The Chant of Savant

Tuesday 23 July 2019

CCM HAWANA HAJA YA KUDHALILISHANA NA KUJIDHALILISHA; TUMIENI BUSARA ZA MWL NYERERE NA MZEE MSEKWA



Image result for photos of nyerere and msekwaImage result for photos of makamba, kinana and dr bashiru ally

Hivi karibuni uliandikwa waraka wa kukanusha tuhuma za mtu mmoja anayejiita mwanaharakati huru ambaye hata hivyo si huru zilizowakumba makatibu wakuu wastaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mzee Abdulrahaman Kinana na Yusuf Makamba. Wawili hawa  walituhumiwa kula njama kumhujumu mwenyekiti wa chama rais John Pombe Magufuli kwenye uchaguzi ujao. Ukweli  wa tuhuma hizi hadi sasa haujajulikana. Hata hivyo, waraka huu ulizua sintofahamu nchini tokana na kurushwa kwa mawasiliano baina ya Kinana na katibu mwenezi wa zamani wa CCM Nape Nnauye ambaye ananukuliwa akimwita majina ya ajabu ajabu rais.
Baada ya waraka huu kuandikwa na kurushwa kwenye vyombo vya habari na kuhujumiana kuanza, wengi wa wana CCMm wakereketwa na wasio na hoja yoyote hata wale ambao wanatafuta kiki wametumia fursa hii kujizolea umaarufu na kujiweka karibu na mwenyekiti baada ya mmojawapo kuitisha press conference haraka na kuwapinga wazee hawa bila kuwatukana na baadaye akateuliwa kuwa naibu waziri. Jambo ambalo limewafanya wengi wasiojua chanzo na ukweli juu ya uteuzi wa mhusika kudhani amepewa dhamana hii tokana na mtifuano unaoendelea. Japo rais ameeleza sababu za kumteua kuwa ni tokana na michango yake bungeni, wapo wasaka madaraka walioona hii ni fursa ya kuwasambulia wastaafu hawa ili waweze kukumbukwa. Wengi wanashangaa usafi wa hawa wanaowashambulia wenzao. Hata kama wazee husika wangekuwa wamepatikanana hatia, haiondoi heshima yao kama wazee, wanadamu na viongozi wa zamani wa CCM. Nani ambaye hatastaafu?
Mbali na wasaka madaraka na matonge, wapo viongozi waandamizi kama katibu mkuu wa sasa Dr Bashiru Ally aliyesikika akiwaita baadhi ya watu mchwa na wapumbavu asijue madhara ya mfano anaoujenga kwa chama. Kabla ya Rwanda kuuana kwenye mauaji ya kimbari, walianza kuitana mende na majina mengine sawa na haya. Kwa anayeijua CCM anashangaa ustaarabu huu umeanza lini na utaifikisha wapi. Hawa wanaharakati nao wanapaswa kusemwa kuwa wanapogundua njama kama hizi, kama kweli wanaitakia mema nchi na hawatafuti tonge, basi waripoti kwenye vyombo husika vya chama ili kuchukua hatua zinazopaswa kuchukuliwa. Pia wanaharakati wanaoonyesha kuwa na tuhuma kila uchao wachunguzwe wanazipataje na wapi na lengo lao la kutumia vyombo vya habari badala ya kutumia vyombo na kufuata njia na taratibu husika. Inakuwaje wanaaminiwa kirahisi na kienyeji hivi? Kwa wanaojua historia na utendaji wa rais Magufuli tangu akiwa mwalimu, mbunge na waziri hadi rais, wanakiri kuwa ahitaji kulindwa wala kutetewa na hawa wanaojiita watetezi wake. Hivyo, CCM wanapaswa wajitahadhari wasiingizwe kwenye mtego huu wa kumalizana, kuumizana, kutukanana na kudhalilishana. Akina Oscar Kambona walipotuhumiwa kuhujumu sera za TANU, waliitwa na kupewa adhabu zao baada ya kupewa nafasi ya kujitetea. Kwanini CCM wamesahau hili kirahisi? Chonde chonde, CCM hamna haja ya kudharauliana. Rejeeni mifano ya viongozi wenye kama vile marehemu baba wa taifa Mwl Julius Nyerere ambaye aliweza kutatua migogoro mingi ya chama bila kudharauliana wala kutukananaa. Mbali na hiyo, hata spika wa zamani mzee Pius Msekwa aliyepokea malalamiko haya kwanza, hakuhemukwa na kutukana zaidi ya kuwashauri wahusika wajitetee au kujibu mapigo ima kwa kwenye mahakamani au wanatakavyoona ingefaa.

No comments: