Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Wednesday 21 August 2024

Hongereni Mafytu Kumpenda Mama

Mwanafalsafa’ maarufu wa Uganda, alhaj, Doktari, field Marshall, profedheha Idi Amin Kaidada  Oumee aliyepata elimu yake mtaani aliwahi kusema kuwa lazima watawaliwa wawapende watawala bila kujali lolote au wanawatenza vipi. Lazima wawasifie hata wakikosea. Wawachekee hata kama wanapaswa kulia. Wawaabudu ikibidi hata kama wao si Mungu. Kwani, kufanya hivyo, huleta ‘amani na maendeleo’ hata kama kuna kero. Kwa kuzingatia ushauri huu wa kitaalamu wa fyatu aliyewafyutua waganda akataka hata kutufyatua kabla ya JWTZ kumfyatua na kumg’oa, mafyatu juzi walionyesha upendo usio kifani. Si walimnunulia maza chopa kwa ajili ya kuivinjali kaya yake tukufu. Ni jambo la kupigiwa mfano na kumshukuru Mungu aliyewapa moyo wa upendo.
            Dunia hii we acha tu. Si walijitokezea wenye wivu tena wa ki-female wakaanza kusema eti ni hongo na kielelezo kuwa kutakuwa na uchakachuaji. Maana, wanasema tena bila aibu kuwa mafyatu waliomnunua chopa, kwanza, wamepataje njuluku na wanategemea kuzirejesha vipi. Wanasema. Akishafyatua ulaji, nao watamfyatua kwa kutaka alipe fadhila. 
        Wanahoji kwanini wasinunune ambulances za kubebea wagonjwa. Au ni yale ya ndata kuwa na ndiga wakati wagonjwa hawana? Hayo si yangu.
        Wafyatuane au la, hayanihusu. Muhimu wasinifyatue na mafyatu wenzangu. Je kama ni kweli kuwa huku ni kufyatuana kunakolenga kulipana fadhila, mafyatu tutanusurika wakati kaya itakayofyatuliwa ni yetu? Je tutakubali kufyatuliwa na hawa wanaofyatuana ili watufyatue? Je tutawafyatua kwa kutowapa kura ya kula ili wasitufyatue au tutafyatuliwa mkenge? Niliwahi kuwadokezea mafyatu wa upingaji walivyowahi kuhoji tukutuku zilizosambazwa nkoani wakisema kuwa bi Nkubwa anawahonga watendaji. Walihoji alikopata hii njuluku tena mabilioni, ananunua, nani, nini, na anategemea kupata nini. 
        Kwa vile mie siyo mpingaji wala muungaji au msifiaji bali mfyatua, natimiza wajibu wangu wa kufyatua bila kuwaudhi wanene ambao hata nikiwaudhi hawana grounds au locus standi kwa lugha ya kisharia, kunifikisha kwa pilato. Hii jamani nayo ni sanaa. Ukiona umefyatuliwa, huna haja ya kunichukia au kulalamika bali kujirekebisha au kufyatua kijanja. Hayo tuyaache. Mibangi hii! Sasa naanza kufichua siri!
            Turejee kwenye ununuzi wa chopa na umuhimu wa watawala kuwapenda watawaliwa hata kama wanawaponda au kuwafyatua.             Kwanza, ni jambo bora kumchangia mama kipenzi kuliko kuwapa njuluku matapeli wa kidini wanaotoza njuluku eti kutoa maombi aka huduma wakati ni huduma. 
        Juzi nilimsikia jembuz mmoja toka kaya ya jirani anayejiita kiboko ya wanga wakati naye ni tapeli wa kawaida. Hivi inakuwaje kaya yetu inageuzwa shamba la bibi tena mwenye kipofu? Kwanini mnaruhusu matapeli tena wenye mtindio wa mawazo na wavivu wa ubunifu kuja na kuwafyatua mafyatu wenu mliowasikinisha na kuwajaza ujinga na kukata tamaa hadi wakaamini kila upuuzi? Au hao nao wanawasaidia kuwafyatua kwa sababu wanawaaminisha mafyatu wachovu na wavivu wa kufikiri kuwa ukapuku wao ima ni kazi ya muumba au wachawi?
         Sijawahi kujua kwanini mafyatu wetu wamekuwa wa hovyo hivi. Hivi, kweli kwa anayejua umaskini waliotegeneza akina Mobutu, kuna la maana unaweza kupata kwa jamaa hawa mabingwa wa utapeli sawa na wale kutoka kwa akina Buhari ambao ujanja wao ni utapeli tu na siyo ubunifu wa maana? Nasikia siku hizi kila tapeli anatumia gea ya kuwowa mabinti wa kidanganyika wasiojua hili wala lile ili kuishi kwenye kanani ya Afrika chini ya mama kipenzi.             Mtaachwa Solemba. Hawa jamaa wakishapata wanawaacha na vitegemezi vyenu kiasi cha kugeuka wajane bila kufiwa. Kuna haya ya kuanzisha safu ya kuwaelimisha mabinti zetu waache kushobokea wageni wasijue hakuna la maana zaidi ya kuwa visa za kuishia kayani. Huku Ulaya ni jambo la kawaida. Wanachotuzidi watasha ni kwamba waswahili wanaotaka kuishi hapa kwa gea ya kuoa, lazima watimize matakwa ya wadada wa huku na kugeuzwa mashine ya kunonihino. We! Koma. 
        Wapo wengi wananyonywa sawa na mabinti zetu wanaonyonywa na hawa matapeli uchwara. Hali ni hiyohiyo bondeni. Nakumbuka mwanamuziki wa kwaya aitwaye Debbie Fraiser aliyeingizwa mjini na tapeli toka kwa akina Buhari na kumharibia maisha hadi kunyotoka roho.  
        Mna habari kuwa hata Brenda Fassie aliponzwa na matapeli haya? Fumbueni macho ya mabinti zenu waache kutumika kama ilivyokuwa zamani ambapo vijana wengi wa kibongo walibebeshwa miunga na kuishia kufungwa na kugeuzwa mashoga kwa tamaa na ukumbaff wao.
        Kimsingi, kumnunulia mama kifaa ni ushahidi kuwa mafyatu wanampenda kama siyo kufyatuliwa na baadhi wenye ukwasi ili wamtumie. Pia, inaonyesha kuwa si mafyatu wote ni mataahira wa kuibiwa na kila tapeli kama yule jambazi toka kwa akina pedejee wanaokuja na kuwaibia au waganga wa kienyeji wanaowaibia wakidai wanawasaidia kutengeneza utajiri wakati wao ni maskini wa kunuka.
        Tumalizie tukiwapongeza mafyatu na kuwashauri wawe macho kuona huu mchezo utaisha vipi nani atamfyatua nani na nani atazembea akafyatuliwa. Hivi nimesemaje? We koma.
Chanzo: Mwananchi leo.

No comments: