The Chant of Savant

Thursday 15 September 2011

WAHAMBA nathi (ulitembea nasi)
Oh wahamba nathi (oh ulitembea nasi)
Oh wahamba nathi, siyabonga (oh ulitembea nasi, twakushukuru)
Siyabonga Jesu (tunakushukuru Yesu),
Siyabonga ngonyama yezulu (twakushukuru samba wa mbingu)
Siyabonga Kakaramba- tunakushukuru mkuu

Nawashukuru walevi
Walitembea nami nawashukuru
Nawashukuru kwa ujinga wao
Nawashukuru kwa kuwauza kama Yesu
Nawashukuru mwamba wa dili mie
Nawashukuru kama mkuu
Mkuu naye anashukuru walevi na wabongolalalanders
Tunashukuru kuwalamba ninini lolo lolo lalalala

Mwanzenu baada ya kugundua kuwa kumbe kaya imegeuka kaya ya madili badala ya maadili, nami nimeamua kuchonga dili langu.

Soma taratibu akina mgosi Machungi wasikusikie wakatia kichumvi. Nina mpango wa kumuuzia kijiwe mwarabu fulani kibopa uchwara. Ameniahidi bonge ya msuli, suti, kandambili na makando kando mengine ya dezo.

Pia katika dili hili sitakula peke yangu. Bi mkubwa atanunuliwa bangili za shaba na batiki mtindo mmoja. Ili kuhakikisha tunajadili na kula vinono wakati wa dili husika, mwarabu ameahidi kutuletea tende na mafuta ya zeituni ili tukarangize nyama ya kijiwe. Ilikuwa atupe tiketi za ndege twende kujinoma kwa mama lakini tumeona hii ni kuharibu fweza bure. Sisi tutamalizia mambo yetu hapa hapa kayani bila kujali nani ataingizwa mkenge.

Mie nina usongo na njuluku na kuukata haraka. Kama atatokea anayetaka kununua watumwa sina neno. Nitapiga bei hata akitaka na wanywaji kahawa nao nawasha kulaleki!

Sijutii uamuzi huu. Kama wakuu wa Danganyika na Bongolalaland wanauza kaya kwa suti na upuuzi mwingine nina kosa gani kuwauza wanywa kahawa waliokwishapigika? Hivi ni kosa kwa fisi kuwararua kondoo au nyoka kung’ata kisigino?

Kama wengine wameuza wanyama tena kwa kuwavusha kupitia viwanja vya ndege vyenye kila ulinzi bila kufanywa lolote, mie nina kosa gani kuuza kijiwe. Ajabu wanyama walipotoroshwa eti walevi wakaambiwa eti hawajui walipelekwa wapi wakati hata wadudu wanajua kuwa walipelekwa umangani.

Sasa kama madege hata ya kijeshi yanaweza kuingia yakatua na kupaa hao uhasama wa taifa wanafanya kazi gani kama siyo kuiba kodi za walevi? Hiyo mamlaka ya anga inaangaza nini kama madege yanaweza kuja na kuzoa wanyama wetu yatakavyo?

Ajabu nyingine ni kuripotiwa kuwa yule ponjoro aliyewezesha dili hili ametoroka akiwa kwenye dhamana! Hii maana yake ni nini kama siyo kudharau mahakama na mapilato wake kama alivyofanya nshomile Ruta hivi karibuni. Ponjoro ametoroka au ametoroshwa ili wazito wasiumbuke ikizingatiwa kuwa yeye ni dagaa aliyekuwa ameletwa na mapapa.

Mara hii mmesahau sinema ya Chauda na uuzaji wa mashamba ya wagosi kule Tanga? Nani hajui kuwa Chauda alitoroshwa ili kulinda siri za wanene kama ilivyo kwenye zali hili la k utorosha mahayawani wetu? Kama rada na makompyuta yamechemsha, kwanini nisiuze kijiwe ambacho mlinzi wake ni Mungu mwenyewe? Huu ni wakati wa kuuza. Hii ni kaya ya kuchuuzana. Bila kuucha mtu au watu huukati bali utakukata.

Nitachofanya, nikishapiga bei kijiwe nachukua hisa kwenye biashara ya Mwarabu atakayoianzisha kwenye kijiwe. Hivi ndivyo wakubwa tunavyokula. Siogopi cha Weeklick au nini nauza tu.

Najua dili hili litapita na hakuna atakayenistukia kwa vile kwenye kijiwe hatuna mabalozi wa kuandika madhambi yetu na kutuma kwao kama jamaa aliyewalipua jamaa wa kuuziana taasisi kwa bei ya suti. Msijeninukuu vibaya. Mie sisemi yaliyosemwa ni kweli au uongo. Nitajuaje wakati madili yao hayanihangaishe isipokuwa hili langu la kuuza kijwe kwa kasi na ari, mori na nguvu mpya.

Wengi watasema naunza kijiwe kwa bei ya kutupwa kwa kuhongwa upuuzi kila aina. Hata wakiniona mie ni mpuuzi anayehongwa upuuzi mie najifanya sisikii. Nikiona wanoko wamezidi namtuma my waifu wangu Silvia kuwatukana wote wanaoishikia bango ulaji wangu. Nitamwambie awaite wapuuzi wao na mama zao.

Mi nilivyo na usongo wa fweza hata mtu akitaka kumnunua bi mkubwa namuuzia. Si bora mshiko bwana kuliko uchovu wakati unaona waliokuwa wachovu jana wakiukata na kuula?

Mie sina roho wala akili nzuri. Sina tofauti na wale jamaa zangu wa mlimani ambao huwaambia watoto wao: umekataa kuiba utakula mafi yako. Jamani nawatania hata kama ni kweli tumezee. Ndiyo mila zenyewe nyingine chafu au siyo meku upo hapo? Yethu mbesa kwanza.

Mie mbele ya fweza ni sawa na mbwa mbele ya nyama au fisi mbele ya fupa. Mie na Yuda hatuna tofauti. Sioni taabu kuzoea vipande thelathini na kumuuza mama yangu hata dingi yangu. Hebu fikirieni. Kama naweza kuwauza madingi wangu wanakijiwe ni nani niwaonee huruma wakati hawajionei huruma?

Kama dili langu litabumburuka wala sitawaita watakaokuwa wanituhumu kuwa wapuuzi. Watetezi wangu hasa bi mkubwa Silvia atasema tuhuma hizi zitalenga kunichafulia jina. Kwanini watakaonituhumu wanichafulie jina wakati nikijua fika hawawezi kugombea kuongoza kijiwe? Najua wenye akili watauliza: kwanini yeye na si wengine?

Najua wengi watanicheka kwa kuuza kijiwe kwa zawadi za misuli, tende na mafuta ya zaituni. Huo ndiyo uwezo wangu wa kufikiri hata ukionekana ni wa hovyo. Si ninauza change? Hata nikigawa kama wale wanaogawa madini na wanyama shauri yangu. Nyie yawahusu nini? Waache Wanakijiwe walalamike. Maana, ndiyo wenye mali. Hata hivyo nani anajali? Mali ya umma haiumi ati. Mmesahau mara hii. Yamefanyika mangapi tena zaidi ya haya? Nani mara hii anajisahaulisha ujambawazi wa HEPA, EITISIELO, AIPITIELO, Dowanis na Richmonduli? Juzi nilisikia wakiuza hata ofisi za mapilato bila hata kuhofia! Nikisema mnaliwa mnasema natukana. Situkani. Huo ndiyo ukweli hata mkiuita upuuzi.

Kuna jambo moja linashangaza hata hivyo. Mbona hao watasha wanaowatuhumu wakubwa wanapotoa misaada yao hatuwaiti wapuuzi? Hapa mpuuzi ni yule anayewaita wenzake wapuuzi na kupuuzia ukweli kuwa naye ni mpuuzi? Hilo mie sijibu. Mtajibu wenyewe.

Like gari ni kama la Maiko Reiza. Ngoja niende kumuuliza ukweli mwingine.

Chanzo: Tanzania Daima Septemba 14, 2011.

No comments: