The Chant of Savant

Monday 1 November 2021

Waraka kwa Waziri Mkuu Asante kwa Kumleta Samia Suluhu Hassan 2025

Mpendwa Waziri Mkuu Majaliwa K Majaliwa, nakusalimu kwa jina tamu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Naomba kabla ya kusema mengi  nikushukuru kwa kumtoa paka kwenye kapu na kuondosha utata na sintofahamu ambayo–––usingefanya hivyo–––ingelisumbua taifa. Juzi vyombo bya habari vilikukariri  kuwa uliwataka mawaziri na naibu wao kuwa wasemaji wakubwa wa mafanikio ya Serikali ili itakapofika 2025, Samia Suluhu Hassan (Rais) apite na kusema kidogo tu.
            Ulikaririwa ukisema wazi kuwa “wambieni wananchi kuhusu mazuri yanayofanywa na Serikali hii, tambueni msimamo na mtazamo wa Rais ili mkawe wasemaje zaidi yeye akija awe na maneno machache ya kueleza.” Hili licha ya kuweka wazi ukweli, linawaandaa wananachi kumtathmini Mheshimiwa Rais ukiachia mbali kumuandaa kwa kufanyiwa hivi ili aweze kupata kura za kutosha kuwashinda wapinzani wake.  Pamoja na uzuri wa kuweka kila kitu wazi, umetangaza vita dhidi ya wapinzani na wale wote wanaowania nafasi hii adhimu na muhimu. Hivyo, ndani na nje ya chama jiandaeni kushuhudia mnyukano hasa kwa wale wasiokubuli kushindwa au wasioona ubora wa wenzao hasa ikizingatiwa kuwa Mheshimiwa Rais hakuwa mmojawapo waliotegemea kuwa tishio kwa azma yao ya kuutaka urais.
            Japo kuna watakaolalamika kuwa mmeanza kampeni kabla ya wakati wake. Heri walio wakweli–––hata wakichukiwa na kulaumiwa–––wataitwa wana wa Mungu. Sina shaka huu ndiyo msimamo wa Mheshimwa Rais ambao hata nami–––kama mshauri wake ambaye hakumteua lakini huwa anamsikiliza–––naunga mkono kwa sababu zifuatazo:
            Mosi, Mheshimiwa Rais hana wasi wasi wa kupoteza. Kwani, alishasema wazi kuwa hakuwahi kuotea kuwa Rais isipokuwa kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu aliyemfanya Rais bila yeye kuomba wala kupigania. Hivyo, hana wasi wasi wa kukosa nafasi hii ambayo sasa ameikalia na anaiweza vilivyo.
            Pili, kwa utendaji wake, sioni kama kuna mtu mwenye akili timamu anaweza kumuweka kwenye kundi la kukosa. Itakuwaje Mungu amuwezeshe kuwa Rais bila kugombea ashindwe au kumnyima fursa ya kuchaguliwa? Hata kama ya Mungu ni mengi, siku njema huonekana asubuhi. Hivyo, wale wanaoona kama Mheshimiwa ameanza kampeni kabla ya muda wake, wakumbue namna alivyoweza kukaria kiti cha urais bila hata kugombea. Wakubaliane na mipango ya Mungu ambaye huwakweza walio chini na kuwashusha waliojuu ukiachia mbali kuwapa nguvu wasio wasomi sana na kuwaacha wana falsafa.
            Tatu, kwa mtaji wake na ule wa mtangulizi wake, sioni mtu au chama kinachoweza kumshinda Mheshimiwa Rais ambaye, pamoja na mapungufu yake kama mwanadamu, ameweza kutosha kwenye viatu vya mtangulizi wake ukiachia mbali kudumisha amani ya taifa na mshikamano wake huku akizidi kuchanja mbuga kimaendeleo.
            Nne, kwa vile mtangulizi wake, Hayati Dkt John Pombe Magufuli alimwamini Mheshimiwa Rais mara mbili, watanzania wana kila sababu ya kumpigia kura za ndiyo kwa heshima ya kipenzi chao Magufuli ukiachia mbali kuonyesha kuweza kuendeleza mipango ya Magufuli.
            Mheshimiwa Waziri Mkuu, sasa nirejee kwako tena. Nakupongeza kwa ujasiri na uwazi wako wa kulisemea hili bila kujali maslahi yako binafsi kama kiongozi wa juu na mwanasiasa. Nina sababu za kufanya hivi kama ifuatavyo:
            Kwanza, umeonyesha wazi kuwa unamkubali Rais wako mbali na kuweka kando ndoto za kugombea mwaka  2025 ukiachia mbali kuwataarifu wanaootea urais kuachana na ndoto hizo au kujiandaa kukabiliana naye kama chama kitaruhusu–––jambo ambalo naona halina sababu hasa ikizingatiwa kuwa CCM tayari ina mgombea mwenye kutosheleza ambaye si mwingine bali Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Hata hivyo, ili kuepuka kutuhumiwa kuwa amependelewa au kubebwa, bado CCM inaweza kufuata utaratibu wake wa ndani wa kuruhusu wanachama wake wanaojiona wanafaa kugombea urais wafanye hivyo ili haki kutendeka ingawa watafanya hivyo ili kutimiza demokrasia. Kwani ,watakuwa wanajua fika kuwa–––kwa sasa–––hakuna mwana CCM mwenye sifa za kugombea urais zaidi ya Mheshimiwa Rais.
            Pili, kutoa kauli hii hadharani ni ushahidi kuwa unasimamia kile unachosema na kutenda. Kauli yako, hakika, itawasaidia wale waliokuwa wakiotea kugombea urais kwa tiketi ya CCM mwaka 2025 kuacha kupoteza muda na kuchapa kazi ya kulijenga taifa badala ya kujiingiza kwenye vita ya kuwania urais. Hili litasaidia kuepusha upotevu wa muda na hata mapambano ya ndani ya chama baina ya makundi hasimu ya kimaslahi aka mitandao.
            Tatu, japo kuna sababu nyingi za kukupongeza–––na pia bila shaka kukutahadharisha kwa hili––itoshe kusema kuwa timing yako ni nzuri hasa kwa siasa na ushindani wa ndani ya chama ingawa inaweza kuwa hatari––––kama tungekuwa na upinzani wenye mashiko na udhu wa kuweza kutoa changamoto na ushindani vya kutosha. Kwa namna hiyo, ni kwamba Mheshiwa Rais, anaweza kuanza kujiandalia kupita bila vikwazo kuendelea kukalia kiti chake. Kwa wanaojua nguvu na mifumo ya CCM, hatari na ushinda mkubwa vimo ndani ya chama kuliko nje yake.
            Hivyo, tumalize kwa kuwasihi wana CCM washikamane na kuhakikisha hili linafanikiwa ili kuendelea kujenga mazingara mazuri ya kuendelea kuliongoza taifa letu. Kwa  upinzani, mmeonyeshwa nani mshindani wenu mapema. Kazi kwenu kuhakikisha nanyi mnatumia fursa hii mkijua kuwa na mpinzani wenu anajua hatari ya kutangaza kugombea mapeman. Kwa watanzania, tafadhalini, hakikisha mnampima kila mgombea kwa matendo na sifa zake. Tunawatikieni kila la heri nyote.
Chanzo: Raia Mwema leo

No comments: