The Chant of Savant

Friday 23 December 2011

vituko vya viongozi wetu na maafa yake! mafuriko siasa mafuriko siasa!

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na Bi. Monica Luis, Mkazi wa Jangwani aliyeathirika na mafuriko ya Mvua kubwa iliyonyesha jijini kuanzia majuzi, wakati makamu alipotembelea katika Kambi ya Shule ya Sekondari Azania jijini Dar es Salaam leo Desemba 23, kwa ajili ya kuwapa pole waathirika wa mafuriko hayo. Picha toka Mjengwa Blog.

Watawala wetu wakishapata hugeuka miungu kiasi cha kuogopa hata kuwakaribia wapiga kura yaani waliowapa huo utukufu. Huyo juu eti anaongea na mhanga wa mafuriko! Hivi kwa umbali huo mrefu kweli wawili hawa wanaweza kuongea lugha moja tena wakaelewana? Huu ni udhalilishaji tosha ambao wananchi wanapaswa kuuona na kuufanyia kazi kwa kukinyima kura Chama Cha Mapinduzi.

Habari zilizolipotiwa ni kwamba wakazi wa mabondeni wameapa kutohama makazi yao kama alivyoagiza rais Jakaya Kikwete. Kwani wao kilichotokea wanaona ni kama ajali tu. Hivyo wataendelea kukaa mabondeni. Je serikali itaufyata kwa kuogopa kupoteza wapiga kura? Je serikali, kama ilivyojiingiza kwenye matatizo, itaendelea kuwaandalia makazi mapya kana kwamba makazi wanayoishi ni halali? Je hawa wakazi wa mabondeni wamejua udhaifu wa serikali kujiingiza kwenye tatizo ambalo si lake? Je wakazi wa mabondeni wanajua jinsi serikali isiyoaminika? Je serikali kuahidi kuwatafutia maeneo mapya ni halali zaidi ya kuunga mkono vitendo vya kuvunja sheria? Kesho tutasikia wamachinga wanaofanya biashara kwenye barabara na maeneo ya wazi nao wakitaka wapewe maduka!

Kimsingi tatizo la mafuriko ni matokeo ya utawala wa kubabaisha na kujuana na utokanao na rushwa, kuchafuana na wizi wa kura.

No comments: