The Chant of Savant

Wednesday 4 October 2023

Tumefyatuliwa, tumefyatuka, sasa tunafyatuana

Sijui nianzeje kufyatua kabla ya kufyatuliwa. Sijui niseme tumechanganywa, tumechanganyikana ama tukachanganyikiwa na sasa tunachanganyana kiasi cha kuzugana na kuzinguana. Tumefyatuliwa tukafyatuka na kupagawa kiasi cha sasa kufyatuana kama kaya hadi wachache kutaka kuwapagawisha na kuwafyatua wengi. Kama siyo kupagawishwa tukapagawa na kufyatuliwa na kufyatuka kabla ya kuwafyatua wanaotufyatua na kutupagawisha, inakuwaje walakaya wapingane na wanakaya au tuseme watu walao wapingane na watu waliwao? Kama siyo ufyatu ni nini? Watuwala wanataka kula zaidi kwa kukaribisha na walaji waitwao wawekaji japo wachukuaji huku watuwaliwa wakipinga kuliwa zaidi. 
Naona yule anabeua midomo akidhani fyatu naanza kufyatuka kabla ya kufyatua mambo bila kujua naweza kufyatuliwa na fyatu waliofyatuka kwa ulaji wakavimbiwa na kufyatuka kiasi cha kufyatua kila awapingaye ufyatu na ulaji wao na wenzao wa kutoka umangani kwa deep world aka deep weed aka ganja aka janga aka fyatua fyatu.
Huna haja ya kufanya hivyo wala kuning’onga dugu yangu. Kama fanya hiwo iko dili kuba kwenda fanyia ile fyatu nafyatuka hadi nachanganya, koroga hadi vote nachanganyikiwa na narogeka hadi sasa hapana jua fyatu va kweli na ongo. Hata hivyo, shetani wa yote haya si ufyatu wetu bali dipii wiid sijue weed sijui wed wa mama sijui ganja. Sijui. Ukitaka kujua zaidi hili dude kawaulize watasha wa Dubei ila angalia usipigwe bei ukaishia kufanyishwa kazi za ndani kunyanyaswa hata kuitwa mtumwa aka abid kwa kitasha.
Wadanganyika tunadanganywa hata pasipostahiki. Chukulia mfano, mtu mzima unadanganywa na chawa badala ya kuwaulia mbali. Kwa namna tulivyopagawishwa na wenye shibe, tumechanganyikiwa hadi kuruhusu chawa kufanya mambo ya kibinadamu! Wabonge wanabonga mambo ya ajabu kiasi cha kuhojia hata uheshimiwa sorry uishiwa wao. Wameishiwa hadi wanageuza bonge tukufu kuwa bonge la mipasho. Wakubwa wanafanya utoto kwenye mambo ya maana.
 Mfano ni kipaza sauti. Da huyu fyatu kweikwei. Anapayuka utadhani maamuma wallahi. Amepagawa sina mfano. Badala ya kuisimamia siri kali, anaanzisha siri kali yake bongeni. Ukimsikia anavyojiita mbukuzi unashangaa alibukua nini wakati akizoza hupati pwenti zaidi ya kuhisi chawachawa. Au ni kwa vile kipaza sauti kimejaa chawa waliogeuka bonge? Kama mwenye kaya amejaa chawa, kipaza sauti kitafurika chawa?
Nilimsikia fyatu anayejiita mbukuzi akiwadanganya wadanganyika kuwa katiba mpya haileti chakula mezani! Seriously? Bila katiba kunena kuwa wanene watakuwa wanene na ulaji wao utakuwa mnene, hawa wanene wanaonenepeana na kutumia mashangingi manene kwa kodi ya walalanjaa wangekuwa wanene hadi wananenepesha hata chawa? Asikudanganye fyatu, mdanganyika, mpagawaji, mbonge, wala chawa. Katiba ni kila ni, isingekuwa tiba, isingegomewa. Bila katiba hakuna chawa, wanene, kaya wala ufyatu utokanao na ulaji wa kilafi.
Najua waishiwa waliishiwa hoja zamani. Wanaoshangaa walivyopitisha deep weed wanajidanganya. Walipogeuka/zwa mabingwa wa mapambio, mipasho, ngonjera, kujigonga, kujikomba, kuzuga na sarakasi ili wajaze matumbo yao yaso shukurani hata kwa kumegewa utukufu. Pamoja na ufyatu wangu, naona kama waishiwa wamegeuka sehemu ya siri kali badala ya kuwa bonge la kuizodoa na kuitoboa siri kali kama walivyotumwa na waliowatuma.Wameishiwa hoja na kujaa vioja kiasi cha kujidhalilisha wao na bonge lao tukutu.  Badala ya kunena, wananuna na kuchawishwa. Badala ya kutoa mwelekeo wanaelekezwa kuzimu kwenye deep world.
Ukiachana na waishiwa, hata maza mwenyewe ametupagawisha hadi tukapagawa na kuchanganyikiwa, na kuchanganyana. Kala pini utadhani deep weed halimhusu wakati ndiye aliyeliibua. Hata wadingi tuliotegemea wangeokoa jahazi wamezama nalo. Badala ya kutoa nasaha wanatoa hasira na usaha. Wana hasira kama Stivi wahasira ambaye akipanua kinywa wanatoka harufu chafu na inzi kiasi cha kufanya mafyatu wakimbie. Ni hatari kiasi gani fyatu mmoja kuwakimbiza mafyatu kwa maelfu?
Nilimsikia doktari Silaha, baada ya kufyatuliwa, akilalamika baada ya kusondekwa korokoroni alipodai katiba mpya. Alifyatuka kuwa hakutaka kutoka korokoroni. Du!  Kama hakutaka, nani alimlazimisha au kamba za siasa za visa na visasi? Si ukubali wewe ni fyatu uliyefyatuliwa na mafyatu unaotaka kuwafyatua ili kulipiza kisasi? Huyu Silaha na Tundi Jisu wamefyatuka kweikweli Nilimuona Jisu kule Rongorongo akihenyeshwa afyate asiende kuwafyatua akina yero ili wagomee kupisha uchukuaji, sorry, uwekezaji wa kimanga na kimangaa.
 Kabla ya kusahau, kuna fyatu moja anaitwa Mdudu na mwenzake Mwambukuzi. Du fyatu wanafyatuka! Kama fyatu wangekuwa fyatu kama hawa si haba. Katiba mpya ingekuwa imeishachakaa. Jamaa wanazoza utadhani wana mageshi sehemu. Hawaogopi hata ndata ambao nao siku hizi wamefyatuka kiasi cha kuwekwa rumenya na chata twawala.
Zama zile fyatu nikiwa chuo kikuu cha Hazard kwa Joji Kichaka nilifundishwa kuwa ndata hawapaswi kushiriki siasa wala kutumiwa kisiasa. Hii huitwa uongozi bora siyo bora uongozi kama ilivyo ufyatuni.
Lo! Kumbe naota!
Chanzo: Mwananchi leo.

No comments: