The Chant of Savant

Wednesday 6 January 2010

Mpayukaji avunja baraza la mawaziri

KATIKA kuufunga mwaka, mzee mzima natoa zawadi ya mwaka mpya nikiwa nimejipanga upya. Niliwahaahidi wanakijiwe kuwa nilikuwa nikijipanga kujibu mapigo si hoja. Sasa najibu kwa vitendo. Na hii si kwa ajili ya kampeni.

Najua wakosoaji watasema narudia utapeli wangu kuwafunga wadanganyika wa kijiwe changu kamba ili niwabamize mkenge kwa mara nyingine. Msiwasikilize hao. Mie bado ni chaguo la Sir God.

Hata hivyo, ni vizuri kuelewa. Raha lazima mjipe wenyewe baada ya hapo. Mpo wadanganyika wangu?

Baada ya wanakijiwe kulalamika sana kuwa nawakingia kifua mafisadi na vihiyo, sasa navunja mwiko kwa kukata kamba zangu za raha jipe mwenyewe. Sasa raha nawapa mimi.

Kutokana na muda kuzidi kunipa kichogo na uchaguzi mkuu wa kijiwe kuwa mlangoni huku nikiwa nimeishiwa na kamba za kuwafungia, mzee mzima nimeamua kuwapa raha kwa kuvunja baraza la mawaziri na kulisuka upya.

Nimelazimika kufanya hivyo ingawa roho inauma kutokana na washikaji zangu kutupwa nje na kuwa mzigo mwingine nyuma ya pazia. Hata hivyo, washikaji msikonde. Mie bado ni wenu nanyi ni wangu.

Nikishawabamiza kenge hawa makenge nitawakumbuka na kuwapa ulaji tena. Nitavunja baraza na kuwarudisha baada ya kupata ulaji. Mtakuwa nje ya ulaji kwa mwaka mmoja ingawa katika siasa lolote laweza kutokea. Tusameheane. Wadanganyika wamenijia juu sana.

Katika kuvunja baraza la mawaziri kuna mambo mengi nimezingatia. Nitaunda baraza dogo ili kuokoa pesa ya wanakijiwe wangu ili wavutiwe nami wanipe ulaji baadaye niwaache solemba. Nitazingatia elimu safi, umri, ukoo, dini, mtu atokako na ushikaji kwa mbali hasa ile mitandao. Hata kuzurura mwaka huu sifanyi.

Wizara ya wanawake na watoto imepiga panga. MAWAWA ya mke wangu inatosha. Shughuli zilizokuwa zikifanywa na wizara hii zitapelekwa kwenye ofisi ya MAWAWA, bi mkubwa atakuwa waziri asiye rasmi.

Wizara ya vijana na michezo nayo inakwenda na maji; sitaki mchezo siku hizi. Nimefuta Wizara za Kilimo na kuanzisha ya umachinga, ushirikiano wa Afrika Mashariki kutokana na washirika wa nchi zisizo na ardhi wala demokrasia kutaka tuungane ili watuibie ardhi na kutorosha madini yetu.

Mkuu wa mkoa wa Bongo, Bill Mukuvi, naye nimemtupa nje kutokana na kuwa kihiyo tena aliyeghushi.

Wizara mambo ya nchi za nje na uhusiano wa kimataifa nitaichukua mimi na naibu wangu atakuwa bi mkubwa mama watoto wangu ambaye atakuwa waziri asiye rasmi. Pia ieleweke, kwa muda nilioruka naye ameonyesha uzoefu mkubwa kutulia kwenye pipa na kupiga picha uwanja wa ndege ukiachia mbali kuwa bingwa wa kubembea na kunipigia kampeni kinamna.

Wizara ya Fedha, Uchumi, Mipango na Biashara nitaibadilisha kuwa ya EPA, kushughulika na ufisadi na umachinga.

Waziri atakayeisimamia nitamtaja baadaye baada ya kushauriana na bi mkubwa kuona atatusaidiaje kuepa Ma-EPA.

Wizara ya Mambo ya Ndani na Usalama wa Raia nimeiunganisha na ya ulinzi na kumpa mtoto wa aliyenitengeneza.

Hivyo daktari Hu-Sen atakuwa waziri mpya wa wizara hii mpya wakati tukimuandaa kuchukua kijiwe cha Zaainzibaa.

Wizara ya Elimu, Utamaduni, Michezo na Ubunifu itafutwa. Wasomi tunao wa kutosha na isitoshe wanaopaswa kusoma ni watoto wetu watosoma ughaibuni. Kama huna pesa uliye tu lazima mwanao aende kwenye kilimo first. Wawe wabunifu ili iweje?

Wabuni jinsi ya kuingilia ulaji wetu siyo na kuleta utamaduni mfu wa kutukosoa na kutuzomea ukiachia mbali kututupia mawe kama kule kwa kina Malafyale?

Wizara killimo, ushirika, mifugo, ardhi na maji viwanda, uchuuzi, masoko, ushirika na ujasiriamali nazo nazifuta. Maana uzoefu umeonyesha ujasiriamali siku hizi haulipi isitoshe nifanyao mimi na bi mkubwa unatosha.

Wizara ya sheria, katiba na haki za binadamu nayo naifuta kutokana na waziri wake kuwa na uogonjwa wa kupayuka. Na isitoshe kila mwanakijiwe anapata haki yake na si lazima wajue sheria. Maana wanaweza kunigeuzia kibao na kunifunga hawa.

Sambamba na wizara hii, ninamfukuza kazi katibu wa chama changu cha Ulaji, Ufisadi na Ubangaizaji mgosi Joe Makambale Machungi na Mkurugenzi wa Tume ya Mawasiliano ya ofisi yangu, Silvia Rweyenshomile (mshiriki mkuu wa unepi). Hawa wamekuwa wapayukaji badala ya watendaji.

Wizara ya Nishati, barabara na uchukuzi kwa sasa aihitajiki kutokana na kujenga bara bara za kutosha na kuwezesha watu kukimbilia mijini. Kama ni kuhitaji nishati, tunayo ya kutosha kiasi cha kuachana na mgao wa umeme.

Wizara ya kazi, ajira na maendeleo imefutwa kwa sababu ajira kwa sasa zinafuata ukoo wa mtu. Hivyo haihitajiki wizara.

Nitangaze rasmi kuwa mawaziri wafuatao nawapiga panga kutokana na kuhusishwa kwenye tuhuma za kughushi, kupayuka hovyo na upuuzi mwingine. Wafuatao hawamo tena kwenye ulaji wangu: Makorongo Muhanga, Meli Nyagu, Imanu Mpimbi, Dad Matoya Dad, na Diodomus Kamirioni.

Pia mawaziri wafuatao nimewalamba wino mwekundu baada ya ama kuchukua wizara zao au kutoridhishwa na utendaji wao. Nao ni Mwalimu Ijumaa wa Kupuyanga, Mwl. Ijumaanne Majembe, Stevie Wahasira, Shemeji Hawanaghasia na Ben Maembe.

Mama Sofii Mpayukaji Yanga nisamehe sana. Imebidi nikupige kibuti kutokana na kuzoza hovyo huku ukijenga mazingira ya mimi kustukiwa na hata wabaya wangu kupata la kusema.

Domo lako chafu limekuponza mshirika wangu. Wewe na mgosi Makambale Machungi siwezi kuwavumilia kutokana na kuharisha kwa midomo badala ya nonihino. Tusaheane. Wa kuuza nyanya mkauze hata wa kufanya uchangudoa mwingine ruksa mradi msiguse kitumbua changu.

Mawaziri wengine mshikaji ambao nimemlamba panga ni Joka Mkunjika na Joni Chilisosiyagati.

Kwanza nyinyi licha ya kutofanya lolote zaidi ya kelele za chura, hamkubaliki majimboni mwenu. Hivyo hamuwezi kuleta ushindi mwakani. Lazima niwapumzishe mwende kwenye vijiwe vya kahawa mkapayukie huko.

Haki ya mama, mwaka ujao baada ya uchaguzi ni wa kurejesha imani kwa kijiwe. Nitafikisha mahakamani watuhumiwa wote wa ufisadi wa kahawa na kashata bila kusahau wauza bwibwi kijiweni.

Sitakuwa na mchezo na mtu. Mwaka ujao ni wa kutimiza ahadi zote bila kubakiza hata chembe. Ni mwaka wa kuwapeleka walevi peponi. Maana wamechoka. Kidumu chama cha ulaji.

Onyo; mtu atakayejitia kiherehere kutaka kusimama nami kugombea ulaji atakolimbwa. Amini si kamba za shehe Ubwabwa. Sikumtuma kunifagilia. Njaa nyingine bwana! Angejua ya kesho si angetabiri kuwa kipindi kile shehe mkuu angemtimua. Mbona hakujitabilia. Upuuzi upuuzi mtupu.

Basi nipigieni makofi kidogo maana nimewapa raha ya milele.

Naona ndata wanakuja wasije wakanikata mitama kwa kumpasha bosi wao. Acha nikitoe na mapema.
Chanzo: Tanzania Daima Januari 6, 2009.

No comments: