The Chant of Savant

Wednesday 21 February 2018

Kijiwe chalaani siasa za kijambazi na mauaji

Image result for photos of akwiline akwilina
Marehemu Akwiline Akwilina aliyeuawa na risasi iliyofyatuliwa na polisi wakati wa kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge jimbo la Kinondonni.
            Wahenga walinena kuwa hakuna kisichobadilika chini ya jua. Baada ya mtindo mbovu wa siasa za kijambazi kuanza kuzoeleka, Kijiwe kimeamua kutia guu na kukemea na kulaani mauaji ya kisiasa yatokanayo na siasa za kijambazi kayani. Baada ya kutoka kwenye matanga ya Daniel John aliyenyotolewa roho kwenye mazingira ya kutisha, Kijiwe kimekaa na kudurusu nini kifanyike dhidi ya kadhia hii.
Mijjinga aliyekuwa rafiki wa marehemu ndiye anaanzisha mada ya leo “jamani wenzangu mnaongelaje mauaji ya vijana wawili hivi karibuni kwenye kampeni hizi zinazoendelea kwenye uchakachuaji wa jimbo dogo la Kinondo?”
“Yakhe wala usinkumbushe hili balaa la kujitakia litokanalo na uchumia tumbo, roho mbaya na unyama vya kutisha wallahi. Yaani kaya ya wapendanao ya mzee Nchonga na Karume yaweza kufikia hapa kiasi cha kutoana roho kwa sababu za ulaji wa dezo? Nalaani sana mauaji haya. Na nasema wazi kuna nkono na ntu hapa wallahi” analalamika Mpemba huku akionyesha wazi kuudhiwa na ujambazisiasa huu.
Mgoshi Machungi Shekiango anaamua kumpoka mic Mpemba na kuzoza “waivyontunduisu Issu niijua titajifunza jambo na kuanza kuheshimu haki za binadamu kumbe wapi? Hawa waionyotoa roho za Danie na yue binti wa chuo waaaniwe siku zote. Sijui ndata wanafanya kazi gani jamani? Mbona huko nyuma hawakuwa hivi?”
Msomi Mkatatamaa akiwa anajiweka vizuri kwenye fomu anampoka mic Mgoshi na kudema “mie tangu aliosokoiniwa Edward na kukolimbwa Horace, nilianza kuwasha taa nyekundu japo mauaji haya yalisimama kidogo tokana na mzee Mchonga kutoruhusu siasa za kijambazi na kuibia wachovu. Ila alipotundulisiwa Tundu, nilibashiri kuwa muonja hasali hachovyi mara moja.  Hivyo, hitimisho langu ilikuwa ni kwamba siasa tulizozoea kusikia kwenye kaya ya manyang’au zilikuwa zimepiga hodi kayani. Je wauawe wangapi ndipo tustuke kama jamii, kaya na watu waliozoea kupendana bila kujali dini, itakadi wala mafungamano ya kisiasa? Tulizoea kuwa mfano kwa wanaopingana kwa kuuana tokana na kupingana bila kupigana. Inatisha; lazima tuseme kwa sauti ya juu ili wahusika wajue tunajua kuwa wapo nyuma ya jinai hii uchwara itokanayo na siasa uchwara. Shame on them all.”
Kabla ya kuendelea Kanji ambaye siku hizi ametokea kuwa msemaji anakula mic “hii iko umma sana. Moyoni yangu naona chungu sana. Kama naveza naveza toka na bundiki yangu kwenda saka jambazi yote na kumalizia mbali. Kwanini naleta siasa ya tumboni kwa kaya salama kama yetu? Mimi iko taka data yote fukuzwa kazini kama nakuta inazembea na kuacha vatu nauawa kama nyama ya mwituni.”
Kapende anaamua kutia guu na mapema “mimi sishangai haya yanayotokea hasa nikiangalia namna ushindani wa kisiasa za ulaji ulivyogeuka mtego kwa wachovu wetu wapendao kula dezo. Hukusikia mjalaana mmoja akikufuru kuwa anampenda mwanaume mwenzake ni balaa asijue tafsiri itakuwa tofauti? Ukisikia siasa za kijambazi ndizo hizi. Sijui hawa wanaotuaminisha kuwa wanataka kututumikia na si kututumia watamuongoza nani wakati wanaanza kunyotoana roho? Je ni kwanini wanene wamefumba macho na kuziba masikio kana kwamba wanaonyotolewa roho ni mbu au mbwa? Baya zaidi wanatuaminisha kuwa wanatupenda wakati wanatuponda na kutunyotoa roho tokana na kutofautiana mawazo na misimamo. Je tutaendelea kuingizwa nkenge hivi kana kwamba sisi ni hamnazo? Napendekeza tuandamane kwenda sentro lau wajue tunaudhiwa na ukosefu wa usalama uliotamalaki sasa.”
Mipawa anaamua kutia guu “mna habari huyu binti aliyepigwa shaba juzi ni mtoto wa rafiki yangu? Sasa kama mchovu anakwenda kwenye mihagaiko yake usawa huu wa vyuma kubana anakuwa na wasi wasi kama atarudi salama, haya maendeleo tunayoambiwa yanataka kuletwa ni kwa ajili ya nani? Kwanini tunaendekeza siasa za chuki na woga bila sababu za msingi zaidi ya tamaa ya kutaka ulaji ili kula dezo? Kama tunakuwa wakweli, pale Kinondo kuna sababu ya kuuana wakati wagombea wanaotaka kuwatumikia wachovu na wanaotaka kuendekeza njaa wanajulikana?”
Kabla ya kuendelea kudema, Mzee Maneno anakula mic “kusema ule ukweli, mauaji ya juzi yamenitisha, kuniudhi na kunidhalilisha kama mwanakaya wa kaya hii iliyosifika kwa amni yake ambayo sasa tunaichezea. Hivi pakichimbika bila jembe tutakimbilia wapi wakati majirani zetu wote walishaharibikiwa?”
Kabla ya kumaliza, Mbwamwitu anajibu kwa kebehi “huenda tutakimbilia bahari ya Hindi ili nyangumi na papa watutafune kama zawadi ya uovu wetu. Nadhani roho za akina Sokoine, Kolimba na Mwangosi zinatulaani na kutuandama. Maana tumejigeuza majuha na wauaji tusijue fika kuwa matokeo ya kupanda mbigiri kuwa ni kuvuna mbigiri hizo hizo.”

Kabla ya Mbwamwitu kumaliza, da Sofia Lion aka Kanungaembe anajiimbia wimbo wake “amani kaya ya amani. Mnachezea amani ili kupata shari siyo? Mnaimba amani na kuborosha maisha wakati mkiharibu na kunyang’anya maisha. Mauaji ya kisiasa yazuiliwe yasigeuke kansa itakayoteketeza kaya. Wanasiasa huja na kuondoka lakini kaya siku zote itakuwapo. Wauao watauawa na wakoao wataokolewa. Kila aishie kwa upanga ajue atakufa kwa upanga. Vibaya hivyo ndugu zangu vibaya hivyo nasema achene kunyotoana roho kwa mambo ya muda ya kidunia.” Kabla ya kuendelea anazidiwa uchungu na kuzimia kiasi cha Kijiwe kuishia hapa ili kumuwahisha hospitali.
Chanzo: Tanzania Daima. Feb., 21, 2018.

No comments: