The Chant of Savant

Wednesday 31 January 2018

Maadili, Magufuli aungwe mkono

Image result for photos of gwajima and magufuliImage result for photos of magufuli and diamond
            Hivi karibuni, kwa mara nyingine, rais John Pombe Magufuli alifanya kilichokuwa kimewashinda wengi tangu kung’atuka baba wa taifa Mwl Julius Nyerere. Magufuli aliamua kuwaondolea uvivu wachafuzi wa maadili ya kitanzania ambao, mara nyingi, ni matokeo ya utawala mbovu, ujinga, ulimbukeni na tamaa miongoni mwa watanzania. Tunachukua fursa hii kumpongeza kipekee kwa kuona zahma hii ambayo ilikuwa ikitishia uhai wa taifa kimaadili.
            Kama taifa, bila maadili, hatuna tofauti na wanyama. Taifa lisilo na maadili, halina utambulisho wake na linaelekea pabaya. Hivyo basi, rais Magufuli aungwe mkono na watanzania wote kuhakikisha tunapambana na yeyote anayetaka kuchezea mila na utamaduni wetu kwa gharama yoyote. Katika kufanya hivi, kuna mambo kadhaa ya kuzingatia.
            Mosi, tusingoje serikali wala kulinda mila na tamaduni zetu kwa hofu ya serikali wala kulamika. Maana, kwa wenzetu, mila na tamaduni ni uchumi. Mfano mdogo ni toka taifa la Marekani ambalo linatangaza na kuuza utamaduni wake dunia nzima kama njia mojawapo ya kuzitawala nchi nyingine. Chukulia mavazi, mitindo, vinywaji na vyakula vya kimarekani vinavyouzwa ulimwenguni kweli kupitia maabala yake ya Holywood na biashara nyingine. Mwl Nyerere aliwahi kusema “utamaduni kuwa ni chombo cha maendeleo.”
            Pili, kama jamii, tuonyesha maadili yetu kama njia ya kututambulisha na kututofautisha na watu wengine. Hivyo, tusichuuze utu wetu kwa kisingizio cha kutengeneza fedha. Hakuna ubishi kuwa kwa sasa filamu na miziki mingi vinavyozalishwa nchini ni vichafu tokana na kukinzana na maadili ya kitanzania. Tumekuwa watumwa wa mila chafu toka mataifa mengine yasiyo na mwelekeo hasa katika sanaa ya muziki ambapo ima tunaigiza Marekani au DRC bila sababu zozote za msingi.
            Tatu, kwa vile serikali yetu imejitofautisha na serikali za hovyo zilizopita zilizoruhusu uoza kimaadili kutokana na kuongozwa na watu ambao hawakuwa na maadili kwa kisingizio cha usasa na kusaka fedha chafu. Tunapaswa tujionyeshe kama watanzania wenye maadili ikiwa ni sehemu ya urathi wetu kama jamii ya watu wenye akili. Mambo ya kucheza miziki au kupiga picha za uchi ni ya kishamba na kilimbukeni. Milegezo, kutoga masikio na upuuzi mwingine lazima vipigwe vita kulhali. Maana vinawekwa wazi wazi kana kwamba ni jambo la maana.
            Nne, tunapopambana na kadhia ua uchafuzi wa maadili tusiangalie sanaa tu. Twende mbali zaidi. Kwa mfano, katika hatua hii, lazima tushughulikie vyombo vya habari vinavyoeneza uchafu kama vile magazeti ya udaku.  Kwani, nayo hayana tofauti na watembea na waonyesha uchi wao ukiachia malimbukeni wa mila chafu za kigeni. Magazeti ya udaku na radio na runinga za kidaku ndivyo vyombo vikuu vya kueneza uchafu huu kwa kisingizio cha kutengeneza fedha. Ni bahati nzuri kuwa Magufuli ameelewa na kufanya mambo ambayo wengi wa waliomtangulia ukiondoa marehemu baba wa taifa Mwl Julius Nyerere yaliwashinda tokana na kutoona mbali ukiachia mbali kuwa bize kwa mambo ya kipuuzi au kuyashiriki. Ukiangalia mema mengi aliyotenda Magufuli unashangaa kugundua kuwa amepitia kwenye mfumo mchafu kama huu. Hakika huu ni ushahidi kuwa Tanzania bado ina watu wema na wenye kuthamini taifa lao.         
            Baada ya kupambana na vyombo vinavyoeneza uchafu, twende mbali na kushughulikia watu has wale wanaoeneza uongo na uchafu kama vile mahubiri ya uongo yanayowaaminisha watu kuwa wanatenda miujiza au kutibu magonjwa yasiyotibika, kuleta bahati na upuuzi mwingine ambao umesababisha taifa letu lichafuke tokana na matokeo ya mahubiri na utapeli huu kama vile mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi na vikongwe kiasi cha kuliacha taifa letu halina sifa kimataifa.

            Kwa uzoefu wangu ni kwamba katika Jumuia ya Afrika Mashariki, ni Tanzania pekee yenye vyombo vya habari vya kidaku na vyenye kuvunja maadili ukiachia mbali utitiri wa waganga wa kienyeji ambao wengi ni matapeli wa kawaida. Kama ambavyo rais Magufuli amekuwa akishangaa na kujiuliza nani alituroga hadi tukageuzwa shamba la bibi. Kwani, tuna watu tena matapeli wa kawaida ambao wametokea kuwa na utajiri wa kutisha tokana na kuwaibia watu wetu ima kupitia dini za kitapeli, uuzaji na usambazaji wa habari chafu ukiachia mbali waganga wa kienyeji. Huwa napendekeza taifa letu kuanzisha sera ya zamani ya kuuliza watu binafsi wanaoibuka na utajiri usio kuwa na maelezo ili kuondoa motisha kwa wengine wenye kutaka kuuibia umma kitapeli. Nchi ilikuwa imefikia pabaya hadi machizi fulani kuanzisha madhehebu ya dini yanayohimiza watu kutenda maovu kana kwamba hakuna serikali. Kwa vile rais Magufuli ameamua kujitofautisha na malimbukeni waliopewa madaraka wakaachi nchi itopee kwenye ufunjifu wa maadili, tumuunge mkono kama wananchi na jamii ili tuondoe kadhia hii ya uchafuzi wa maadili kwa faida na heshima yetu kama jamii ya watu. Maana, ilifikia mahali watu wakaanza kuogopa hata kutazama runinga kwa hofu ya kuonyeshwa uchafu wakiwa na watoto na jamaa zao. Hongera kwa mara nyingine rais Magufuli kwa kuanza kurejesha na kutetea maadili ya kitanzania.
Chanzo: Tanzania Daima, J'tano, Jan., 31, 2018.

No comments: