The Chant of Savant

Tuesday 7 April 2015

Kijiwe chakumbushia escrow

wiki hii yataelekezwa zaidi mjini Dodoma, kujua hatma ya watuhumiwa ...
         Baada ya kuona kasi na namna kashfa iliyozamisha njuluku kibao za wachovu, Kijiwe kimeamua kurejesha suala zima kwa hadhira lau ihoji kama si hivyo basi ichukie ili wakati wa kupiga kura iwaadhibu hawa matwahuti na majambazi wanawaibia wadanganyika.
Mijjinga anaingia akiwa na gazeti la Kijiweni Daima. Baada ya kuamkua anamwaga stori, “Wazee mna habari kuwa kuna ufisadi mkubwa unapangwa na mafisi na mafisadi waliozoea kutuibia? Rafiki yangu ambaye ni shushushu amenipasha kuwa wameamriwa waanze mpango wa kutumia uchakachuaji ujao kupiga njuluku za wadanganyika hasa katika manunuzi ya zana wanazotangaza wakati ni bomu tupu.”
“Hii kali kweli kweli. Yaani pamoja na kuiba njuluku za EPA hawajaridhika!” anajibu  Mzee Maneno. Na kuendelea, “Sina shaka na habari hii kutokana na nijuavyo uroho, roho mbaya, ufisi na ufisadi wa watu wetu.”
Kapende anachomekea, “Nami naamini habari hii hasa ikizingatiwa kuwa wezi wetu wanawachukulia wadanganyika kama hamnazao na wasahaulifu hakuna mfano. Wanawadharau sina mfano.”
“Wewe unaongelea huu ujambazi wa escrow ambapo wahusika wako kitanda kimoja na hao mnaotegemea wawatendee haki kwa kuwakamata wenzao? Hii kaya ya sijui majuha au wagonjwa mie sijui.Nani anakumbushia uchache wetu au njuluku za Uswazi?” Mipawa anazoza kwa hasira. Kabla ya kuendelea Mgosi Machungi anamkatiza, “Hebu Pawa tiombe msamaha kwanza. Unawezaje kutiita mujuha  na wagonjwa wakati tinapinga huu wizi?”
Mipawa anakwanyua mic, “Mgosi yaani nawe unajiweka kwenye kundi la wanakaya hii? Sisi ni wana Kijiwe na si wanakaya hii japo tunaishi kwenye kaya hii.  Hivyo, ninapokandia, siwahusishi wote wanaopiga vita huu ufisadi.”
“Hapa timeewana,” Mgosi aonyesha kuridhika huku akigonganisha mkono na Mipawa kama wafanyavyo marasta. Anaendelea kula mic, “Kwei hii kaya ni ya mabunga na wehu. Uimuona yue fisadi aiyekusanya mashehena na waganga njaa eti kwenda kumipa pesa agombee uahisi? Kwei nimeamini. Namna hii escoo nyingi zitatokea. Hivyo, sitashangaa kusikia kuwa baadhi ya wagombea wanahonga njuuku za escoo akiwamo huyu habithi na fisadi wa kutupwa wa Richmondui.” 
“Usitutie madole ndugu yangu. Japo ameshindwa hata kabla ya kugombea, usinitajie huyo fisadi. Natamani nile nyama yake.” Mheshimiwa Bwege anadakia. Kabla ya kuendelea, Mbwamwitu anamuonya, “Mheshimiwa angalia hiyo lugha usijetutukana tukashikana mashati bure.”
Mheshimiwa Bwege anajibu, “Siwezi kuwazuia kufikiri na kutafsiri mtakavyo. Namaanisha kuturejeshea kumbukumbu za uchungu ndugu yangu. Mna habari juzi nilimuona Muongo akitanua kana kwamba si mhalifu anayepaswa kunonihino kwenye debe.”
Sofia Lion aka Kanungaembe kaguswa pabaya. Alikuwa akitafuta pa nafasi sasa kaipata. Anakula mic, “Acheni wivu. Mtu akitajirika nyie mwadhani ameiba au kufanya ufisadi. Mmeambiwa mtukufu atawashughulikia watuhumiwa. Kumbuka hawa ni watuhumiwa tu.”
Kabla ya kuendelea Mbwamwitu aliyekuwa akitafuta upenyo wa kuchomekea anamchomekea Sofi, “Malizia wivu wa kike.” 
Sofi anamdharau Mbwamwitu na kuzoza, “ Nasema hawa ni watuhumiwa. Hawajakutikana na hatia. Hujui sheria nini?”
“Mbona watuhumiwa wa wizi wa kuku wanawekwa rumande hawaachwi kama unavyotaka au wameishakukatia nini kama yule Nguuumo wa Ikuu nini?” Kapende anauliza huku akionyesha wazi kumdharau Sofi.
Mipawa naye anaongezea huku akimtazama Sofi na kutabasamu, “Sofia acha utani. Nani amshughulikie nani wakati kambale wote wana sharubu? Yaani kwa akili zako ulitegemea nyani amhukumu ngedere kwa wizi wa mahindi shambani mwa bibi siyo? Umenoa.”
Mpemba aliyekuwa kimya muda mrefu akivuta uradi anaamua kutia guu, “Wallahi mie nshangaa sana. Ilikuwaje huyu jamaa akawaamuru wezi wa HEPA wakarejesha njuluku kama alivosema.  Sasa ashindwani kuwaamuru na hawa watu wake warejeshe njuluku yetu kama hashirikiani nao ati? Mie antia wasi wasi kusema ule ukweli. Agwaye wezi utadhani ndo walomweka madarakani.”
“Sofi imekuingia hiyo? Maana ni bonge la pwenti au siyo? Patamu hapo au vipi?” Mbwamwitu anamtania Sofi huku akimsukasuka.
“Je nawe imekuingia kiasi cha kufurahia hivyo?” Sofi anajitetea. Kabla ya kuendelea Mbwamwitu anamchomekea kwa mara ya pili.
Mbwamwitu anajibu, “Nadhani Ami alikulenga wewe baada ya kulalamika Kanji haridhiki. Anakwanyua mic, “Tafadhili dugu yangu Bwamwitu acha chomeka Sofi. Kwanini veve penda chomeka Sofi kila siku?”
Kijiwe hakina mbavu. Mgosi Machungi anapaza sauti, “Kanji chonde chonde hiyo uga sema veve tusi kuba tupu dugu yangu.”
Msomi Mkatatamaa aliyekuwa amechelewa kuingia kijiweni anakamua mic, “Nimekusikia ndugu yangu mheshimiwa Bwege. Usemayo ni kweli, Muongo alipaswa kuwa Keko au Segerea tena akingojea kunyongwa. Pia si yeye peke yake. Hata akina Seti Singha na Rugemalayer walipaswa kuwa wemeishaoza makaburini kama tungekuwa tunachukia ufisadi. Sasa wanatukoga na kusema yako wapi.  Wao ni lisirikali ndani ya lisirikali. Si unaona Rugemalayer na Seti Singha ndiyo hao wanazidi kuchonga madili mengine. Sitashangaa kama hawatakuwamo kwenye dili hili la uchakachuaji. Nshawaambia siku nyingi, hawa fisi wanatumiwa na wakubwa wasiotaka mambo yao yajulikane ingawa yanajulikana.”
“Hapa najua unayemlenga. Lazima jamaa atakuwa anakula nao hasa ikizingatiwa kuwa ndiye aliyewezesha kuingia kwa balaa hili kayani.”
Kijiwe kikiwa kinanoga si mashabiki wa timu za mpira wakaja na fujo zao wakidai wanashangilia ushindi wakati wengi si mashabiki kitu bali vibaka. Kuepuka kuwashushia kichapo tuliamua kujiondokea tukishangaa wanavyoweza kushangilia mipira wakashindwa kutumia usongo huo kuwabana mafisadi.
Chanzo: Tanzania Daima Aprili 8, 2015.

No comments: