The Chant of Savant

Tuesday 14 April 2015

Kijiwe chalaani ugaidi


Tokana na shmbulizi la kikaitili na kipumbaavu lilotokea nchini Kenya, Kijiwe kimegundua baadhi ya sababu za wale wajinga na vihiyo wanaitwa wasomi kushiriki ushenzi na jinai hii.
Mpemba leo ndiyo kafungua dimba. Anaweka vizuri saluni au msuli kwa lugha rahisi na kuchonga, “Yakhe mmesikia hili shambulio la kishenzi na kitwahuti lilotokea kule Kenya? Wallahi lasikitisha sana ati.”
Mgosi Machungi anadakia, “Hakuna kiichotishangaza kama wasomi kushiiki ushenzi huu. Hivi kwei hawa ni wasomi kwei au vihiyo wanaoitwa wasomi?”
Mijjinga akiwa anasogeza gazeti mezani vizuri anakwapua mic na kusema, “Nadhani ni makosa kuwalaumu hawa wauawaji tuliodhani ni wasomi wakati si wasomi kitu bali vihiyo kama anavyosema Mgosi. Tulaumu mfumo mbovu wa elimu nchi za kimakonde ziliorithi kwa wakoloni.”
 Anakunywa kahawa kidogo na kuendelea, “inabidi tchunguze mfumo wetu wa elimu. Maana haiwezekani msomi wa kweli akarubuniwa na ahadi za kijinga akaamua kuua watu bila sababu kama ilivyotokea Kenya.”
Kabla ya kuendelea Kapende anachomekea, “Usishangae hawa wasomi uchwara walioua kule Kenya, kwani wana tofauti gani na hawa vilaza waliojazana maofisini walioghushi hadi udaktari wa falsafa?”
Mzee Maneno anachomekea, “ Usemayo shehe ni ya kweli. Nasikia jamaa waliwahonga ndata wakapitisha mzigo wa kwenda kuulia watu.”
Msomi Mkatatamaa anachukua mic kwa madaha na kudema, “Nakubaliana na alhaj Kapende kuwa hawa hawana tofauti na wahalifu waliojazana maofisini, mipakani, viwanja vya ndege na kwingineko nyeti. Kama wanaruhusu bwimbwi na  vipodozi na madawa feki kupita watashindwa kuruhusu silaha? Kama wanaruhusu mauaji ya walemavu wa ngozi, faru na tembo hata wengine kushiriki kuwasafirisha wakiwa hai watakataa fedha? Wao wanajali nini? Siku hizi watu wanaweza kuwauza hata mama zao ilmradi wapewe fedha utadhani watakufa nayo.”
Mbwa mwitu anachomekea, “Uliona wale vigori waliotaka kwenda Syria tena naambiwa wasomi? Vigori au masharmutah wanatafuta mabwana hao baada ya kuchemsha huku. Wanaweza kuwa vyangudoa wanaotumia dini kutafuta malaya wenzao.”
Anaendelea, “Pia kuna haja ya kuchunguza baadhi ya ahadi za ngono na upuuzi mwingine vinavyovutia vijana wetu vihiyo na wavivu wa kufikiri.”
Mipawa anakula mic, “Unataka kusema waliponzwa na ngono hadi wakaamini kila bangi siyo?”
Mbwamwitu anajibu, “Nani asiyependa kanchezo hako?”
Mijjinga anarejea, “Hata hivyo mimi siwashangai. Hawana tofauti na mafisadi wanaoua watu kwa umaskini sema tofauti ni kwamba wahanga wa ufisadi wanakufa taratibu tofauti na hawa wanaoua kwa ghafla.”
Anaendelea, “Umenikumbusha yule habithi madevu aliyekuwa akiwahadaa wapumbavu eti wamfie God wakati yeye alikuwa amejificha Abbotabad na manzi zake akijifua.”
Mpemba anakatua mic, “Yakhe ukisikia unafiki ndiyo huu. Hivi kweli mwanadamu anaweza kumpigania Mungu ambaye hafi wala haonekani au ni bangi na ujinga vinawasumbua?”
Kapende anajibu, “Unashangaa mwanadamu kumfia Mungu siyo? Mbona wapo wengi hasa wachunaji wametokea kuwa mabilioni hadi wengine kununua vyopa kwa kuwahadaa wajinga eti wamtolee Mungu utadhani Mungu kapuku anayeshobokea madafu machafu ya Bongo.”
Mipawa anakula mic, “Hapa umenena. Ujinga ni mzigo na wajinga ndiyo waliwao. Ukishobokea upuuzi wanakutumia. Ukiwa hamnazo ukaamini kila upuuzi utaumia na kuumiza wenzako.”
Msomi anatia guu tena, “Nadhani Bongo itatoa wengi wa wapuuzi hawa hasa ikizingatia ilivyo kaya ya washirikina na wapenda dezo. Hamuoni wanavyomaliza ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi na vikongwe tokana na imani hizi za kipunguani na kivivu?”
 Mgosi anakatua mic, “Hata hivyo tisilaumu sana. Unategemea nini kaya ikitawaiwa na washiikina, wasanii, wezi, mafisadi, wapenda raha na dezo?”
Sofia Lion aka Kanungaembe hakubaliani, “Hapa najua mtamlaumu kila mtu ilmradi msuuze roho zenu na urongo wenu. Unaweza kutupa ushahidi na majina ya hao unaowaita washirikina wanaotutawala kama siyo umbea?”
Mbwa Mwitu anamchomekea Sofi“Dada Sofi umeingiliwa na nini dadangu? Yaani pamoja na mauaji yote haya ya kikatili na kishirikina ya ndugu zetu bado hujaona ushirikina wa kimfumo?”
Mijjinga anachomekea, “Unandhani wangekuwa wanaua watawala wangeua hata wawili kabla ya ndata kuingilia kati?”
Msomi anawapa tafu Mbwamwitu na Mijjinga, “Msemayo ni kweli. Ukiona huu ushenzi unaendelea jua kuna namana wakubwa wanavyonufaika hasa ikizingatiwa kuwa wakati wa uchakachuaji huwa tunawaona wanavyoshindana kwenda Bwagamoyo kufanya ushirikina ukiachia mbali kurhusu matapeli kutangaza upuuzi huu wazi wazi hata kwenye vyombo vya habari.”
Kanji aliyekuwa akiongoea na bi mkubwa wake Kastuli huko Bombay anaamua kutia guu, “Mimi shangaa sana. Vatu nakosa utu naua hata toto ya shule!  Om sai ram.naombea dua ile toto nauawa Kenya. Kama gaidi nazidi kamata chinja yote kama nafanya kule Bombei. Ile napanga fanya gaidi taogopa sana.”
Mzee Ndevu anachumokea,“Nasikia na jamaa yetu big huwa ana kigagula ambaye huwa habanduki kwenye debe kila aendako.”
Mpemba anajibu,“Utegemea ni unapotawaliwa na vihiyo na viherehere?”
Mbwa mwitu anachomekea tena, “Kaka hapo umeua. Umetumbua kwenyewe. Kumbe chanzo siyo hawa wajinga wajinga wadogo wadogo bali wale wakubwa wakubwa siyo?”
Kijiwe kikiwa kinanoga si kunguru akanaswa kwenye nyaya za umeme. Acha kila mtu atoke mkuku tukidhani magaidi wamevamia kijiwe!
Chanzo: Tanzania Daima Aprili 15,15.
 

No comments: