The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Sunday, 9 August 2026

Ukiona hivi, jua uchumi wa Fyatuland ‘umekua’kkkk!


Mtanange baina ya wanene na wanaojishaua kuonyesha mabulungutu ya njuluku mitandaoni una somo kubwa. Unafikirisha, kutekenya akili japo ni aibu na kiini cha ujambazi uliohalalishwa kwa mlango wa nyuma. Nani anapaswa kumaripia nani wakati wanene nao wanafanya hili? Tokana na kadhia hii ya kutaka misifa uchwara, ulimbukeni, na uzwazwa, Fyatu Mfyatuzi napanga kuanza kile kiitwacho kwa Kisambaa lifestyle audit. Hivyo, yeyote atayeonekana akijishebedua na kurusharusha njuluku hovyo kwenye matukio kama harusi, ubarikio, ufunguzi wa nyumba na mengine lazima anieleze amepataje hiyo njuluku ilhali Mafyatu walio wengi wanalia ukapuku.
            Kwanza, nitaanza na wanene wenzangu wanaohonga Mafyatu mchana kweupe wakichangia miradi iwe ni ya mahekalu ya kitapeli yaitwayo ya Sir God na mengine. Lugha za munene mkuu xyz anamwaga njuluku nataka ife haraka sana. Hizo njuluku kazipata wapi na vipi kama siyo kwa kupiga? Kwanini kila anayeukwaa unene anaanza kuwa na ‘huruma’ hadi kumwaga njuluku zetu kama vile ni zake? Mbona akina mzee Nchonga, pamoja na kukaa kwenye maulaji na kufanya makubwa, walikufa makapuku? Tunamdanganya nani ili iweje na kwanini?
 Tuanze na sisi wanene ili kuonyesha uongozi na uwajibikaji na si uongo na usanii. Lazima tuongoze tokea mbele na si nyuma. Je, njuluku tunayotumia na kufuja tunaipata kihalali au ni jinai inayoanza kuhalalishwa? Haiwezekani mafisi, mafisadi, na majizi yatukoge na mabulungutu ya noti ilhali wengi wanakufa kwa mabulungutu ya hasira na ukapuku. Lazima watueleze na tuelewe ‘miujiza’ wanayotenda hadi kuwa wakwasi hivi.
            Naona yule anatikisa kichwa na kusonya kwa ufyosi. Ukome. Tueleze tuelewe ulivyochuma hiyo njuluku mnayofanya ikose thamani kwa manavyoigawa. Nataka kuchukua hatua hizi madhubuti si kwa sababu ya husda wala wivu. Nachelea kuingizwa cha kike na wauza mihadarati, watakatishaji njuluku, majambazi, mafisi, na mafisadi wanaotuumiza na kujidai kutusaidia kwa kumwaga njuluku kwenye matukio ya kishakunaku na kilimbukeni.
            Hivi kweli inawezekanaje wakati huu ambapo mchizani Tarampu amesababisha kupanda bei ya wese na kuathiri kila kitu kupata njuluku ya kumwaga kama njugu? Kweli, mmejua kututenda! Kama nyinyi ni wakwasi na wakarimu hivi, kwanini hizo njuluku msizipeleke kunakostahiki? Hamuoni mahospitali na mashule yetu yalivyo kwenye hali mbaya?
            Tuache uzwazwa, roho mbaya na uroho. Utakuta jitu ambalo ni toto la kapuku lilololalia ngozi ya kondoo likijilimbikizia na kufuja mali za Mafyatu bila huruma halafu linajionyesha kwenye matukio uchwara kuwa lina njuluku na upendo! Mingine utaiona imejiwekea misafara mirefu ya ndinga na ving’ora ili kuepa misongamano liliyoisababisha kutokana na upofu, uroho, na ulimbukeni mbali na ufisadi na ukosefu wa uadilifu na ubunifu. Kwani, hatuwaoni? Mifyatu mifisi na mifisadi inaleta miradi ya kipigaji na kufanya maisha yawe magumu. Miundombinu yetu ni mibovu. Misongamano inazidi kutusonga hadi tunakuwa na msongo wa hasira na mawazo halafu inakuja mijizi na mijambazi kutokoga kwa njuluku zetu! Mkome kabla ya Mafyatu hawajakomaa, kufyatuka na kuwakomesha kwa kuwafyatua ili muache kuwafyatua kizwazwa.
            Licha ya kutaka kuanzisha lifestyle audit, nataka Mafyatu wafyatuke na kuuliza kama hawa wanaomwaga njuluku wanalipa kodi vilivyo. Pia, lazima Mafyatu wafyatuke na kujua kodi walipazo zinatumikaje. Je, zinaleta matokeo tegemewa na stahiki? Je, wahusika wanaweza kutuonyesha vyanzo vya ukwasi huu mchafu na wenye utata?
            Kwa vile mie ni profesa wa uchumi, nataka kuhakikisha Fyatuland haigeuzwi kaya ya ubishororo na ulimbukeni. Haiwezekani kaya kapuku inayoishi kwa kubomubomu na kukopa kopa ikawa na mabilionea wa kuibuka ghafla bin vu bila Fyatu mkuu kufyatuka na kuwafyatua. Natitachukua hatua zitakazowafyatua mafyatu kufyatuka na kufyatua wawafyatuao ili haki ifanyike na kweli ijulikane. Fyatuland haiwezi kuwa kaya ya kambale ambapo kila mmoja ana sharubu. Nitazikata hizi sharubu uchwara na zenye kutia shaka.
            Juzi, wakati fisadi mmoja mnene akipaki alionunua kwa kupiga njuluku za Mafyatu ndege alimnyea wakati akishuka. Kumbe na hayawani wanachukia ufujaji wanaofanyiwa Mafyatu wasiofyatuka hadi wanajirhusu kufyatuliwa tena kifala! Mtaani kwake, kila arejeapo, kunguru humzomea sana. Kumbe hata ndege wamefyutaka hadi kuchukia machukizo na makufuru wanayoshuhudia baadhi ya Mafyatu wakifanya kwa kutapanya njuluku!
            Kama haitoshi, kuna Fyatu alijifyatua na kuniita jizi na jambazi nambari moja kwa sababu alisema kuwa nina mamlaka ya kukomesha ujambazi huu wa wazi lakini sifanyi hivyo kutokana kuwa mshirika mkuu. Alihoji nashindwa wapi wakati taknolojia imerahisisha kwa kukamata ushahidi unaoweza kutumika dhidi ya wahalifu hawa wanaojifanya wanazo. Alinipa hadi clips zilizojaa mtandaoni zikiwaonyesha hawa majambazi wakimwaga njuluku. Aliongeza kuwa kuna majambazi yanashinda baa bila kujulikana yafanyapo kazi wala kazi yafanyayo lakini, kwenye sherehe, yanamwaga njuluku kama hayana akili nzuri.
            Nimalizie nikionya. Wote mliojijaza mitandaoni, naja. Akina Masunga kule Ngw’amapalala na Zanzui jiandae. Loh! Kumbe naweweseka usingizini!
Chanzo: Mwananchi Jtano iliyopita.

Kukosana katika ndoa yaweza kuwa fursa

Katika maisha yetu ya ndoa tuligundua kuwa hakuna kitu kinaua ndoa kama ukimya hasa wawili mnapokosana na kukaa kimya au kuepukana bila kuwa tayari kulikabili tatizo. Badala ya kuambiana makosa na ukweli, wengi, hununiana kiasi cha kila mmoja kukaa kimya na kuumia kivyake. Hii, licha ya kusababisha kukua kwa tatizo, husababisha hata magonjwa ya akili hata mwili.
Kuna kisa cha Ajak na Anyuak tulichiosimuliwa. Kisa hiki kinahusisha wanandoa wawili waliokosana na kukwepa kutatua matatizo yao kiasi cha mmoja kuishia kujuta na mwingine akiteketea huku kila mmoja akitamani angesema badala ya kujikalia kimya.
          Kama binadamu na wanandoa wowote, wawili hawa walikosana sehemu katika maisha yao ya ndoa. 
Kwanza, baada ya kuoana, waligundua kuwa wana tabia tofauti kinzani. Mmoja alikuwa muwazi na msemaji ilhali mwingine alikuwa mkimya na mwenye kuficha hisia zake. Hali hizi, licha ya kusababisha msuguano kitabia, ilisababisha kila mmoja kuanza kujifungia kwenye miili yao na kuteseka kimya bila kukabiliana na matatizo waliyosababishiana.
        Pili, baada ya wawili kukosana, walianza kununiana na kutowasiliana wakiamini tatizo lingejiishia. Lakini tatizo halikuisha bali kuzidi kuwa kubwa. Baada ya hapo, walianza kuepukana au tuseme kukwepana. Mwishowe, walitengana ndani ya nyumba yao na kuanza kuishi nyumba moja lakini vyumba tofauti. Katika ndoa, hii ni hatua na adhabu ya mwisho kwa wawili waliozoea kuwa kitu kimoja. Kutengana kimwili pia husababisha kutengana kiakili kiasi cha kila mmoja kumuona mwenzie kama mgeni na hata adui. Hivi kuna haja kufikia hatua hii hatarishi? Tutajibu baadae.
          Tatu, baada ya tatizo kuzidi kukua na mateso ya kisaikolojia kuongezeka, wawili waliamua kuachana wasijue kuwa halikuwa jibu wala suluhu. Wakiwa kwenye mgogoro wao, aliingia mtu wa tatu ambaye hawakujua kuwa alikuwa sehemu ya mgogoro. Punde, mtoto wao mkubwa aligundua tatizo lakini, naye kama wazazi wake, akaamua kukaa kimya asijaribu kuwakabili wazazi wake na kuuliza kunani. Hali hii ilimtafuna sana na kumsononesha sana hadi akajikuta amechanganyikiwa tokana na alivyowapenda wazazi wake.             Kufupisha hadithi ndefu, mtoto huyu alijinyonga nje ya nyumba yao baada ya kushindwa kukubali kuwa wazazi wake walikuwa wameachana na kila mmoja kuchukua njia yake.
Picha ya matukio hayo hapo juu inatuleta kwenye nini kifanyike.
        Kwanza, mkikosana msinuniane kwa muda mrefu. Kwani, si wa kwanza wala mwisho kukosana. Binadamu wote hukosana, hukabiliana, kukaa chini pamoja, au kuomba msaada na kutatua matatizo yao na maisha huendelea.
        Pili, kama kununiana kunawapa fursa na namna ya kutatua tatizo, nuniane kwa muda mfupi ili hasira zipoe halafu haraka sana muanze majadiliano ya kutatua tatizo.Wagombanao ndiyo wapatanao.
        Tatu, kabla ya kuchukua hatua za kununiana, ni vizuri mkajua kuwa ukimya au kukwepa tatizo ni gonjwa baya sana na madhara yake ni makubwa mno.
        Nne, mjue na kukikiri. Ndoa yenu si ya malaika wala mataahira wasiojitambua bali binadamu wenye akili na tabia tofauti. Hivyo, lazima mtakosana tu mtake msitake. Cha mno ni kukubali kuwa kukosana ni sehemu muhimu ya ubinadamu inayowawezesha kusababisha matatizo na kuyatatua tokana na aina ya matatizo na welewa wa wahusika.
        Tano, mjue kuwa kukosana ni fursa ya kubainisha tofauti na udhaifu wenu ambavyo huzaa ubora pale mnapoyakabili na kutayatua matatizo kwa njia zinazostahiki badala ya kukwepana au kununiana au kukaa kimya, kukomoana, au kususiana. Katika maisha, migongano na tofauti ni mambo yasiyoepukika. Hata njiwa, pamoja na kusifika kwa upendo, hukosana na kuyamaliza.
        Sita, mkikosana na kununiana msitegeane au kuviziana juu ya nani achukue hatua kwanza kuanza kutatua mgogoro kama wahusika hapo juu. Kwani, kunyamaziana au kuviziana ni ushahidi kuwa nyinyi ni wajinga ambao wanashindwa kujitambua, kutambuana, na kutambua matatizo yenu ili muyatatue.
        Saba, ni vizuri kujichunguza na kuchunguzana na kupeana mirejesho ili kujua aina na ukubwa wa (ma)tatizo ili muweze kuyatatua pamoja kwa haki na na ridhiko. Hapa, lazima muwe wakweli katika kueleza mnavyoliona au kulijua tatizo ili iwe rahisi kupata ufumbuzi baada ya kujua ubora, udhaifu, welewa, hata kutoelewa tatizo.
        Mwisho, msikimbiane mkidhani mnatatua tatizo wakati mnaliongeza ukubwa wala msifikirie kuumbana upya bali kujikubali kama mlivyo.  Fanyeni kukosana kwenu kuwa fursa ya kujuana na kusaidiana katika maisha ya ndoa.
Chanzo: Mwananchi Jpili iliyopita.