Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Thursday 29 August 2024

Ni CcM policy au geshi la polishi?


Katiba ya mafyatu inatoa haki na uhuru kwa kila fyatu kukutana na fyatu yeyote unayemtaka kutembea au kuandamana na unayemtaka kwenda unakotaka kusema unalotaka imradi usivunje sheria ya kaya ambayo nayo siyo maagizo au mapenzi ya ndata na wanaowatumia tena vibaya. Unapozuiwa kufanya hayo hapo juu na mengine kama au kukaribiana nayo, anayefanya hivyo havunji sharia tu bali katiba yetu virakaviraka ya mwaka 47. Kisharia, bila kujali cheo au sura ya yeyote, anayezuia uhuru wa kikatiba ni mhalifu sawa na wahalifu wowote.

 Kikatiba, haki na uhuru tajwa hapo juu siyo utashi wala hisani toka kwa yeyote hata awe mnene kiasi gani. Kaya ya mafyatu hutawaliwa kikatiba na siyo kichata wala kichawa. Uhuru ni haki ya kila fyatua. Msigeuze uhuru kuwa udhuru. Mbona mkipiga njuluku au kuzitumia vibaya Hamshikwi na kuswekwa lupango? Mbona mkipiga mnada kaya hamshikani, kufungana, hata kuswekana lupango?
            Mbona mafisi na mafisadi walioingia mikataba inayoanza kututokea puani hawakamatwi au ndata hawawaoni au wanawaogopa kwa vile wengi ni wanene au makuadi na washirika wao? Mbona tunawaona wakipeta na wengine hata kupewa ulaji zaidi ili wavimbiwe wafe, au kuna namna?

Wako wapi waliouza bandari, maji, na hata hewa? Wako wapi walioingiza madudu kama Buzwagy, Mwanakaya, IpTL, Kagoda, Eskorow, waliochoma banki yetu kuu na wengine wengi waliokwisharejesha namba? Kwani mtaishi milele kumbaff nyie?

Leo, tena kwa hasira na kifyatu, nitafyatua sakata la kuwadaka na kuwatia adabu viongozi wa upingaji. Japo mimi si wakili wao wala sitaki kujifanya kuwa, kwani wapo kisheria au kihiari? Je siasa ni haki au hisani? Hamjui kuwa maulaji yana mwisho? Wako wapi waliowabia kura za kula, wengine kuwapoteza mbali na walionusurika mitutu? Si wameyaacha maulaji na kutokomea kwenye kaburi na sahau? Hamuoni maulaji yaliyowahangaisha sasa yanaliwa na wengine tena ambao hawakuwa na nchango wowote zaidi ya unafiki na ufichi?

 Nashauri maulaji yasituchoganishe na kutufanya kunyatuana roho, kudhalilishana, na kutesana bure. Duniani tunapita. Kwanza, maulaji yenyewe ni ya mafyatu ukiachia kuwa ni ya muda. Kuepuka udhalilishaji, ukandamizaji hata uonevu, basi futeni vyata vya kisiasa na kusajili geshi la polishi kama chata cha siasa muone, maana limekosa kazi mbali na kufanya kazi za kisiasa na siasa za visasi na kutumika hovyo. Japo sipendi wala si mwanasiasa, napanga kuingia kwenye siasa ili nikomeshe siasa za visasi. Kwa nilivyo gwiji na nguli mwenye ushawishi, naamini nitabadili upepo wa kaya kisawasawa na kufanya kiumane nchana kweupe. Nashangaa. Tunaambwa vyata vipo kikatiba, vinapiga ruzuku mbali na kelele halafu vinakandamizwa. Basi, tangazeni kaya ya chata kimoja tujuwe na muone watasha watakavyowawashia moto na kuwanyima misaada japo Uchumi mnao lakini mnaukalia kama alivyowahi kusema mzee Nchonga (RIP sana tu).

Kila uchao mafyatu wanatekwa na kuibiwa. Ajabu hakuna ndata wa kuwalinda au kuwashukia wezi. Ajabu ya maajabu, magari ya wagonjwa na madawa hakuna wala njuluku ya kuajiri matibabu ila ipo ya kununua mibomu ya kutoa machozi, risasi, virungu, na zana nyingine za ghasia! Vitegemezi vya makapuku vinakaa chini na kukosa maticha ilhali ndata wanatesa! Hata nao hawajitambui. Hawa wanaowadhalilisha na kuwatesa ni ndugu zao hata kama hawawataki wala kuwaheshimu na kuwajali. Msitupeleke Bangla--- ambako mama alitemeshwa ulaji baada ya kulewa maulaji na kujisahau akayafanya kuwa urathi wa kifalme asijue hajui kuwa hajui.

Nani aliwachagua nyinyi na kuwapa power na utashi ya kukandamiza wenzenu wanaofanya usanii kama nyinyi? Tangu tunyake udhuru, sorry, uhuru, mmefanya nini cha maana zaidi ya kujihudumia kwa migongo yetu? Leo hii bei ya kila kitu imepaa huku wanene wachache wakitanua na kutapanya kama hawana akili nzuri. Mnataka tunyamaze au kupongeza wakati tunaumizwa na kudhalilishwa?  Kwani mafyatu hawajui wala kuona?

Zamani nikirejea toka kuutwika, lau, nilikuwa na jeuri ya kuwaletea vitegemezi pipi. Siku hizi, narejea home kwa kujificha kama mwizi ili vitegemezi visinione na kutaka zawadi. Ni maisha gani usawa huu wa karne ya sayansi na tekelinalokujia? Wanene wachache wasiojali mafyatu wanazidi kuongeza nafasi za ulaji hata zisizo kwenye katiba kama ule wa Dot p’Bitek, waziri mkubwa mdogo. Kwani hatujui wala kuona? Nawashangaa hata wanasharia wetu. Kwanini msiende kwa pilato na kuzuia israfu hii ya wazi au hamuoni? Lo! Nimepayukaje? Nimesema eti cheo cha p’Bitek ni unconstitutional au? Hayo tuyaache. Wajinga ndio waliwao. Mwalimu wangu usinibaini. Nikipata kumi tano zako. Hiv ndata wanaoatwanga wapinganji wanakumbuka viapo vyao? Ikitokea wanaowachapa wakaukwaa unene watakuwa wageni wa nani? laiti wangejua kuwa kazi ngumu ni kupanda na siyo kushuka! Wangejua hili, wangefanya wafanyayo kwa haki na tahadhari. Ngoja nikapate kanywaji nipate usingizi na kuepuka makelele ya yule kiumbe ajifanyaye ananipenda. Nimesemaje?

Chanzo: Mwananchi Jumatano iliyopita.

No comments: