The Chant of Savant

Wednesday 9 July 2008

Kijiwe chastukia ulaji wangu kama mkuu

Baada ya nambari nonihino kujipaka uchafu kutaka kumsafisha Ewassa na wezi wengine huku ulaji wa vitambulisho visivyo vitambulisho kitu ukizidi kuwatoa roho wakubwa, nami kama Mkuu wa Kijiwe nimetoa ulaji kwa marafiki zangu.

Yupo mbwa mwitu ambaye hupenda kumuita fisi na wengine.

Kama ilivyotokea kwa jamaa kubadili picha, kisa? Ile ya kwanza ilimuonyesha amechoka, nami nimeamua kubadili suti yangu maana ina rangi kama za chama fulani cha kigaidi hasa kwa njuluku za umma kiitwacho Epuka Paka Adokoa au EPA.

Ingawa wanakijiwe wanajifanya wajanja hasa baada ya mie na mbwa mwitu kuwaibia uchache wa kahawa na kuishia kwenye matumbo yetu machafu, kipindi hiki nimewapiga bao la kisigino wasisituke.

Kununua suti mpya ya mkuu mie baada ya kushauriwa na wataalamu wa mavazi, si haba kwa Kijiwe maskini.

Mjadala unaanza hivi.
Mbwa Mwitu ambaye ni mnufaika nambari wani analianzisha. "Mnaonaje tukabadili gwanda la Nabii? Maana naona wakati akivaa hili kwanza alikuwa amekonda ukiachia mbali kufanana na kile chama cha majizi."

Mgosi Machungi anadakia mic. "Akini huu ni wizi wa pesa ya Kijiwe. Tiambiane ukwei. Hata kama tinaigiza mfano wa jamaa na picha, tijue tinaibia umma."

Mpemba hangoji Mgosi wa Mtibwa amalize. Anakwanyua mic. "Yakhe mie sina hamu! Watu waiba kwa kila kisingizio ati. Mara twaambwa vitambulisho. Mara picha ya Jamaa sasa nawe waja na gwanda! Ama kweli hii Kaya ya Mabwege hata kama Mwakiembe kapinga kuhusiana na wanohiiino."

Kapende anarukia. "Nyie hamjui huku ni kuwatengenezea ulaji akina Richmond na Kagoda wa Kijiwe hiki sawa na wale akina Rost Tamu wa Idodomya. Kwanza nasikia jamaa anataka kuishia mitini na njuluku zetu kama Jitu Patili." Anamkazia macho Mbwa ambaye anaonyesha kuchukia dhahiri.

Makengeza kaona upenyo. Anadandia mic. "Mzee umenena. Wajumbe wengine hapa wana ufisadi wa kimawazo. Hawafikirii kama Chitaahira, Annae Abdi-ala, Kriz Mdomokaya, na majuha wengine wa Idodomya wanaoitwa wahishimiwa wakati na mafisi tu."

Mzee Maneno anadakia. "Bwana usitake kunitapisha. Hii mijamaa inayowakilisha mitumbo yao hovyo kabisa. Yaani inaropoka, kulindana, kusafishana utadhani haina akili!"

Akatua kashata na kuendelea. "Mzee huu mradi wa gwanda naupinga. Ni ufisadi mtupu. Kwani anayeongoza kijiwe ni gwanda au wewe.? Kama wao wameridhia na upuuzi wa kutuibia siyo Kijiwe hiki patachimbika bila jembe na patakuwa hapatoshi. Na jua huu siyo mkwara kama wa jamaa walioapa na li-bajeti likapitishwa licha ya kupewa takwimu mfu na Mustafu Mkulu. Ohoooo!"

Mzee Ndomo anatia guu kwa mbwembwe. "Wazee hapa tukubaliane. Tupinge upuuzi huu kwa nguvu zote. Kwanza tusiogope chochote. Hatuna utaratibu wa kukalisha na kutishana wala kusafishana kama wao. Na isitoshe hatuna ufisadi wala mtindio wala utapia mlo wa mawazo kama wale."

Huku Mbwa Mwitu nami tukiwa tumebung’aa tusijue jinsi ya kusafishana wala kupata wajumbe mataahira kama Chitaahira au Mdomokaya na Annafisadi wa kututetea wizi wetu, mara Mpemba anapigilia msumari wa mwisho.


Anakula mic. "Yakhe tusiwe kama wale wevi na wanga waniowangia hata kwenye ukumbi wa kijiwe. Tusiuze Kijiwe kama wao walivouza Kaya. Tupige vita kila aina ya ufisi na ufuska wa kimawazo."


Anakwanyua kashata na kupiga tama tatu nne za kahawa na kuendelea. "Yule Chitaahira nyie hamunjui. Alighushi vyeti ati. Na huyu mama Annafisadi mwajua maisha yake huko nyuma? We mwache akiendelea na ufuska wake tutamwaga nchele hadharani wallahi."

Kabla ya kuendelea Kapende anamchomekea. "Huko nyuma ulipajuaje au ni yale yale ya Ohio na vyangu wa Idodomya ndani ya ulaji? Kwanza ungejua huyu sista wangu. Kuna kipindi eti alitaka shule ya sekondari moja iitwe jina lake chafu! Tulikuja juu njomba hadi akamwaga manyanga."

"Weye wauliza swali au jibu kusema ufuska wa Ohio? Kwani bila kutoa chauchau wadhani watu wawezapewa ulaji wasipowakilisha ntu isipokuwa matumbo yao na wale waliowapa takrima wakawateua?"

Anamkazia macho Kapende huku akinywa kahawa yake.

Mgosi Machungi hangoji mambo yampite. Anadakia. "Wagosi tiambiana ukwei. Hii kaya iishafiishika. Kinachoongeza mapigo ni kuwa na wakuu waiofiisika kimawazo na kimaadiii. Wanakula hata bia kunawa! Nyie mnashangaa ya Annafisadi! Mbona hamshagai ya mke wa Kaisai kuanza kukwapua kama mama Tunituni! Mbona tinajua kuwa ananunua mimai kibao kila sehemu?"

"Ama kweli kaya hii ni kata mti panda mti. Tumeondokana na Tunituni sasa Cheka cheka tukiendelea kumchekea atatuliza tena zaidi ya Tunituni." Anachomekea Mzee Ndevu aliyekuwa kajiinamia kwa muda mrefu.

Msomi alichelewa ingawa aliwahi maongezi yote. Anakula mic kwa mbwembwe kama kawa.
"Wazee, kwanza tukubaliane kuwa mradi wa gwanda ufe hapa hapa."
Anageuka na kuniangalia na kuendelea. "Bwana Nabii, kubali hapa umechemka. Angalia usiwe kama Mfalme Suleiman aliyeshindwa kuzuia tamaa zake au Daudi na mwanae Absalom waliomuudhi Bwana. Yaani kesi ya kuibiwa fedha ya kijiwe haijaisha unaanzisha ulaji mwingine!"

Anamgeukia Mbwa Mwitu na kusema. "Mkuu utamponza Nabii bure. Usiwe kama Ewassa na Kikwekwe au Roast Tamu ambao zinaanza kumtokea puani. Kama walivyosema waliotangulia, hiki Kijiwe siyo cha mabwege kiasi cha kuanza mambo ya kibwegebwege."

Ananigeukia na kusema. "Samahani Bwana Nabii kwa kutumia lugha kavu kavu. Huyu au wale waliokushauri kuanzisha mradi huu hawakutakii mema. Au nawe unaye Bi. Mkubwa mpenda hela kama jamaa zetu?"

Anakatua andazi na kushushia na tangawizi kidogo na kuendelea. "Sihitaji kuapa na kuwakariri akina Sophocles, Socretes, Aristoto na Plato kama mama nanihii aliyeapa baadaye akanywea na bajeti ikapita. Wala sina haja ya kuogopa kutishwa na akina mama Annafisadi au Mdomokaya na Chitaahira bingwa wa kughushi na kuongopa. Naongea kama mjumbe mwenye haki zote za kufanya hivyo na kueleweka. Lazima tuonyane na kushauriana tusijeishia kuwa kama wabaya wetu wanaoanza kulana wao kwa wao huku viapo na maazimio vyao vikigeuka uongo, upuuzi na maigizo mengine kwa wanakaya. Tukubaliane kuwa kama hawa hawataacha ujuha na ulafu kuna siku wana kaya watawatolea uvivu. Hata upambwe vipi huu ni wizi. Kijiwe nasi tukatae wizi huu wa kubadili gwanda sawa na ule wao wa kubadili picha. Mbona tumegeuzwa migebuka kila bwege atuguguna! Sasa muda unakwenda na wao wameshikilia politiki. We waache tutakutana mwakani. Mwenye macho na aone na mwenye masikio na asikie tena vizuri. Kutachimbika bila jembe na kutakuwa hakutoshi hata kama ni kukuu. Ila nasi tuache uzembe wa kuchagua mijitu isiyo na visheni bali misheni tu."

No comments: