The Chant of Savant

Tuesday 13 December 2022

Ushindi wa Moroko Kombe la Dunia ni wa Waafrika au waarabu?

Mchezaji wa Timu ya Taifa ya Moroko, aitwaye Sufian Boufai alizua gumzo kwenye mitandao ya kijamii. Hii ni baada ya kusema kuwa ushindi wa awali wa Moroko dhidi ya Timu ya Hispania ulikuwa: kwanza, ni wa Waarabu na pili, wa Waislamu wote duniani. Wengi wasiojua ubaguzi na kujikana kwa hawa ndugu zetu Waafrika tena Waberiberi wa Jangwani wenye asili ya Afrika Magharibi walighadhibika sana. Kwa tunaojua, tulifurahi kuwa angalau wajinga wengi wanaodhani hawa ni ndugu zao japo ni ndugu zao waliojikana, wamepata somo na ukweli mchungu na unaoudhi lakini wenye kuweka huru. Hata kabla ya kuharibikiwa na kuvurugika, wenzetu wa Zimbabwe walitutenga tusifaidi walichokuwa wakifaidi.

Kwa yeyote anayejua watu wenye damu ya kiarabu–––hata kama ni ya kuchovya––––sawa na wabuguzi wengine kama vile wahindi, wazungu na wengine, atakubaliana nasi kuwa hawa jamaa, licha ya kujikana ni wabaguzi wa kunuka. Ukiachana na Boufai ambaye hafai kabisa, rejea namna imla wa zamani Muamar Gaddafi alivyosema baada ya Umoja wa kujihami wa Ulaya (NATO) ulivyomuonyesha wazi kuwa ulimaanisha kumuangusha na hatimaye kumuua. Katika kutapatapa alisema kuwa kama NATO wangepindua serikali yake, Ulaya ilipaswa kujiandaa. Kwani, alitishia kufungulia Waafrika maskini na wajinga ambao–––kwa mujibu wa Gaddafi–––wangetishia na kuvuruga ustaarabu wa Ulaya.

Japo wengi hawakujua kigeugeu na unafiki wa Gaddafi–––hasa pale alipojifanya Muafrika–––japo alikuwa muafrika mbele ya macho ya waarabu wakati moyoni alikuwa anatamani kuwa mwarabu. Mwanzoni, Gaddafi kama wenzake wengine wenye asili ya Afrika alidhani alikuwa mwarabu. Hata hivyo, alipokwenda kwenye umoja wa nchi za kiarabu akataka kuuburuza walimwambia wazi kuwa yeye si mwarabu bali Mwafrika atokeaye kwenye bara ambalo wao, kwa dharau, huiita Afriqiya lililoundwa na himaya habithi ya Umayyad mwaka 703 ikijumuisha nchi zinazoitwa Maghreb kwa pamoja za Algeria, Libya, Mauritania, Misri, Moroko na Tunisia. Watu wan chi hizi ambao wengi ni waberiberi ni masuriama wa Kiafrika na kiarabu.    Kichekesho ni kwa ndugu zetu wa Chadi, Eritrea, Ethiopia, Somalia na Sudan Kaskazini. Eti hawa nao wanatubagua kwa kujiita waarabu wakati wakienda uarabuni wanaitwa watumwa ili kutambua asili yao. Hivyo, tunapoongelea suala hili la ubaguzi wa kipumbavu, hatutaki kuonekana tunawaonea wenzetu wa Moroko ambao walionyesha wazi hisia zilizofichwa kwa Waswahili wengi ambao hudhani hawa jamaa ni ndugu zao.

Wabaguzi na wajinga hawa wana kitu kimoja cha kushangaza. Kama wanachukia Afrika hivi, si wajiondoe waende huko wanakootea kuwa kwao wakati hawakubaliki kwa vile si kwao. Waswahili tunapaswa kujitambua na kuwatambua wenzetu ili kunusurika na ubaguzi huu wa wazi. Kimsingi, unapokuwa Amerika au Ulaya, unabaguliwa. Lakini si kwa kiwango na machungu sawa na hawa wenzetu wa Maghreb, Mashariki ya Kati, China, India, Ufilipino na mataifa mengine ya Asia. Nani angeamini kuwa hata ndugu zetu wa Afrika ya Kusini wanatubagua wakati, licha ya kufanana, ni sisi tuliowezesha uhuru wao toka kwenye makucha ya makaburu.

Nimeandika makala hii baada ya mwanangu kutoka shule akijisifu na kushangilia kuwa Moroko imeshinda. Kwa vile, alizaliwa hap ana hajawahi kufika Afrika, kila kinachoitwa Afrika kwake ni almas tokana na ubaguzi wa hapa. Fikiria. Nilimkatiza furaha yake kwa kumwambia kuwa hawa Moroko ni Waafrika wanaouchukia Uafrika na Afrika. Alibaki kubung’aa asijue la kusema. Sikuona haja ya kumdanganya wakati najua hali halisi ya nyumbani si kwa Afrika tu bali hata kwa Tanzania ambako wamejaa watu kama hawa. Wanajionea fahari ya kuwa si Waafrika wakijiita majina yote, masuriama, waarabu na upuuzi mwingine mwingi. Wanaishi maisha ya kujikana na ndoto wasijue huwezi kuukimbia ukweli.

Kama jamaa zetu wa Moroko, wengi wa ndugu zetu wanaishi kwenye dunia ya kusadikika kiasi cha kujikwaza na kutukwaza sisi tunaojitambua na kuwatambua na kuwazodoa huku tukipaswa kuwatahadhali.

Tumalizie. Kwa kilichoonyeshwa na wamoroko, ushindi wao hauna lolote kwa Afrika. Kwani, kama alivyosema Boufai, ushindi wao ni wa waarabu na waislamu. Ijulikane wazi. Waislamu wanaomaanishwa hapa si ‘watuma’ toka Afrika bali wote wenye damu ya kiarabu au waarabu feki kama wao. Je hapa, Afrika ina cha kushangilia kama mwanangu asiyejua siasa za Afrika na ubaguzi wa ndugu kwa ndugu hadi kuuzana utumwani kwenye karne ya 21 kama ilivyogunduliwa na kulipotiwa hivi karibuni kwenye nchi za Libya na Mauritania ukiachia mbali ukatili na utumwa wanaokumbana nao ndugu zetu Mashariki ya Kati?

Wenye akili, wanaojithamini na kujiamini tieni akili mkiwafumbua macho wenzenu kwa elimu hii mpya ya Ukombozi na suto kwa kidhabu hawa wanaojikana wasijue hata huko wanakojipeleka wanakanwa.

Chanzo: Jamhuri Leo.

No comments: