The Chant of Savant

Monday 22 March 2021

HUYU NDIYE MAGUFULI NILIYEMSHUHUDIA


Kila nilipomuona au kumsikiliza rais John Pombe Maufuli, mara zote nilikuwa najaribu kwa kila niwezavyo kumdurusu ili kuweza kuona kile ambacho wengi hawkukiona au kama walikioona basi kwa utofauti nami. Mara na siku zote niliona kiongozi mwenye moyo mkubwa, mawazo, ndoto, dhamira, visheni, uzalendo na uthubutu visivyo vya kawaida wala shaka katika kuisafisha nchi kutoka kwenye ufisadi, uhovyo na uzembe. Mie si mwanachama wa chama chochote na nasifika kwa kuwa na chembe nyingi za upinzani kuliko kuunga mkono. Hata hivyo, leo natoboa siri yangu kuhusiana na nilivyomuona kipenzi cha watanzania marehemu rais John Pombe Magufuli ayetutoka juzi tu na kutuacha tukilalamika. Pia nachukua fursa hii kumuombea mrithi wake Mama Samia Suluhu Hassan avivae viatu vikubwa ajabu katika wakati huu mgumu. 
        Katika kauli mbiu ya Magufuli ya Hapa Kazi Tu, niliona kiongozi anayehangaika na ndoto misheni na visheni kubwa visivyoweza kuzuilika nia ikiwa ni kutaka kuiondoa nchi kwenye utegemezi wakati imejaliwa raslimali nyingi za thamani; kiongozi ambaye hayuko tayari kukata tamaa; ambaye amedhamiria kuhakikisha visheni yake inaeleweka bayana kwa wananchi wake ambao japo si wote wanaanza kumuelewa. Ndiyo maana, niliweza kuandika vitabu viwili yaani Heko Rais Magufuli na kingine kwa kushirikiana na rafiki, ndugu, baba yangu  Mheshimiwa Dk Pius Msekwa, Spika wa Bunge mstaafu aliyekubali kunipokea kama mwanae kunilea kimawazo na kitaaluma. Hakika, nilona kiongozi ambaye uhubiri maji na kunywa maji na si kunywa mvinyo; ambaye hutenda asemayo na kusema ayatendayo; ambaye kwa weledi anaelewa hatari na ugumu wa kile anachofanya; ambaye anaonekana kudhamiria kuupoka ushindi kwenye meno ya kushindwa.
        Kusema ule ukweli wa moyoni, nilimuona kiongozi ambaye wengi walishindwa kumuelewa–––kama walimwelewa si kwa kiwango walichopaswa–––ambaye katika zama hizi za ufisadi wa kutisha ni sawa na sindano kwenye lundo la nyasi. Sina nia ya kumkweza. Niliona mtume maskini ambaye–––kama alivyowahi kusema Mwl Julius K. Nyerere–––huwa hakubaliki kwao. Rejea namna nchi nyingi zinavyomuenzi Dk Magufuli wakati watu wetu wakimng’ong’a na wengine kumkataa hata kumdhihaki, kumzushia hata kumhukumu kabla ya kumaliza kazi aliyokwisha kuianza katika uhai na mauti.  
        Hadi kifo kinamnyakua, daima, nilimuona kiongozi asiye na mzaha; aliyekataa kuwa sahihi kisiasa; ambaye kwa ukweli na uwazi, alisema kilikuwa moyoni bila kujali chochote; ambaye hakutafuta sifa na upumbao lakini kuiondoa nchi kwenye ugumu wa kimfumo uliosababishwa na bindamu; na ambaye mapenzi, nguvu na uthubutu wake kwa nchi yake, mbali na kutokuwa na kifani–––pasi shaka, havimithiliki au kuweza kutiliwa shaka. 
        Hakika, nilimuona kingozi shujaa ambaye alikuwa tayari kufia kile anachoamini; ambaye aliwachachafya na kuwatetemesha mafisadi kiasi cha kupewa majina mbali mbali mabaya na mazuri kutegemea na upande aliposimama mtu. Nilimuona kiongozi ambaye, mara nyingi, alikuwa mkweli na asiyeyumba pamoja na ugumu wa kupambana na kung’oa maovu, rushwa, ufisadi, uzembe na ukosefu wa nidhamu katika shughuli za umma; kiongozi mweye kujitoa mhanga ambaye amekuwa kwenye nafasi za juu serikalini kwa zaidi ya miongo miwili; ambaye aligahamu kujiuza kwa sababu ya fedha na vitu.  Ndiyio maana nashindwa kumpongeza au kumpa pole mrithi wake, Mama Samia Suluhu Hassan ambaye ana mtihani na mzigo mzito kichwani, mabegani hata moyoni. Mungu amsaidie lau avivae viatu vya marehemu na atoshee. AMINA.
        Tukiwaza kwa pamoja, kwa kiongozi aliyefanya kazi muda mrefu hivi angeshindwa kujitajirisha kama angeamua? Magufuli aliwahi kusema kuwa kuna wahuni walitaka kumhonga na kumwekea fedha kwenye akaunti za nje lakini alikataa kujiuza na kuwauza watu wake.
        Haswa, nilipomuona Magufuli, niliona kiongozi jasiri na shupavu anayejipambanua kwa kuondoka na ukale akilenga kuwafanya sasa iwe bora ya kesho kwa ajili ya taifa na watu wake; kiongozi ambaye mawazo yake yaliwekwa kwenye maendeleo ya watu wake na mwenye dhamira ya kuleta mageuzi pale ambapo wengi hugwaya. Naweza kukosea katika hili lakini ni kwa kiasi kidogo; naweza kuwa sahihi lakini si vinginevyo. Ukitazama mambo ambayo Magufuli amlishafanya, tena kwa muda mfupi, bila shaka yoyote naweza kusema kuwa aliwekeza vilivyo kwenye kesho njema ya Tanzania. Hata hivyo, je watanzania walielewa visheni ya Magufuli vilivyo? Mama Samia anapaswa kufanikisha hili pamoja na ukubwa na ugumu wake. Mungu amsimamie na kumuongoza. AAAMIN.
        Masihara pembeni, Magufuli alikuwa kingozi ambaye, kwa dhamira na ujasiri, aaliamini kuwa elimu ni ufunguo na muhimu katika kesho njema ya taifa; kiongozi ambaye, chini ya uongozi wake, kulikuwako ongezeko la watoto wanlioandikishwa shuleni ukiachia mbali upatikanaji wa uhakika wa mikopo kwa ajili ya elimu ya juu bila kusahau kuimarika kwa huduma kama vile afya ambapo sasa hospitali hazipokei fedha za kumuona daktari bila kupewa chochote kama ilivyokkuwa awali. Namshukuru Mungu. nilimuona kiongozi ambaye chini ya uongozi wake Tanzania imeshuhudia kurejea kwa ufanisi katika shughuli za umma, na juu ya yote, kurejea madili tunayoshuhudia kwenye ofisi za umma. 
        Zaidi ya hapo, nilimuona kiongozi ambaye kwake umuhimu wa kuunganisha miundombinu kitaifa, usafiri na usafirishaji, tena vya kisasa, kujenga barabara, madaraja, viwanja vya ndege, vivuko, reli kama vile reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway (SGR), kusambaza umeme hasa vijijini,kupata vyanzo vipya vya nishati kama vile ujenzi wa mradi wa umeme utokanao na nguvu ya maji wa bonde la Stiegler na mengine kiasi cha kuigeuza Tanzania kuwa karakana ya ujenzi chini ya kile nikiitacho ku-Magufulisha Tanzania havina mjadala. 
        Kwa mfano, kwa mujibu wa Radio Vatican (Desemba 18, 2017), chini ya Magufuli, Tanzania iliwezea kukarabati barabara zenye urefu wa kilometa zipatazo 2,571 na kuongeza idadi ya watalii toka watalii 1,137,182, mwaka 2015 hadi 1,284,279 mwaka 2016. Sambamba na hili, mwaka 2017, serikali iliweza kuunganisha mamlaka za wilaya zipatazo 117, ofisi za posta zipatazo 71, vituo vya polisi vipatavyo 129, hospitali zipatazo 90 na mahakama zipatazo 27 kwenye mkonga wa taifa bila kusahau shule 425 a mbazo zitapata iternt bure. Hili si jambo dogo wala maendeleo kidogo.
        Kwa nyongeza, kwa mujibu wa the Maverick (Feburuari 14, 2016), Magufuli alipoingia madakani ukusanyaji mapato kitaifa ulikuwa jumla ya shilingi za kitanzania bilioni 900. Punde tu, ukusanyaji mapato ya taifa uliongezeka kufikia shilingi za kianzania trilioni 1.5. Sambamba na hili, zaidi ya wafanyakazi hewa 10,000 walibainishwa na kufukuzwa kazi na kuokoa zaidi ya dola za kimarekani bilioni 2 kwa mwezi (BBC, Mei 16, 2016); bila kusahau walioghushi na wengine kama hawa ambao nao pia wanaendelea kushughulikiwa. Je kweli hili ni jambo dogo? Kwanini tusimpongeze Magufuli kwa uMagufulishaji Tanzania? Linapokuja suala la utulivu na amani, Tanzania bado ina amani ukiachia matukio kidogo ya jinai; na yote hii inatokana na uwezo wa Magufuli wa kuunganisha umma akijibainisha kama mtu asiyekata tamaa na mwenye uwezo wa kusaka anachotaka na kukipata kwa gharama yoyote.
        Kwa ufupi, nilimuona kiongozi ambaye Tanzania ilimhitaji kwa mda mrefu baada ya kung’atuka kwa kiongozi mwingine jasiri na mzalendo wa kweli Mwl Nyerere; kiongozi ambaye vizazi vijavyo vitataja jina lake kwa kicho na kiwewe kama ataendelea na kasi, msimamo na staili hii na kama ataungwa mkono katika mipango na miradi yake bila kutetereka.
SAMAHANI, SIWEZI KUENDELEA. MACHOZI YAMEZIBA USO WANGU. MUHIMU NAMUOMBEA MAMA YETU SAMIA MUNGU AMSIMAMIE AVAE VIATU VIKUBWA HIVYO NA KUFANIKISHA MAMBO MAKUBWA HAYO. AAAMIN.
Chanzo: Raia Mwema leo.

No comments: