The Chant of Savant

Wednesday 11 March 2009

Anna Tamaa na mafisadi wengine mpo?





Juzi nilifurahi na kulia kwa mpigo pale rafiki wa baba yangu rais Bingu wa Mutharika alipoamua kufanya kweli kwa kumtolea uvivu jamaa yangu Elisoni Bakuli Miluzi. Alimfungulia mashtaka ya kuibia kijiwe njuluku zipatazo dola 11,000,000. Aibu ya aibu kumbe jamaa alichomoa njuluku zilizotolewa na wafadhili kwa jamaa zangu maskini wa Maravi! Kumbe nimegundua sababu ya wakuu wetu kwenda ughaibuni kila siku kusaka njuluku kwa kutumia majina yetu.


Pia nilifurahi nusu kuuawa na ulabu kwa sherehe pale mama Regina Chiluwa alipohukumiwa mvua tatu na nusu lupango kwa kupatikana na hatia ya kuibia kijiwe na kununua nyumba mbili ukiachia mbali kupokea runinga ya serikali na kukutwa akiwa na njuluku dola za kimarekani 100,000 ambazo alishindwa kuzitolea maelezo. Pia mali zote zihisiwazo kutokana na ujambazi mbuzi huu zimeamriwa kutwaliwa na sirikali. Maskini Regi. Alipelekwa lupango siku hiyo hiyo kuanza kusotea hukumu huku Fred akiishia kutoa mimacho kama bundi. Atang’atwa na mbu na kupigwa na baridi!


Je wezi wetu akina Anna Tamaa wa Makapu atakuwa amejinyakulia mali na njuluku kiasi gani yarabi? Sijui kama siku ile alilala mama huyu ambaye mzee wake yumo kwenye hati hati ya kufikishwa kwa pilato hata kama Njaa Kaya Kikwekwe amesema hatamfungulia mashtaka kwa vile lao moja na wanafanana. Hata hivyo poa. Ipo siku. Kinachowatia kiburi na upofu-madaraka, kuna siku kitafikia mwisho waionje joto ya jiwe.


Nilikunywa kama sina akili nzuri pale fashsti wa Usudani Omari Aliaye Bashir alipofunguliwa rasmi mashtaka ya kuua, kubaka na kudhalilisha wachovu wa Dafuri. Kwa sasa jamaa yumo kwenye 18 ya Luis Moreno-Ocampo ambaye alikuwa mwalimu wangu wa sheria kule majuu kabla sijafukuzwa kwa ulevi na kuishia kughushi digrii yangu kama jamaa zangu ambao nasikia siku hizi wanachangamkia nafasi kwenye vyuo huria ili kuhonga wapewe za kweli. Huu ni upande mmoja wa furaha.


Upande wa pili wa majonzi na machozi ni pale nilipolia kama kichanga kusikia kuwa Li-sirikali lina mpango wa kununua mikangafu ya Dowani binti Richmonduli! Mwe! Hawa wanatuona sisi mataahira siyo? Mbona ni wao waliotwambia kuwa mashini zile zilikuwa mbovu kiasi cha kutowahi kuzalisha hata voti moja ya umeme! Wameingiwa na nini yarabi? Thanks Lord mwishowe wamefyata mkia.


Kilichonitoa machozi ni kuona jamaa yangu Mzito wa Makabwe naye akilambishwa sukari kiasi cha kuwageuka umma. Kumbe jamaa hovyo! Kumbe waliosema kuwa alipata ujiko kwa kismati ilhali yu fisadi hawajakosea. Tusimlaumu au kumtetea Mzito. Wajanja wanasema kinachogomba pale siyo maslahi ya taifa bali ya binafsi. Ni vita ya mafisi wa Dowani na IPTELO.


Nikirejea kwa Dowani na majenereta uchwara yake, tuambizane ukweli bila kumung’unya. Huu nao ni ufisadi tena ufisi. Hivi mnadhani hatujui hata kama tu walevi? Mngenunua uchafu wa Dowani mngewawapa ulaji akina Ewassa bin Richmond . Jamaa hawa hawatosheki. Wametuibia. Tumeendelea kuwalipa mafao ya ustaafu wakati hawakustaafu. Hawaridhiki bado. Kwanini wanatugeuza shamba la bibi yarabi! Poa. Ipo siku yao iso jina.


Ajabu ya maajabu nilisoma utumbo wa Silva Rwamunyama yule kahaba mkuu wa waandishi aliyewekwa kinyumba na Njaa Kaya. Alikuwa akilaumu vyombo vya umbea kwa kuandika kuwa kukuu kumeingilia kwenye dili la majenereta uchwara ya Dowani! Kwani hatujui? Kwanini kununua mikangafu tena kwa bei zaidi ya maradufu ya mpya kana kwamba tu vipofu na mataahira? Huu ni ulaji na jinai hata kama unawahusu wakubwa. Eti naye Daktari Iddiliisha Rushdie naye anatoa ushauri! Mbona anajulikana alivyokwanyua njuluku kwenye dili la rada yeye na Enderea Chenga? Huyu hana udhu. Ni mwizi hata kama ana ulaji mkubwa.


Huyu na Bill Ngereja hawana maana kabisa. Hawana tofauti na Leo Maasha wa kutaka kutuibia kutumia vitambulisho uchwara. Nasikia anafanya mipango aanzishe dili la vitambulisho vya zeruzeru na faru kwa vile ni viumbe walioko hatarini kutoweka! Naye ipo siku yake.


Kweli waso haya wana mji wao walijisemea watu wa mipasho. Nani angekubali upuuzi wa kuwazawadia Dowani ulaji ilhali waliishatuibia? Ajabu hatujifunzi. Dowani Bin Richmond wajukuu wa Rosti Tamu L’Aziz wamegeuka Lisirikali ndani ya Lisirikali. Uchu mwingine ni mbaya kuliko hata wa mbwa na fisi. EPA wewe, Richmond umo, CIS wewe, Dowani umo, kila kitu umo. Je hii dunia ya Wadudi utaimilki wewe? Itakumaliza kabla hujaimaliza.


Hata hivyo tusishangae sana . Watu wanatafuta takrima kwa ajili ya uchafuzi wa mwakani ili waendelee kutumaliza. Je nasi tutaendelea kujirahisi na kujiruhusu watumalize? Hovyo!


Kweli nimeamini usomi wa mpumbavu hauondoi upumbavu wake. Jitu linajinakidi lina PhD tena ya uchumi linahujumu uchumi! Iddiliisha anaitwa Daktari. Ajabu anatumiwa na matapeli vihiyo kunyea kambi? Hapa msomi nani? Heri yangu najulikana mlevi lakini nina mapwenti. Unadhani mchezo kuchonga kila wiki na usiishiwe? Jaribu uone kama ni mchezo.


Hayo tuyaache. Hivi Dowani imewapa nini hadi inaweka wanaume wazima kimada nanyi mnaridhia? Tunawalipa mishahara minono na marupurupu. Hamridhiki hadi muwekwe kinyumba na tapeli. Ama kweli kunguru hafugiki na fisi ni fisi hata awe na madoa. Fisi ndi fisi walijesemea wanyasa. Mbwa ni mbwa hata kama ni wa kizungu.


Tumalizie tulikoanzia. Tulipotaka kumsulubisha Ben Tunituni Makapu tuliambwa ana kinga. Ana bonge ya tunguli tuliambwa. Je na huyu Bi Tamaa analo tunguli kama la Ben au tunafungwa kamba na jamaa baada ya kunusa upepo wa kitakachomsibu siku akitua mzigo? Tuhoji hata kama tumelewa. Je changa la macho hadi lini? Tutaendelea kuwa shamba la bibi hadi lini? Dawa ya jipu ni kulitumbua. Tutumbue jipu hata kama ni kwa maumivu makali. Baada ya kulitumbua tutalala angalau usingizi kama akina Banda pale Mulungushi na Kalulushi.



Tumalizie kwa kunukuu maneno ya spika Six. Richmonduli na Dowani ni mtu na binamu wake. Na Ewassa na Njaa Kaya na Rosti Tamu ni mtu na kaka yake. Jiandae kulazwa gizani ili mbwage manyanga wezi wetu wale. Je IPTL nayo binamu yake nani? Mwenye akili atie akilini. Ila tufanyieni sanaa zenu. Ipo siku iso jina mtalia na kusaga meno. Na hizi kura za wanaoua matupinkele si ushahid wa Li-sirikali kuishiwa? Mbona hamuandai zoezi la kura za mafisadi? Au mnaogopa mtajinasa kwenye nyavu zenu?
Chanzo: Tanzania Daima Feb. 11, 2009.

No comments: