The Chant of Savant

Friday 12 September 2014

Msikatae uraia pacha bali ufisadi pacha

Sikutaka kujiingiza kwenye mjadala ulioanza kugeuka dimbwi la topee baada ya vihiyo kila namna kujiingiza na kujifanya wataalamu wakati hamna kitu. Nimelazimika kuingia ili kuweka baadhi ya mambo sawa.
Walevi kwa mtima nyongo hakuna mfano! Baada ya kuwa nawamegea vipande vya nyuzi toka ughaibuni si waliona nafaidi sana. Kunikata ngebe, japo si wote, wale wenye mtima nyongo na kijicho si wamekamia kutunyima sie tuishio ughaibuni uraia pacha wakati wao wakiendelea na ulaji pacha kupitia ufisadi na ujambazi mwingine. Juzi nusu nijinyotoe roho baada ya kusikia majibu ya lisirikali kuwa halitakubali walevi kuwa na uraia pacha lakini hapo hapo likaridhia ulaji pacha na ufisadi pacha ambapo wageni wakishirikiana na raia wenye ulaji pacha huhomola kaya kana kwamba haina mwenyewe. Unakuta jitu limepewa ukubwa, linahakikisha mkewe mwanae hata mtoto wa rafiki hata shoga yake na nyumba ndogo wanaajiriwa kwa vile wana uhusiano nalo. Jamaa zangu wa Uhamiaji mliohamisha maadili na kuweka madili ya kuajiriana kiushikaji mpo hapa?
Hivi kitendo cha mtu mmoja na watu wake kuchukua ajira zote za walevi au kugeuza madaraka ya umma kuwa ya ukoo ikilinganishwa na uraia pacha ni kipi haramu na hatari kwa usalama wa kaya? Je hawa wanaotwambia kuwa uraia pacha utasababisha tishio kwa usalama wa kaya wakati kaya yetu haina usalama kutokana na maadui wa ndani yaani watu wake, si urongo mtupu? Hivi tangu maadili yazikwe na kuzaliwa madili mnadhani adui wa kaya wako nje ya mipaka ya kaya au wale wale waliozaliwa humu tena wengine wakapewa madaraka makubwa tu?
Wauza bwimbwi, silaha, mafisadi, wala rushwa, wauaji elimu, wakwepa kodi, wazururaji kwa kutumia njuluku za walevi, wanaojiri ndugu zao, wanaogeuza ofisi za walevi kuwa za koo zao na hata wachukuaji wanaoitwa wawekaji wamo kayani humu humu na ni hatari kwa usalama wa kaya kuliko hata ebola.Ukiangalia rongorongo na visingizio vinavyotolewa kutuminyia uraia pacha, unagundua kuwa hakuna sababu za msingi baliwoga na mtima nyongo. Wapo wanaohofia kuwa walevi wakiruhusiwa kuwa na uraia pacha kutakuwapo na utata na hata ukosefu au mkanganyiko wa uzalendo. Urongo mtupu na roho mbaya. Kwani kaya nyingine zilizoruhusu si kaya na hazina dhana ya usalama wa kaya? Kwa baada ya kuondoka Mzee Mchonga (Mwenyezi Mungu amrehemu) ni mzalendo gani amebaki? Mnaujezea shere uzalendo siyo? Go tell it to the birds.
Wapo warongo na wanywanywa na wachovu wanaokokoteza hoja waliothubutu hata kuongelea dhana ya uaminifu usiogawanyika (indivisible loyalty). Go tell it to the birds, guys. How dare you bring such nonsense as if you are the first hunk on earth to be created? Kwanini mnawapotosha walevi tena wengine kujifanya mmesomea mambo ya uhamiaji wakati ni vihiyo tu wa kawaida walioajiriana kiukoo? Je hii yaweza kuwa tatizo kwa kaya au woga na ujinga tu?  Dhana hii ya woga, hata hivyo, haina mashiko na ni mufulisi. Inakuwaje kaya matajiri zenye vifua na kila madude na neema zinaruhusu makapuku toka Afrika na Asia wachukue uraia wao bila kuhofia huo ujinga wa uaminifu usiogawanyika?  Je uaminifu na uzalendo wa mtu unategemea idadi ya uraia au hulka na tabia ya mhusika?
Lazima tukubaliane hata kama ni kilevi na kibangi bangi. Kama mtu ni jiz, mpuuzi, mkwapusi na fisadi hata awe na uraia robo bado ataharibu tu.  Je hawa tunaoshuhudia wakiichuuza kaya yetu kwa wachukuaji wanaowapamba kuwa ni wawekezaji wana uraia pacha au uroho pacha? Wale walioingiza IpTL, EPA, Richmonduli, Kagodamn, Meremetuka na ujambazi mwingine nao wana uraia wa kaya nyingi? Juzi nilicheka nusu nimunamune kwenye sarawili. I will tell you what. Kihiyo mmoja aliyedaiwa eti ni mtaalam wa Uhamiaji eti alidai kuwa walevi wakiwa na uraia pacha watafanya makosa na kutoweka kiasi cha kushindwa kurejeshwa! Wooooii! Huyu kweli anajua maana na kazi za Interpol? Mbona wale walioficha mibilioni ya njuluku Jersey wamo mitaani na mnakula nao mkishindwa kuwafikisha kwa pilato? Nani awaguse wamwage mtama wakubwa zenu waaibike? Je h awa nao wana uraia pacha au ufisadi pacha?
Sijui kama wauza bwimbwi, wanaotorosha mitaji, wala rushwa hata ya ngono, wezi wa mali ya walevi, wazuraraji ughaibuni wanakoficha njuluku zetu, wanaojiriana kwa ukoo, wanaoruhusu mihadarati kupitia viwanja vya ndege, wanaoingiza wageni na wanaosafirisha walevi wana uraia pacha kama siyo upogo pacha.
Hivi walioba njuluku za ESCROW, Tanisco, Rada na ndege ya dingi nao wana uraia pacha siyo? Kimsingi, kinachofanya uraia pacha kuwa tatizo ni woga usio na msingi wowote.
Tuhitimishe kwa kuwashauri hawa wanaoleta rongorongo na visingizio vya kitoto waache na kueleza sababu zenye kuingia vichwani za kutuminyia uraia pacha. Wajue. Mlevi kama mimi siombi wala kubembeleza kwa vile uraia wangu ni wa kuzaliwa. Isitoshe, kama hamtutaki, kwanini kila siku mnatuletea umbea na upuuzi wa kutulaumu kuwa hatuwekezi home. Ili muwe na siasa chafu mtuhujumu na kutuingiza mjini kama mlivyowafanyia walevi siyo? Mmenoa.  Nyie pamoja na kutuminyia mnaendelea kubomoa kaya badala ya kuijenga halafu badala ya kuwajibika eti mnatuminyia uraia pacha. Nadhani tatizo si uraia pacha bali ufisadi, ubabaishaji, wizi, rushwa, upogo na upuuzi mwingine pacha. Mbona jamaa zetu wa kigabacho wanao uraia tena si pacha bali lukuki na wanaendelea kutorosha njuluku mkila na kulala nao? Na wazenj nao mbona wanao pacha na bado mnawakumbatia? Acha niende kuongeza kanywaji na tubangi ili niendelee kuwapasha.
Chanzo: Nipashe Sept., 13, 2014.

2 comments:

Anonymous said...

Hapa kijiweni ulevini tunaongeza mwalimu NN Mhango...Hivi Sasa na hii inayosemakana idara ya Diaspora naona ilikwisha zikwa baada mtiarahamu wa idara ya ahamaji kujenga hoja kwa sababu za kutoka sayari ya Mars.

Diaspora ni hatari sasa bado tuu inamwakilishi hapa sirikalini si inaweza kuleta yale mambo ya hatari ya usalama wa Taifa hii.

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Anon asante sana. Umesikika na nadhani wahusika wataelewa kuwa janja yao ishafichuka.
Karibu tena uache unyayo mwanakwetu.