Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Wednesday 31 July 2024

Sir God Ameniamuru Nilete Dini ya Ukombozi

Baada ya kugundua kuwa mafyatu wake wengi wameharibikiwa na kuchanganyikiwa kiasi cha kufyatuliwa na kudhalilishwa na kila tapeli, Sir God ameniamru nilete dini ya Ukombozi. Hii ni baada ya kuona kuwa matapeli wengi wanawafyatua mafyatu waliogoma kuelimika wakawafyatua wanaowafyatua. 
        Nimeona mafyatu wangu wakiuziwa kila upuuzi kuanzia maji tena machafu, mafuta tena ya kishirikina, notebooks, kalamu, leso tena chafu, wengine wanavuliwa hata nonihino na kushikwashikwa vyote ukiwa ni utapeli kuwaibia wajinga ufanyawao na wajinga wenzao waavivu wa kufikiri na kubuni mambo ya manaa. Ni ujinga pande zote matapeli na wanaotapeliwa. Wengi hata hiyo elimu hawana. Wala hawana ubunifu wa kubuni vitu visivyo vya kikumbaff kama hivi. Wote wanahitaji ukombozi utakaoletwa na dini ya Ukombozi. Mafyatu wanadhalilika hakuna mfano. Wanahitaji Mkombozi ambaye ni mimi na ukombozi ambao ni dini ya Ukombozi. Wale uliotegemea wawazindue, wanawafyatua au kushirikiana au kuwafumbia macho wanaowafyatua.Wahenga kweli walisema wajinga ndiyo waliowao.
            Kwa vile imemfurahisha Sr God nipambane na jinai hii kwa kunishushia dini yake, msishangae mkisikia naongea lugha msizoelewa. Hata hivyo, hamtashangaa. Kama matapeli toka kaya nyingine wanakuja na kuwafyatua, kwanini mnishangae mie ninayewashangaa? Hamjawasikia wanaokuja na kujianzishia madhehebu ya kinyonyaji na kitapeli huku wakiuwauzia ujinga na woga? Naona yule anatikisa kichwa akishangaa sirkal iko wapi? Kwani wawili hawa wana tofauti? Kazi ya sirkal si kuwafumbua macho mafyatu. Kazi yake ni kuleta wachukuaji, sorry, wawekezaji waje wafaidi vinono vya kaya yetu. Tena nimekumbuka. Dini ya Ukombozi itawasaidia hata wanasiasa wanaotaka kushinda uchaguzi. Nawashauri waje niwaombee ilmradi walete mbuzi na ng’ombe na kutembelea Chegama.
        Kuanzia sasa nitaitwa Daktari, Genero, Papa, Mtakatifu,  Mtukufu, Mwenye maono, Mponyaji, Muota ndoto, Mtabiri Dk, Alhaji, Mhashamu, His Excellency, His Eminence, HH etc. Fyatu Mfyatuzi bin Mfyatuaji bin Mfyatukage wa Mfyatulizi mwana wa Mfyatukizi mjukuu wa Fyatuafyatua mwana wa Mfyatuizi kijukuu cha Mpayukaji Msemahovyo Msemakweli.
        Kijiji changu cha Chegama, kuanzia sasa, ni sehemu takatifu kuliko zote duniani. Hapa ndipo Mafyatu tulipotua tulipotoka mawinguni na kuanza kuijaza dunia. Mafyatu wote duniani walitokea kijiji hiki ambacho wao huita Bustani ya Edeni. Tokana na utukufu wake, Mafyatu wote duniani wanaamriwa kuja kutembelea sehemu hii takatifu mara tano katika maisha yao bila kujali ni makapuku au wakwasi.
        Nyumba nilimozaliwa, kuanzia sasa, ni hekalu la Sir God pia sehemu ambapo mafyatu watakaokuja kuonyesha utii wao watazunguka na kubuni lolote la maana watakalo na kulipata hapo hapo.
        Kwa vile Sir God amenipa madaraka ambayo hajawahi kutoa kwa yeyote isipokuwa mie,  kuanzia sasa, picha zangu zitasambazwa dunia nzima na mafyatu watakuwa wakiziweka kwenye sehemu maalumu za ibada. Kila picha itauzwa kwa dolari za Kiamerikani elfu tano. Itabidi kila kijiji kuchangishana na kuhakikisha wanakuwa na picha yangu kama mwakilishi wa Sir God aliyeniamuru kuleta dini ya ukombozi.
        Kuanzia sasa, kila fyatu atapaswa kutoa kafara ya mbuzi au ng’ombe jike kulingana na maelekezo yangu anapotembelea sehemu takatifu ya Chegama. Hawa wanyama watatunzwa hadi siku ya mwisho watakapochinjwa kwenye karamu ya mafyatu wote duniani. Hivyo,  nitaiamrisha sirkal kupanua eneo la kijiji ili kuweza kutunza zawadi hizi za Sir God mwenyewe.
        Kuanzia sasa sitatembea kwa miguu. Sir God ameniamuru niiambie sirkal kunijengea hekalu kila kaya, kuninunulia mashangingi idadi nitakayo, mashua na ndege ili kuniondolea msongo wa mawazo nna kuweza kuizunguka dunia haraka na kwa raha nikitangaza ukombozi wa mafyatu wote duniani. Nitatumia mahekalu yangu matakatifu kwa ajili ya kuwakirimu watakaokuja kuonyesha heshima yao Chegama. Mashangingi na ndege vitanisaidia kutembelea duniani nikionyesha utajiri wa Sir God na upendo wake kwa mafyatu wanaoibiwa na matapeli wanaomtumia.
Kuonyesha kuwa mie si mganganjaa, msakatonge, tapeli au jinga kama wale, kuanzia leo nitakuwa nafanya muujiza mkuu ambao ni kutoa mhadhara kuwa hakuna miujiza duniani bali ukumbaff na ujinga. Kupitia ufyatukaji, nitakuwa nikifungua vichwa vilivyogandishwa na woga wa uvivu wa kuchapa kazi. Nitawaelimisha mafyatu namna ya kufyatua wezi wanaowaibia ili waweze kutajirika badala ya kutegemea kuombewa.
        Nitafanya miujiza ya kuwafyatua mafyatu waache ukumbaff. Mfano, wote wanaotegemea waganga wa kienyeji au wachunaji waitwao wachungaji walewe kuwa ni wakumbaff. Kwani hawapo? Ni wangapi wanawajaza mafweza wanganganjaa na wachunaji eti wapate utajiri bila kufikiri wala kuchapa kazi? Ni akina mama wangapi walioishiwa kimaadili wanakimbizana na kudhalilishwa kwa waganga wa kienyeji eti wakitafuta dawa ya mapenzi wakati hakuna? 
        Siku hizi wameanza kuua zeruzeru kutafuta bahati wakati ni ukumbaff. Wangapi wanaamini kwenye ukumbaff wa kutoana kafara ili watajirike? Wangapi wakiwaona mataahira kwenye jamii fulani tajiri zinazosifika kuoana ndugu kwa ndugu na kuzaa mataahira wakadhani eti hao mataahira ndicho chanzo cha utajiri wasijue chanzo ni kuoana ndugu kwa ndugu? Kwani hayapo haya?  Hili ndilo lengo la kuanzisha dini ya Ukombozi. Semeni hamna.Hivi kumeishakucha?
Chanzo: Mwananchi leo.

No comments: