kupata jicho la pili/ushauri? Juzi, nilimsikia bosi wenu ‘akiamuru’ vyombo vya uhasama, sorry, usalama vijichunguze. Je hii ni sahihi au vunga ili joto lishuke? Nani aweza kujichunguza akatenda haki hasa kama si mchizani na si malaika au Chizi Mchizani mwenye nguvu za ajabu za kanywaji? Je hii ni haki na sahihi? Je mmeshaurina naye au la? Kwanini? Kama mmemshauri, anasemaje  na mnasemaje? Je hili la kuwajibika, kujiwabisha, au kuwajibishwa ni gumu kiasi cha kuhitaji PhD kama yangu? Kati yenu na bosi wenu, nani mngetaka abebe hili zigo la kashfa na uchafu, maana naona Chakudema wameamua kukinukisha kama mbaya, mbaya japo ndata nao wametunishia misuli. Je watawazuia bila kukomesha utekaji na upotezaji machizani.
            Du!  Kumbe nafasi imejaa! Ngoja niishie kabla sijatekwa na kunyotolewa roho.
Chanzo: Fyatu Mfyatuzi.

Nilivyojinusuru Kutekwa

Nikiwa kwenye basi naelekea zangu home si zikaja njemba saba hivi zikiwa na defender uchwara yenye nambari fichi. Bila hili wala lile, si zikaniamuru nishuke ziniteke. Weee! Nilijiinua kwenye siti na kupiga samasoti za ki-Bruce Lee na kupaa hewani usiambiwe! Bila kufanya ajizi, nilichomoa pingu zangu na kusema “mnarekodiwa na kurushwa mtandaoni live.” Kabla ya kutafakari, nilikunja ngumi na kujiweka tayari kana kwamba niko kwenye goju ryu session. Nilifanya Banguazhang, Choy Li Fut, Hua Quan, Wudang, Wing Chun, na mitindo kama ishirini hivi kwa kasi ya umeme. Njemba hazikuamini macho yao.
Kuona na kusikia hivi, njemba zilianza kuonyesha kugwaya waziwazi huku zikitazamana na kuishiwa maneno zisiamini kuwa mie ni fyatu asiyefanyiwa masihara hata na siafu. Nami bila kungoja, nilipiga tena samasoti na kusimama yowe tayari kufanya maangamizi. Nilisema ‘hatekwi fyatu hapa. Mie ni bwanga la mjini kwa kisambaa. Kabla ya kuendelea, nilitoa cha moto na kuweka kidole kwenye usalama tayari kufanya maangamizi, maana siku hizi tunaruhusiwa kuwa nacho. Sikupindisha maneno. Nilisema “nikienda home nitaangalia sura zetu halafu nami na mafyatu tuwatafute tuwateke na kuwapeleka kwenye runinga ya mafyatu ili mafyatu wote wawaone.” Nilipiga tena samasoti, kutunisha misuli huku nikinguruma kama chui alindaye vichaga vyake, na kuzoza “ tuhesimiane. Mjue tutawanyaka na kuwataabisha kabla ya kuwapoteza. Tutawateka bila kuwapoteza kabla hamjatwambia nani aliwatuma na kwanini mlitaka kunifyatua msijue mie ndo mwenyewe Fyatu Mfyatuzi aliyefyatuka na afyatuaye bila kuogopa lolote wala chochote.”  Njemba kuona na kusikia hivyo, zilitoka harakaharaka na kuingia kwenye defender yenye namba za kutia shaka na kutokomea. Mafyatu waliokuwapo walianza kuzoza kuwa huyu si bure. Ima ni mwenzao au ni komandoo. Mie nilichuna.
            Kwa taarifa ya watekaji, mimi natembea na kamera fichi inayorekodi kila ninapokwenda isipokuwa nikichepuka, huwa naizima ili bi mkubwa asinifyatue. Kutekana, kwangu, ni mambo ya kizamani na kinyama. Ni ushamba na ukumbaff ambao sasa nimeamua kuukomesha haraka ili tuishi kwa amani na ustawi.
            Hivyo, nashauri mafyatu wote, kuanzia leo, wajichue kwenye madojo ili wawe fit kupambana na watekaji na ikibidi nao wawateke ili waonje joto ya jiwe ka jusi. Pia, nawashauri mafyatu wote kuanza kutembea na kamera fichi ili kuwafichua hawa watekaji waliojificha. Pia, nina mpango wa kuiomba sirkal ituruhusu njemba zilizomanya makung Fu na magujulyo kama sisi kumilki na kutembea na pingu ili tuisaidie kuondoa aibu na kadhia hii ya kishamba. Kama nyie mnateka mafyatu wasio na hatia si muende mukawateke mafisadi. Kumbaff zetu kubwa. Unapomteka fyatu na kumnyotoa roho, unaumiza familia yake na jamii. Unanyotoea mlipa kodi na mpika kura ya kula ya wanene. Mnataka wanene wasichaguliwe na kunenepa siyo? Mshindwe na mlegee. Nawachukieni sana nyie wana hizaya. Mnafanya mafyatu wachukie ndata na sirkal bure tokana na ujuha wenu. Sisi ni mafyatu wa amani hata kama ni ya imani. Hatutaki utekaji. Sasa nawaamba msikie na muelewe. Nasi wahanga tuaanza kuwateka ili mjue raha ya kutekana ilivyo. Haiwezekani njemba kama mimi niliyesomea Uchinani na Ujepu mambo ya karate, Kung Fu na madude mengine ya kutisha ninyamaze wakati mafyatu wangu wanateketea kwa kutekwa na kunyotolewa roho. Si utani wala mkwara. Nitakula nanyi chungu kimoja tuone. Mkizidi kujito akili, najitoa ufahamu. Hatuwezi kugeuka kaya ya watekaji utadhani wote woga.
            Ili kuepuka kuwateka bi mkubwa na vitegemezi vyangu, kuanzia juzi, nimeanza kuwafundisha madude yangu ili nao wasaidie kupambanana kansa hii ya kishenzi. Senzi kabisa na mkome na kukomaa kabla hamjakomolewa na hao mnaodhani na nyanya kuteka na kupoteza. Nasema, tena kwa herufi kubwa. Hatekwi fyatu hapa. Ukiteka tunateka, ukipoteza tunapoteza ili tuone. Kama mbaya mbaya. Loh! Mna habari mie ndiye nilikomesha komando yoso na panya road? Kama hamjui, mtajua hamjui. Dawa ya fire ni fire au siyo?
            Sasa msiseme sikusema. Nasema tena kwa kujimwambafy. Ukija kuniteka, jua nitakuteka kabla hujaniteka. Ukija kunipoteza, utapotea na kupotezwa ukijiona. Nataka nianzishe chuo cha makarate na makung fu ili nitoe mafunzo bure ili kuhami na kulinda mafyatu wangua. Hawakunichagua niwe mzigo kwao. Nitawakomboa liwalo na liwe.
            Hivyo, natangaza hadharani, kuanzia leo, watekaji wajue. Ukija kuniteka, nakuteka. Ukija kunipoteza, nakupoteza. Ukija kunifanya kitu mbaya, nakufanyia mara mia. Mie sina mchezo wala utani na maisha. Kwanza, tunaishi mara moja. Pili, msidhani wote ni wachovu wa kutenza kichovu na kijinga. Kwa wasionijua. Mie ni komandoo aliyesomea vyuo vyote vya kikomandoo duniani. Nina mikanda kama sabini hivi ya Karate na Kung Fu. Na kuanzia leo, mjue, nina cha moto, pingu, vitoa machozi, pilipili washa, na zana nyingine ambazo ni top secret. Cha mno, mjue nawajua watekaji na mafyatu wasiojulikana. Nitawaambia mafyatu nyinyi ni nani pale nitakapowateka kabla ya kuwapoteza.
            Ngoja. Hii defender inataka nini? Ngoja nitoke nduki wasije wakaniteka nikawateka na kuwapoteza bure. Tuonane wiki ijayo jamanini.
Chanzo: Mwananchi J'tano iliyopita.

Monday 30 September 2024

Mkeo Siyo Ngoma Upige




Mkeo ni mwenzi. Umtunze akutunze, umpende akupende, na ukimtesa utateseka. Hata hivyo, kuna imani potofu za baadhi ya makabila ambazo hatujui kama ni za kweli kuwa bila mume kumtandika mkewe inaonyesha hampendi vilivyo. Kadhalika, kwa baadhi ya makabila na karibu yote, dhana hii inashangaza na kufanya hata kuwa vigumu kuielewa achia mbali kuikubali. Gereza ni gereza hata liwekewe vyakula safi na kila anasa. Na kipigo ni kipigo na hakuna kipigo kizuri, kinachokubalika au kuzoeleka.
        Kabla hujaamua kumpiga au kumdhulumu mwenzako, jiulize. Je ningekuwa yeye ningependa nitendewe au nitenzwe vipi? Tunarudia. Mkuki kwa nguruwe kwa binadamu mchungu. Sie waandishi siyo malaika. Pia, siyo mashetani. Tuna udhaifu wetu kama binadamu wengine. Ila tuna ubora ambao tunaweza kusema wengi hawana au unaoweza kuwafunza wengine vitu vya maana tokana na uzoefu wetu katika taasisi hii adhimu na ngumu. Pamoja na kukaa kwenye taasisi hii yenye kila aina ya changamoto na maadui, hatujawahi kupigana au kuitana majina mabaya hata siku moja. Tumewahi kununiana. Hili ni jambo la kawaida kwa binadamu. Hatujawahi kutukanana hata siku moja.
        Hatuandiki haya kinadharia, kujifurahisha, au kumfurahisha yeyote bali kufunza na kushare uzoefu wetu. Tumeyaishi na kujua kuwa yanawezekana. Kama yamewezekana kwetu, kwanini yasiwezekane kwa wengine? Amani, furaha, na ufanisi katika ndoa ni suala la uamuzi ila ni muhimu. Hata mafarakano, huzuni, na maanguko katika ndoa ni masuala ya kupima na kuamua.
Tutoe mfano wa mwanandoa anayemdhulumu au kumuumiza mwenzie. Je ni haki kwa mwanandoa huyu kutegemea kutendewa kinyume na atendavyo? Wahenga walisema kuwa dawa ya moto ni moto. Japo wanawake, mara nyingi, hawatumii fujo kama wanaume inapotokea ndoa ikawa na dhuluma na unyanyasaji, wana namna yao ya kulipiza kisasi hata kama wapo pia wanaosamehe, kuamua kuachana, au kuvumilia hata kuachika. Kumpiga mkeo, licha ya kumuumiza na kumdhalilisha, ni kumuonea na kumdhulumu. Ni dhuluma kama dhuluma nyingine.
        Kuna rafiki wa familia ambaye alikuwa na tabia ya kumtukana na kumpiga mkewe tena mbele ya watoto wake wachanga bila kujua kuwa angewaambukiza watoto uhovyo na ukatili huu.             Siku moja akiwa kazini, mtoto wake mmoja alimuomba mama yake ampe ice cream (hatuna Kiswahili chake). Mama alimpa ice cream. Hata hivyo, mtoto hakutosheka, pamoja na kupewa ice cream nyingi tu tena jioni jambo ambalo humsababishia kukosa usingizi na si jema kiafya.         Mtoto aliomba tena apewe ice cream. Safari hii, mama alimkatalia. Bila hili wala lile, yule mtoto mdogo alimrushia kibao mama yake huku akifoka kama afanyavyo baba yake. Kujua tatizo vilivyo, mama hakumrudishia kibao zaidi ya kumuonya asirudie. Mtoto naye hakukubali, badala ya kumpiga tena, alimwambia “kwanini nisikupige?”  Mama alimjibu mtoto “kwanini unipige kosa langu nini?” Mtoto alijibu “mbona baba huwa anakupiga na haelezi ni kwanini?”
        Mama alimdanganya mtoto kwa kumshauri asome kitabu na mtoto alisahau lakini bila kujutia. Je wewe baba unayempiga mkeo, ungekuwa wewe ungefanya nini? Ungemfanya nini yule mtoto? Si rahisi kujibu. Na kama ukijibu, majibu yatakuwa mengi na tofauti. Kwa ufupi ni kwamba, kama walivyosema wahenga, kazimbi si mchezo mwema.         Watoto wetu ni sisi wa jana na kesho. Hivyo, tunapofanya mambo, tusijiangalie au kuwaangalia tu wale tunaowaonea au kuwadhulumu. Dhuluma kwa mama ni dhuluma kwa mtoto. Hivyo, iwe ni mila au imani, kumpiga mkeo si jambo jema. Kuna jenga chuki ya chinichini na madhara yake yanaweza kuwa makubwa na ya muda mrefu kuliko unavyoweza kudhani. Mtoto wa nyoka ni nyoka.
        Hivyo, ni vizur ukajua kuwa kupigana ni udhalilishaji na ukatili. Je hakuna njia nyingine za kuonyeshana mapenzi au kutatua ugomvi?
Kisa kingine, kuna jamaa mmoja alizoea kumpiga mkewe mara kwa mara. Mama alichukia na kumwekea kisasi. Alipougua akawa hana uwezo wa kujisaidia, alihitaji mkewe amsaidie. Mkewe alimjibu “sitakusaidia ili upone uendelee kunipiga. Nawe, acha ugonjwa ukupige uonje uchungu wa kuumizwa.”
        Tumalazie. Mkeo siyo ngoma upige. Ni binadamu mwenye kuumia, anayehitaji heshima na mapenzi na si matezo na udhalilishaji. Je unapata faida gani kumuumiza mwenzio uliyeahidi kumpenda, kumlinda, na kumtunza ili naye akutenze hivyo?
Chanzo: Mwananchi jana.

Saturday 28 September 2024

How Berlin Conference Clung on Africa: What Africans Must Do

 



ISBN9789956554645
Pages478
Dimensions224x170 mm
Published2024
PublisherLangaa RPCIG, Cameroon
FormatPaperback

How Berlin Conference Clung on Africa

What Africans Must Do

by Nkwazi N. Mhango

The book How Berlin Conference Clung on Africa: What Africans Must Do aims to expose the root causes of Africa’s struggles, including colonialism, greed, and artificial national divisions. It examines the lasting impact of the Berlin Conference of 1884-85, where European powers divided Africa, leading to dependence and underdevelopment. The book also criticises the role of African leaders in perpetuating these divisions and hindering progress. It argues that the artificial borders created at the Berlin Conference have been detrimental to Africa, and calls for unity and a rejection of the colonial legacy to achieve true independence and prosperity.




Wednesday 25 September 2024

Kwanini Tumeamua Kuwa Wafungwa wa Hiari?


Mafyatu wenzangu naomba nianze na swali la kifyatu. Umewahi kujiuliza ni kwanini tumejigeuza au kugeuzwa wafungwa katika magereza ya kujitakia tena kwa kuyajenga wenyewe? Naona yule anatikisa kichwa. Nadanganya au huoni? Nenda uishiko. Kama kuna kibopa, angalia mjengo wake. Kila mjengo uitwao mjengo, umezungushiwa kuta. Je kuna tofauti gani na gereza? Je hili ndilo jibu? Je tatizo ni nini? Je tufanye nini? Je hatujiingiza hasara wakati njuluku ya kuondoa insecurity ni ndogo kuliko ya kujenga mikuta?

 Hata magereza yana nafuu kwa sababu unatumikia kifungo chako unaachiwa huru. Hili gereza la kujitakia ni la maisha. Kuwa huru ima ufe au upae mbinguni na mwili wako kama kile kitegemezi cha Josefu wa Nazareti kwenye zile ngano za zamani. Pia, unaweza kuwa huru kama utakuwa apechealolo aka kapuku.Japo ukapuku ni kitu kibaya, lau unakupa uhuru ambapo ukwasi unawafanya mafyatu wenye nao kuishi magerezani tena ya kujitakia na kujilipia. Hapa ndipo ulipo mzizi wa shule ya leo.

Acheni ufisadi kwani unazalisha wizi iwe ni wa kujitakia au kulazimika.

Tumegeuka jamii ya mijizi, mibaka, na vibaka. Mtu analala maskini. Anaamka tajiri. Hatuhoji wala kushuku ni miujiza gani amefanya! Hivi hawa mafyatu wanaokokotoa mafyatu badala ya kokoto mbona hawakokotoi hawa majambizi? Leo jambizi linatufyatua na njuluku zetu. Badala ya kulifyatulia mbali likafyatukia ima gerezani au kuzimu, eti tunaliabudia. Ebo! Enyi mafyatu wakumbaff, nani aliwaroga hadi mkafyatuka kinyume na kuabudia majizi na masanamu?

Mie Ntume Fyatu kwa mafyatu nasema, fyatueni majizi na majambazi wa njuluku zenu bila kujali cheo wala saizi. Inakuwaje mnaabudia mihalifu na kuwadharau madingi waadilifu waliotumikia jamii kwa uadilifu maisha yao yote wanaishi kimaskini wakati vibaka waliozaliwa jana wanaishi na kuogelea kwenye utajiri usio na maelezo wala kueleweka? Tell me. Naona yule anacheka akidhani sikijui kitasha wakati nilizaliwa utashani na kukulia umakondeni. You get it or it gets you? Usinicheke kwa kuongea broken ingilishi wakati wewe unaongea kiswanglish kama waishiwa wa njengoni. 

Mafyatu wa hovyo na wenye roho za wizi wanasema eti ujanja kupata. Ujanja si kupata ni umepata kihalali? Kama wewe umetumia kalamu kuiba, kwanini mafyatu wasitumie mapango kukuibia? Kama umetumia mtutu kuiba, nawe lazima tukunyake. Kama unateka wenzako na kuwapoteza, lazima tukunyake liwalo na liwe. Unapofyatua au kupiga njuluku za mafyatu, unatengeneza jamii isiyo salama na maskini. Wanene wanazidi kuiba ili kujenga mikuta na kuongeza walinzi wasijue kifo kinapenya hata kwenye moto.

         Hata ujizungushie mibomu ya nyuklia, kifo kikiamua kukutembelea kinakunyotoa roho tu. Je hizi kuta zinakupa uhakika wa kutofanyiwa kitu mbaya? Hebu jamanini tufikiri pamoja. Tumeishiwa akili hadi tunajisalimisha kwa jinai tena jumla na kirahisi hivi? Nani katuroga ingawa fyatu simo?

            Huwa nashangaa kuona mafyatu wakishangaa wafungwa wanapokuwa wamelindwa. Kwani, hao mandingi wenu hawalindwi kama wafungwa? Hawafungwi na ulaji wao tena mwingi wa haramu? Kama siyo wafungwa, kwanini wanalindwa? 

        Mbona mimi silindwi? Si kwamba mie sina njuluku za kuweka mabaunsa, sina kwa sababu siyo mhalifu wala siyo mshamba na wala usalama na uhai vyangu havitegemei ulinzi bali uadiilfu wangu. Hivyo, sihitaji makandokando wala makomando, kunilinda au kujieleza. You know what I mean. Nani anapenda kuishi kama msukule kulindwa wakati ulinzi wa kweli ni kugawana na kutendeana haki? 

        Hapa Ukanadani, majumba yetu hayazungushiwi kuta bali maua. Unaweza hata kulala mlango wazi na usiwe na hofu kwa vile kila fyatu hapa anakula na kushiba. Hili ndilo jibu la kuwa huru na salama. Pia, hili ndilo kubwa nililojifunza utashani. Lazima wanene wahakikishe wadogo wanapata milo yao yote mitano kwa siku. Nani anataka ulinzi wakati ulinzi wenyewe bandia? Anayelinda Mungu. Huoni hata papa na wachungaji mbali na wachunaji wanaojifanya kutenda miujiza wanalindwa na binadamu na bunduki kwa vile hawamuamini Mungu wanayemhubiri na kutumia kutengeza njuluku? Mie siyo bwege wa kupatikana nikidhani nimepata kama wao wanaolindwa kama wahalifu.

            Leo naandika kwa uchungu tokana na mafyatu wangu walio wengi wanavyosota. Pia, wote tunaangamia na kuangamizana tokana na kutoa majibu yasiyo sahihi katika matatizo yetu kama jamii ya mafyatu. Ukitaka jamii iliyo safi na salama, tenda haki. Hakikisha kila fyatu anafyatua milo yote mitano kwa siku uone. Badala ya kupoteza njuluku kwenye vikuta na walinzi, unakuwa na ulinzi wa uhakika. Huku hutuogopi ndata wala kutekwa. Nani atamteka nani wakati utekaji ni jambo la kijima na kinyama? Hata waanimo hawatekani. Huku waanimo wana haki sawa na mafyatu. Hivyo, usishangae jirani yako kuwa sungura tena aliyenona asiyeogopa kufyatuliwa na fyatu jangili kama huko.’

            Leo, nawataarifu kuwa nimeastaafu siasa. Hivyo, nitakuwa nafyatua mambo ya kijamii na siasa kwa mbali pale nitakapohisi kufyatuliwa. Wasalaaam.

Chanzo: Mwananchi leo.

Tuesday 24 September 2024

Mume Si Fedha, Elimu, wala Madaraka


 

Hivi karibuni kumezuka matapeli hata wadhalilishaji, tena wengine wasomi, wajiitao wataalamu wa ndoa na saikolojia ya mwanamke wanaipotosha jamii hata kuiibia kwa kisingizio cha kutoa ushauri juu ya ndoa. Watu hawa, kwa kujua na kudandia mfumo dume, wawe wanaume hata wanawake, waganganjaa, waganga wa kienyeji, na viongozi wengi wa dini wa kujipachika wamejigeuza wataalamu wa saikolojia ya ndoa na wanawake. Wanatoa ushauri ambao hauingii akilini vinginevyo mwenye kuuchukua na kuuamini ima awe na mjinga hata mpumbavu wa kutupwa, kuzidiwa, kutapatapa au kukata tamaa.
            Hivi karibuni tulitumiwa clip ya mshauri anayetambulishwa kama daktari wa saikolojia. Jamaa huyu anaongea bila aibu tena kwa mjumlisho (generalisation) na kujiamini. Anadai eti wanawake ima ni kama watoto au ni watoto kwenye masuala ya kutafuta fedha. Anadai kuwa kila mwanamke anaamini kuwa kila mwanaume ni gwiji wa kusaka pesa. Hivyo, wanaume wasilalamike wanapokuwa hawana fedha. Je hii ni kweli?
            Sisi kama wanandoa ambao tumedumu kwenye ndoa kwa miaka 27 tumestushwa na ushauri huu wa ajabu na hovyo. Kwa kutumia ujuzi na uzoefu wetu, tumeona huu ima ni kutojua, udhalilishaji wa akina mama au hata kuganga njaa.  
    Kwanza, haiwezekani wanawake wote, kama binadamu yeyote, wakawa na tabia sawa katika jambo moja, yaani uwezo wa mwanaume kutafuta fedha. Hata wanyama hawana tabia moja inayofanana kwa wote kwenye jambo moja. Hata mbuzi hawafanani kitabia. Mmoja anaweza kupenda kushambuliwa mashamba na kula mazao. Mwingine anaweza asipende kushambulia mashamba kwa vile alishaumizwa alipofanya hivyo nakadhalika.
         Kimsingi, uwezo wa mtu wa kutafuta au kutotafuta fedha unategemea mambo mengi kama vile mipango, motisha, uzoefu, malengo, makuzi, ndoto, aina ya jamii anamotoka, muda, mazingira, aina ya shughuli anayofanya kumuingizia fedha nakadhalika
        Pili, ni imani potofu kufikiri kuwa kila mwanamke, ima ni tegemezi au anaolewa kufuata fedha na si kutekeleza malengo na mipango yake kama binadamu. Hivyo, licha ya kuwa udhalilishaji na uongo, ni ujinga na upofu kudhani kila mwanamke anaingia kwenye ndoa kutafuta au kufuata fedha. Ingekuwa hivyo, wanaume maskini wasingeoa. Haimaanishi kuwa hakuna watafuta fedha katika ndoa hasa wanaosukumwa ima na tamaa binafsi au baadhi ya mila za kinyonyaji kama vile kutaka mume awe buzi la kumtunza mhusika na watu wake. Hii siyo kwa wote.
        Tatu, ni imani potofu na kutowajua wanawake kama binadamu wa kawaida wenye uwezo sawa na wanaume kudhani kuwa ni tegemezi kwa wanaume, hivyo, wanafikiri kuwa kila mwanaume ni mashine kutapika fedha yaani Automated Teller Machine (ATM) ambayo huwa haiishiwi au kukosa fedha. Hata ATM, wakati mwingine, huishiwa fedha na kungoja wahusika waongeze nyingine.
        Nne, kuna wanawake matajiri ima wa kutafuta au kurithi wanaojua kuitafuta, kuitunza na kuitumia kuliko wanaume ambavyo pia wapo wanaume wa namna hii. Unapodai eti wanawake wote wanaamini wanaume ni ATMs, unajikumbusha kuwa wapo matajiri, wasomi, wenye madaraka tena makubwa kuliko waume zao? Hawa nao si wanawake?
        Tano, ni wanaume wangapi waliooa wanawake matajiri kama vile Mtume Muhammad aliyemuoa Khadija mama aliyerithi utajiri mkubwa licha ya kuwa mfanyabiashara maarufu zame zile kule Makka. Je hili nalo watalisemeaje hawa watalaamu wetu wenye kutia shaka? Je waliioa tena wanajulikana toka kwenye familia maskini nao vipi?
        Pamoja na utaalamu, usomi na mengine kama hayo, wengi tunashauri kutokana na maisha yetu yaliyojengwa katika misingi fulani. Hivyo, usishangae mshauri unayemuamini au kumtegemea sana, akashauri kitu kisichokuingia akilini. Hivyo, tunasema asemacho kinaweza kuakisi ya maisha yake binafsi ambayo pia yanaweza kuhitaji ushauri japo yeye ni mshauri. 
        Binadamu hawezi kukimbia maisha na tabia zake. Kinyonga hata abadili rangi zake vipi bado ni kinyonga. Kama umesomea ushauri na maisha yako hayafanani na unachoshauri au unashauri utopolo, jua kuna tatizo. Faida za kitu chochote lazima zianze nawe. Huwezi kuhubiri maji ukanywa mvinyo. Kwa ufupi, katika ndoa, mume au mke si elimu, fedha, au madaraka bali ni mume au mke basi. Mengine, ni makandokando tu.
Chanzo: Mwananchi J'pili.

Tuesday 17 September 2024

FYATU MFYATUZI: Mrume kutoka kama manzi, unataka nini?


Juzi si nilifyatuka nikataka kufyatua nisijue fyatu mwenyewe nuksi! Si katika kujimwambafy, mtaani kwetu, nikakutana na njema amevaa hereni, suruali za kubana, na akijitembeza kinamna nikamshobokea lau nimfyatue. Fyatu nilidhani mwenzangu mdenge kumbe mrume aliyeanza kujiharibu hata kabla ya kuharibiwa. Ongea kidogo Bi Mkubwa asikusikie ukanifyatulisha au maadui zangu wakainyaka na kunirostisha kama yule katibua mkuu wa CcM aliyefyatuka na kukwareka asijue atafyatuliwa na kukitoa bila kuaga. Hivi dume zima kuvaa hivyo untakani jamani? Afa fyatu akikutokea un’anza kusema eti waogoopa poopobawa! Hapa unamaanisha nini kama siyo biashara tena biashara yenyewe chafu na haramu jamani? Je hawa mafyatu wanaoyafanya haya wanajua madhara yake kwao binafsi na jamii kwa ujumla au ni ulimbukeni wa kuigiza kila uchafu toka majuu ambako upopobawa umehalalishwa na kutetewa kama haki za mafyatu?  Kama mnataka kuishi kama watasha wakati nyinyi si watasha si muende kwao muone watakavyobagua. Si mlimsikia yule Bwana Mkubwa wa Rumi akifyatuka kuwa sasa makasisi waubariki upopobawa? Hayo tuyaache na kuwaachia wenyewe.

 Bila hili wala lile si nikadhani kaingia kwenye kumi nane zangu. Bila ajizi si nikatupa nyavu ili nimnase huyu msupu kumbe dude! Ile kupiga mbinja, si fyatu akafyatuka na kuchaji akitaka kunikungfuu eti namgeuza totoz. Lahaula! Kwanza, sikujua la kusema wala kufanya mbali na kupigwa butwaa nisiamini. Sasa kama wewe si totoz, mrume mzima unatilia vipuri kama totoz tukufanyeni kama siyo kufyatuka tukakufyatua? Basi, jamaa lilijifanya linayaweza ma kung-fu na magujulyoo! Kwa vile fyatu nina blackbelt, si nilimfyatukia kwa kupiga show kwa kusamasoti na kukrow hadi hadi akafyata. Utani tuache.

Huu ulimbukeni utamaliza baadhi ya mafyatu wetu. Sijui ni ufyatu, ujinga, au ukumbaff, sijui. Nisaidieni kabla sijapagawa na kujinyotoa au kumnyotoa fyatu roho. Unakuta fyatu jeusi kama lami eti linachora tattoo. Kwanza, mnajua maana yake? Ukiyaambia mafyatu yachanje kama akina njomba, yanasema hayo ni mambo ya kizamani na ya kishamba wakati mishamba ni yenyewe miana hizaya! Hii ni nini kama siyo kumtafuta paka mweusi kwenye kiza tena kinene? Kwani hizo tattoo na chale zina tofauti na upya gani kama siyo ukumbaff? Mikumbaff mingine ikiwa misupastaa siku moja kwa vile inafokafoka kwenye mic, inatoga masikio, inavaa milegezo, na kujichorachora mitattoo na kujiona iko Hollywood. Mtaliwa. Shauri yenu hata kama chama twawala chawala lakini si hivo mtavoliwa nawaonyeni fyatu nyie.

            Tokana na kukosa fyatu waliofyatuka kimaadili, siku hizi maadili yamegeuzwa madili. Zamani huteuliwi wala kupewa ulaji wa umma bila kufanana na umma. Mfano, zama zile, lazima kila anayeteuliwa iandikwe historia yake. Siku hizi? Hata msafara wa maza ni siri. Wateule wake ni siri. Wanaandikwa majina bila kueleza walivyozaliwa, kukua, kusoma, kuoa au kuolewa. Nani anataka aseme kila kitu wakati kuna hata wakwe wa maza waliopewa unene tokana na ukwe na siyo sifa? Nani anataka kutangaza majina ya wanaoandamana naye wakati kuna wengi wasiostahiki wanaofaidi ulaji wa dezo. Kaya hii inaliwa. We acha tu. Badala ya njemba kufyatukia kuliwa huu yanafyatukia na kushobokea ukumbaff wa maigizo ya kila uchafu.

            Turejee kwa huyu sijui nimwite sheitwan au aduw’Allah. Hata sijui. Baba zima eti linaweka kipindi puani halafu linataka lisipelekewe mashambulizi. Kama wewe unayaweza, dada zako watafanya nini mwana hizaya wee ibn muthnaxyz wal mujirm na mumu nyambaff kabisa? Sasa mnanilazimisha kufyatua kimanga kama Dip Weed na washikaji zake kule kukuu! Hivi nayo imefilia wapi au mafyatu wamefyatuliwa na kufishwa kinamna hadi wakaufyata ili waliwe uzuri? Mkiendekeza ukumbaff na ulimbukeni huu, mtapotezwa. Hivi jibaba linalojifanya manzi linaweza kufyatua vitegemezi vya nguvu kama vyetu? Mambo ya totoz waachie wao ufanye mambo ya warume hata kama ni kabuyange.

            Fyatu zima linajigeuza bwabwa. Hivi wazazi wako wangekuwa kama wewe ungekuwapo? Lazima niwafyatukie lau kieleweke. Sijui kwanini wanene wenye maulaji hawayafyatui mafyatu kama haya yanayosababisha laana Kayani na wana maslahi gani nayo? Wenzenu kwenye miji ya Gomla na Sodimu waliteketezwa, halafu mnatulete laana na ukumbaff wenu? Au mnafuata mafyatu ya kitasha yanayotaka kuwapunguza baada ya uzazi wa mpango kugoma kwa kuwaingiza kwenye gharika hili la kujitakia? Nyambaff kabisa. Mnaniuzi hadi natamani nifyatue hii mifyatu kwa kuinyotoa roho.

            Juzi nilisikia eti na manzi nao wanafanyiana mambo ya kabuyange! Kwani mawe ya kusagia yameisha hadi nao wafanye hayo mambo? Loh! Hicho kisagio mnacho au kujihadaa ili mfanane na watasha uchwara waliolaaniwa na kutaka laana zao zienee duniani ili wote tukose? Nenda kayafanye sauzi uone watakavyokuletea watu wa kukufanyia vitu ili ukome na kukomaa. Bahati yenu. Ningekuwa dingi wa kaya hii mbona ningewanyotolea roho mbali lau muwahi kuonana na ibilisi bosi wenu. Yaani warume wameisha hadi manzi wasyagane au mibaba igeuzane mitutu wakati manzi bwerere?

Hivi nimesemaje?

Chanzo: Mwananchi Jumatano iliyopita.

Monday 16 September 2024

Ndoa ni darasa jifunze na ufunze


Tuanze na kisa cha wanandoa wawili marafiki na wageni waliotutembelea hapa nyumbani. Walitoka Toronto kuja Manitoba. Hivyo, ilibidi walale lau tujadili hili na lile. Baba ni kutoka nchi jirani ya Tanzania. Mama ni mkanada mzaliwa wa Toronto. Ilipofika wakati wa kulala, tuliwakumbusha watoto wetu kwenda kupiga miswaki na kwenda vyumbani kwao. Baada ya hapo, na sie tuliwaaga wageni wetu kuwa tulikuwa tunawenda maliwatoni kupiga mswaki. Hawakuamini kama ambavyo nasi hatukuamini baada ya kueleza mshangao wao. Wale wanandoa walitushangaa kwanini tunapiga miswaki kabla ya kulala. Nasi, tuliwashangaa. Mama alisema kuwa akipiga mswaki wakati anakwenda kulala, asingeweza kupata usingizi mbali na kinyaa cha kufanya hivyo! Nesaa naye alimwambia kuwa akilala bila kupiga mswaki, asingepata usingizi. Hivyo, tulishangaana kama ambavyo hushangaana kwenye mbalimbali ambapo huishia kujisuta wakidhani wanawasuta wenzao.

Sasa unaweza kujiuliza. Kama una mazoea safi ya kupiga mswaki kila ulalapo , utajiuliza hata kushangaa inakuwaje walale bila kupiga miswaki. Ukiangalia kisa hiki, kinahusu jambo dogo lakini lenye umuhimu mkubwa na la binafsi lakini kinaweza kukufunza mengi. Je ni mangapi wanandoa hawayajui japo ni muhimu?

            Mnapofunga ndoa, kila mmoja anakuja na mambo yake, yawe mazuri au mabaya. Kila mmoja anakuja na mazoea yatokanayo na malezi, mazingira hata uchaguzi na utashi wake. Ni kapu mchanganyiko. Hivyo, mnapoanza kuishi kama wanandoa, jambo kubwa na la muhimu ni kuwa tayari kujifunza na kufundisha. Ndoa ni kama darasa au shule isiyokuwa na mwisho. Ili kuifanikisha, wanandoa, bila kujali viwango vya elimu au umri, lazima wawe tayari kuwa wanafunzi na walimu kwa wakati mmoja. Ukiangalia hili la kutopiga mswaki wakati wa kulala, pia laweza kuwapo la kulala bila hata kuoga. Binadamu ni viumbe wachafu. Unapalala mchafu, unategemea kweli mambo yaende vizuri? Umeshinda unakula, kujisaidia, kutoa jasho na mengine. Sasa inakuwaje unalala m chafu? Je kwa wale waliozoea kulala bila kupiga mswaki au kuoga hawajapata la kujifunza hapa? Je wale wenye utamaduni wa kuyafanya haya hawana la kuwafundisha wasioyafanya?

            Binadamu tuna mazoea na mila tofauti na saa nyingine kinzani kiasi cha kuchekana na kuishia kujicheka bila kujua. Mfano, kuna jamii huko bara Asia ambayo huamini kuwa kuramba vidole ni kuonyesha kuwa chakula kilicholiwa ni kitamu! Ukila na kumaliza bila kuramba vidole wanakushangaa kama unavyowashangaa kwa kuramba vidole. Pia, huko huko, wapo wanaokula kwa kupwakia na wengine wakiongea. Ukila kimya, bila shaka watakushangaa kama utakavyowashangaa. 

        Pia, kuna mazoea mabaya zaidi kwa wanandoa kula chakula cha usiku (wakubwa mnatuelewa) kwa kupigishana makelele bila kujali watoto hata kama wapo chumba cha pili hasa kwenye jamii za kibinafsi za Magharibi. Wakati kwa Waafrika hili ni mwiko, kwa wenzetu hutushangaa inawezekanaje kula chakula cha usiku cha baba na mama bila kupigishana makelele. Nasi huwashangaa inakuwaje wapige makelele kama nguruwe kiasi cha kuharibu watoto wao.

 Kwa watu hasa wa Pwani, haya ni makufuru. Je wanapooana watu toka kwenye hizi jamii tofauti, kweli hawana la kujifunza na kufundisha? Inakuwaje mtu ule kama mbwa, kuramba vidole, au kupwakia kama fisi? Unaweza kuhoji.

Turejee kwenye ndoa kama darasa hata shule. Je wewe au mwenzako alishawahi kukutana na mazoea, mila, au tabia ambazo ni tofauti hata kinzani na za mwenzako. Je huwa mnafanya nini mnapojikuta kwenye hali kama hii? Kama hamjawahi, mkijikuta kwenye hali kama hii, mtafanya nini? Hapa hakuna jibu moja. La muhimu, ni wote wawili kuwa tayari kujifunza na kufundishana bila kila mmoja kushikilia lake ndiyo sahihi. Mfano, katika kisa cha kutopiga mswaki, kupiga mswaki wakati wa kulala ni bora kuliko kutofanya hivyo. 

       Pia, katika kisa cha kupwakia kama wanyama na kuongea wakati wa kula, kukaa kimya ni bora kuliko kutofanya hivyo. Hata hivyo, tuonye. Mazoea ni magumu kuyaacha hasa yanapokuwa sehemu ya makuzi na malezi ya binadamu.

Tumalize kwa kushauri kuwa, katika kutatua matatizo kama hayo, wanandoa wanapaswa kuwa flexible (hatuna Kiswahili chake). Wawe tayari kujifunza na kufundisha na si mara moja bali miaka yao yote.

Chanzo: Mwananchi jana.

Thursday 12 September 2024

Tumekuwa Mateka wa Watekaji


Hapo zamani kaya ikiwa kaya, tulizoea kusikia utekaji na uuaji wa watu kisiasa kwa majirani zetu. Majirani zetu wa kaskazini mashariki walisifika kwa mchezo huu mchafu uliofyatua vigogo wengi wa kisiasa wakiwamo mwaziri kabla ya wale wa Kaskazini magharibi kuchukua ukanda. Ni pale nduli alipompoka madaraka Oboto ambaye naye alimpoka madaraka kabaka tena kwa kumtumia nduli huyuhuyu.
        Sasa inavyoonekana ni zamu yetu. Zamani tukiitana ndugu. Kila fyatu alikuwa ndugu wa mafyatu wote zama za mzee Nchonga (RIP SANA Nguli). Baadaye alikuja mzee Ruxa (RIP SANA Mwamba) kabla ya kuja kwa mzee Ben Nkapa (RIP SANA BRO). Baada yah apo alikuja BoysIIMen, na baadaye Jiwe (RIP). Katika awamu zote tano, mambo ya mafyatu kutekwa na kufyatuliwa na mafyatu wasiojulikana yalianza zama za jiwe. Hapa ndipo ulipomzizi wa kadhia hii ya ajabu na aibu kwa kaya iliyosifika kwa udugu, upendo, usawa, na mshikamano tena vya kupigiwa mfano. 
        Pamoja na mazuri yake kivitu, jiwe hakufanikiwa kiutu pamoja na kujiita mtetezi wa mafyatu wanyonge. Ni bahati mbaya, pamoja na ukali wake, Jiwe aliondoka bila hata kumnyaka mmoja wa wale waliojulikana kama wasiojulikana ingawa walikuwa wakijulikana. Kama wanaharakati huru ambao hawakuwa huru bali udhuru walijulikana, iweje wauaji wasiojulikana wasijulikane kwa lisrikal lenye kila aina ya wataalamu wa uchunguzi na udukuzi.
        Sina haja ya kumlaumu marehemu. Cha mno, historia huwa haina huruma wala upendeleo. Huripoti kitu kama kilivyofanyika au kutokea. Kwa muktadha huu, sasa najikita kwenye jinai, uchafu, na unyama wa kutekana na kutoana roho kwa mambo ya kidunia kana kwamba kuna atayeishi milele. 
            Ni kama tumekubali kutekwa na kugeuka mateka wa watekaji wetu. Je hawa ni nani, wanatoka wapi, kwanini wanaua mafyatu hovyo, wanatumwa, wanajituma, na nani anawalea hawa maafriti nduli wakubwa? Je vyombo vyetu vya uhasama, sorry, usalama, navyo viko wapi? Ndata wetu ambao mara nyingi wemejionyesha kushabikia na kutumiwa na chata fulani nao wako wapi? Je tunaanza kuwa na utawala wa kimafia bila kujua? Je tutaendelea kukubali kuwa mateka wa wahuni wachache hata kama wanaowatuma wanaweza kuwa na maulaji? Maana haieleweki mafyatu wanyotolewe roho mchana kweupe na hakuna anayeshikwa. 
            Je lisrikal liko wapi? Je nalo linahusika? Kwanini wanaotekwa na kunyatuliwa roho ni wa chata kimoja kati ya utitiri wa vyata vya upingaji? Je huu ni mchezo mchafu wa siasa? Je mafyatu wa kaya hii wakimbilie wapi? Je kasi ya lisrikal walilochagua na kulipa kodi kila siku ni nini? Je tuanze kulichunguza? Kwani, likijichunguza, hakuna atakayepatikana wala kujulikana. Kwa taarifa zilizopo ni kwamba kaya ishapoteza takriban mafyatu 80. Je wafe wangapi ndo wahusika wastuke na kutenda haki hata kusitisha kadhia hii?  Maswali ni mengi kuliko majibu.
            Yeyote anayewatuma, sababu zozote zinazowasukuma, yeyote anayewalea anapaswa kujua kitu kimoja. Wanaweza kumgeuka naye akajikuta kwenye wahanga sawa na wahanga wengine. Kabla ya kupinduliwa, Obote hakudhani kuwa uhuni lingekuwa tatizo lake wala jambo ambalo lingemfyatua na kumtemesha ulaji. Hivyo, nasi, tunapaswa kuwa makini kama mafyatu wenye akili timamu na tunduizi wanaoisoma historia na kujifunza namna ya kutatua baadhi ya matatizo kama hili la utekaji wa kaya na mafyatu wake. 
Haiwezekani mafyatu wafyatuliwe kila uchao halafu tunaambwa mambo poa. Hivi hawa wahanga wa utekaji huu siku watakapokengeuka hali itakuwaje? Mafyatu si wanyama, wadudu wala mataahira. Ni viumbe wanaobadilika na wasiotabirika. Hata hawa waliobadirikiana na kugeuziana kibao ni mafyatu kama hawa wanaofyatuliwa na hawa wahuni.
         Kwa vile huwa nasikia kuwa rahis wetu ni msikivu, si vibaya kumpa ushauri wa bure kuwa hali hii isipokomeshwa, uwezekano wa kuwachochea mafyatu ambao wanajiona kama wahanga wasio na mtetezi wala pa kwenda, kuamua kufyatuka na kuwatafuta hao wanaowateka ili nao wawateke waonje ladha ya dawa yao. Nadhani wanachosahau hawa watekaji, watesaji, na wauaji ni kwamba wao ni mafyatu tena wenye familia, ndugu, jamaa ambao wanaweza kujikuta katika ulipizaji visasi mbali na kutaka kukomesha hii jinai na dhuluma.
Kwanini tunaweza kupata ndata wa kuzuia maandamano au kukamata ng’ombe kwenye mbuga za wanyama lakini hawapo wakukamata watekaji au nao wametekwa bila kujijua? Uadui hata ugomvi wa kisiasa humalizwa kisiasa na si kihuni na kikatili hivi. Hii ni aibu kwa kaya yote. Je tumeishiwa kiasi hiki hadi tunatekwa na watekaji kiasi cha kugeuka mateka wa wawatekaji!?
Tumalizie. Chonde chonde msiharibu sifa nzuri ya kaya yetu. Maulaji yana mwisho. Na isitoshe, hakuna anatayeyafaidi wala kuishi milele. Kuna haja ya kujirudi na kuachana na uhuni wakati huu ambapo mnaweza kuwapa sababu ya baadhi ya wahuni na maadui wasiotakia kaya yetu mema kuanzisha machafuko na vita uchwara kama kule Somaliya. Tunfahamiana hapa? Hivi ni asubuhi au usiku? 
Chanzo: Mwananchi jana.