The Chant of Savant

Tuesday 18 May 2021

Kama Samia Ni Mama Yetu, Maria Nyerere na Bi Titi Ni Nani?

Si nadra siku hizi kusikia watu–––hasa wateule wake au wale aliowabakiza kwenye ulaji–––wakimwita rais Samia Suluhu Hassan ‘mama yetu’ ili kumfurahisha na kulinda ulaji wao. Kama tutakuwa wakweli kwa nafsi zetu, je kweli SSH ni mama yetu? Kwangu mimi, SSH ni rais wa JMT basi. Kwanini ninafikiri hivi? Nina sababu zifuatazo:
        Mosi, Samia si mama yetu bali rais wetu hasa ikizingatiwa kuwa umama wa taifa haupewi mtu kwa sababu ni rais bali kutokana na mchango wake kama upo. Je tukilinganisha mchango wa SSH na akina Maria Nyerere, mjane wa baba wa taifa au Bi Titi Mohamed, mama aliyepigania uhuru wetu hadi kuathirika kifamilia kwa kuachika na kufungwa tena kwa kusingiziwa kweli tunaweza kusema kwa haki na heshima kuwa SSH ni mama yetu?
        Pili, kama ni umama utokanao na urais, inakuwaje watangulizi wake kuanzia Mzee Ali Hassan Mwinyi, Hayati Benjamin Mkapa, Jakaya Kikwete na Hayati Dkt John Magufuli hawakuitwa baba zetu? Hapa kuna nini au ni ule udhalilishaji wa mfume dume kama siyo tabia ya kujikomba ambayo ilianza kuota mizizi kwenye awamu ya tano tokana na ukali wa Magufuli? Tulizoea kusikia mke wa Magufuli, mama Janet, akiitwa na walipoende kujipendekeza kwa mumewe wakimwiti ‘mama yetu kipenzi’ sifa ambayo imepotea ghafla baada ya mumewe kufariki na kutokuwa madarakani. Je ni kweli mama Janet alikuwa kipenzi au madaraka ya mumewe? Mbona siku hizi tunasikia akiitwa mjane wa Magufuli bila sifa ya kipenzi kuendelea kutajwa kama kweli alikuwa akipendwa kweli? Je kwanini SSH, ghafla amegeuka mama wa kila mmoja wakati alipokuwa makamu wa rais aliitwa jina lake la SSH? Kunani hapa? Hata hivyo, hili linahitaji wenye kuona mbali na ndani zaidi.  Je hawa wanaomwita SSH mama yetu wanamaanisha hivyo au kujikomba na kumzuga aendelee kuwabakisha kwenye ulaji? Je––kama tutafuata vigezo––SSH anastahiki heshima ya mama yetu ambayo kwa maana nyingine ni mama wa taifa wakati mataifa karibu yote–––tokana na mfumo dume–––huwa hayana mama wa taifa isipokuwa baba wa taifa?
            Kwa kujua tabia ya kujikomba inayoendana na madaraka, namshauri rais SSH akemee utapeli huu usiokuwa na sababu yoyote bali kujikomba na kumpumbaza na kumdanganya adhani wanampenda wakati si kweli. Hebu fikiria. Alipokuwa madarakani, Dkt Magufuli alikuwa akisema kila jambo na kuungwa mkono huku waliomzunguka wakimsifia na kujichekesha ilhali walikuwa wanalenga kumtumia na kumfurahisha ili wanusurike. Ukiangalia kwa sasa ambapo wale waliokuwa wakijifanya watu wake walivyomgeuka na kuanza kubomoa mema yake, utajua ninachomaanisha. Mfano wa karibu ni ile hali ya baadhi ya waliokuwa karibu naye kuanza kutetea bila aibu mambo ya aibu ana ajabu kama vile mradi mbovu wa ujenzi wa bandari ya Bagamoyo ambayo Hayati Magufuli alipiga kalam una kutamka wazi kuwa hata mwendawazimu asingeweza kuuruhusu. Mbali na hiyo, rejea kubadilika kwa ghafla kwa wapiganaji wa miamvuli waliotuaminisha kuwa taifa letu lilikuwa hali corona na lilikuwa likilindwa na Mungu kiasi cha kutovaa mabarakoa kwa vile Hayati Magufuli aliyapinga wanavyovaa mabarakoa. Je huu si ushahidi wa unafiki na imani za woga? Sina ugomvi na kuwepo kwa corona. Je kwanini mliokuwa mmezunguka Hayati Magufuli hamkumshauri au kuachia ngazi pale alipokuwa ameshikilia msimamo kuwa tulihitaji kinga ya Mungu na si barakoa na chanjo?
            Taifa letu ni ajabu kidogo. Ilifikia mahali watu wanajua kabisa kuwa walikuwa wakihatarisha afya zao na wengine ilmradi waendelee kuwa madarakani wasijue wangeweza kufa na kuyaacha. Kwa kuzingatia tabia hii ya ajabu na hovyo, namshauri rais SSH asikubali kuitwa mama yetu wakati wanaomuita hivyo wapo wanawake wenye umri mkubwa kuliko yeye ukiachia mbali wanaume wanaoweza kumzaa. Nisisitize. Tuwe wakweli kwa nafsi zetu badala ya kuendekeza njaa na unafiki. Tunawapotosha viongozi na wananchi wetu.
            Tokana tabia hii ya kinyonga, nachelea kuwa baadhi ya mambo aliyokataza Hayati Magufuli yanaweza kurejea taratibu kama vile safari za hasara na hovyo za maafisa wa serikali nje, matumizi mabaya, wizi, uzembe na mengine mengi. Rejea kadhia ya hivi karibuni ambapo wadau wa bandari walivyosikika kwenye mitandao wakilalamika kuwa bandari imerejea ujahiri wa awali ukiachia mbali wizi hata ujambazi kuanza kuibuka hata kabla ya Hayati Magufuli hajaoza.
            Biblia ina maneno ya busara yasemayo ajikwezaye atashushwa. Pia tuongezee kuwa akubalie kukwezwa asipostahili atashushwa na wale wale wanaompaka mafuta kwa mgongo wa chupa au kumtwisha kiremba cha ukoko. Namshauri rais SSH ajikumbushe kisa cha Yesu siku ya matawi alipoingia Jerusalem akiwa amepandishwa kwenye mgongo wa punda huku wanawake wakitandika khanga zao na wengine matawi ili apite. Je alipokamatwa, watu wale wale walisema? Walisema “asulubiwe” hata bila makosa. Kumbuka. Kabla­­­––kwa mujibu wa biblia­­­––Yesu aliweza kulisha umati pale alipobadili samaki sita na vipande vya mikate watu wakala na kusaza. Ajabu, baada ya hapo, ni wanufaika wale wale walisema bila aibu wala woga asulubiwe. 
            Mfano mwingine ni wa Musa. Alipowatoa wana wa Israeli Misri alishangiliwa sana. Cha ajabu, akiwa jangwani njiani kuelekea Kanani, walimgeuka wakakufuru wakisema walikuwa wamechoshwa na mana na pia walitaka wamuone Mungu vinginevyo wangemuua Musa. Mfano mwingine ni wa baba wa taifa. Alipokuwa kitini walimwimbia mapambio, ngonjera na nyimbo zote za sifa. Alipostaafu walimwita ‘Baba aambiliki” wakati walikuwa wakigwaya kumwambia zaidi ya kumsifu hadi wakaja na kile kilichoitwa zidumu fikra za mwenyekiti wa CCM. Je zilidumu au zimeishia wapi baada ya yeye kuishia? Hawa ndiyo wanadamu. Hawana tofauti na ndege kwenye mti wenye matunda. Yakiishia, nao wanaishia bila hata kugeuka nyuma kama ambavyo kwa sasa naona wakimpa kichogo Hayati Magufuli ambaye amebakiza wanyonge wake tu ila siyo wale walioshiba mikononi mwake. Hii ni kutokana na ukweli kuwa ukiwa na madaraka, ulaji au utajiri na nguvu watakusifia. Zana hizi zikishakutoka waliokuwa wakijifanya kukupenda wanakuponda. Waliokuwa wakikweza wanakushusha na kukushua. Jifunzeni toka kwa Hayati Magufuli na yanayoendelea. Leo sisemi mengi zaidi ya kuuliza tena. Je kweli SSH ni mama yetu au rais wetu? Je anahitaji sifa hii kweli? Namshauri SSH akatae unafiki na unywanywa wa kutaka kuingizwa mkenge na wasaka tonge na wachumia tumbo ambao wako tayari kucheza ngoma yoyote ilmradi tonge liende kinywani.
Chanzo: Raia Mwema kesho.

No comments: