The Chant of Savant

Wednesday 31 December 2014

Kijiwe chalaani mizengwe ya escrew


          Leo Msomi amejilawa kweli kweli. Anaingia akiwa ameweka ndita usoni huku akiwa amevaa magunia. Leo wanakijiwe wote wametinga kwenye magunia, kwa mara nyungine, kama alama ya kuombolezea kaya yetu inayoliwa huku ikiojiona.
          Msomi hata aamkui zaidi ya kumwaga usongo wake. Anakwanyua mic na kuchonga, “Wapendwa, kwanza najua mna majonzi kama yeyote ambaye si fisadi wala nepi yao. Pili, najua mna maswali mengi kuliko majibu kuhusiana na usanii na ujambazi vilivyotokea. Tatu, najua mnalaani jinai yote tena kwa herufi kubwa.  Nne, hebu tujifariji kwa lau kufanya kile ambacho wataalamu wa utatuzi wa migogoro yaani Conflict Resolution Studies professionals huita venting au kumwaga usongo. Je mnakielezeaje kigwena cha tarehe 21 Desemba baina ya Njaa Kaya na wazembe wa  Dar si Salaama?”
          “Yakhe wantibua sasa. Unfurahisha ulipoita ule mkusanyiko kigwena. Ungeongeza: kile kigwena cha kuhalalisha haramu na ujambazi kayani wallahi. Sijui hawa watu wameingiliwa na nini! Wafanywe nini na vipi ndiyo wakengeuke wajue wakati wabadilika?”
          Kabla ya kuendelea Mgosi Machungi anampoka mic na kuronga, “Hakuna kitu kiiniumiza kama kuona wae wote walioiba njuuku yetu kuwekwa eti kipoo utadhani ni ughai. Yaani huyu anadhani kumtoa kafaa poofwesa Ana Kajuamlo Tiba atatuliza mizuka yetu? Lazima tikubaiane jinsi ya kuwashughuiikia hawa wezi.”
          Mijjinga ananyakua mic, “Yule mama aliniudhi kuitisha mkutano wa waandishi wa umbea na kujitapa eti hakuwa na hatia na hivyo asingewajibika kwa kuhofia eti kutoitendea haki dhana nzima wakati alinuka na kuchafuka kulhali. Kusema ukweli nimefarijika kuona alivyotimuliwa kama mbwa koko. Halo halo nenda Ana nenda tu wala usilalamike.”
          “Hapa ndipo Njaa Kaya kawapiga wadanganyika changa la macho. Hukuona watumiwa wazembe wa Dar walivyolipuka kwa shangwe wasijue wanashangalia maafa yao. Shame on them all! Yaani tumekubali kafara ya ngurumbili moja wakati kuna mamia nyuma ya pazia!” Anazoza Mipawa.
          Kapende anapoka mic, “Inashangaza pamoja na unshomile na uporofwesa wake hakuliona lililokuwa likimjia ukiachia mbali kutumiwa na mafisadi kama nepi na zana. Kwanini hakujinyamazia kama kondoo akangoja kuliwa huku akitulia tuli kama alivyotulizwa na Jimmy Rugemalayer ambaye alimchengua hadi akampa vijisenti vya ugolo?”
          Mbwamwitu anadandia mic na kupayuka, “Huyu bi mkubwa kiboko! Anamchengua fisadi hadi anamkatia bilioni na ushei! Sijui alimfanyia vituz mtindo upi tapeli huyu hadi akamzimia hivyo! Hata hivyo namuona mjanja. Maana huo mshiko ni mkubwa kuliko hata marupurupu ambayo angepewa baada ya kumaliza ngwe yake kama waziri.”
          “Nyie hamjui, nyuma ya pazia yanafanyika mambo hadi watu wanakatiana mishiko mizito. Nisichoelewa hadi sasa ni mantiki ya kuweka wezi wakubwa viporo. Je huyu bibie kaponzwa na kiranga chake cha kujifanya anajua falsafa hadi akanonihino bila kuchamba au ameisuka na bingwa wa sanaa ili kuokoa jahazi? Maana hakuna anayeongelea tena zile bilioni 400 wala kushinikiza mibaka husika inyongwe kama siyo kuvuliwa nguo na kufanyiwa kitu mbaya.” Anazoza Mipawa huku akiwasha sigara kali.
          Kanji kapata upenyo. Anakula mic, “Pawa veve kosea sana. Hapana pendekeza vatu fanyia kitu baya venzao. Hii si tawala ya sheria.”
          Kapende anamkwapua mic Kanji na kuchonga, “Peleka tawala yako ya sheria India. Wewe unaona kuhalalisha ujambazi na ushenzi ndiyo utawala wa sheria? Utawala wa sheria ilikuwa ni kuwanyonga hawa gendaeka lau tupumue. Maana wamezidi.”
          “Nani amnyonge nani wakati wote ni nyani wakifanya unyani wao? Nadhani huyu mama nshomile ameponzwa na domo lake kuongea bila kuwasiliana na kichwa. Jitu limepokea mshiko wa wizi tena kwa kutoa huduma chafu halafu linasema eti halioni kosa.” Msomi anaongea kwa hasira.
          Kabla ya kuendelea Mheshimiwa Bwege anachomekea, “Msomi una maana bi mkubwa alimkatia mavitus Jimmy na Jimmy akaamua kumkatia pochi siyo?”
 “Who knows? Lolote lawezekana hasa ikizingatiwa kuwa bi mkubwa ni open check usawa huu? Maana katika tambo zake zote za kutowajibika hakutaja mshiko wote mzito kama huo alipewa kwa kazi gani. Bila shaka ni kazi ya siri isiyopaswa kujulikana.” Msomi anajibu huku akijiweka vizuri kwenye benchi.
          Sofia Lion aka Kaungaemba kashika pabaya! Anamnyang’anya Msomi mic kwa hasira na kuzoza, “Una ushahidi na unachosema au unadhani wote ni kama wewe kuvutiwa na mambo ya nguoni?”
          “Kama unataka ushahidi nenda kawaulize waliokatiana. Kama si hivyo mbona wahusika hawataji walilipana nini na kwanini?” Mzee Maneno anaamua kumjibia Msomi anayebaki kutabasamu.
Kepende anapoka mic mic na kusema, “Nadhani dada Sofi anajiumiza bure. Hivi yeye angeahidiwa njuluku lukuki hivi angebania?”
          Msomi huku akicheka anachomekea, “Muulize Sofi. Nadhani analo jibu.” Baada ya kuona Sofia amekaa kimya Msomi aliendelea, “Mie hakuna waliponiacha hoi hawa mafisadi kama kumtoa kafara porofwesa na kuwaacha wezi wenyewe wakitanua. Nani anahimiza Muongo, Ndururu, Mkuyati, Endelea Chenge hata Njaa Kaya wawajibishwe wakati ndiyo wenye dili zima? Tungeachana na dagaa kama Porofwesa na kuwashughulikia papa hawa kwanza ingeleta maana.”
Kijiwe kikiwa kinanoga si alikuja Ana Kajuamlo Tiba kutuhutubia akitubia. Tulimkamata na kumpeleka kwa Rugemalayer akamtulize na kumkatia tena.
Chanzo: Tanzania Daima Desemba 31, 2014.

No comments: