The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Wednesday, 14 January 2026

Tulaani na kundunisha udini wa kudunisha dini zetu

Fyatuland ina visa, visasi, vitimbi, vitimbwiliko usipime. Japo, tunaonyesha kuanyamazia na kuwashabikia, kuna mafyatu wanaofyatuka hovyo hovyo wakicheleta na kuchezea hatari wasijue zahama wanayotengeza. Wapo mafyatu uchwara waliojipa, sijui kupewa vibali vya ‘kuvuruga’ amani wakidai na kujifanya wanaitetea. Sijui nani huyu mchizani anayewatuma hawa wahuni, apate nini, na iwe nini? Nijuavyo, dini ni suala la kibinafsi. Inapoanza kugeuzwa suala la umma na kuanza kuuma umma, ujue mwisho na matokeo yake ni zahama kama siyo kiama tena vya kujitakia. Yote ni matokeo na kujipendekeza, kujikomba, njaa, na uzwazwa.

            Fyatuland haina dini ila madini kama urani(um) ya bwana nonihino bingwa wa kufyatuka fyatuka na kupayuka payuka  bila kufikiri. Sijui viumbe habithi kama hawa huwa wanajisikiliza au kusikiliza wale wanaowaonya. Linatoka fyatu, sijui baada ya kula ndumu au ulabu, linafyatuka na kutishia kukata mafyatu vichwa. Kwani, lenyewe halina kichwa au linacho ila cha panzi? Ajabu, hata mafyatu wenye heshima zao wanakubaliana na uduni na uhuni huu uliojifunika udini usio na lolote wala chochote bali kujitoa ufahamu na kuishiwa akili na busara. Ni aibu fyatu mzima kujifanya hamnazo na kufanya mambo ya kitoto halafu akataka aitwe mtu mzima! Mtu mzima au mtu mzima hovyo?

            Kwa taarifa yenu, dini, mikakati uchwara, njaa, na kujikomba kwenu havitufai wala hatuvihitaji. Kama wataka siasa, vua gwanda la udini duni, na uvae la siasa utie timu uwanjani tukuone, kukusikia, na kukusikiliza kabla hatujakulaani na kukudharau. Inakuwaje mafyatu hawa laanifu wanajifanya kutetea mafyatu wazima tena wenye power kana kwamba ni watoi wachanga? Hovyo kabisa. Mjue. Tunawajua na hata uhovyo na uduni wenu.

            Msitake kutifua historia chafu ya dini hasa zilivyosaidia kueneza ukoloni, na sasa, uzwazwa wa kuamini miujiza ya uongo vinavyowasumbua mafyatu wetu. Juzi, kaya jirani, ilifuta hizi dini duni kibao za kujipachika, kuchonganisha, na kuwaibia mafyatu. Mijitu yenyewe iliogopa umande. Ajabu, inajitia kujuajua wakati haijui kitu bali kuganga njaa na utapeli vya wazi. Je, nani aliwaroga mafyatu hadi baadhi yao wanafyatuka na kufyatua vitu vya hovyo na hatarishi bila kuwashikisha adabu?

            Japo si wote, tuna matapeli wengi wa kiduni aka gwajimmy et mashehetani sasa kuliko wakati wowote katika historia ya Fyatuland. Fyatu, tena tapeli na vivu la wazi, linaamka asubuhi na kujivisha vyeo vikubwa na vitakatifu. Ukiuliza limesomea lini, nini, na wapi, linaanza stori za Fyatu na Fyatuzi. Ho, nilikutana na Jizazi, mara hivi mara vile. Kumbaff kabisa. Muiache Fyatuland yetu. Ukisikia kuisha na kuishiwa ndiyo huku. Dingi zima linafyatuka vitu ambavyo hata machizi na wapiga ndumu wala walevi hawawezi kwa kuchelea aibu na kutiwa adabu.

            Hakuna kinanisononesha na kushangaza kama tunavyowavumilia waharibifu hawa waliojaa uduni waliojificha kwenye udini na uhuni uchwara. Tuwafichue, tuwalaani, kuwaonya, na kuwaadhibu kabla hatujaharibikiwa. Ukichanganya matapeli haya na siasa za majitaka, ndo usiseme. Leo, wanaweza kujifanya wanakupenda ilhali wakuponda ukahadaika usijue hawana tofauti na vyangudoa wa kawaida. Lao ni tonge hata wapewe na fisi au fisadi.

            Wapo wanaojifanya wanaipenda kaya wakati wanaichukia kwa machukizo wanayotenda. Wanapanua vinywa vyao vichafu na kufyatuka uchafu hadi wote tunaonekana wachafu na mataahira. Fyatu Mfyatuzi si mwoga wala taahira. Napanga kuomba kibali cha kuwashughulikia hawa matapeli hadi wakome na kukomaa kabla hawajatukomoa. Hawa ni ndumilakuwili au sigara kali. Inakuwaje fyatu zima linalojitia zimo kutetea amani tena ya imani na kusaza haki? Je, waweza kuwa na amani bila haki? Heri kuwa na haki kwanza. Kwani, italeta amani. Amani hata ifagiliwe na kulindwa vipi, haiwezi kushamiri miongoni mwa ubatili na ukosefu wa haki. Amani gani wakati mafyatu wanatekwa, kupotezwa, hata kunyotolewa roho? Amani gani wakati baadhi ya mafyatu wanapiga njuluku zetu, kuhomola, kuhondomola ilhali wakitubagaza na kutubananga?

            Sambamba na wanasiasa wenye visa na visasi wafyatukao bila mdomo na ubongo kuwasilishana ni kero na tishio kwa kaya yetu. Wapo walioshiba kiasi cha kutapika na kunonihino mle mle wanamolia utadhani mainzi mafu! Linakurupuka fyatu tena lenye maulaji makubwa na kuwasimanga mafyatu wachovu. Linaunda hila na uongo na kuwageuza mataahira wakati wana akili timamu. Kwani, hatuwajui wapigaji wetu? Kwani, hatujui hata rongorongo zao? Mbona kila kitu kiko wazi?

            Njaa haina mwisho hata uivalie kibwaya vipi. Njaa ni kansa inayosumbua Fyatuland ambapo wachache wanashiba ilhalil kaumu ikisota njaa. Halafu, linatokea zwazwa linasema eti tu matajiri kiasi cha matajiri na washiri wetu kutuonea wivu! Kwa visa, visasi, na uduni huu! Tulaani vikali na kudunisha udini duni unaotaka kudunisha dini na kaya yetu. Heri ya mwaka mpya.  Hapa natia nukta. Waktabahu, ila al-liqa.

Chanzo: Mwananachi leo J'tano.

           

No comments: