The Chant of Savant

Thursday 29 July 2010

Uchaguzi ukiisha tegemea dikteta si Mkuu

Nawajua walevi. Hawajijui wala hawanijui vizuri. Na hawatajijua hadi yawakute zaidi ya haya ambayo yameishawakuta wasijifunze. Najua walevi watanichagua kwa kishindo wakidhani mambo yatabadilika wasijue ndiyo yanaanza! Nibadilike nini wakati hii ni lala salama? Anyway, nitabadilika na kuwa imla.

Kwa vile ni lala salama, watakapoanza kustuka mie nitakuwa nawaambieni laleni salama na hii ni ngwe ya lala salama.

Kwa vile nawajua walevi, ni wa hovyo. Sikuogopa kuwatahadhalisha baada ya kudharau tahadhali nyingi kuwa nitatoa makucha baada ya kuchaguliwa kwenye ngwe ya lala salama. Nimesema wazi. Nitawafunga wale wote wanaonikosoa achia mbali wanaonikandia na kufuatafuata ulaji wangu.

Wale wambea ambao kwenye kijiwe tunawaita wambea au magazeti wajiandae kukisikia kijiwe. Nitawakomesha ile mbaya. Nitawafungia kuingia na kutoa upuuzi wao kijiweni. Nitaruhusu wale wanaoniunga mkono na kunipigia debe tu huku wakijigonga kwangu.

Na mfahamu. Hii ndiyo fasheni kwa sasa. Hata mkuu wenu wa kaya ameishaonya kuwa akishaukwaa mjue mtakoma. Ule mchekea mliouzoea hasa wale ndugu zangu wa magazeti na wanaojiita wakereketwa wa dini fulani wakae mkao wa kuliwa. Hamkuona makucha yake pale Yanga alipomtumwa mwana kuwakomesha akina Kifukwe? Hamkuwaona akina Masahauni walivyosahaulika baada ya kugusa ulaji wa washikaji wa mwana? Kaeni mkizubaazubaa. Shauri yenu. Tusilaumiane.

Ametangaza rasmi kuwa baada ya uchaguzi yule Chekacheka mliyezoea kumuona atageuka kuwa Nunanuna huku akiwa amevimba kama nune. Wale ndata ambao hawakuwa na kazi ya kufanya kuwakata mitama wakosoaji sasa wakae mkao wa kula. Sipate picha jamaa atakapokuwa ameuvaa utunituni akiukimbia unjaa kaya itakuwaje? Au ndiyo maana amemnonesha bi mkubwa ili kufanya majaribio ya kutuna na kununa? Naona keshaanza kwa kuvaa miwani tinted ili asiwaonee aibu wala huruma wadanganyika watakaojipendekeza na kumpa kula zao wakidhani zitawaletea maisha bora badala ya maisha ya kiimla.

Anayebisha aangalie alivyowaminya wana nambari wahedi wakagwaya hata kumchalenji ukiachia mbali kuwaminya hadi kumchagia mshiko wa kununulia urahisi. Hakuna uimla mbaya zaidi ya huu tena unaofanywa chini ya kivuli cha domoghasia muitayo demokrasia. Kitaalamu huu huitwa uhuni wa kisiasa wenye kisasi cha kihuni.

Watakaotaka kuula waanzishe mkakati mchafu kama ule wa SHIHATAI wa kutaka kumsafisha Ewassa ili hapo baadaye ajaribu kumrithi mkuu. Hamkuona mkakati ulivyoanza kuiva kwa kumwengua daktari wa Kushaini na kumuweka mgonjwa aitwaye Ughaibuni Bilhali? Shauri yenu. Kama hamnielewi basi endeleeni kuingizwa mkengeni kwa mara nyingine.

Wasiishie hapo. Lazima wajipendekeze pendekeze kwa mkuu ukiachia mbali kuishi kwa kutegemea mtandao wa mafisadi wakiongozwa na baba lao.

Nani alijua kuwa fisadi kama Ewassa angepata ithibati ya kuhojiwa na yule jamaa aitwaye Mtindo Mwando ambaye naye ameanza kuishiwa? Ajabu ya maajabu eti akina Mwando na kundi lake wanataka kumfufua maiti? Hata ahojiwe uchi Ewassa hawezi kuwa mkuu wa kaya hata kwa sekunde moja. Anaweza kutuuza na makaburi yetu kwa uroho na ufisi wake.

Bila aibu linasema eti lilionewa wakati liliinea kaya kwa kuchota njuluku. Eti linasema ni clean yaani halina kinyongo. Kwanini halisemi liko clean kwenye ufisadi?

Kaya hii kweli Danganyika ya wadanganyika! Kesho utasikia majambazi mengine kama Roasttamu, Jose Mainji, Jeff Sambodo yule aliyewahonga chakudema pesa ya ufisadi nayo yakija kuhojiwa ili yasafishike. Kusuru wa kusumu.

Kabla ya kuendelea ngoja kwanza niwamegee kituko. Una habari; baada ya kumkaripia Sofi fyatu wa lion kutokana na kuwaambia wake zetu watunyime nonihino wana Sisiemu wamefyatuka hadi gabacholi mmoja kujiamini na kutoa mshiko wa mamilioni kwa Chakudema? Huyu haogopi mke wake kumnyima nonihino kwa sababu mama wa kigabacholi si limbukeni kama wa kiswahili.Haya tuyaache.

Hata hivyo wengi wanasema sasa Chakudema sasa imeanza kudema kwenye nyavu za mafisadi hasa pale itakapoumbiliwa na jamaa kama alivyowafanyia akina Jose Butuka. Inashangaza kuona akina daktari Silaha waliofichua ufisadi wote wasimuulize gabacholi kama mshiko wake ni safi au matokeo ya ufisadi wake na maswahiba zake akina Joseph Mainji na magabacholi wengine walioshikilia uchumi wa kaya!

Sisi wakubwa unajua: si majuha. Tuna sifa kama ya yule mwarabu na ngamia wake tunapokuwa tunasaka ulaji. Huwa warahimu kama ua na wakarimu kama vyangu. Tukishawatwisha mkenge hugeuka kuwa makenge kweli kweli. Ukitaka kujua ubaya wa kenge jaribu kuigiza mambo yake. Yeye akiona mvua inanyesha anatimkia ziwani, mtoni hata baharini kuikwepa mvua. Ukimshambulia anakuumiza na mkia wake bila kujali kuwa naye anaweza kuumia!

Nasi kadhalika. Unapojifanya unajua kutusakama tunakugeuzia kibao. Badala ya sisi kuonekana makosa yetu, wewe unaonekana mchochezi hata kama unacholonga ni ukweli mtupu.

Nimewapania waleta fujo wanaotaka kuvuruga amani kijiweni. Yaani wao wanahanikiza kuzuia watu tusihomole wasijue wanavunja amani ya kijiwe! Nani aliwambia kuwa mali ya umma inauma? Sasa kelele za nini tunapouma pesa ya umma wa walevi? Ukitaka nawe njoo ule. Ni kuamua kujitoa kimasomaso na kugombea ulaji au kujipendekeza kwetu sisi tulio na mamlaka na unakatiwa chochote kitu unatuliza njaa zako badala ya kututilia kitumbua mchanga.

Kama mkuu ngwe hii ya lala salama sitamvumilia mtu hata awe anasimamia ukweli kiasi gani. Najua kipindi kilichopita sikuchukua hatua yeyote kutokana na kuwazunga walevi wauingie mkenge upya kwa kunichagua. Sasa ngoja waukwae halafu watajua kama mimi ni bingwa wa sanaa au longo longo.

Kama mkuu, nitaanza kumpiga mwanangu Kidume vuvuzela ili hapa baadaye agombee ulaji kama Jan wa mgosi Makambale ambeye anawania jimbo la Umbuji.

Bi mkubwa nshamwambie azidishe juhudi kukusanya mshiko kwenye NGO yake ya MAWAWA ili hapo baadaye tusiumbuke wala kulaumiana. Lazima anunue mijumba chekwa kama Anna Tamaa wa Tunituni. Hii ni ngwe ya kukomba si kuhomola tena. Nataka mkuu wa kijiwe ajaye asikute akiba hata chembe. Nataka akianza naye aanze kivyake vyake ingawa wakati mimi naanza nilikuta njuluku jaalo.

Kuhusu mkakati wa kupambana na wanywanywa, kwanza niseme wazi. Ulianza zamani. Kuna watu tuwaitao magazeti kijiweni nshawalambisha kunisifia hata nipaswapo kupigwa mawe. Hamjawasikia? Yupo Tazama bin Rai na wengine wengi wanaofanya kazi hii ambayo wabaya wangu huiita unepi.

Leo sichongi sana. Nakwenda kusoma vitabu vya akina Idd Amin, Mobutu Seseseko, M7, Marcos, Causescu, Suharto na wengine ili kujua siri ya uimla wao.

Naona mindata inakuja. Kwa vile jamaa keshatangaza wazi atatufiligisa kiimla, acha nitimke yasije yakaanza nami.
Kulaleki tumekwisha.
Chanzo: Tanzania Daima Julai 28, 2010.

No comments: