The Chant of Savant

Tuesday 15 November 2022

Tuvunje Idara ya Uokoaji na Kuajiri Wavuvi

Kwanza, nitoe salamu za rambirambi kwa wafiwa wa ajali ya hivi majuzi ya pipa. Pili, nitoe dua kwa manusura nikiomba Dingi Mwenyewe wa upstairs awaponye haraka. Tatu, naombea kaya itie akilini iache ubangaizaji na usanii kwenye mambo siriasis. Nne, sina haja ya kufanyia mzaha balaa la ajali ya ndege iliyotokea mjini Bukoba hivi karibuni baada ya pipa la Presisheni Air kushindwa kutua uwanjani tokana na hali mbaya ya hewa kuishia kutua kwenye ziwa na kuua watu 19 huku 24 wakiokolewa na wavuvi pamoja na kutokuwa na ujuzi wa darasani zaidi ya ule wa University of Street. Msiojua kimombo nendeni Mombo wakawatafurie. Ila chunga msikute Mombo nao wanaongea Kisambachi na si kimombo. Sasa najiuliza kilevilevi. Je ina maana mkoa mzima wa Kagera hauna kikosi cha uokoaji? Kama kipo, kinalipwa kwa kazi gani wakati kazi ambayo kinapaswa kufanya ilifanywa na wasamalia wema tena wachovu? Je kikosi cha uokoaji cha mkoa kilikuwa wapi kama kipo? Nauliza si kinomi wala kinoko bali kilevi tu. Je kilifanya mandingo gani hata baada ya kufika wakati vyombo vya umbea vilionyesha wavuvi wachovu wakiweka maisha yao hatarini na kutumia mikono mitupu kuvuta ndege? Kweli hujafa hujaumbika! Nani alidhani mvuvi angemuokoa mwenda kwa debe au mtumbwi kuvuta pipa? Imetokea tena mbele ya mato yangu. Mitumbwi ilivuta pipa. Nani alitegemea mvuvi tena wa kasia angemwokoa rubani? Lazima hapa tuheshimiane na kuthaminiana. Ngoja niulize zaidi kilevilevi. Je tatizo hapa ni kikosi au idara ya uokoaji au taifa kwa ujumla. Je tulijifunza nini tokana na ajali ya MV Bukoba.
Kwanza, niseme. Ajali ya juzi ni ya kwanza kwa shirika lililoanzishwa mwaka 1993.Tumeambiwa kuwa ajali ilisababishwa na hali mbaya ya hewa ambayo haiepukiki. Je kwanini rubani hakupelekea ndege Chato au Mwanza hata K’Empala? Je hakuwa na mafuta ya kutosha? Je alifanya maamuzi ya haraka? Si rahisi kuujua ukweli hadi ripoti ya uchunguzi itolewe. Ama kweli ajali haina kinga japo si vibaya kujiandali ajali wakati wowote. Hivyo, hatuna haja ya kulaumu au kulishuku shirika wakati tukingojea ripoti kamili ya uchunguzi wa ajali hii. Ila kama kaya hata kama ni ya walevi, kuna mengi ya kusema. Nsingependa kutupia lawama kikosi au Idara ya Uokoaji na Majanga ambayo sina shaka hupangiwa bajeti kila mwaka. Pia, sina jema la kusema kuhusiana nayo. Nikijitenga na tambo uchwara za wanasiasa ambao baadhi yao waliwamwagia sifa wavuvi wa BK, akina nshomile sana hadi my dogi anajua kiinglish, kuwa wameiwakilisha Tanzania kwa kuonyesha ushirikiano, napendekeza Idara na Vikosi vya Uokoaji vifutwe na badala yake waajiriwe wavuvi. Hawa, licha ya kuwa shupavu na wazalendo wa kweli, wana uwezo wa kutoa matokeo tegemewa hata bila kufunzwa wala kuajiriwa. 
Inakuwaje tunakuwa na mapipa ya kuwahisha wanene kwenye tukio kutoa siasa lakini hatuna midudu ya kuokoleana? Je ni kwanini wanene hawaoni kuwa inaweza kutokea, hata kama siwaombei, wakajikuta siku moja mikononi mwa wavuvi? Kwanini wanashindwa kununua vifaa tena vinavyoweza kuwasaidia lau wao wanaopanga mapipa. Hapa najua. Wakiamua kununua, watanunua vinavyowahusu na kuwaacha makapuku wategemee wavuvi zali likitokea.
Hata hivyo, si wavuvi peke yao. Karibu watanzania walio wengi wana hulka hii ya kujua la kufanya pale wanapoona na kuzoea kuwa mamlaka hazina cha kuwafanyia kama wajibu wake. Mfano mdogo, ilipotokea ajali, mawaziri na wanene wengine walijisomba na kupanda madege na mashangingi kwenye kutoa hotuba za kisiasa. Je hiyo pesa waliyotumia––––ambayo inatokana na kodi za wahanga na makapuku wengine wa kaya hii––––wangeielekeza kwenye kununulia zana na uokoaji u kujiandaa na kupambana na janga––––wangepunguza hatari kiasi gani? Ukiangalia ujio wa Waziri Mkubwa, Waziri wa Lindo, Waziri wa Mambo ya Kaya, Waziri wa Uchukuaji, Katibu Mueneza rongorongo wa Numero Uno, Wakuu wa vyombo vya mausalama na wakuu wa mikowa jirani na posho walizolipwa na mafuta waliyounguza kwenda kutoa siasa, kama wangejizuia wakatuma hata baruapepe na hiyo fedha ikanunua vifaa, tungesonga mbele kiasi gani? 
Wengi hadi sasa wanajiuliza mantiki ya ‘kuwajali’ sana wahanga wa ajali ya ndege wakati wale wa magari ambao ni wengi tokana na ajali hizi kutokea mara kwa mara, ni nini? Je ni kwa vile wao ndio watumiaji wazuri wa pipa? Je ni kwa sababu ajali husika inatangazwa kila kona guniani? Je ni kutokana na ukweli kuwa watu wanaosafiria ndege siyo wachovu wa kawaida, hivyo ni wenzao lazima wawajali maana leo kwao kesho kwa wengine? Je sababu ni nini?
Japo situmii ubongo kufikiri––––kwani natumia ulabu––––napendekeza Idara na Vikosi vya uokoaji ima vifutwe na kazi yao kupewa wavuvi au wanene wake wapugwe kigodo na kuteuliwa wavuvi watenda kazi wawafundishe kazi hawa waduanzi wasiojua hata thamani ya dhamana zao. Inakuwaje kaya, tena inayofisika kwa midini na mimali kibao kutokuwa na zana za uokozi angalua hata wa wanene? Leo chichemi mengi njomba. 
Chanzo: Jamhuri leo.

No comments: