The Chant of Savant

Saturday 26 December 2020

Tunamaliza na Kuanza Mwaka 2021 Bila Mkapa


Kwanza, kwa kipekee zaidi, tutume salamu na heri za Noeli na Mwaka Mpya 2021 kwa wapenzi wote wa safu hii pia tuwaalike katika kumkumbuka mzee wetu Benjamin William Mkapa rais wa awamu ya tatu aliyetutoka tarehe 24 Julai, 2020. Kifo cha mzee Mkapa kilitokea wakati safu hii haijarejea hewani. Tunaomba kufunga mwaka huu kwa: mosi,  kutoa salamu za rambirambi kwa taifa na familia. Pili, kama kumbukizi la mzee Mkapa, safu hii leo imeamua kudurusu namna atakavyokoswa hasa mwaka 2021 tunaotegemea kuanza  siku chache zijazo inshallah. Kwa tuliomfahamu mzee Mkapa kama gwiji la diplomasia na usuluhishi, kifo chake si pigo kwetu tu bali kwa nyanja ya diplomasia na usuluhishi Afrika na Duniani kote. Binafsi, mzee Mkapa alinisaidia mawazo wakati naanza kusomea shahada yangu ya uzamivu (PhD) kwenye masuala ya Amani na migogoro pale nilipomuomba anipe uzoefu wake. Hii ni baada ya rafiki na ndugu yangu mzee Pius Msekwa–––sasa ‘Daktari’, aliyetunukiwa shahada hii ya heshima hivi karibuni–––kunipa baruapepe yake. Nilimuandikia kumueleza shida zangu. Naye, bila kusita, alijibu “Bwana Mhango, naomba unipe muda kidogo kwani sijisikii vizuri.” Kusema ukweli majibu yake ya kiungwana na kinyenyekevu yalinipumbaza ukiachia mbali kutoa mawazo yake tena yenye kujibu maswali mengi na marefu ya kitaaluma bila kuacha kuniambia kuwa nikihitaji zaidi nisisite kumueleza. Alinipa moyo kusoma ili baadaye niitumie elimu yangu kwa faida yangu na taifa jambo ambalo licha ya kufanya nimkumbuke, sitalisahau.
Kutokana na namna nilivyowasiliana na mzee Mkapa, tena kwa kujibu yeye mwenyewe na si wasaidizi wake, nilipoandika tanzia ya kifo chake, wapo––hasa mahasidi na wakosoaji wake¬¬––walionitumia salamu binafsi kusema kuwa ima sikumjua mzee Mkapa au niliamua kumpendelea na kumpamba. Mmojawapo alijifanya kuzungusha akisema “siamini aliyeandika tanzia hii ni wewe. Maana kiingereza kimepwaya tena broken.” Nilicheka na nikamjibu bila hasira kuwa: kwanza, kiingereza siyo lugha yangu. Na pili kuwa ni hicho hicho kilichopwaya na broken ndicho kilichoniwezesha kukubaliwa kusoma shahada ya uzamivu tena kwenye nchi inayotumia kiingereza kama lugha yake ya kwanza ukiachia mbali kuandika vitabu zaidi ya 20 vya kitaaluma kwa lugha hii hii. Ni bahati mbaya ujumbe ulifika na mhusika hakunijibu tena. Maskini huyu jamaa¬¬–––ambaye ananizidi kiumiri ila si kitaaluma pia namheshimu–––hakujua kuwa mzee Mkapa alikijua kiingereza kama alivyo mzee Msekwa lakini hawakuwahi kuniambia kuwa kiingereza changu ni cha kuungaunga. Hata kitabu cha Magufulification, the Concept that Will Define the Future of Africa and the Man who Makes Things Happen nilichoandika na mzee Msekwa ukiachia kitabu kizima cha tenzi za kimombo kiitwacho Kudos to President Magufuli mbali kazi nyingine ambazo mzee Msekwa amenishirikisha zote za kimombo na hakuwahi kulalamikia kizungu changu. Kwa vile mimi ni mtanzania, kama Mkapa, pamoja na kujua kimombo, bado najivunia lugha yangu ya taifa ya Kiswahili.  Mwingine nilimwambia kuwa mzee Mkapa, sawa nawe na nami, alikuwa na mapungufu yake kama binadamu, ila mazuri yake yalishinda mabaya yake. Nilimwambia kuwa asiye na dhambi awe wa kwanza kumtupia mawe mzee Mkapa tena akiwa marehemu kama yeye ataishi milele. Ni kweli mzee Mkapa wapo aliowakwaza. Wamesamehewa akina Idi Amin itakuwa yeye? Juzi juzi nilikuwa nawasiliana na ndugu Madaraka Nyerere juu ya upatanisho wa marehemu baba yake (baba wa taifa). Na alikuwa na moyo mkunjufu kunitambulisha kwa Jaffar Amin (mtoto wa Amin) kuhusiana na harakati zao za kuzidi kuleta Tanzania na Uganda karibu.
Tuache chuki na utani. Mzee Mkapa, ni mtu aliyeutumikia umma kwa maisha yake yote tena kwa moyo mmoja na mkunjufu. Pia hakuwa mgeni kwa watanzania na hata kimataifa. Burundi bado wanamkumbuka kwa mchango wake katika kuleta amani kwenye taifa hilo ambalo lilipata utulivu baada ya Mkapa kuwasuluhisha. Uganda hawatasahau alivyowasaidia kuunda serikali baada ya kuangushwa kwa Idi Amin. Pia mzee Mkapa alisifika kwa ujasiri wake––na wakati mwingine––ubabe kidogo pale alipoudhiwa. Hata hivyo, alikuwa mtu mnyenyekevu, msomi na muwazi. Rejea sera yake ya Uwazi na Ukweli iliyowasilisha falsafa yake kiutawala. Hata hivyo, mzee Mkapa hakuwa malaika. Pamoja na hii, ni mmojawapo wa viongozi waliokiri mapungufu yake na utawala wake pale alipoandika wazi wazi kwenye kitabu cha maisha yake cha My Life, My Purpose A Tanzanian President Remembers kilichotoka mwaka mmoja kabla ya kufikwa mauti.  Katika kitabu hiki,  Mkapa alikiri wazi wazi kuwa kulikuwa na mapungufu katika baadhi ya sera zake kama vile uwekezaji ambao ulizua manung’uniko kwa baadhi ya watanzania. Kitendo chake cha kukiri tena wazi wazi kwa maandishi kinamuweka kwenye daraja la juu la viongozi waadilifu. Maana walatin  husema verba volant, scripta est manent est yaani maneno huupaa, lililoandikwa ni la milele.
Pamoja na kufanya mengi ambayo si rahisi kuyaorodhesha, marehemu mzee Mkapa atakumbukwa kwa kuanzisha the Tanzania Social Action Fund (TASAF) ambao umesaidia watanzania wengi kupambana na umaskini. Mbali na hili, kitaifa, kama alivyowahi kusema rais John Pombe Magufuli akielezea alivyoteuliwa na Mkapa kuwa waziri, kuwa Mkapa ndiye alianzisha sera ya Tanzania kujenga barabara na miundombinu kwa fedha ya ndani jambo ambalo rais Magufuli amelipanua na kufanikiwa kuwa na miundombinu imara na miradi mingi ya maendeleo ndani ya muda mfupi; jambo ambalo limeishangaza dunia wakiwamo hata maadui zake. Rais Magufuli hafichi kusema kuwa mzee Mkapa ndiye mentor wake kisiasa na kisera. 
Tumalizie kwa kumkumbuka marehemu mzee Benjamin Wiliam Mkapa (Mungu ampe pumziko jema peponi). Hakika mwaka ujao utakuwa na pengo tokana na kifo cha mzee Mkapa. Lala Mahali Pema Peponi Mzee Benjamin William Mkapa. Hamba Kahle Ubaba Mkapa. 
Chanzo: Nipashe Jumapili leo.

No comments: