The Chant of Savant

Wednesday 14 August 2019

Kiswahili Kitaendelea Kuwa Lugha ya Ukombozi wa Afrika

 Image result for photos of kiswahili           Pamoja na kuwa na baadhi ya maneno toka lugha nyingine za kigeni kama vile Kiarabu, Kiingereza na nyingine pia zenya asili ya Afrika kama vile Kishona, Kizulu, Kinyanja, Kibemba na nyingine, licha ya kuwa lugha yenye chimbuko lake Tanzania na lugha ya taifa pia, Kiswahili ni lugha ya Kiafrika inayopaswa kutumika Afrika. Tangu aingie madarakani, rais John Pombe Magufuli, bila kujali wakosoaji, hata waliomkejeli kuwa hajui Kiingereza, amesimama imara kukienzi, kukitumia na kukiuza Kiswahili duniani. Hivi karibuni waziri wake wa Mambo ya Nje Prof Palamagamba Kabudi alikaririwa akisema kuwa mawaziri wa Jumuia ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamependekeza kwa wakuu wa nchi kupitisha lugha hii kama mojawapo ya lugha zitakazotumika kwenye Jumuia hii. Lugha nyingine zote zinazotumika kwenye Jumuia hii ni za kigeni na kikoloni ambazo ni Kiigereza, Kifaransa na Kireno. Hivyo, kwa namna ya pekee, wakuu wa SADC ambao wengi wao ni matunda ya Kiswahili, tunawasihi na kuamini watapitisha ombi hili mara moja ili lau kutambua mchango wa Kiswahili na Tanzania kwenye ukombozi wa Kusini mwa Afrika.
        Mbali na kutambua mchango wa Kiswahili na Tanzania, Kiswahili kitakuwa lugha pekee ya Asili ya Afrika na ya Ukombozi kutumiwa na nchi wanachama. Hii ni njia sahihi ya kujikomboa (true decolonisation) ukiachia mbali kuondoa sumu ya ukoloni (detoxification).  Mbali na SADC, Jumuia ya Afrika ya Mashariki (EAC) ishakiridhia na kukitumia ukiachia mbali nchi kama vile Rwanda na Sudan ya Kusini kukitambua umuhimu wake huku Afrika ya Kusini, kwa kutambua mchango wa Kiswahili na Tanzania kwenye ukombozi wake kuamua kifundishwe mashauleni. Tunaamini. Kuna siku Kiswahili kitakuwa si lugha ya EAC wala SADC tu bali lugha ya Afrika. Na hili likitimia, Afrika itakuwa imeanza kupiga hatua kwenye ukombozi wa kweli.
    Ukiachia mbali na kuwa lugha ya asili ya Afrika, Kiswahili, kitawafanya Waafrika kujifunza na kukijua kirahisi kutokana na asilimia kubwa ya Waafrika kuwa na lugha zenye kufanana kitabia na kimuundo. Pia Kiswahili, kinaweza kuleta manufaa ya kiuchumi kwa Afrika kwa maana kwamba, fedha nyingi zinazotumika kutafsiri kwenye mikutano ya Kiafrika zitatumika kwenye maeneo mengine. Hata gharama ya kufundisha Kiswahili si aghali kama vile lugha za kikoloni ambazo bado Afrika haijazimanya vilivyo. Hivyo, kutegemea wageni kuwafunza watu wake wanaoshughulikia masuala mbali mbali. China, Japan, Urusi hazikufikia kwenye maendeleo yake kwa lugha za kikoloni. Korea pia kadhalika. Kwanini Afrika isiweze?

No comments: