The Chant of Savant

Friday 25 December 2009

Kanada yaomba Kijiwe msamaha

ISIKUNI sinyuka nomkwezeli. Usimuamshe aliyelala. Qabu Unoqolomba efile. Ni furaha mama yake Qolomba amekufa- huyu mama alikuwa mtu mbaya hakuna. Hivyo, kifo chake kilikuwa ni faraja hakuna mfano.

Uyakulila ngasonye uxele inkawu. Utalia kwa jicho moja kama nyani. Hii hutumika kumzuia mtu kuyaita matatizo.

Leo nimeamua kutoka na Kihoxa lau nieleweke. Simuombei yeyote dua mbaya. Ila kama kuna anayenitenza au kututenza ubaya si vibaya kuomba ubaya umrudie. Mambo ya kutemeana mate hayo!

Kabla ya kuanza kuwapa nyuzi za safari yangu nchini Kanada na Denmark kwenye mkutano wa mazingira utokanao na uwekezaji mbovu hasa kule Mwanza na Mara, naomba niwape chache kuhusiana na harusi ya kukata na shoka iliyokusanya vigogo hadi walinzi wakahofu Al-Qaeda au Al-Shaabab wangevamia. Sitataja majina ya wajumbe nilioandamana nao. Maana siku hizi hii ni siri kwa ajili ya usalama wa taifa.

Harusi tajwa ilikuwa ni ile ya kumuanga Daktari Hada mtoto wa bwana Ewassa.

Ila mambo yote yalikwenda kama ilivyopangwa isipokuwa mkuu wa kaya kijiweni alichomoa dakika za mwisho ili asionekana kama anamuunga mkono rafiki yake.

Habari za hivi karibuni ni kwamba wanakutana faragha. Hata wangejificha na kukutania mwezini, tunajua lao moja na wanaendelea kulindana na kula pamoja.

Ndiyo maana wezi wa Richmond wakiongozwa na pacha wake wanaendelea kupeta. Halafu eti huyu mmpe ngwe nyingine. Ili awafanye nini? Mtajaza.

Kuhusu harusi hii iliyojaa minuso na ushufaa kwa kifisadi, niligundua kitu kimoja. Kumbe wakubwa wanashindana kuwa na watoto madaktari ukiachia mbali kuonyesha mshikamano wa kifisadi!

Kuna Dk. Kwekwe pale Muhimbili; Dk. Kahame Mnazi mmoja na sasa Dk. Luwasha Temeke. Mwananyamala sijazinyaka kama yuko Dk. Mwingine mtoto wa Kigogo. Bado wale “madaktari” wa kughushi na kuiba njuluku pale BoT na wale walioshonana kwenye baraza la mawaziri na Bunge. Mpo hapo wadanganyika?

Kuna haja ya kuchunguza kama hawakughushi kama baadhi ya wazazi wao ambao Mkuu wa Kaya ameamua kutowashughulikia kutokana na sababu azijuazo mwenyewe.

Nilikuwa kule Calgary kwenye jimbo la Alberta. Nilikwenda kujifunza kuchimba mafuta bila kuchafua mazingira na utumiaji mzuri wa pesa zitokanazo na raslimali hii adhimu kwa manufaa ya umma.

Baada ya kunyaka taarifa kuwa tumetemewa mate, niliwasiliana haraka na waziri mkuu bwana Stivini Haapa na kiongozi wa upinzani profesa Maiko Iginatio wakaomba msamaha sana. Iggy aliniambia ifuatavyo: Votre pays recevait beaucoup d’argents. Si, nos compagnes faisaient bon et grand business la.

Hapa alimaanisha kuwa kwa uwekezaji wa kipumbavu makampuni yao yanachuma pesa nyingi hivyo sisi ni watu muhimu. Hata hivyo viongozi wote wa Kanada waliniomba msamaha sana.

Hata washikaji zangu walionipa mwaliko yaani Vijiwe vya Kuikosa serikali (VIKOSE) walishangaa wepesi wangu wa kufuta hoja na matatizo. Walishangaa niliwezaje kuwasiliana na waziri mkuu na kiongozi wa upinzani hata kabla ya serikali.

Niliwajibu kuwa serikali ina namna yake ya kikiritimba ya kushughulikia matatizo. Hapo ndipo nilipochomoa nakala ya gazeti moja la Kiingereza la Bongo likimnakiri waziri wa sharia akisema bosi wake hana ubavu wa kukamata mafisadi asijue alikuwa akizoza kama mwanasesere. Maana sisi magwiji wa sharia tunajua anao uwezo sema amekosa nia tu.

Pia niliwafahamisha kuwa kwetu matatizo huwa yanatatuliwa kwa mdomo kila baada ya miaka mitano unapokaribia uchaguzi. Walishangaa sana kusikia hivi wakauliza kama wananchi nao wanakubali usanii huu. Sikutaka kuingia undani wa hili kwa vile wangeniona nami kenge kwa kuwa mmojawapo wa wadanganyika hawa. Tuyaache.

Nilipata simu toka kwa Mgosi Machungi na Kapende. Ila nilikuwa nimeishazinyaka kwenye TV ya Canadian Broadcasting Corporation kule. Kwenye CBC niliona mtaalamu wa mabao akijieleza kwa Kiswahili nilistuka nikidhani nilikuwa naota. Punde si punde si ndiyo nikaipata.

Kumbe jamaa wanaijua Danganyika kweli. Maana mmoja aliniuliza kama ugomvi ulitokana na jamaa kutaka kumpiga bao Mkanada? Sikuzungusha. Nilimjibu. Mambo ya mabao yametoka wapi hapa? Kuna mmoja aliniudhi nusu nipasuke. Yeye alikuwa akitoa maoni kwenye CBC. Akasema eti amewahi kuishi Bongo ni nchi fisadi hakuna mfano. Eti angetamani yale mate angetemewa mkuu. Nilijaribu kupiga simu kumtetea mkuu wangu bila mafanikio.

Jamaa alizoza mambo mengi ya ajabu. Alisema kuwa eti sisi tunaishi kama wanyama porini ambako watawala wetu ni simba wanaoweza kuchagua kumla yeyote bila kujitetea.

Yeye alisema anadhani yule jamaa alihamaki baada ya kuwa amepigwa mabao sana. Sasa ndugu zangu wa mabao mjue. Hata watasha wanajua na kuyachukia mabao yenu.

Huyu jamaa hakuficha Jina Lake, anaitwa Tell it All. Alinichefua ingawa alichosema ni ukweli. Alisema kwa Kifaransa chake kibovu asijue mie nakimanya kuliko Wafaransa wenyewe.

Hata wewe msomaji ukijifanya kukosoa Kifaransa changu nikatwika tusi kulaleki. Ukizidi nakutemea mimate.

Tuendelee na jamaa yetu. Alisema. Notre pay contribuait beacoup d’argents au Bongo. Le president, leur femmes avec les enfants et les ministres vivent bien parce que nous les donons d’argents pour le government et corruption est plus grand la.

Tafsiri. Nchi yetu hutoa pesa kwa Bongo kiasi cha kumwezesha mkuu wenu, mkewe, watoto na mawaziri kuishi vizuri tena bila kufanya kazi na ufisadi uko juu sana.

Hivi mtaendelea kuomba omba hadi lini? Hamuoni aibu? Nadhani hii ndiyo sababu nyingine ya bwana Jean Tuchete kuwatemea mimate. Na mna bahati kama jina lake lilivyo angewakeketa. Utani mwingine unaumiza.

Nilipiga simu siku nzima ili kuwambia CBC waondoe uchafu huu bila mafanikio. Walinikatia simu tu. Maana simu zao si kama za Bongo. Nilipiga nilipokuwa kule Ukanada nikawa naambiwa eti salio langu halitoshi wasijue nilikuwa nikitumia dola siyo uchafu huu wa madafu.

Anyway, ndiyo huo uwekezaji wa kisasa aliotuambia Tunituni na akaungwa mkono na Mkuu wa Kaya kijiweni aliyekwenda nje kuwakuwadi wawekezaji ambao hadi sasa hataki kuwagusa wasimuumbue.

Jamaa huyu mshenzi kweli. Alisema pia huenda jamaa alimtemea mate mtaalamu wa mabao kutokana na kutoelewana kilugha. Maana alisema kuwa licha ya mandata wa Bongo kutojua ung’eng’e, kama viongozi wao, wengi wameghushi vyeti au kuwekwa pale na ndugu zao ili kutengeneza mshiko.

Du! Jamaa wanaijua Bongo kuliko hata mimi! Alisema wao hawana ujuzi hivyo wanakimbilia kupokea mshiko hata bila kujua nini kinaongelewa na wasijue watu wengine ni kunguru si kuku waliozoea kuwala!

Ingawa nilijibu kisiasa, jamaa alikuwa na pwenti. Maana kwa muda niliozurura kule kwa pesa za kijiwe na bi mkubwa wangu, hatukuona askari barabarani akiongoza magari. Kwanza baridi itamnyotoa roho ukiachia mbali kuwa na mataa karibu kila makutano ya barabara.

Unajua siku ile nilipokuwa kule Edmonton kushangaa ilipowahi kufanyikia michezo ya Olimpiki joto lilikuwa negative 46? Ukiongeza na windchill ilikuwa kitu kama negative 58. Hii maana yake ni uchukue joto la Bongo utoe nyuzi 32 au 36 halafu utoe 58. Sijui kama unapata picha.

Sisi watalii wanaotumia pesa ya kijiwe hata jamaa yenu na bi mkubwa wake Shorty wanaweza kuwapa picha maana wanatumia kodi zenu za kijiwe.

Huyo anayekuja sijui ni mtasha au tupikenkele. Acha nitimke asijeniloanisha na mimate yake nikaukwaa bure!

Chanzo: Tanzania Daima Desemba 23, 2009.

No comments: