Kuna usemi wa hovyo. Kila nikiusikia, natamani nifyatuke na kuwafyua wadudu hawa wawe ni wadudu au ngurumbili waliofilisika kimawazo hadi kuwa hivyo walivyo hovyo. Msemo unaonichachefua na kunifyatua si mwingine bali ule wa chawa na uchawa ambapo chawa wenyewe ni mafyatu. Mwanzoni, nilidhani chawa wamepata miujiza kiasi cha kufyatuka kama mafyatu na kugeuka mafyatu lakini si mafyatu kufyatuliwa hadi wakajigeuza au kugeuzwa chawa.
Kwanza, siamini wala kukubali kuwa fyatu mzima na akili zake anaweza ima kujifanya, kufanywa, kujiita, kuitwa, kugeuzwa au kujigeuza chawa. Chawa na fyatu wapi na wapi na katika nini na lini na iwe nini kwa ajili ya nini na nani? Fyatu mwenye akili timamu hawezi kuvumilia achia mbali kufuga chawa. Sijui kama chawa wana akili au ubongo hata uwe kiduchu kiasi gani. Sijui hata kama wana utashi au utambuzi wa kujua wafanyacho zaidi ya kusukumwa na silika kama hayawani wengine kama wao.
Chawa anapoitwa fyatu ni poromosheni na fyatu anapoitwa chawa si dharau na matusi tu bali demosheni. Kwanza, sijui. Inakuwaje fyatu mzima akubali kuitwa au kuita wenzake chawa asione aibu wala kuhofia kuonekana hayawani na zwazwa. Inabidi nirejee kwenye kabrasha langu la mabuku ya saikolojia nijikumbushe kitu hii.
Tofauti na chawa, kazi ya mafyatu ni kufyatua kila kitu, fyatu, na chawa bila kujali ukubwa wala unene wao. Hivyo, siamini hata kidogo kuwa fyatu mwenye akili timamu anaweza kuchawawishwa na kuchachawizwa hadi akakubali kuwa au kugeuzwa chawa. Ili iweje? Ili apate nini? Hata kama mie ni fyatu, lazima niseme tena bila kufyatuka. Hakuna binadamu anaweza kuwa chawa wala chawa kuwa binadamu.
Kuwa, kufanywa, au kuitwa, kugeuzwa hata kuihisiwa kuwa chawa ni kufuru na maudhi kwa mwenyezi Mungu mwenyewe na mafyatu hata wadudu. Ni hayawani na vichaa pekee wanaweza kunyonywa na chawa kwa vile ni hayawani. Hawana uchaguzi wala uwezo kama mafyatu. Sitaki kufikiri. Sijui inahisika au kuwa vipi kwa fyatu kujilinganisha au kugeuzwa hayawani kama mdudu chawa. Sitaki kujua wala ku-imagine.
Kwa wale waliokua na kwenda shule wakati wa Ujamaa, tuliozoea kuwaita wanyonyaji kupe, si kwa sababu ya ufyatu wao bali hatari, madhara, uchafu, udhalili, na uhovyo wao. Tofauti ni kwamba, mafyatu wanyonyaji walipoitwa makupe, hawakupenda tusi hili. Nasi, tuliwaita vile si kwa kuwasifu wala kutaka watusifu bali kuwakatisha tamaa waache ukupe au unyonyaji.
Kuna tofauti gani kati ya uchawa na ukupe? Kama wahusika wanamaanisha chawa kwa sababu ya unyonyaji na uchafu wao, hapa sina neno. Nijuacho, hakuna kupe waliojitangaza kuwa makupe au sisi tuliowaita makupe kuwavumilia na kuwafanya sehemu ya maisha au harakati zetu. Tuliwachukia. Walituchukia. Tulichukiana. Je kwa chawa hali ikoje? Mie si chawa. Sijui chawa wanajiteteaje kama wanao utetezi kutegemea na uteuzi wao.
Je ni kwanini tuliwachukia kupe? Nani anapenda kunyonywa? Nani anapenda kufuga viumbe visivyo na faida bali hasara na hatari? Wale watunzao wadudu wanyonyaji hufaidikaje nao? Je kunyonywa kuna raha au karaha? Nani anaweza kufuga maradhi kilio kisimfichue? Ni mpumbavu gani huyo anayengoja kufichuliwa na kilio badala ya kutibu ndwele? Wanyama kama ng’ombe, nyati, tembo na wengine hunyonywa na kunguni. Kwanza, ni kwa sababu wao ni wanyama. Pili, hawana dawa na nyenzo nyingine za kuwaangamiza japo wana utashi. Tatu, wana damu nyingi kuliko mafyatu. Nne, pamoja na kutokuwa na dawa na nyenzo, hawawapendi kupe.
Turejee kwenye chawa au machawa kama wasemavyo watoto wa njini siku hizi. Nina swali. Je chawa anaweza kuishi bila ya kuwanyonya awanyonyao? Je anayenyonywa anaweza kunyonywa bila kuwa na damu na uchafu, bila kusahau ujinga au kukosa uwezo kabisa wa kuwateketeza wadudu kama wanyama hapo juu? Je sasa nani hawa wanafuga machawa na kwa nini ili iwe nini? Je chawa wanaweza kuwapo bila damu na uchafu? Je nani hawa wachafu wanaofuga chawa na ili iweje? Kuna haja ya kuwasaidia ima kuwaosha wawe safi na kuachana na mateso ya kunyonywa na aibu ya kuitwa wafuga chawa au kuwapulizia dawa ya kuua wadudu kama tufanyavyo kwa mbuzi na ng’ombe ambao huwa tunawapelekea joshoni mara kwa mara.
Kimsingi, fyatu anayekubali kunyonywa na chawa bila kuwaua au kujisafisha, anahitaji msaada sawa na chawa wanaomnyonya. Unachoweza kufanya hapa, ni kuua machawa ima kwa kumuosha mhusika, kusafisha nyumba yake huku mkimfundisha faida za kuwa safi na madhara ya kufuga chawa au kupulizia dawa za kufyatua wadudu. Je anayefuga chawa na chawa nani mjanja? Je kati yao, nani anahitaji ukombozi? Kumbe nililewa na kulala kwenye mtaro!
Chanzo: Mwananchi leo.
No comments:
Post a Comment