The Chant of Savant

Sunday 28 February 2021

Maalim Seif Sharif Hamad Alikuwa ni Zaidi ya Chama


Kwa wanaomfahamu vizuri marehemu Seif Sharif Hamad, aliyekuwa Makamu wa kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, watakubaliana nasi kuwa makala moja hata kitabu, havitoshi kumuelezea. Hivyo, katika safu ya leo, tutajaribu japo kumdurusu kwa ufupi ili lau kuambua somo tunalopata tokana na kifo chake na mstakabali mzima wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Kimsingi, Hamad alijikita kwenye siasa za Visiwani huku akitumia vyama vilivyoundwa Bara. 
        Hakuna ubishi. Hamad alikuwa mmoja wa wanasiasa nguli nchini hasa kwenye siasa za upinzani na hata ung’ang’anizi hasa ikizingatiwa kuwa anaweza kuingia kwenye historia ya Tanzania kama mtu aliyegombea urais mara nyingi kuliko mtu yeyote tena bila kuupata. Ni mmoja wa wanasiasa waliotawala sana hasa kwenye siasa za upinzani na visiwani. Kwani aligombea urais wa Zanzibar kwa miaka 25 kama tutaanzia mwaka 1992 uliporuhusiwa mfumo wa vyama vingi nchini aligombea mwaka 1995, 2000, 2005, 2010 2015, na 2020 jumla mara sita hadi anakufa mwaka 2021.  Ukimuita mwanasiasa king’ang’anizi au mwenye maslahi fulani binafsi, unaangalia hili la kugombea mara nyingi kana kwamba hakuna wengine wenye uwezo wa kufanya hivyo baada ya kutimliwa toka Chama Cha Mapinduzi (CCM). Tokana na ha hulka hii, ilifikia mahali ikawa vigumu kutofautisha kati ya Hamad na CUF kama ambavyo ilikuja kuwa kwa viongozi wengine wa upinzani ambao huafanya vigumu kuvitofautisha kati yao na vyama vyao ambavyo walivegeuza kama mashamba yao au mali binafsi.
        Historia ya Hamad inaanza pale alipoteuliwa kwenye utumishi wa umma na serikali ya awamu ya kwanza Visiwani ambayo ilihitaji wataalamu baada ya kufanya mapinduzi. Maalim Seif kama alivyokuja kujulikana, alikuwa na dhamira ya kuwa Mwalimu. Hata hivyo, alibadilisha mwelekeo baada ya kuteuliwa. Ili kufanikisha lengo lake, Hamad alianzia siasa zake ndani ya CCM kabla ya kumgeuka aliyemteua kwenye ulaji, marehemu Aboud Jumbe alipofichua mbinu yake ya kutaka serikali huru ya Zanzibar. Hata hivyo, Hamad naye aliishia kutemwa toka CCM ndipo akaanzisha chama cha Civic Union Front (CUF) pamoja na marehemu James Mapalala ambaye baadaye alimnyang’anya chama kabla naye kunyang’anywa chama na profesa Ibrahim Lipumba hali iliyomlazimisha kukimbilia chama cha Alliance for  Change and Transparency (ACT)-Wazalendo baada ya kujaribu kukirejesha chama mikononi mwake bila mafanikio. Baada ya pigo hili, wengi walidhani ulikuwa ndiyo mwisho wa Hamad. Kabla ya kuwaacha hoi pale alipogombea tena kupitia chama chake kipya na kufanikiwa tena kurejea kwenye ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais Visiwani ambayo, kimsingi, ilitokana na Maridhiano au Muafaka aliouasisi Hamad mwenyewe na kufanikiwa kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais cheo ambacho hakikuwahi kuwapo awali. Hapa kuna swali. Je huu ndiyo mwisho wa nafasi hii ambayo wapo wanaoiona kama ya upendeleo kwa upinzani hasa ulioogozwa na Hamad Visiwani? Maana aliyeongoza vuguvugu ni Hamad hata bila kuwa na chama. Rejea alivyoweza kuhamia ACT-Wazalendo na kuidhoofisha CUF Visiwani. Japo Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kusema kuwa hakuna aliye maarufu zaidi ya chama. Ni zama zile. Kwani ukiangalia historia ya Hamad Visiwani utagundua kuwa alikuwa ni zaidi ya chama.
        Kutokana na umaarufu wake na namna alivyoendesha siasa zake, hakuna shaka kuwa alijitengenezea marafiki na hata maadui. Umaarufu wa Hamad ulianza kuvuka mipaka ya Zanzibar pale alipoteuliwa na marehemu Aboud Jumbe (rais wa awamu pili Visiwani) na kumgeuka hadi kumchomea utambi kwa chama akatimuliwa. Baada ya hapo Hamad aliendelea kukwea hadi kufikia kuteuliwa kuwa Waziri Kiongozi. Hata hivyo, aishiye kwa upanga atakufa kwao. Kwani, kama ilivyokuwa kwa Jumbe, Hamad alijikuta akitimliwa chamani hadi kukimbilia kwenye upinzani ambako alianzisha CUF akiwa na James Mapalala kabla kumgeuka, kumuengua na kuchukua chama. Kama ilivyokuwa kwenye kesi ya Jumbe, dhambi ile ile ilizidi kumuandama Hamad. Kwani naye alijikuta akienguliwa na kutupwa nje ya CUF kiasi cha kukimbilia ACT-Wazalendo ambacho chini yake kulitokea sintofahamu pale ACT-Wazalendo ilipomuunga mkono mgombea wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwenye uchaguzi uliopita huku kikimpa mgongo mgombea wake Bernard Membe. Hivyo, unaweza kumuita Hamad mwanasiasa kigeugeu kisiasa hata kama alikuwa na msimamo kwenye mambo mengine. Hata hivyo, hili linakuwa na ukakasi hasa ikizingatiwa kuwa huwa wengi wana tabia ya kuwasifia marehemu badala ya kuelezea ukweli wa namna walivyoishi.
        Kwa ujumla, Hamad alikuwa mwanasiasa mtatanishi ambaye aliweka mbele maslahi yake kuliko kitu chochote. Hatusemi hili kwa ubaya dhidi ya marehemu. Kama siyo Hamad, Zanzibar na hata Tanzania, zisingekumbwa na misukosuko zilizopitia hasa machafuko yaliyosababisha mauaji ya baadhi ya watu Visiwani kiasi cha Tanzania–––kwa mara ya kwanza katika historia ya uwepo wake kama taifa–––kuzalisha wakimbizi wakati ilizoea kuwa kimbilio la wakimbizi kutoka karibu majirani zake wote.
        Tumalizie kwa kusema kuwa Hamad alikuwa si mwanasiasa wa kawaida. Unaweza kumuelezea utakavyo tokana na ule upande wake uliouna. Na huo siyo mwisho wa kumjua Hamad.
Lala Mahali Pema Peponi Maalim Seif Sharif Hamad.
Chanzo: Nipashe Jpili.

No comments: