The Chant of Savant

Saturday 8 February 2014

Mlevi aonya walevi wa politiki


Baada ya mlevi kushuhudia na hata kusikia walevi wa politiki wakivuana nguo hadharani, ameamua kutoa somo ili kuonyesha tofauti kati ya walevi wa kanywaji na walevi wa politiki.
Ninafanya hivi kuepuka aibu inayotokana na mchezo huu mchafu wa mitandao ya kilevi ya kuhujumiana, kuumbuana, kutukanana hata kupakaziana ingawa mengi yanayosemwa na hawa walevi wa politiki yana ukweli.
Ila kwa vile mie si mlevi wa politiki yao nawaachia wenyewe sawa na aibu yao.
Bila kurudia mauzauza na mfukunyuku, kasheshe, mshike mshike kindaki ndani na ulimpyoto walivyoshuhudia wale wa taputapu baada ya walevi wa politiki kustukiana kuzidiana kete kwenye mchezo wa kuwanyonya walevi, napenda kusema wazi kwa niaba ya walevi kuwa sisi walevi wa kanywaji huwa hatuna upogo ufyole na ulimpyoto wa kuvuana nguo hadharani japo huwa tuna sifa ya kutoboa siri bila kificha na kutomuogopa mtu.
Hata hivyo, huwa tunafanya kweli panapo ukweli na haki na si kutafuta ulaji wa dezo kama wale.
Hivyo, leo nitaonyesha tofauti baina ya makundi haya mawili ili wasomaji na wachovu wajue.
Hii itaepusha dharau na kinyaa na kuepuka kuanza kutuona sisi walevi wa kanywaji hovyo sawa na wale mapolitiki.
Ulevi wa mataputapu una hatari zake kama vile kuangusha gari mitaani kiasi cha wahuni kutaka kukufanyia vitu vibaya ukiachia mbali kukamatwa na ndata mara kwa mara wanaotaka kukutoa kitu kidogo na kikubwa kutokana na njaa na ufisi na ufisadi wao.
Unaangusha gari na kupona wakati mwingine kuokotwa na wapita njia na mambo yanaishia pale.
Ukitoka pale unakwenda kuwekwa kiti moto na mamsap akidai ni kwanini unamuaibisha hivyo.
Unapiga magoti na kumshika miguu na kuomba msamaha ukiapa kwa miungu yote kuwa hutarudia kumuangusha na mambo yanaisha.
Bi mkubwa kwa vile ameishakuzoea, anasamehe yanaisha na kungoja zali jingine.
Zifuatazo ndizo tofauti baina ya walevi wa kanywaji na wale wa politiki.
Mosi, wakati walevi wa kanywaji huangusha gari yaani miili yao, tatizo la walevi wa politiki  ni kuangusha kaya nzima kiasi cha kuruhusu wezi wa kila aina waitwao wawekezaji kuja kuharibu na kuhatarisha maisha ya walevi wote na vizazi vijavyo hasa kwa kutumia kufisidi hata kuiba na kula bila kunawa.
Pili, sisi walevi wa mataputapu si wezi wala majambazi kwa kiwango cha haya ya politiki.
Tatu, sisi hujiibia vidani na vipesa vya akiba vya wake zetu. Ikizidi sana huiba vifaranga ili kuuza na kupata lau mnuso.
Nne, walevi wa kanywaji wakiiba vitu vidogo vidogo kama vile vidani vya wake zao, wale wa politiki huiba madini hata majumba na ardhi.
Mara hii mmewasahau walevi wa politiki walioiba nyumba za walevi wakagawana na kudai watajenga nyingine! 
Uliza hizo zilizojengwa ziko wapi na kama zilijengwa ziligharimu kiasi gani cha walevi?
Tano, wakati sisi tukiiba vifaraga tena vyetu vyenyewe, walevi wa politiki huiba wanyama mbugani kwa njia ya ujangili na wakati mwingine huuza hata wakiwa hai.
Mara hii mmesahau jinsi majambazi haya manono yalivyoiba wanyama wenu yakanajisi hata uwanja wenu wa ndege kwa kupitisha wanyama hai kwenda Umangani!
Nani anaongelea huu ujangili tena? Nani anayakamata haya majangili yaliyoshirikiana na jangili la kigabacholi yakavusha wanyama hai kupitia Kia? Sisi hujiibia vijisenti tena vya ugoro.
Yenyewe yanaiba kuanzia EPA hadi Richmonduli na kuendelea kujikausha kana kwamba hayajulikani wala hayahusiki.
Sita, sisi hujivutia bangi na kunusa bwimbwi kidogo wakati yenyewe yakiingiza na kutoa tani za madawa hayo tena wakijenga mijumba ya bei mbaya na wengine kutumia uchache utokanao na bwimbwi kuingia kwenye siasa ili wafanye zaidi.

Kwani hamjui siri ya kushindikana kuwakamata wauza bwibwi? Nani amkamate nani iwapo kambale wote wana sharubu?
Saba, sisi hatuwauzi wake wala watoto wetu tofauti na wao. Je! walevi wa politiki wanafanya nini? Wanawauza walevi mchana kweupe tena wakiwahadaa kuwa hayo ndiyo ‘better life for all while it actually is worst life of all’.
Tena wanauza hata vizazi vijavyo kwa ‘just ten percent of’ rushwa.
Nane, sisi walevi wa mataputapu hupenda mapupu na utumbo na finyango kidogo.
Walevi wa politiki hupenda salala ukiachia mbali kupenda mashangingi ya kibongo na ya Kijep ya Ujapani.
Hamkuwasikia mjengoni wakizodoana kuwa kila mtu ana chakula pale? Hamjaona vimwana wanaoibuka ‘from the blue’ na huishiwa na ‘Foundations’ za uongo na ukweli?
Kama bi Mkubwa wa WaMa anakula kwa njia hiyo, kwanini wadogo zake nao wasifaidi?
Wenzetu kwa kulewa politiki na mashangingi sina mfano! Hamkuona juzi mashangingi ya kisanii yakijiweka karibu na wao ili nayo yafaidi ulaji wa kishangingi na kishankupe wa kula bila kunawa kwa mikono miguu na hata mikia?
Hamkuyaona mashumbwengu, machangudoa, machangupaka na machanguchangu chakachua cha wenzangu ya kike na kiume yakijiweka karibu na mibaka na walevi wa kipolitiki ili yatufaidi?
Tisa, sisi walevi wa mataputapu tunajivunia elimu yetu ya kupayuka. Waulize wale wa politiki wanajivunia nini zaidi ya kuibaka hiyo elimu na kuiharibu kiasi cha kukosa maana?
Shukuruni Kawa-dog upo hapo? ‘Thank Lord’ mshirika wako Phil Muongo Mulugoo goo goo ame-go.
Atokomee mwana kutokomea. Nawe mshukuru mshikaji wako ambaye ameamua kutumia uswahiba wenu kuua elimu kama alivyowahi kusema Dokta Silaha.
Hata hivyo, mnajali nini na mnaogopa hasara gani iwapo viegemezi vyenu vinasoma ughaibuni na vingine hata kughushi huko?
Siku hizi kughushi ni dili. Faza na Maza wanaghushi hata watoto na wajukuu na vitukuu.
Kweli mbigiri huzaa mbigiri na mafisadi huzaa mafisi na mafisadi!
Acha niwahi kwenda kuwasuluhisha Malisera, Makambaaa, Makondaa Mshindwayi na Mjega wanaovuana nguo wakigombea maslahi uchwara ya mitandao ya ulaji wa dezo ya urahisi.
Naenda kuwapa ‘fwact’ kuwa wakiendelea kuvuana nguo kwa maneno tutawavua nguo kimakwelini na kitakachowakuta wasitulaumu.

Wajua nini kitawatokea? Si umma utawaona kuwasanifu na kuwacheka!
Chanzo: Nipashe Jumamosi Feb., 8, 2014.

6 comments:

Jaribu said...

Hata Dakta Unasemaje? hanywi, lakini madhara yake ni makubwa kuliko ya walevi. Yeye na mke wake hawanywi lakin i wamesababisha hasara nyingi kwa taifa kuliko walevi wengi "combined."

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Dakta yumo kwa sana. Anakunywa sana. Tofauti na walevi wa kanywaji yeye anakunywa tu-blood. Blood suck so to speak. Anavyotumia njuluku za walevi huku wao wakiteketea what do you call that kama siyo bloodsucking? Huwa sipendi kumwita dokta kwa sababu siku nitakapokuwa dokta wa kweli sitaki nifananishwe naye. Jaribu una vituko. Unasema mke wake hanywi? Mbona anakunya kanywaji aina ya WAMA sawa na kale ka EOTF kama mama kidhabu aitwaye Anna Tamaa Mkapa Makapu? Nakumbuka tukiwa sekondari tuliwahi kuigiza mchezo unaoitwa "TUNAKULA MAITI" tukiipiga vijembe serikali ya mzee Mchonga zama za Salim Ahmed Salim akiwa waziri mkuu soon baada ya kuuawa Sokoine kwenye mazingira yenye utata. Hivyo wenzetu nao wanakula maiti sema maiti wenyewe wanaotembea. Naona tuachie falsafa ya kanywaji hapa.

Jaribu said...

Huwa namwita Dakta kwa sababu sitaki kumwita jina ambalo linamfaa, kama "juha". Lakini labda unaweza kupata faraja ukizingatia kuwa hata waganga wa kienyeji nao wanaitwa Dakta. Labda ungemouonea huruma Dakta wa kweli Jane Goodall alipokutana na Dakta Bandia Msoga. Wapambe wake kama akina Michuzi wako, "hapa ni Dakta Kikwete akiwa na Dakta Jakaya Mrisho Kikwete." Kama wanavyosema ndugu zetu weusi hapa, "Negro Pleaase!!

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Alaa! Sasa nimekuelewa. Najua hata kumwita dakta pekee kwa mtu ambaye anajua maana ya udaktari wa heshima ni dharau tosha. Hao uliowataja bila kuramba matako na viatu vyake hawawezi kupeleka mikono kinywani. Hata hivyo, tusiwalaumu hasa watu vihiyo ambao bila kujikomba watakufa njaa. Kwa wasomi wa kweli elimu maana yake ni uasi dhidi ya uovu. Kwa vihiyo hata wenye shahada za juu kama Rweyependekeza elimu ni ujanja wa kujikomba na kupata mlo toka kwa juha au muung mtu yeyote.
Acha niishie hapa nikingoja kusikia dakta Salma Kikwete hivi karibuni.

Jaribu said...

Dakta Salma Kikwete? Hiyo inaweza imkafanya mtu ukafanye "hara-kiri!"

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

hara-kiri imeshindikana kwa akina Madabida, Chenge, Idris Rashid, Lowassa, Said Mwema, Mkapa, Kikwete, Anna Mkapa, Mwinyi, Mzuzuri, Malima, Makamba, Msekwa, Mungai, Kawambwa aka kawadog, Balali, Rostam na wengine wengi walioasisi na kutenda ufisadi itakuwa kwa huyu kihiyo wa kuhurumiwa?