The Chant of Savant

Tuesday 29 November 2022

CCM Wanapochomoleana Fyuzi, Walevi Tuchomoe Nini?


Zamani nilidhani ulabu huwalabua walevi nisijue na wanasiasia kadhalika. Juzi nilicheka baada ya kushangaa mbali na kuhuzunika. Sijui ni njaa au ulabu, wala mie sijui. Nilipomsikia Katibu mkuu wa zama wa Numero Uno na Katibu Mkuu Kiongozaji Mstaafu Balozi wa ghafla bin vu Bushir Aliye Kakufurwa, sikushangaaaaaa saana tu mbali na kuchanganyikiwa hata kuudhika. Bushiri––––siyo yule bin Salum–––habithi aliyewatesa na kuwauza babu zetu utumwani, alikaririwa hivi karibuni akiramba matapishiye. Aliporusha mabomu yake, mlevi mmoja alisikika akisema “Msomi gani huyu asosoma alama za nyakati?!!!” Kama mpiga ulabu, nilimjibu “usomi wa mlevi hauondoi ulevi wake. Hivyo, nilitoa hitimisho kuwa huyu Bushiri na yule wa utumwa wote sawa tofauti ni njeo na watokako mbali na. namna wafanyayo wayafanyayo. Yote katika yote, wote ni wauzaji wa roho za walevi. Hivi inakuwaje bata ancheke kuku kuharisha? Inakuwaje ngamia amcheke nungu ng’ombe? Inakuwaje Bushiri awazodoe wenzake huku akijifanya anawapa ushauri walevi waliwaji wanaosifia ulaji wanaopewa na Maza wakati yeye alikuwa akisifia kila alichofanya Mwendazake?  Muda wote wanaliwa wewe ulikuwa wapi kama kweli unawapendaga? Kipindi hiki umenoa na itakula kwako kama siyo kuula wa chuya. Haingizwi mkenge mlevi hapa.
Baada ya kupiga ulabu wa kisiasa na kuutumeshwa na Maza baada ya yule aliyemtengeza kuitwa na Mola wake, Bushiri aliamua kuja na staili yake ya kulipiza kisasi. Alilamua kujitia uchizi kiasi cha kufyatua fyuzi kama wasemavyo wenzake. Akisikia neno kuupiga anaudhika hadi kuanza kupinga kuwa walevi wasiseme Maza anaupiga mwingi. Japo usemayo ni kweli, wewe si mkweli. Si mkweli kwa sababu unajifanya mwenzetu wakati u mwenzao. Unajifanya kutetea walevi kwa uongo huku ukiuficha na kuuepa ukweli. Mbali na kutuambia walevi urongo, unatuhadaa eti unaona haki wakati wewe ndiye kuhani wa kuifuja na kuikanyaga. Unasema watawala ni wanyonyaji wakati ukiwa kwenye utawala na utu wala yaani Uheshimiwa Chawa–––kwa mujibu wa Kibajaji na Msukuma. Siku zote chawa humnyonya binadamu. Okay. Kama maadui zako ni chawa, wewe ni nani? Nani alikupigia kura ya uheshimiwa wako kama siyo Maza kukuepusha aibu na kukupa uheshimiwa ambao sasa hivi wenzako wanauita uchawa?
Sitaki nikuite mnafiki. Wenzako watafanya kazi hiyo barabara  japo ni sifa mbaya sana hata kama unayo. Je imekuwaje ukasahau ulivyokuwa ukisifia kila alichokuwa akifanya mwendazake hata kama hakikuwa sahihi? Ni kwa sababu ya kulinda ulaji wako binafsi au unafiki? Ulipokuwa kwenye ulaji, madhambi ya kusifu na kushukuru uliyatenda vyema. Inakuwaje sasa yawe nongwa yakifanywa na wengine wanaolinda ulaji wao? Ama kweli nonihino haoni nonihino lake. Au teseme ni yale ya mwalimu wangu usinibaini, wajinga ndiyo waliwao. Wajinga wanaweza kuliwa wakiona na kunyamaza lakini si walevi. Walevi lazima watapiga kelele kama unavyowasikia wakimuwakia mlevi mwenzao. Tofauti ya walevi wa ulabu na ule wa maulaji ni kwamba wale wa maulaji wanasahau haraka. Huwa hawana kumbukumbu. Wanachokumbuka ni ndoto na ulaji wao.
Hivi huyu Bushiri huwa ana washauri? Je huwa anapitia taarifa zake za huko nyuma alipokuwa akiteuliwa kila uchao hata bila ya sifa na uzoefu? Namkumbuka akiwa pale Chuo Kikubwa akitema cheche. Hata hivyo, aliporambishwa ulaji si akasahau kila kitu na kupwakia matapishi yake! Hapa ndipo niliona usomi uchwara wa wale waliotumia muda mwingi madarasani wasielimike. Si vibaya kupewa ulaji. Unapoupata, lazima utumie busara. Usipayuke. Ikitokea ukapayuka, ukitimuliwa unauchuna kama siyo wewe na kujifanya kuwa kilichotokea ni ajali kama ajali nyingine. Kwanini Bushiri hakuuchuna kama Porofwedheha Kabundi aliyesifika kujidhalilisha akaishia kuweka kando na akauchuna na kuumia kimya kimya? 
Wahenga walinena. Aliyeko juu mngoje down. Akitua down utamsikia akilalama utadhani hakutokea huko. Ningekuwa Bushiri, ningetafuta chuo kikubwa nikapiga chaki au hata madrasa nikafunza vimamuma badala ya kujivua nguo. Hebu angali anavyoshukiwa na wasaka tonge tena wasiojua hata darasa ni nini. Sijui ndiyo ile dhambi inamtafuna. Hata sijui. Kama kusifia ni sera ya chama, wewe ni nani wa kuionea kichefuchefu wakati ulaji wako wote unatokana na hulka na tabia hii? Inakuwaje uone ubaya wa kushukuru na kusifia baada ya kupunguziwa maulaji kama siyo ujinga na unafiki? Wote waseme. Lakini siyo Nshomile Bushiri Kaakulwa.
Ngoja nikaupige ulabu mwingi. Leo chichemi mengi dugu yangu pendwa sana Bushiri. Nenda kwa Maza omba yeye sahama kabla kukata ile laji yako nakupa kiburi. Veve iko bunge ya kulu. Vako naita veve chawa. Kwanini chomoa fyuzi kufanya ile mingine adui vako nayo chomoa? Chomeka fyuzi dugu yangu kabla mama chomoa veve dugu yangu. Kama veve chomoa fyuzi dugu yangu levi tachomoa nini? Tuonane next time.
Chanzo: Jamhuri

No comments: