The Chant of Savant

Wednesday 21 March 2018

Kijiwe chaipongeza Sauzi kwa kumshitaki Xuma

          Baada ya Mpayukaji kurejea kayani akitokea Sauzi alipokwenda kutetea na swahiba yake mkuu rais mpya Matamela Rama, alitoa taarifa kwa kijiwe kilichoamua kutia neno kwenye kile kinachoendelea kule Sauzi. Hii ni baada ya Mpayukaji kukitonya kijiwe kuwa dingi wa zamani wa Sauzi Jack Xuma angefunguliwa mashtaka ya ufisadi na utumizi mbaya wa mamlaka ya kaya. Kijiwe kimeipongeza Sauzi kwa kufanya maamuzi magumu usawa huu.
Baada ya kumaliza kutoa taarifa, Mpemba anakula mic “Yakhe kwanza nkupongeze kwa uchambuli ulo wa kina na kisayansi kuhusiana na sakata la uoza kule Bondeni. Nakushukuru sana. Kwani, ninapoongea, ndo vyombo vya habari vya Bondeni vyatanza Xuma atafungliwa mashtaka wakati kijiwe kilishazinyaka tokana na uswahiba wako na rais Rama.”
Kapende anakatua mic “mie sishangilii hasa nikizingatia Wasauzi wanavyochukia wageni tena tuliowapa tafu kwenye kudai uhuru wao. Sishangilii kwa vile mie siyo Msauzi. Nitashangilia siku Xuma wetu wakifanyiwa kama kile alichofanyiwa Xuma mwenyewe ingawa mechi yenyewe ndiyo inaanza. Tutajuaje kama hataachiwa?”
Kabla ya kuendelea, Msomi Mkatatamaa anampoka mic na kuronga “hapa kwetu usitegemee kitokee hiki hasa ikizingatiwa kuwa ulaji wetu ni wa kurithishana tofauti na Bondeni ambako rahis Rama alimpiga mweleka mshirika wa bedroom wa Xuma Nkosizile aliyetaka kurithishwa na mumewe. Hivyo, hizi ni cases mbili tofauti ndugu yangu. Hata hivyo, kitendo hiki cha kumfungulia mashtaka Xuma, kitatoa somo kwa wezi wetu wenye mamlaka kuwa mambo huwa yanabadilika na aliyesimama aangalie asianguke. Hawa wetu we wape time. Kuna siku watalipa; na kama si wao wake zao, watoto wao wa wajukuu zao. Kulipa ni lazima. Wasipolipa wao angalau Mungu ataingilia kati na kuwatia magonjwa na kashkash nyingine wasiishi kufaidi njuluku zetu.”
Kabla ya Msomi kuendelea, Mipawa anapora mic na kuzoza “nakubaliana nawe ingawa si kwa kila wazo hasa ikizingatiwa kuwa mambo huenda yanabadilika. Kuna siku iso jina itatimu makaburi aliyokataa kuyafukua dingi yatafukuriwa tu na mifupa na uozo wao vitajulikana. Hata hivyo, kuna siri gani kuwa Xuma wetu walipiga njuluku zetu? Nani hajui? Dingi anajua na hata ndege na wadudu wanajua achia mbali waja kuwa wajalaana hawa walipiga. Kuna siku nao watapigwa tu hata kama si chini ya zama hizi za ukondakonda na ugufu..ugufu.. We koma!” Msomi anajionya na kuachia mic.
Mgoshi Machungi wa Shekiango mwana wa Mashindei anaamua kula mic “Msomi hapa umeniacha hoi uiposema ugufu gufu bia kumaiza. Kwa ukonda konda na nakubaina nawe kuwa waiozoea kupiga sasa wamekonda kama Xuma ambaye bia shaka atakuwa ameishaanza kukonda kama siyo kuonja joto ya uRamaphosa. Kama aivvyosema Kapende, natamani Xuma wetu nao wabatizwe kwa moto na siyo kuendekezwa wakati wachovu wetu wakiendeea kutesaka tokana na wizo na upumbavu wao.”
Kanji ambaye ametokea kuwa msemaji siku hizi anakwanyua mic. Anasema “kama Juma nakula juluku ya Sauzi sasa sirkali fanye kila naweza kutoa juluku kwa fuko hata tumboni yake. Mimi iko chukia sana hii Juma namna nadhalilisha vanavake. Nakumbuka kasfa ambapo Juma natembea na toto ya rafiki yake na kuambukiza yeye kimwi.”  Kabla ya kuendelea Mbwamwitu anamkosoa Kanji “Kanji ni Xuma siyo Juma dugu yangu.”
Kanji anaendelea “mimi hapana ona tofauti kwa jina ya Swahili. Juma na Zuma yote dugu moja sawa na Mahindra na Mahondra kule Bombei. Yote ni gabacholi.”  Kijiwe hakina mbavu namna Kanji anavyoanza kukubali jina la gabacholi.
Gau Ngumi aka Linungaembe ambaye ni mwanakijiwe mpya na shoga na swahiba yake Da Sofia Lion aka Kanungaemba anakula mic “hata mimi simpendi huyu baba hasa tokana na ukware na ufisadi wake. Jamaa ana tamaa. Kila mwaka lazima aongeze mke. Sijui Wasauzi walikuwa wamekunywa kanywaji gani hadi kuruhusu mharifu kama huyu kuwa dingi wao!”
Kabla ya kuendelea, Mijjinga anamkumbusha “unashangaa Wasauzi badala ya kujishangaa. Mbona nyinyi mlibambikwa bonge la Msanii Njaa Kaya na kinyago cha mpapure Denjaman Wasauzi wasiswashangae? Umesahau kuwa siasa za uswazi zinakwenda kiswaziswazi na waswahili wote bara zima wote ni sawa inapokuja kwenye kubambikizwa au kubambikana mikenge?”
Kabla ya kuendelea Mpemba anakula mic “yakhe kubaliana nawe wallahi. Kwani huyu Zuma ana makosa gani makubwa tofauti na yale walotenda akina Xuma wetu? Kama kuchezea na kunajisi patakatifu pa patakatifu na wetu walifanya hivo. Kama ni kuuza kaya kwa akina Gupta nasi wetu waliuza kwa mabwana zao hata kama si magabacholi kama hawa wa Xuma. Kwa taarifa yako, kambale wote eti wana sharubu.”

Kijiwe kikiwa ndiyo kinaanza kuchanganya si ukapita msafara wa Xuma wetu ukielekea kwenye maonesho ya KumiKumi. Acha tuutoe mkuku huku tikimwagia mashangingi maji machafu yakisindikizwa na mawe. Kama si ndata kutuzidi nguvu tungenkamata na kumfanyia kitu mbaya huyu mjalaana.
Chanzo:  Tanzania Daima leo Machi 21, 2018.

No comments: