The Chant of Savant

Wednesday 24 January 2024

Mjue Katibua Mkuu Mpya wa Chama cha Mafyatu (CcM)

 

Baada ya aliyekuwa katibua mkuu wa Chata cha Mafyatu (CcM) kufyatuliwa na kashfa ya ukwaree, juzi tulipata mrithi wake. Tulikutana kisiwani Mafia kuteua katibu mkuu mpya kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na kufyatuliwa kwa Mchongo. Loh! Sasa nataka kufyatuka! Namaanisha Chongo loh, sorry, katibua muwajibika alitibua wakamtibua akatibuka na kutokomea. Tokana na chata letu kuwa la koo maarufu nene zenye historia ya ulaji Kayani, tulifyatua sifa za wale waliopaswa kujipima kugombea nafasi hii yenye ulaji na ushawishi mnene kwa mafyatu. Zifuatazo ni baadhi ya sifa walizokuwa nazo wagombea:
        Mosi, walipaswa kuwa mafyatu wa vigogo wa chata. Kama maza au dingi wako hakuwa/kuwahi kuwa kigogo, hukuona ndani. Tulishauri wasio vitegemezi wa vigogo kutotupotezea muda kuleta maombi wala kuwa na mawazo ya kupitishwa. Siku zote, tumekuwa wazi katika hili. Kauli mbiu ya chata letu inafahamika. “Chata lina wenyewe na wenyewe ni vigogo na tugogo na vitegemezi vyetu.” Hivyo, msishangae kukiona kitegemezi chetu Daktari wa Falsafa na propaganda dogo Imma Mchimvi Nkwazi wa Ngwenyama ambaye ni kitegemezi changu na Bi Mkubwa wangu Nesaa kupitishwa na kupeta kuwa katibua mkuu wa chata la shoga yake mama yake. 
        Pili, mbali na kuwa kitegemezi cha kigogo, muombaji alipaswa awe na PhDii ya kweli ni si ya kuungaunga au ya kughushi au ya heshima zilizogeuka za dharau. Kayani kwetu, bila PhDii halisi na siyo hizi za heshima na zile zinazotolewa na kupelekwa kwa wanunua kama pizza huna chako. Tulitaka wasomi waliopiga shule kwelikweli na siyo  wa kughushi au kujipachika kama matapeli wachunaji wengi wajipachikao vyeo vitukufu vya kiroho kuficha uroho wao na ufisadi wa kuuza neno la Mungu. Hii ililenga kuwafyatua maadui zetu wapingaji watuogope na kuufyata. Juzi nilisikitika sana kwenye inshu ya mageshi kugeuzwa wazoa taka.
        Mnakumbuka namna yule Chiwawa wa maza alivyojibu upupu na upuuzi badala ya kujibu hoja? Sie siyo kama wale wawalao mafyatu tena kwa kubabaisha na kutumia chawa na viwawa. Sisi, tunatumia wasomi waliova na kuivika wawafyatue wanaotaka kuufyatua ulaji wetu mnene na mtukufu. Alhamdullillahi hukutuletea Chiwawa japo umetupa madoamadoa kama Katibua wa chata lako mpyaaa.
        Hapa lazima nikazie. Hatukutaka mafyatu waliowahi kujipa udaktari hata kabla ya kuusomea. Namkumbuka mmoja kwenye chata la wale aliyekuwa akijiita doktari hadi janja yake ilipofichuka akaamua kuregea shule na kupewa. Sina hakika kama aliisomea na kuifyatua kihalali au alipewa kama wale wengine wenzake kwenye chata lao niwajuao vilaza wanaojiita madoktari kama mimi wasijue yangu nimeihenyekea ughaibuni tena kwa miaka.
        Tatu, ili uteuliwe katibua wa CcM, lazima alipaswa kuwa tayari kuacha ndoto ya kugombea urahisi kunipinga mimi. Hii nafasi, nilishasema wazi, ni yangu. Hapa hapakuwa na cha domokrasia ya ndani ya chata wala nini. Lazima nipite. Na atakayejitia kiherehere kunipinga ajue nitamfyatua tu. Akijitokeza, nitamnyamazia, ila ajue, baada ya mafyatu kunipa kijiti, nitakitumia kumfyatua. Nitamkong’ota kulhali ajue mie siyo wa kuchezea.
        Nne, alipaswa kuwa mkatili ili kuendesha operesheni ya tokomeza uchawa (otu) katika kaya na chata. Hatukutaka machawa wanaoeneza magonjwana kunyonya damu za mafyatu. Tulitaka fyatu safi na katili ambaye akisikia neno chawa anapata kichaa na kufyatua vitu vyake.
        Tano, hakupaswa awe au aliwahi kuwa msaliti. Kwa fyatu yoyote ambaye ima amewahi kulazimika kujiuzulu wadhifa wowote, kutangazwa msaliti na kupewa adhabu ya kutogombea nafasi yoyote kwa miaka minne, hii nafasi haikumfaa wala hakutufaa. Nani anataka msaliti? Chata letu siyo karai la kufuliwa makapi na uchafu au kokoro la kuvua kila aina ya taka zipatikanazo ziwani na nchi kavu. Chata letu ni chata safi na tukufu lisilotaka mabaka, magamba, au kuwa chaka la mabaki, wasaliti, chawa, na wachumia tumbo wenye uchu wa Madaraka, wala si madhabahu ya kusafishia wenye dhambi za usaliti.
        Leo sisemi mengi. Nadhani nimeeleweka vilivyo. Tusijelaumiana kuwa sikuwaonya. Narudia, bila jina kuba au kuwa toto ya gogo hapana laji yako dugu yangu. Nendauza nyanya dugu yangu au cheza bahati nasibu naweza pata laji huko.
Hivi katibua wa CcM ni nani eti na sifa zake ni zipi nunc pro tunc? Hilo bomba nawaachia muwaulize wanasharia.
Kama wewe dingi au maza wako hakuwa kigogo na haukuwa na PhDii ya ukweli, usingeona ndani. Wote waliojitia kufyatuka, walinoa. Tulihakikisha tunapitisha vitegemezi vyetu kulinda na kuepuka kuhatarisha maslahi yetu. Si inapendekeza? Naona yule anatikisa kichwa kwa hasira. Huna haja ya kujitia presha. Utake, usitake, ndivyo ilivyo, chata letu lina wenyewe na wenyewe ni sisi vigogo na koo zetu, watoto, vijukuu, vitukuu, vilembewe, vilembwekeza na vinyinginyika, kuku, mbwa, chawa, na hata panya wetu. Kwani nani alikuzuia au madingi wako kuwa vigogo? Ukitaka ulaji, basi kafyatue au kafyatuliwe na kitegemezi cha kigogo kama braza Moody Mchengeta.
 Geshi ni kama gesi. Likiripuka, wote tunalipuka. Chondechonde msiliingize kwenye siasa zenu za majitaka/uchiwawa/uchawa. Kazi yake si kuzoa taka wala kusafisha vyoo. Hizo kazi zina wenyewe kwenye mamlaka za mawilaya na siyo geshi letu tukufu.
Chanzo: Mwananchi, leo.

No comments: