The Chant of Savant

Tuesday 27 May 2014

Kijiwe chalaani umafia wa EWULA

BAADA ya kunyaka habari za kunyotoana roho kunakofanywa na wanaotuibia, Kijiwe kimekaa kutoa tamko.
Msomi Mkatatamaa ndiye anayelianzisha baada ya kuingia. “Waheshimiwa mnaona na kushuhudia yale ambayo nimekuwa nikionya mara kwa mara?”
Mpemba anadakia, “Wamaanishani; mbona ushaonya juu ya mengi msomi?”
“Yakhe naongelea haya madudu yaliyofichuliwa na CAG pamoja na mauaji ya jamaa wa EWULA alipotaka kuonyesha wenzake wanavyoula wakaamua kumnyotoa roho ili waendelee kuula.”
“Kumbe unaongelea huyu mugabo aliyenyotolewa roho na kudaiwa alijinyotoa? Hapo nimekupata mkuu.” Anachomekea Mijjinga ambaye kama kawa ameulamba ile mbaya.
Kanji anachomekea, “Veve pata somi vapi bona tusi yeye bwana?”
“Kanji usikonde hata nami nimempata aliyosema. Hivyo, achana na hiyo tusonge mbele na mada ya leo au vipi?”
Mipawa aliyekuwa anavuta sigara kali yake anaamua kuisigina na kula mic, “Kama anavyosema Msomi, tuachane na kupatana na mambo madogo kama hayo. Badala yake tujadili huu umafia unaoanza kushamiri ambapo watu wananyotoana roho ili kuficha madhambi yao.”
Mgosi Machungi anakatua mic, “Wakiuana wao kwa wao fit. Wamekuwa wakitinyonga kwa kutiibia kuna kosa gani wakitoana oho? Kinachogomba hapa ni kwamba unajengeka umafia. Kama wananyongana wao ukiwaona kuwastukia si wanakuua na ukoo wako.”
Msomi anakamata mic, “You are dead right Mgosi. Hapa kinachofanyika ni kujenga mazingira ya kuweza kuficha madhambi yao ima kwa kuwaua na kuwanyamazisha washirika zao au whistleblowers. Nadhani tusipobadili mfumo wa kijambazi tutaangamiza kaya.”
Kabla ya kuendelea Kapende anakatua mic, “Naungana nawe Msomi. Ulimsikia mheshimiwa Nunduu alivyosema kuwa wahalifu wachache wenye madaraka wanasamehe kodi za mabilioni kwa kuhongwa vijijumba?”
“Huyo naye mnafiki mkubwa. Kuonyesha lao lilivyo moja alishindwa kuwataja kwa kuogopa naye kutajwa kama ilivyokuwa kwenye sakata la waheshimiwa waishiwa kughushi vyeti huku mkuu akiangalia tu kana kwamba naye ameghushi.” Anajibu Mijjinga haraka.
Sofi Lion aka Kanungaemba anaamua kudema, “Nyinyi mlitaka amtaje nani wakati alikuwa akitoa matamshi ya kisiasa? Hata hawa mnaowasingizia kuuana mnawaonea hasa ikizingatiwa kuwa uchunguzi unaonyesha marehemu alijinyonga.”
“Go tell it to the birds Sofi. Siku zote nashangaa nini kimekuingilia kiasi cha kushabikia uovu hata kama unatendwa na chama chako. Kujinyonga gani iwapo wanasema walikuta dimbwi la damu na kwanini baada ya kuhojiwa na waheshimiwa? Hata kuku wanajua kilichofanyika. Hapa tatizo kama alivyosema Mgosi kuwa unajengeka umafia na janja ya kuwanyamazisha whistleblowers au kuwatisha washirika wao katika jinai hii. Mara hii mmesahau Aminia Chifwupa alivyokolimbwa kwa kuingilia dili za unga?”
“Mie hakuna waheshimiwa waliponiacha hoi kama kuambiana kuwa kwenye mjengo wamejazana walioghushi.” Mbwa Mwitu anadakia.
“Unashangaa nini wakati Pita Msigua alishasema kuwa majangili na walioghushi ni maswahiba wa rahisi na rahisi mwenyewe asikanushe? Unategemea nini au nini kifanyike iwapo walioghushi na vihiyo wote ni marafiki wa mkuu?” Anakatua mic Mipawa.
Mpemba naye anajikusuru na kula mic, “Huyu Nsigwa ankuna wallahi. Maana mojawapo wa hao vihiiyo ni Bill Lukuvii toka huko huko. Waloghushi kweli wana dhiki kiroho. Tulivowaghasi lau wangejibu.”
“Kaka wajibu nini wakati ni ukweli wengi ni madaktari feki? Ngoja niwataje tena ili msiwasahau. Yupo Merry Naguu, Makorongo Muhanga, Emmy Nchimbii, Diddie Massaburii, Vicky Mwambalashwa, Matthew Mataayo, Dorolos Kamalaa, Raph Chengeni na wengine ambao nitawataja wiki ijayo.” Anazoza Msomi.
Kabla ya kuendelea Sofi anakatua mic, “Unao ushahidi wa tuhuma hizi kwa waheshimiwa?” Msomi hajibu. Badala yake anampa kitabu cha Keineruga Msemakweli.
Waswazi wasivyopenda kusoma, Sofi anatoa mimacho kama gabacholi aliyekamatwa na bwimbwi.
Kuona hivyo Kanji ananyakua mic, “Veve zani hii Semakweli semakweli au politics? Mimi ona iko siasa ya maji taka.”
“Kanji unaambiwa kilichoandika cha milele halafu unatia shaka? Kweli hizi ni siasa za maji taka ambapo sirikali inaundwa na wahalifu tena vihiyo. Hukuona yule kihiyo mwingine Hawa wana Gasia alivyosiama kuwatetea majambazi wenzake akisema kuwa na upinzani nao unao vihiyo walioghushi?” Anachomekea mzee Maneno.
Mijjinga anazidi kukandia, “Nilitamani waanze kutajana ili tuongeze orodha ya walioghushi ambapo watu kama Jan Makambaa, Saadaa Mkuyati yule wa Njuluku na naibu wake Adamu Kagoma Milima waongezewe kwa kujidai wana masters wakati hata bachelor hawana. Bahati nzuri wote nawafahamu ndani na nje.”
“Mijjinga unaua. Yaani unawafahamu ndani na nje?” Anatania Mbwa Mwitu.
“Hata mie nanfahamu huyu Mkuyati. Hana hiyo master wala bachelor. Sijui hata hiyo diploma alo nayo kama ya ukweli. Si hawa twawaita maamum kumaanisha vihiyo kama huku msemavo.” Anazidi kukandia Mpemba.
Baada ya kugundua kuwa mada imehama toka EWULA na kwenda kwenye kughushi, Msomi anaamua kuirejesha. “Msemayo ni kweli. Baada ya jamaa kuona kughushi na kutuibia kiasi cha kuwa mizigo kama alivyosema shujaa Msigua, wameamua kuanza kunyotoa roho yeyote anayefichua dhambi zao hata awe mwenzao. Maskini kijana wa watu amepotea bure.”
Mipawa hakubaliana na Msomi. “Hajapotea bure hasa ikizingatiwa kuwa alikuwa akila nao. Tusiporejesha sheria za maadili na kutaka kila mtu kutaja mali zake tutaangamia kama kaya.”
Kapende anadandia, “Hiyo sahau. Unaona mkuu anamaliza ngwe mbili na hataji unadhani kuna atakayetaja? Wengine wakitaja tutakufa kwa shinikizo la moyo kwa walivyo matajiri tena wana wa maskini wa kunuka.”
Mchunguliaji anakamua mic, “Dokta Kapende usemacho ni kweli. Hukumsikia yule Nshomile Jemus Rugemaliiira kuwadi wa kawaida anasema eti bilioni 120 ni vijisenti vya ugoro? Mijizi mingine bwana. Kama ni vijisenti hiyo bia ya Mabi-bo alikojificha anauza ya nini kama ni tajiri? Hawa walipaswa kunyongwa.”
“Hoo Tate nane uzanitonesha! Kwei hawa na wae waiogushi wanapaswa kunyongwa. Siku akija mkuu mwenye akiii na udhu wataumia wengi kama si kuuawa.” Mgosi anazoza.
Kijiwe kikiwe kinanoga si likapita shangingi la mkuu wa EWULA. Tulilikimbiza kwa hasira ili tumkamate tumnyotoe roho halafu tuseme amejinyonga mwenyewe lakini wapi!
Chanzo: Tanzania Daima Mei 28, 2014.

No comments: