The Chant of Savant

Wednesday 26 December 2012

Tathmini ya kufungia mwaka


NITAJE au nisitaje? Wajua? Mke wangu mama Kidume anamilki NGO ya MAWA ambayo imetuingizia fweza kiasi cha kuwa tajiri hata kuliko mimi mwaka huu.
MAWA licha ya kumuingizia bi mkubwa mshiko wa nguvu, imesaidia kupeleka huduma mbali mbali kama elimu na afya kwenye jimbo na mkoa wangu na ule wa bi mkubwa. Kwa kutumia jina la kaya tumeweza kusheheni huduma makwetu huku tukiwaacha walevi wakiparurana kwa ajili ya huduma hizi.
Hii inaitwa huduma ndani ya hujuma. Hata pesa ninayotumia kunywa gongo huwa mara nyingi inatokana na hii taasisi nyeti ya MAWA.
Mwanangu kidume naye hakubaki nyuma. Nimempitisha kiasi cha kuweza kugombea ulaji kwenye umoja wa vijana wa kijiwe. Kidume anayemiliki kampuni ya KUCK yaani Kidume Untachable Kid of Chief naye ametengeneza mshiko si kawaida.
Huwezi ukaamini hata yule mwanangu mlevi Milaji naye ni bilionea kwa sasa! Atashindwaje wakati dili zilikuwa za kumwaga? Kwanza ukiwa na ukuu kila kiumbe anakuabudia. Unaonekana kama malaika. Hata hivyo inabidi tuchukue chetu mapema tukijua fika kuwa ukuu ukituondokea waliokuwa wakituabudu.
Watatushit na kukimbilia watakaokuwa wamechukua nafasi yetu. Hivyo usishangae kusikia Mpayukaji amejitahidi kufanya kila kitu hasa ndani ya mwaka uliopita. Si haba. Nilipanua idadi ya nyumba ndogo zangu. Nyumba ndogo hamsini na saba na wanaharamu arobaini na wanne. Hata walevi walifuata mfano wa kiongozi wao kwa kukazana kuzaana na kuijaza kaya.
Haya ni matokeo ya sera bora ya mgao wa mameme ambao umewapa fursa ya walalanjaa kuzalisha wengine ili tuendelee kuwanyonya na hata kuwauza.
Hivyo wale waliokuwa wakilaumu miradi kama Kagodamn, HEPA, Richmonduli na Dowans washindwe na walegee.
Hawakujua tulipoianzisha tulilenga kuongeza idadi ya watu ili majirani zetu wasije kutuvamia na kutupiga hata kwa mingumi kwa kutumia wingi wa watu wao.
Pia mwaka huu ulikuwa ni mwaka mmoja tangu kusafirishwa kwa wanyama waliokuwa wakila majani na kuharibu mazingira.
Najua wengi walichonga kuwa tumeuza wanyama nje bila kujua kuwa tulikuwa tunawapunguza ili kuepusha uchafuzi na uharibifu wa mazingira.
Kwa kimombo hii inaitwa ecological equalization based on termination and elimination aimed at making billions for a cabal of swindlers and mightier thugs like us.
Kuonesha sayansi hii ya kuhamisha wanyama inavyopaswa kuwa sera ya taifa, tunamaliza mwaka kwa kuwa na mtaalamu wa kuhamisha nyara aitwaye Amdaraamani Kinamna kama mkuu wa chama. Pia katika safu za juu tumemrejesha mtaalamu wa mambo ya HEPA aitwaye Phil Mangura ili kwenye uchafuzi ujao atusaidie kutengeza mshiko mwingine kama ule uliotumika kutuingiza kwenye ulaji kwenye uchafuzi uliopita.
Ndugu walevi, ikumbukwe pia kuwa huu mwaka unaoisha ulikuwa ni mwaka wa kuwapa nguvu ndata.
Hii kwa kimombo huitwa empowerment and embarrassment of the criminals especially when those supposed to stop crime commit it at a very high magnitude.
Kutokana na kutaka ndata wawe na nguvu za kutisha ili walevi wawaheshimu, tuliwaruhusu kuua kila wanayeona ni tishio kwa ulaji wetu. Walianza na Mwangosi na kuendelea na wengine wadogo wadogo.
Ila katika utekelezaji wa empowerment yao kulitokea kitendo kinachopaswa kulaaniwa dunia nzima.
Wapiganaji wawili waliuawa kule Ngala. Hata hivyo, tutahakikisha waliotenda kitendo hiki ambacho hata Mungu hatakisamehe watasakwa wao wajukuu zao hata vitukuu na kuadhibiwa ili liwe somo kwa wengine.
Ndugu walevi, mtakumbuka kuwa mwaka huu mzee mzima na bi mkubwa wangu hatukuzurura kwenye vijiwe marafiki. Hii ni baada ya kusikia mkilalamika sana. Hivyo, kuonesha tunawaheshimu tulipunguza kuzurura.
Hivyo mwapaswa kunipigia makofi ili kunipa moyo wa kuendelea kuwasikiliza hata kama wakati mwingine nitawasikiliza na kuwapuuzia.
Ndugu walevi, hotuba yangu haiwezi kuisha bila kutaja mafanikio katika sekta ya pesa ambapo kaya yetu imefanikiwa kuingia kwenye kumi bora kwa kuwa na uchumi mzuri kiasi cha kuzalisha pesa nyingi hadi nyingine kukoswa pa kuiweka.
Hivyo, tuliamua ipelekwe Uswisi. Hii itasaidia kutangaza kaya yetu na kuweza kuvutia wachukuaji sorry wawekezaji.
Wapinzani wetu walijidai kutusingizia kuwa pesa hii ilifichwa kule kiwizi. Kwa kujua janja yao tuliwaanzishia kampeni chafu na ya kisayansi ambapo kinara wao bwana Willy Silaha tulimzushia kuwa ni mwanachama wetu.
Hivyo, badala ya walevi kuendelea kujadili mambo ya Uswisi walidakia hili la kadi nasi tukaendelea na mipango yetu ya kukuza uchumi kwa njia ya kuhamisha pesa ili isiwe nyingi na kufanya kila mtu kuwa nayo hivyo watu wakaacha kuzalisha.
Kitaalamu hii huitwa, financial relocation aimed at avoiding overflowing knock on effects.
Ndugu walevi, Mwaka unaoisha umeonesha mafanikio katika ujenzi wa mahekalu. Sasa hivi kaya yetu inaheshimika na kuogopwa kutokana na kuwa na mahekalu mengi yenye hata hadhi kuliko lile la Sagrada familia kule Barcelona.
Nadhani mlisikia watu kama Eze Maige wakitajwa kuangusha mijengo ya bei mbaya tena kwa kununua kasha kwa dolari. Huu ni ushahidi kuwa sera zetu zimeleta ufanisi hakuna mfano.
Pia kaya yetu imefanikiwa kujitangaza kimataifa. Kila wiki tumekuwa tukipokea ujumbe toka majuu ukituletea jezi za mipira kama alama ya kuonesha sisi ni wachezaji bora katika utawala. Hamkuona juzi pale kijiweni nilipoletewa jezi ya timu maarufu huko Ukamerunini iitwayo I have forgotten everything except fooling the mighty.
Wakati tukijiandaa kufunga mwaka, tunazidi kuwaahidi kuwa tutafanya maajabu mengi ili kuhakikisha tunaendelea kujulikana ulimwenguni. Kwa mfano, tumeazimia kukaribisha wawekezaji hata wachukuaji wengi ili kujulikana zaidi ulimwenguni. Tutapanua huduma zetu kwa kuwa wakarimu kwa wageni wetu. Tutazidi kuwapunguzia kodi huku tukizidisha mgao kwa walevi ili wazaane sana. Pia mwaka ujao tutaanzisha utaratibu wa kuyatibu mateja yaliyo maarufu. Hii ndiyo njia mujarabu ya kupambana na unga.
Badala ya kupambana na wauza unga unapambana na wala unga. Maana wanaouza hawaathiriki kama walaji. Wauza unga wanatajirika hivyo hakuna haja ya kuzuia watu kutajirika. Badala yake tutawaacha wauze. Sisi tutashughulikia kutibu mateja. Pia mwaka ujao tutaendelea kuwaenzi wasanii kwa kuwakaribisha kwenye pakuu pa pakuu ili kuwaingiza mkenge waendeleee kutupigia debe sisi na usanii wetu.
Kumbe leo ni boxing day! Acha niwahi nyumbani kufungua zawadi ili huyu mama asijenizidi ujanja.
Chanzo: Tanzania Daima Desemba 26, 2012.

No comments: