The Chant of Savant

Tuesday 20 April 2021

JPM Aachwe Apumzike Hawezi Kuja Kujitetea


 Baada ya kufariki ghafla kwa rais Dk John Pombe Magufuli, na makamu wake Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuchukua ukanda kwa mujibu wa katiba, kuna mambo mengi tena ya kipuuzi–––kwa kukopa maneno ya Mheshimiwa Mbunge aliyekerwa–––yanaanza kujitokeza hata kabla mwili wa marehemu haujaoza wala arobaini yake kwisha. Wameanza kujitokeza watu–––tena wengine wanufaika na juhudi za Magufuli–––na kuanza kumsema vibaya na kumuonyesha kama mtu mbaya. Wengine wameanza hata kuponda miradi aliyoikatalia kama vile mradi wa ujenzi wa bandari mpya ya Bagamoyo ambao Marehemu alisema hata kichaa asingeweza kuupitisha. Ni ajabu. Hata kabla mwili wake kuoza, wameshajitokea ‘vichaa’–––tena wengi na wengine waliokua karibu naye–––wanaotetea mradi ‘kichaa’ husika. Je hapa tatizo ni Magufuli au mradi wenyewe? Je kuna namna tunavyoweza kuuboresha mradi husika ili kuondoa mapungufu yake–––kama yanaondosheka–––ili uweze kuleta manufaa kwa pande zote, yaani kwa taifa na mwekezaji? Je serikali iko tayari kuweka wazi mradi mzima kwa umma ili ujionee na kuamua kama unafaa au la? Je hawa wanaoanza kuutetea hata kwa kumsema vibaya marehemu wamehongwa? Mbona hawakuyasema haya wakati Marehemu akiwa madarakani? 
        Kuna  haja ya watanzania kujulishwa figisu figisu zinazodaiwa kuufanya mradi husika kuonekana kutofaa wala kupitishwa na utawala uliopita tokana na sababu ambazo Hayati Magufuli aliweka wazi kuwa mradi hauna maslahi yoyote kitaifa. Siyo hawa hawa waliokuwa wakimsifia kwa kila alilofanya ambao sasa wanamponda na baadhi ya miradi aliyoanzisha kama kufufua ATCL NA kununua ndege kwa taslimu? Je hii inajenga picha gani? Yaani tumekuwa wa hovyo hivi? Tumekuwa wasahaulifu kirahisi hivi tena ndani ya muda mfupi? Nadhani, rais Samia anapaswa kuwatahadhari na kuwaogopa hawa kama ukoma. Kwani kuwasema watu vibaya ni sehemu ya tabia zao wasizoweza kuziacha. Leo wamemgeuka na kumdhulumu Magufuli ndani ya muda mfupi. Kesho, watamgeukia yoyote akiwamo rais Samia wanayemsifia wakati hajamaliza hata siku mia lau awape picha ya anakoelekea. Maana hii ni tabia yao. Huu ndiyo tunauita umalaya wa kisiasa.
        Maneno makali na ya uchungu ya Mheshimiwa Livingstone Lusinde (Mtera-CCM) hayawezi kupita bila kudurusiwa ili kuambua lao somo au masomo. Lusinde alikaririwa na vyombo vya habari akisema “hivi leo ni mbunge gani hakutetewa na Magufuli,  tupo humu ndani kwa sababu ya Magufuli na Samia. Walipita kila sehemu  kuwaombea kura. Kuna watu hapa walikuwa hawachaguliki lakini Magufuli na Samia wakapita wakasema tupeni huyu tutafanya naye kazi tutamrekebisha,  kwa sababu yao wakachaguliwa.” Haya maneno ni mazito na yana ukweli. Pia, yanaonyesha si uchungu wa mbunge bali hata ithibati yake hasa wakati huu ambapo kila mtu anajitahidi kujipendekeza kwa rais hata kwa kumhujumu au kumvunjia mtangulizi wake aliyemfanya kuwa rais. Hili hawalioni. Lusinde anaendelea kusema “leo Magufuli asemwe vibaya na sisi tupo hata 40 haijafika, hili jambo halikubaliki, hawa watu washike adabu na adabu ziwashike. Hatutaki warudie tena mambo ya kipuuzi kama hayo.”
        Mbali na Lusinde, mwingine aliyeguswa na uzandiki na unafiki unaoendelea dhidi ya Hayati Magufuli ni mheshimwa Lembris Noah (Arumeru Magharibi-CCM) aliyekaririwa na vyombo vya habari akisema “jamani akina Yuda wamejitokeza kumsaliti Dk Magufuli na Serikali yake. Inasikitisha mzee wa watu ametangulia mbele za haki hawezi kujitetea nyie mlioko ndani na nje mnataka kumdhalilisha. Haiwezekani kabla ya kumdhalilisha na Serikali yake ya awamu tano nina uhakika Mungu atawashughulikia usiku na mchana.” Kama alivyowaita mwenzao, kweli wanaomsema vibaya au kumgeuka Hayati Magufuli ni wasaliti ambao mheshimiwa anawalinganisha na Yuda Iskariot aliyemchuuza Yesu–––anaye alizoea kumbusu kama ishara ya upendo–––kumbe unafiki mtupu kwa vipande thelathini vya fedha.
Somo kubwa na muhimu nililojifunza kwenye kadhia hii ya kumhujumu Hayati Magufuli ni kwamba baadhi yetu ni wepesi wa kusahau. Pia ni kwamba wengi wa watu wetu wanafikiri kwa matumbo badala ya vichwa–––sitaki niseme–––ashakum––––manonihino. Kwani, hawa wanaomponda Magufuli watakumbuka 2025. Watakaposhindwa ulaji watamkumbuka na kumlilia sana. Maana, kama alivyosema Lusinde,wamejaa wengi bungeni ambao wasingechaguliwa kama si juhudi na ushawishi vya Magufuli wanayemgeuka wakijua hawezi kuamka na kuwakaripia hata kuwashangaa walivyo wasahaulifu na wa hovyo.
        Leo tunawaona wanaotumia ndege alizonunua Magufuli wakizikandia na kudai ni ushamba kununua ndege kwa fedha taslimu kana kwamba hawajui adha na utumwa wa madeni. Kimsingi, ni kwamba ni wachache wanaoweza kuona mbali na kile alichokiona Hayati Magufuli. Pamoja na kutojua kwao, bado wanajifanya wajuzi na wakosoaji wazuri wasijue watakuja kula maneno yao pale wakati utakapowadia. Wanamdhihaki mtu aliyependwa na wanyonge wasijue wanyonge hawa hawa wanasikia na kuona kila kitu.  Unachoweza kuwaambia wanaomkosoa na kumsimanga Hayati Magufuli ni kwamba kuna siku watakula maneno yao kiama chao kikiwadia miaka michache ijayo tutakapokwenda kwenye uchaguzi ujao. Kweli  wasaka tonge ni viumbe wa ajabu. Yupo aliyefikia kutaka kudanganya dunia kuwa hata mradi wa Bwawa la Nyerere si muhimu kwa vile umeme wake eti ni aghali kuliko wa gesi. Sijui watu wengine–––tena wanaojiita wasomi waliobobea–––wanafikiriaje kiasi cha kuzidiwa na hata wale wanaowaita darasa la saba wenye akili na busara kuliko wao.
Tumalizie kwa kuwaomba watanzania kuwa wakweli kwao binafsi na hata kwa umma wakijua wazi kuwa hatarudi kuja kujitetea. 
        Hata hivyo, rekodi ya utendaji wake itamtea si leo wala kesho bali hata kwa vizazi vijavyo. Na si kwa Tanzania tu bali ulimwengu mzima. Magufuli hakuomba apendwe. Anapendwa tokana na utendaji wake. Tuache kigeugeu, unafiki, ubabaishaji na uzabazabina. Tuwaheshimu marehemu na tujenge taifa letu kwa kuwa wakweli badala ya wababaishaji na wasaka tonge kama wanaomgeuka Magufuli wanavyoonyesha. Acha wote waseme ila siyo wana CCM hasa wabunge ambao wengi wamenufaika na utendaji na ushawishi wa Hayati Magufuli (Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Ni ushauri wa bure.
Chanzo: Raia Mwema kesho.

No comments: