Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Thursday 15 August 2024

Nashauri Kununua Majenereta Kuendeshea SgR


Baada ya kuwafyatua kwa SgR kufanya majaribio, nilionya kuwa safari zingeanza pindipo mwana wa Adam­­­––––yule fyatu wa kiyahudi anayeabudiwa na mafyatu wengi duniani hadi wenzake mafyatu wanasema kwanini tusiwaabudie wote wakati hawana lolote zaidi ya mikwara na kuiona bora kuliko wengine wakati ni hovyo–––akirudi si waliamua kunifyatua na kujifyatua na kuanza majaribio. Nikiri. Nilikosea. Juzi mtukufu mpendeka, msikivu, mwenye maone, Doktari rahis Mama alizindua safari za mwanzo. Je hizi safari zinazopigigiwa upatu ni endelevu na fyatu au danganyifu? Wale wanaoelewa nilichofyatua, wako wanafyatua maandalizi ya kuja kwa njemba hii iliyopumbaza wengi kuwa iliwaokoa wakati iliwatonya kuwa kila fyatu atabeba furushi lake mwenyewe siku ile ikifika. Chonde chonde, wale makanjanja wenye uroho wa kiroho msianze kuwafyatua na kuwachuna mafyatu zoba yanayoamini kila kitu hadi wanaitwa kondoo na kuchungwa na wachunaji wanaoishia kuwachuna na kuwasikinisha wakijiona kama mataahira. Yangu mato.
        Gwaijimmy, Katortoise, Gamanyie, Mwakasegie, Lusekelelo, Godavie, Muingirer, Mwamposer, Mutalemewa, na matapeli wachunaji, sorry, wachungaji mnanipata? Yaani hamuoni ni dhambi kuwafyatua mafyatu wasio na hatia bali ukumbaff na kukata tamaa? Je mnajua yaliyoibuliwa kuhusiana na mwenzenu Tii Bii Joshuer, beberu fyatu aliyefyatua watumishi wake njuluku hata uroda? Mnamfyatua nani wakati soon mtafyatuliwa na God mnayemtumia kuwafyatuliwa na kuwatapeli mafyatu majuha? Mshajiuliza, mkizeeka na kukaribia kufyatuliwa mtafyatua nini lau kuepuka kuingizwa motoni hata kama hamuamini kuwa moto upo?
        Kwanza, sijui kama hawa walioamua kunizodoa kwa kufyatua kiini macho wana umeme, uaminifu, utaalamu, uwajibikaji, na uzalendo vya kutosha kunifyatua kwa kufanya kweli kabla sijaja na fyatuafyatua na zomeazomea zaidi hadi kuwafyatua mafyatu wakawafyatua tofauti na mlivyotegemea wala kuotea. Basi, ngoja niwafyatulie kweli. Mnaweza kujimwabafy kuwa bwawa la Mzee Mchonga limeanza kufyatua umeme msijue watendaji wetu uchwara wanaweza kulihujumu au kuzembea kikaumana tena. Jikumbusheni jinsi bundi na ngedere walivyoifyatua SgR juzijuzi.
            Hivi tunakosa umeme tokana na kukosekana umeme au ubunifu na uzalendo wa kutunza miundumbinu yetu mbali na lisrikal kupenda kutumia umeme tena hovyo bila kulipa ukiachia mbali kuwa linapigwa njuluku kila siku na linabaki kutoa mimacho kama panya aliyefyatuliwa na ntego? Huwezi kutegemea mambo yaende kisayansi na vyedi wakati wahusika wanaishi kwa kujikomba, kusifiana, hata utopolo bila kuchapa mzigo. Huwaoni? Kila anayeongea utamsikia “napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu yada yada yada… na ukumbaff kibao.’ 
            Anaendelea “pia, napenda kumshukuru mno na sana bila kukoma wala kukomaa mtukufu, mpendwa, mpenzi, mwenye mapenzi yasiyomithalika kwetu hata kuliko mshirika wake wa bedroom, mwenye masikio makubwa na asiye na mdomo, asiyejivuna hata akijivuna, doktari, profesa emeritus, al- hajat, ustaadha, sheikha,  sayidat rahis yada yada yada na pumb’a kibao.” Unategemea mafyatu kama hawa wasiojiamini, wanaodanganya, wanaodanganyana, na kusifiana badala ya kufyatuliana ukweli wanaweza kupambana na tatizo kama hili linalohitaji umahiri, ukweli, na weledi bila kusahau ufyatu?
            Hapa tunachoona ni kupakana mafuta kwa mgongo wa chupa kwa kufyatuana kwa kusifiana kwa sababu tunapenda kusifiwa na kuabudiwa. Mie mafyatu wangu, pamoja na kujua ni daktari wa kweli na siyo hawa madoktari wa heshima, niliwapiga marufuku kuniita daktari. Ndiyo maana hata kwenye uga huu huoni udaktari wangu tena usiofeki kama wa akina au wa kuzawadiana au wa kununua kama wa akina Gwaijimmy na matapeli wenzake. 
            Kesho mtasikia na waganga wa kienyeji wakiitwa doktari hata maprofesa! Hata hivyo, kama maprofesa wenyewe ni akina wa jalalani, tutegemeeni? Tokana na uzoefu wetu, kufyatuliwa, kuanza safari na kufanikiwa ni vitu tofauti. Kwa vile kaya yetu ni ya majaribio, wanaweza kufanya majaribio hata milioni. Je lengo la kuzamisha matrilioni ya madafu kwenye mradi huu ni kufanya majaribio au kufanya kweli? Je hizo njia zilizojengwa na makandarasi wa kutia shaka, zinaaminika na zina thamani sawa na njuluku tunayopigwa baada ya wanene wachache kula dili? Je tatizo hapa kama ambavyo imekuwa, ni nini kama siyo wanene wetu?  Kesho umeme ukigoma, tutapigwa kwa kisingizio cha kununua portable jenereta za kuzalisha umeme wa SGR. Unacheza na kaya hii sanii siyo?
        Najua mafyatu wengi hawakuambua. Niliposema majaribio nilimaanisha majaribio ya kufanya kweli siyo kutuonyesha vichwa viwili vitatu vya treni na kuminya. Narudia, hili halifanyiki na kufanikiwa hadi mwana wa Adam arudi. Atarudi lini? Msiniulize. Kawaulize wao. Pia, hakuna haja ya kuchukiana maana mie si wa kwanza kutoa ahadi hii. Atarudi kweli au la? Nani anajua wakati wote mtakuwa mmeishafyatuliwa na kulala milele bila kujua ukweli mchungu yote ilikuwa fumbo la imani la kuwafyatulia mafyatua wasifyatuane kinyama. 
        Naona yule anatikisa kichwa na kufyatua midomo kwa hasira. Huna haja ya kunichukia. Simpo, anapofyatuka fyatu na kurudi kwa mfyatuaji wake huwa si mnasema uilaze pema roho yake milele baada ya kumuweka kwenye makazi yake ya milele. Unajua maana ya milele? Hivi safari za majaribio zimefikia wapi na zimefanikiwa au kukwama kiasi gani? Je usafiri wa kweli utaanza lini, maana kwenye mitandao sioni kitu tena? Basi, jiandaeni kununua majenereta kuendeshea SgR. Vipi mafuriko Bwala la Mwl Mchonga? Du! Kumbe napanga kuwasaka bundi na ngedere niwatie adabu!
Chanzo: Mwananchi jana.


No comments: