The Chant of Savant

Wednesday 25 June 2014

Kijiwe chalaani kaya kugeuzwa Matonya

BAADA ya kugundua ukweli mchungu kuwa libajeti la kaya ni mazabe matupu kutokana na kucharara, licha ya kukaa kama kamati ya kunusuru na kurejesha heshima ya kaya, kijiwe kinalaani kwa nguvu zote hali hii ya kujitakia tokana na ombwe la watu makini kuongoza. Baada ya uongozi kugeuka uongo, kijiwe kilijua hali hii itatokea.
Mpemba anaingia akiwa na gazeti la TZ Daimu na kusema; “Tulisema kuteuliwa Sada Mkuyati kuna namna hasa wizi wa njuluku wallahi.”
Mgosi Machungi anadakia; “Yakhe bado umemng’ang’ania Sada Mkuyati siyo? Hata angeteuliwa Maaika, kwa vie genge la ujambazi ni lile lile, njuuku zingeibiwa hasa ikizingatiwa mwakani tina uchakachuaji. Lazima wezi washinde kwa kununua, kuhonga, kuchakachua hata kuvuuga. Hujui!”
Msomi Mkatatamaa anadakia; “This is too much. It is even more than too much. It is perilous, lugubrious, cantakerous and rubiginous. Loh! Nimechanganya kikameruni tokana na hasira.” Anaomba msamaha na kuendelea; “Kila mwaka upuuzi ule ule. Hakuna kinachonikera kama kugundua kuwa kaya imefilisika wakati viongozi mufilisi walioifilisi wakiendelea kutajirika wakitanua na kukufuru. Kama hakuna njuluku, wanayotanulia kwenye ziara, matamasha, posho za makalio na hata sherehe zisizo na kichwa wala mguu zinatoka wapi?”
“Msomi usitoneshe donda. Nikikumubuka ufujaji kwenye sherehe za muunganiko wa vitisho vya geshi sina hamu. Tatizo si kufilisika kifedha bali kimawazo. Tatizo ni vipaumbele. Hamuijui Danganyika nini? Si waende pale WaMA na EOtF wakakope kama wamefilisika?” Mijjinga anaamua kukandia.
Mheshimiwa Bwege anakatua mic; “Nyie hamjui. Hawa jamaa hawajawahi kuwa na shida ya njuluku bali wehu na matumizi mabaya ndivyo vinavyowasumbua. Hivi kaya yenye madini mbuga za hayawani, ardhi, mito, milimia, mabonde, wachovu, maji, jua, ndege na kila kitu inaweza kuwa kapuku hivi au ni kujitakia kutokana na uvivu wa kufikiri ulioanzishwa na Tunituni Ben Makapu aliyeuza kaya kwa zawadi ya pipi, suti na upuuzi mwingine? Hata vijikaya vidogo vinatucheka na kutuchezea tokana na utaahira wa wakuu wetu! Mwalimu, uko wapi?” Anaangua kilio.
“Mheshimiwa Bwege leo umeongea sina hamu. Kumbe ubwege wako si wa jina bali utani ambao unaweza kumaanisha kinyume!”  Mipawa anadakia.
“Mie Mswahili ati.  Sisi hufunga nyama au kufumba asiyekuwa Mswahili asielewe. Twaweza kukukuteta usijue tumekuteta. Naweza kusema kitu ukaishia kukielewa kinyume sawa na jina langu. Kama mabwege basi mwawajua tena sana, hasa wale wanaopewa dhamana wakaichezea na wale wanaowapa dhamana waichezee ila si mie mwanakwetu.” Bwege anajitetea huku akitabasamu kwa kusifiwa.
Sofi Lion Kaungaembe anakatua mic; “Bwege huna haja ya kutukana watu kwa vitu vya kichochezi. Mmeambiwa sirikali haina njuluku mwang’ang’ania ipo ipo wapi?”
Kapende hangoji wengine waseme. Anakwanyua mic; “Njuluku ipo na ipo Banki Kuu ndiyo maana akina Mkuyati, We-remaa, Maswie, Ndururu, Mwongo na wengine wameweza kukwapua bilioni 200 bila kufikishwa kwa pilato kwa sababu kuna njuluku kibao za kuchota kule au vipi. Najua hawawezi kufikishana kwa pilato kwa vile wamekatiana.”
“Ati wamefanya nini?” Anauliza Mchunguliaji. Kapende anajibu; “Wamekatiana baina ya wezi na wale waliowatuma kufanya wizi huo kwani siri? Hata Takokuru inajua ila kwa vile wote lao moja hakuna wa kumshughulikia mwenzake.”
Mijjinga anakatua mic; “Usemayo kweli Dokta Kapende. Kusingekuwapo njuluku Matonya wetu mkuu na bi mkubwa wake na waramba viatu wao wasingekesha kwenye madege wakizurura na kutanua ughaibuni. Nashangaa mwaka huu hajaenda Brazil kuangalia kipute cha world cup. Angalia hata suti anazovalia ukiachia mbali siku nyingi anazolala kwenye mahoteli ya nyota tano majuu. Nadhani tatizo hapa ni kukosekana mtu mwenye akili timamu na uzalendo kuongoza kaya. Period.”
Mzee Maneno aliyekuwa kimya muda mrefu anakatua mic; “Huyu jamaa mwisho. Kombe la Dunia halijaisha. Anaweza kutafuta kisingizio akaenda kule kujinoma kama kawaida yake.”
Mpemba kama kawa anarejea; “Njuluku wanayo Wallahi tena kwa sana. Angalia mishangingi na mishumbwengu ya kijep wanioendesha huku wakihonga mishangingi ya kayani malaki kama tulivoona Jonii Kombo akila mavituz ya kijibinti tena kidogo kuliko bintiye. Hawa jamaa wachafu kweli kweli!”
Msomi anadakia; “Nadhani wameathiriwa na mchezo wa kuomba. Kama hakuna njuluku mbona wanasamehe kodi wachukuaji ambao kila mwaka wanaondoka na mabilioni ya dola? Hawa ni wapuuzi wa kawaida ambao ujuha wao ni sawa na yule kenge juha ambaye alinyewa mvua akaamua kukimbilia mtoni asijue yapo maji mengi. Kimsingi, wanachoomba si chochote wala lolote bali mabaki ya njuluku wanazoachia. Mwalimu aliwahi kusema kuwa uchumi wanao ila wanaukalia. Huwezi kutapanya njuluku kwenye upuuzi halafu ukaanza kulalama na kuomba kama hamnazo. Lazima uwe hamnazo.”
Mipawa anadakia; “Msomi hujakosea. Umesahau. Kama hakuna njuluku mbona baadhi ya vigogo wanahamishwa na kukaa hotelini huku wilaya na mikoa mipya ikifinyangwa kukidhi matakwa binafsi ya marafiki zao? Nasikia jamaa wanatumia kisingizio cha kubomu kujilipa njuluku na kwenda ughaibuni kuweka njuluku Uswizi na kukagua akaunti zao.”
Kanji ambaye alikuwa kimya muda mrefu anaamua kula mic; “Kama kuu hapana kaa hoteli biashara ya hoteli taumia. Veve hoji sana juliku ya siri kali kwani ya veve?”
Msomi anakwea mic kwa hasira wazi wazi; “Siku zote nilidhani Kanji umesoma kumbe bomu tu! Hujui kuwa bila mimi kulipa kodi hiyo siri kali inayowapa kiburi haina lolote? Hujui kuwa malalamiko ya Sada Mkuyati kuwa hakuna njuluku yanalenga kupata kisingizio cha kupandisha kodi ambayo itafanya kila kitu kipande na maisha kuwa kichwa chini miguu juu japo yamekuwa hivyo kwa zaidi ya miaka thelathini? If you can’t get such simple issues there is no difference between you and the govt and its head and tails.”
Kijiwe kikiwa ndiyo kinanoga si likatokea shankupe la kijep na shangiki Mkuyati. Acha tulitoe baruti! Tungemnyaka, tungemfanyie kitu mbaya.
Chanzo: Tanzania Daima Juni 25, 2014.

No comments: