The Chant of Savant

Tuesday 28 November 2023

Formula ya Kuchanganya Dini na Siasa bila Kufyatuliwa



Tokana na kuwa gwiji la sayansi na sayansi ya jamii, leo nawafyatulia kanuni ya kuchanganya vitu mojawapo ikiwa dini na siasa. Kwa waliozaliwa miaka ya 47, tulifundishwa na kukatazwa kuchanganya dini, siasa na vitu vingine ingawa tulichanganywa hadi tukachanganyikiwa na waliotuchanganya wakaishia nao kujichanganya, kuchanganyikiwa, na tukachanganyikiwa wote. Profesa Mchongaji alilipigia ngebe hili kwa sana tu. Kadiri siku zilivyokwenda, wakaja matepeli waliomzidi kete na kuchanganya dini na siasa kwa kuthibitisha kuwa viwili hivi vinachanganyikana kirahisi kutokana na historia ya uumbwaji wake tena bila kufyatuliwa. Kwa ufupi, mwiko huu ulifyatuliwa na mafyatu wakaendelea kufyatua ulaji kwa kuchanganya dini na siasa hasa baada ya kuishiwa na kugeuka kokoro kwa kukumbatia kila msanii hadi chawa.
            Ni rahisi kuchanganya dini na siasa. Wanachama wa vyama wana dini. Viongozi wa dini ni waumini. Huwaoni wakati wakiapishana au kusimikana kwa wale wanaolazwa kifulifuli ili kusimikwa. Akiapishwa rahisi, lazima maaskopo na mashehena wawepo kumbariki japo wao wakisimikwa hawabariki bali kuwaahidi kula nao. Dini na siasa kayani zinachanganyika kibaguzi. Uliwahi kuona viongozi wa dini asilia wakimbariki askopo au rahisi? Kwanini? Ubaguzi na ukoloni mtupu. Hata wakuleishi na wakolosai, pamoja na uadui wao mtaani, wanachanganyikana Yerushaláyim na kwenye ngwalangwala na ndege na usafiri wowote hata mitaani kwenye nyumba za kupanga hata vitandani tena kwenye nyumba za chapchap.
            Kwa wanaotaka kuchanganya dini na siasa, lazima wafanye yafuatayo:
Mosi, anzisha dhehebu la dini ili kupata umaarufu na ushawishi mbele ya mafyatu wa kisiasa watakaotaka kukutumia kuwapumbaza mafyatu waliosikinishwa kutoasi aka kufyatuka waliowafyatua na badala yake kuamini kuwa kuna miujiza ya kuweza kufyatua utajiri kwa njia ya maombi na mazingaombwe mengine.
        Pili, jikombe kwa wanene na chata twawala ili uwe mnene na kula nao kwa kuwafyatua mafytu waliofyatishwa na kila sanaa na ngonjera iwe ni za amani, imani, mshikano hata umoja japo si wamoja. Umoja gani wakati tuna machogo na wazenj? 
Pili, shabikia amani, mshikano na umoja wa walaji aka wafyatuaji dhidi ya imani ya haba na hovyo ya wafyatuliwa aka waliwao wanaosikinisha na mafyatu wanaowafyatua kwa kutumia dini na siasa. Ukitaka kujua zaidi mambo ya kufanya, jikumbushe ngurumbili kama vile Gwamajima na Rwakatarehe toka kaya ya lalalala waanzilishi wa uchanganyaji na ufyatuzi huu.
        Ili kuthibitisha mashiko ya kanuni na nadharia ya kuchanganya dini na siasa, ngoja nipanue wigo kwa kugusia dhana kuwa kila kitu kinachanganyika na vingine. Kinachotakiwa ni sayansi ya ufyatu, ufyatuaji,ufyatukaji, na ufyatuzi. Wapo wanaoamini kuwa mafuta na maji havichanganyikani wakati vinachanganyikana. Acheni uvivu wa kufikiri kama alivyowahi kusema kaka Ben. Nenda jikoni. Mafuta na maji havichanganywi kutengeza mchuzi au kuokoa maisha? Waulize zimamoto. Maji huzima moto na moto hukausha maji. Ke na Me vikichanganywa hutegeza To… Nimesema toto au to? Tuachie wengine.
            Duniani, kama ukiwa mwanasayansi kama mimi, kila kitu kinachanganyikana. Jiulize shaitwani na bwana Godi hawakuchanganyikana kwenye bustani ya Fyatu Mfyatuaji aka Edeni?
        Wengine husema eti dhambi haiwezi kuchanganyikana na mema wakati vinachanganyikana. Nenda kwenye nyumba za ibada. Wenye dhambi wananchanganyikana na wasio na dhambi. Yesu alijichanganya na wenye dhambi hadi mafyatu wakamshangaa kabla hajawafyatukia. Au jiulize. Mbona njuluku watoazo mafisi na mafisidi kama sadaka au zaka hata kama chafu ua wizi hazikataliwi? Nenda mahakamani. Mahakimu na majaji watoa haki wananchangamana na wahalifu watafuta haki. Je kwa wale wanaopata chochote hawachanganyikani na wale wanaowatoa chochote? Kama madaktari na wagonjwa wanachanganyikana, hakuna kisichochanganyikana.
        Giza na mwanga vinachanganyikana. Anayebisha aamke asubuhi aone machweo mwanga unapochanganyikana na kiza na kuzaa asubuhi au jioni. Chakula na vinywaji na sumu vinachanganyikana. Huamini bado? Kaulize hiyo mibia, misoda na mavyakula ya makopo mnayopwakia yanatunzwa na nini ili yasiharibike kama siyo sumu? Bata huitwa na kusifika kwa uchafu na uharishaji. Inakuwaje analiwa na kupendwa nyama yake?
        Unyama na utu vinachanganyikana vizuri tu kama vitachanganywa. Ukibisha, jikumbushe au waangalie mafyatu wanaofanya mambo ya kinyama na wakabaki kuitwa mafyatu au wanyama wanaotenda wema kama kuongoza au kuokoa mafyatu lakini bado wakaendelea kuwa wanyama. Uchafu na usafi vinachanganyikana. Kama huamini nenda kwa dobi au wanaoosha vyombo. Maji safi ndo husafisha kilicho kichafu baada ya kuchanganyakina. Kama hii haiingii akilini, jiulize.  Kwanini nchi zinazojiita zimeendelea wanachuja maji machafu toka majumbani na kutengeza maji safi?
        Kwa ufupi, hakuna kisichochanganyika. Ni suala la kujua namna ya kufanya hivyo. Hivyo, nimethibitisha bila shaka lolote. Dini na siasa si zinachanganyikana bali zilishachanganywa sana tu.
Hivi niko wapi?
Chanzo: Mwananchi kesho.

No comments: