The Chant of Savant

Saturday 16 April 2011

Mubarak mkewe, watoto na wakamwana watiwa ndani na chama chavunjwa

Familia ya Mubarak enzi zao

Makao makuu ya DNP yakifuka moshi baada ya kuchomwa moto na waandamanaji wenye hasira
Gamal na Alaa Mubarak zama zao

Mabalaa yamezidi kuiandama familia ya imla wa zamani wa Misri, Hosni Mubarak. Serikali nchini humo imeamuru Mubarak, mkewe, watoto na wake zao kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma za ufisadi. Hii ni kutokana na tabia iliyojengeka barani Afrika ambapo mtu mmoja akichaguliwa kuwa rais familia nzima nayo huwa marais.

Tumeyaona haya nchini Tunisia ambapo mke wa rais na kaka zake walihujumu nchi kwa kiwango kikubwa. Nchi za jirani za Kenya na Uganda hali inatisha. Imla za zamani wa Kenya Daniel arap Moi aliwaruhusu watoto wake kulifilisi taifa hilo. Nchini Uganda utawala wote ume mikononi mwa imla wa nchi hiyo Yoweri Museveni.

Nchini Libya tumeshuhudia watoto wa imla wa nchi hiyo aliyemo matatani Muamar Gadaffi wakiwa wasemaji na makomanda wa majeshi ya nchi bila stahiki yoyote kikatiba. Nchini Afrika Kusini Duduzane Mtoto wa rais Jacob Zuma anasifika kujipatia mabilioni tokana na baba yake kuwa rais.
Tukirejea kwa Mubarak ni kwamba watoto wake wawili wa pekee Gamal na Alaa wametupwa kwenye gereza kuu la Tora mjini Cairo.

Familia ya Mubarak inaaminika kuwa na mali za mabilioni ya dola zilizopatikana kutokana na kuliibia taifa. Mubarak na familia yake wanasadikiwa kuwa na utajiri mkubwa kuliko hata Bill Gates tajiri wa pili duniani.
Hiyo ndiyo sura ya watawala wa kiafrika ambao kama makupe, wanajitajirisha na koo zao kwa mgongo wa watawaliwa maskini.

Kukamatwa kwa Mubarak kulipaswa kuwa somo kwa wezi wetu madarakani. Lakini je wanasikia? Watasikiaje wakati hawana masikio na ubongo ambavyo vyote vimemezwa na matumbo yao?

Masahibu ya Mubarak, familia yake na waramba viatu wake hayakuishia kwenye kutiwa korokoroni. Chama Chake cha National Democratic Party nacho kimefutwa. Hakikupewa hata nafasi ya kujivua gamba. Kwani mahakama kuu iliamua kuvunjwe ili kuondoa historia chafu ya udhalilishaji wa taifa.

Baada ya kuvunjwa kwa chama cha NDP mahakama imeamuru mali zote za umma zilizokuwa mikononi mwa chama kama ilivyo mazoea ya vyama tawala, zimeamriwa kurejeshwa serikalini mara moja.
Chama kilichokuwa kinatesa na kunyanyasa, licha ya kunyanyaswa na kuteswa na maandamano yaliyomtoa Mubarak madarakani, hatimaye, kimeuawa rasmi. Je vyama vikongwe na tawala barani vinajifunza somo gani? Je kujivua magamba ya uongo na ukweli inatosha kuvibakiza madarakani? Kwa nchi zenye kutawaliwa na vibaka na mibaka yenye vyeo chini ya magenge yaitwayo vyama tawala zinapaswa kutia maanani na kuamini kila kitu kinawezekana umma ukiamua.

No comments: