The Chant of Savant

Tuesday 6 March 2012

Nakwenda kwa mama kutuliza hangovers

BAADA ya kupona kufa kutokana na migomo ya matabibu, Dk. Mpayukaji Nkwazi Nkuzi Mhango Msemahovyo, na marafiki zake kina Mgosi Machungi, Mzee Maneno, Mchunguliaji na wengine wapatao 50 wamepata ofa ya kwenda kwa Mama kutumia na kupunguza hangovers za kahawa na kinywaji.

Wakati tukipanda pipa na kujitoma zetu kwa mama, wanywa kahawa wengi walikuwa wakilalamika kuwa tumechukua njuluku za kijiwe kwenda kutanua.

Hakuna kilichowakera wanywa kahawa kama mimi kuwa naandamana na marafiki zangu na mke wangu karibu kila mahali. Hakuna kilichonikera kama kusikia upuuzi huu wakati pesa tunayotanulia si yao bali wafadhili wetu ambao leo sitawataja.

Kwanini nisiende kwa mama baada ya kumaliza mgomo wa wachemsha kahawa waliokuwa wakitaka kuongezewa marupurupu hasa kashata na maadazi kutokana na kazi yao ya kuhakikisha uhai wa wanywa kahawa haudhuriwi na uchafu hata polonium kama ile ya daktari Mwakiwembe?

Kabla ya kuendelea, wajua kuwa kijiweni kwetu umetokea mchezo mbaya wa kurogana na kulishana hata kupakana sumu? Juzi Msomi Mkatatamaa alikuwa akilalamika kuwa anahisi amegusishwa Polonium kiasi cha kuanza kuwashwa washwa sehemu za nonihino.

Kwa vile kumalizana imeanza kuwa fasheni kwenye kutafuta ulaji, wanywa kahawa wengi walitaka nitoe maelezo.

Nami kuona zali hili ni kubwa kuliko ubongo wangu wa P’eege nimeamua kwenda kwa mother kutuliza akili ili mambo yapoe kama alivyowahi kusema Willy Mkama kuwa Waingereza wakiona mambo yamepamba moto huunda Royal Commission kuwazuga wajinga kuwa wanachunguza ili mambo yapoe na yakipoa wanaendelea kuhomoa kama ilivyo kwa Bongolalaland ya Danganyika ambapo mafisi na mafisadi hushika kani huku walala njaa wakiendelea kutolewa njuluku na kusota.

Hebu turejee kwenye malalamiko ya wanywa kahawa. You know what. Hawa jamaa wanaungua ugonjwa uitwao Ammaglobulimenia yaani kuwa na mfumo uliovurugika mwilini.

Matokeo yake ni kuugua ugonjwa wa Bulimia unaoandamana na mwingine uitwao Megalomania. Watu wanaougua ugonjwa huu huwa wanajifanya hamnazo. Hata uwambie nini huwa hawashughuliki na kujibu wala kutoa maelezo. Kwa mfano, mgonjwa wa Bulimia ukimwambia kuwa anachofanya ni kibaya hufanya zaidi.

Huwezi kuamini eti wanasema nami naugua Bulimia kwa vile wakiniambia niache matanuzi mimi na marafiki zangu natanua zaidi. These guys are super stupid so to speak. How can a big guy with all ulaji under my control be that silly? Hooey! Samahani nimechonga umombo kwa sana kama maandalizi ya kwenda kuchonga na kwini.

Pia nachonga umombo kuwaonyesha wanaoshuku udaktari wangu wa kupewa kuwa nimebukua hata kama sikupata honours. Hayo tuyaache.

Wanywa kahawa kwa umbea sina hamu. Yaani mie kuandamana na maswahiba zangu 50 imekuwa stori. Je, wanataka niende na wangapi? Mwakani nitakwenda na 800 kama alivyokuwa akifanya shujaa wangu Mobutu Sese Seko Mwizi wa Zabanga kule DRC.

Hawa jamaa hawajui kuwa waliponichagua kuwa mkuu wao hawakujua kuwa sikugombea kuwaendeleza bali kujiendeleza mimi na nyumba yangu.

Hawajui kuwa nilipowaahidi maisha ya kuukata nilimaanisha yangu marafiki zangu na nyumba yangu? Kalagabaho na shauri yao! Imeandikwa kuwa mchungaji atakunywa maziwa ya kondoo awachungao. Kosa langu nini kula pesa ya nyinyi niwachungao? Pia imeandikwa kuwa ya Kaisari muachie Kaisari.

Kwanini wanywa kahawa hawataki kuniachia yangu kuwa yangu? Niliwahi kuuliza swali hili Msomi Mkatataama aakijibu kuwa wanachotaka si ya Kaisari maana kahawa si mali ya Kaisari yaani mimi bali wao. Jamaa mshenzi!

Ana maana kuwa hata walipa kodi wana haki ya kujua kodi yao inatumikaje kwa vile ni yao na si ya mkuu siyo? Wee koma. Sasa unaanza kugusa pabaya! Kama mkuu anawala waliwa wewe yakuhusu nini iwapo nawe unawala wanywa kahawa? Wajinga ndio wafanywao punda.

Sijui niwambie nini hadi waelewe. Huwa nakwenda nje mara kwa mara kubomu ili maisha yasonge mbele. Wengine husema eti nakwenda kufanya biashara na kukagua akaunti zangu huko. Well, hata kama ni hivyo, kwani nimewazuia wao kwenda? Sasa nasema wazi wazi.

Huwa napenda kwenda ughaibuni kutafuta wawekezaji wa kuja kuchukua sorry kuwekeza kwenye kijiwe. Bila mimi kwenda kule wawekezaji watagoma. Mbona watu wanasahau mapema! Bila ya yule jamaa yangu Ni Ziro Kamalagi kwenda kusaini mkataba wa Buzwagiii kule London tungekuwa na wawekezaji kweli? Au wanatumia akili mbovu ya Mzito Kabwela anayetaka kaya iache kuwalipa washikaji wa wakubwa waitwao AIPITIELO matrilioni eti wawekeze kwenye gesi.

Huyu kijana hana adabu. Anataka wazito wale polisi? Inaonyesha hata kwenye kijiwe kuna watu wa Mzito Kabwela. Maana nakumbuka alikuwa akipita kupata kikombe cha kahawa. Huenda aliacha magugu nyuma alipopita. Namshauri akatapeliwe kule Loliyondo kwa kupewa kikombe kichafu cha kutibu ujinga cha mchungaji Ashomile Mwatapeli.

Nasikia jamaa huyu kanogewa na kutangaza miujiza mingine ya kuwatapeli wajinga ndio waliwao waliojazana Bongolalaland ya Danganyika. Kwanini hawatumii vichwa wanatumia masaburi?

Nikifika London lazima nikajinome kwenye mitaa ya Trafagar, nitabembea na bi mkubwa pale Brent Park (Siyo Jomeika ambako iliniwia soo), Hounslow, Richmond, Kingston upon Thames, Buckingham, Gunnesbury, Isle of Dogs na kwingine. Wajua nimekulia London?

Ukiachia upuuzi wa malalamiko ya wanywa kahawa, hawajui kuwa mie huwa sipendi kukaa sana kijiweni. Huwa naboreka kukaa kijiweni nikisikiliza malalamiko mbali mbali ya wanywa kahawa.

Ili kuepuka kuusonesha moyo wangu kwa kuletewa habari mbaya kila siku, huwa napenda kwenda nje kutumia. Hivi utajisikiaje iwapo kila siku utaletewa mashitaka yanayowahusu watu wako hasa mke, watoto na marafiki kuwa wanatumia ukuu wako kujineemesha kwa kukiibia kijiwe? Wanataka nikae kijiweni waje siku moja wanilazimishe kuamrisha watu wangu waaibishwe na mgambo wa city kwa kutumia ulaji wangu kujineemesha?

Hata hivyo kuna kosa gani kwa mke wa mkuu wa kijiwe kuwa mkuu wa wanawake wote au mtoto wa mkuu wa kijiwe kuwa mkuu wa vijana wote?

Naota nakuwa kwini siyo! Pesa ya safari hii imetolewa na kwini. Ila usimwambie mtu.

Chanzo: Tanzania Daima Machi 6, 2012.

No comments: