
Ni ajabu kidogo kwa watu wenye akili kukimbilia kuchota mafuta huku wengine wakiwa wanavuta sigara ukiachia mbali kutochelea kuwa unaweza kutokea mlipuko na kusababisha maafa kama yaliyoshuhudiwa Morogoro. Pamoja na ujinga na umaskini, pia ujinai na roho mbaya vinachangia kadhia hii. Kabla ya kuchukua hatua ya kwenda kuiba kwenye chombo kilichopata ajali, jifikirie. Je ningekuwa mimi mhanga ningependa nitendeweje? Isiwe mkuki kwa nguruwe kwa binadamu mchungu. Ni jambo la aibu kwetu kama taifa kuendelea kuthamini udohoudoho kama huu kiasi cha kuhatarisha maisha ya wengine. Tunatoa mkono wa rambirambi kwa wafiwa tukiomba wawe ni mabalozi wazuri wa kuelezea kadhia hii ya kutumia ajali kama fursa ya kujipatia kipato. Tusiogopane kuambiana ukweli. Kwani kufanya hivyo ni maafa zaidi ya haya tunayoshughulikia. Inabidi, kama taifa, tukemee vikali tabia hii ya maangamizi ya kujitakia.
No comments:
Post a Comment