The Chant of Savant

Friday 16 August 2019

Kanada Marekani na Uingereza Hawana Udhu wala Sifa ya Kutufundisha Haki za Binadamu

     Image result for photos of the flags of canada UK and USA    
          Hivi karibuni, kumekuwapo na sintofahamu kuhusiana na haki za binadamu nchini Tanzania hasa baada ya kukamatwa kwa mwandishi mmoja wa habari. Hakuna anayeuunga mkono ukiukwaji wa haki za binadamu. Hivyo, mataifa tajwa hapo juu, kupitia mabalozi wao, yalitoa shutuma dhidi ya serikali ya Tanzania kuhusiana na kile yanaochokiona kama ukiukwaji wa haki za binadamu. Kukemea ukiukwaji si wa haki za binadamu tu bali chochote kinachofanana na hiki ni jambo bora. Cha msingi, anayefanya hivyo, asiwe na ajenga zake za siri kama ilivyo kwa mataifa tajwa ukiachia mbali ukweli kuwa nayo yamekuwa yakikiuka haki za kibinadamu tena si taifa moja bali mengi duniani kwa miaka mingi.
       Kwa ufupi, Kanada imekuwa ikitekeleza mauaji ya kimbari dhidi ya wakazi wa asili wa taifa hili ambao hujulikana kama First Nations, Aboriginals na majina mengine. Kwa wanaoishi Kanada, wanajua ni hali gani watu hawa wamekuwa wakiishi kuanzia kunyang'anywa watoto wao na kupelekewa kwenye makambi ya mateso yaliyoitwa  residential schools ambamo waliteswa, kubakwa, kuzuiwa kuongea lugha zao, kuabudu dini zao, na mambo mengine. Pia wazazi wao hadi sasa wengi wanaishi kwenye maeneo tengefu yaitwayo reserves. Kama haitoshi, weupe walinyakua ardhi ya watu hawa wa asili kiasi cha kuteketeza mawindo na maeneo mengine yaliyokuwa yakizalisha chakula chao. Walivuruga utamaduni na maisha yao kiasi cha kuwageuza makasha ya kile walichokuwa kabla ya kutawaliwa. Weupe walileta silaha nyingi za maangamizi ya kijamii kama vile madawa ya kulevya, magonjwa na pombe mambo ambayo yameharibu watu hawa ambao kwa sasa wamebakia kuwa asilimia 4.9 kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2016. Je kwa namna hii, Kanada ambayo imetekeleza unyama huu kwa miaka 151 ina udhu kweli kwa kukemea kile inachokifanya tena kwa kundi kubwa la watu?
      Kila mtu anajua namna waingereza walivyotawala nchi nyingi duniani wakaziibia na kuziacha maskini huku wakitaka waendelee kuzitawala kwa mlango wa nyuma. Wanadai hakuna haki za binadamu, je wahamiaji wanatendewaje nchini Uingereza hasa watu weusi? Je Malkia wa Uingereza naye amechaguliwa kidemokrasia kuongoza taifa hili koloni na beberu? Je unajua kuwa ni uingereza hii hii iliyomuweka madarakani imla Idi Amin wa Uganda aliyeua Waganda akaishia kuivamia Tanzania akitaka kuchukua ardhi yake? Nani asiyejua kuwa mataifa haya licha ya kujua kuwa rais wa zamani wa Msumbiji , marehemu Samora Machel angekuawa na makaburu wa Afrika Kusini, yaliendelea kuwaunga mkono kulhali ili kuendeleza utawala wao wa kinyama na kibaguzi uliovunja haki za binadamu nchini humo kwa miaka mingi tu kabla ya kuondolewa mwaka 1997.
    Kwa upande wa Marekani, taifa lililojengwa kwenye misingi ya dhuluma na vurugu, wengi wanajua ilivyovuruga nchi za Afghanistan, Irak na sasa inanyemelea Venezuela. Marekani inasifika kwa kupindua marais wazalendo na walioonyesha kutaka kukata mizizi ya ukoloni kwa kulinganisha bara la Afrika kama vile Kwame Nkrumah (Ghana) na Patrice Lumumba (DRC). Je hawa hawakuwa na haki sawa na binadamu wengine? Je haki zinazovunjwa ni za makundi madogo kama vile waandishi wa habari, mashoga na wanasiasa tu wakati umma umeteseka kwa miaka mingi tokana na madhara ya ukoloni mkongwe na mkoloni mambo leo wakati hawa wanaojidai kutetea haki wakiwa kimya na ima kushiriki mateso haya au kuyanyamazia ukiachia mbali kuyashiriki?
      Kwa sasa, wakati Marekani ikihanikiza na kushinikiza Tanzania kuhusiana na uvunjwaji wa haki za binadamu kwetu, imo kitanda kimoja na maimla kama vile Paul Biya (Cameroon), Teodoro Obiang Nguema (Equatorial Guinea), Ali Bongo (Gabon) na wengine wengi wanaojulikana kwa uvunjaji wa haki za binadamu tena kwa muda mrefu.
   Kwa kuangalia rekodi za mataifa husika, kabla ya kupitisha hukumu, tunapaswa kujiuliza, je ni kitu gani wanachotafuta katika kelele zao kama siyo ajenda za siri? Kama kweli wanataka haki kwanini hawazitendi kwao tena kwa makundi makubwa ya watu na nchi?
Image result for photos of the flags of canada UK and USA and Tanzania

No comments: